Kwa Nini Yakupasa Uhudhurie “Ujitoaji Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya
Siku tatu zenye kuthawabisha za maagizo ya Biblia zakungoja wewe kwenye “Ujitoaji Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa Mashahidi wa Yehova. Kwa njia ya hotuba na mahoji na drama moja yenye kutoa maagizo, mwongozo muhimu wa Biblia utaandaliwa. Uwepo saa 4:20 Ijumaa asubuhi wakati mkusanyiko unapoanza kwa muziki.
Programu ya Ijumaa asubuhi itakuwa na hotuba “Kuepuka Midomo ya Maumizo” pamoja na hotuba yenye maana juu ya mwanzo wa fundisho la Utatu. Alasiri, wazazi watapewa shauri la upole wakubali daraka lao la kiadili la kuandalia watoto wao urithi wa kiroho. Halafu, vijana watatiwa moyo wamfanye Kristo kuwa kiolezo chao na kufanya ukweli uwe wao wenyewe. Programu ya siku hiyo itamalizia kwa mazungumzo ya uandalizi mzuri ambao unafanywa hasa kwa ajili ya kusaidia vijana.
Jumamosi itakuwa siku nyingine kamili ya maagizo ambayo yatazungumzia ubatizo wakati wa asubuhi na alasiri hotuba zinazostahiki kuangaliwa juu ya Baraza Linaloongoza la Kikristo na jinsi sisi tunavyoweza kushirikiana nalo leo. Vipindi vya alasiri vitamalizia kwa hotuba yenye maana “Biblia—Neno la Mungu au la Wanadamu? ”
Jumapili asubuhi, maagizo ya wakati wake yataonya dhidi ya “mtu wa kuasi [sheria] na dhidi ya kukengeushwa na mambo ya chakula na kinywaji, kujipamba, na tafrija. (2 Wathesalonike 2:3) Hiyo itafuatwa na drama ya ki-siku-hizi ikikazia umaana wa kujitiisha wenyewe kwa Mungu. Kisha, wewe hutataka kuikosa hotuba ya watu wote, “Ukombozi Wakaribia kwa Ajili ya Watu wa Ujitoaji Kimungu! ”
Wakati wa Desemba na Januari mikusanyiko itapangwa katika Kenya, Tanzania na Uganda ili kuwe na mmoja karibu na kwenu. Pata habari kutoka kwa Mashahidi wa Yehova wa kwenu ujue wakati na mahali pa ule ulio karibu zaidi nawe.
[Picha katika ukurasa wa 32]
Mkusanyiko wa wilaya katika Verona, Italia