Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w90 8/1 kur. 26-31
  • Sisi Tulilea Watoto Wanane Katika Nidhamu ya Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sisi Tulilea Watoto Wanane Katika Nidhamu ya Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kujifunza Njia za Yehova
  • Utumishi wa Wakati Wote
  • Kulea Watoto
  • Kupainia Tena!
  • Matunda Ambayo Huleta Thawabu Nyingi
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kumtumikia Yehova Tukiwa Familia Iliyoungana
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Wakumbuke Watumishi wa Wakati Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Yehova Alibariki Uamuzi Wangu wa Kupiga Moyo Konde
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
w90 8/1 kur. 26-31

Sisi Tulilea Watoto Wanane Katika Nidhamu ya Yehova

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA OVERLAC MENEZES

“Walifika wakiwa wamepanda baiskeli yenye viti viwili.” Hivyo ndivyo Jornal de Resende lilivyoanza ripoti yalo ya ukurasa mzima juu ya familia yetu katika 1988, tulipokuwa tukiondoka Resende kwenda Lages kusini mwa Brazili.

RIPOTI ikaendelea kusema hivi: “Bila shaka, watu wenye umri mkubwa zaidi watakumbuka mume na mke waliovutia uangalifu wa Resende kwa njia yao asilia na ya aina yake ya kusafiri: baiskeli yenye fremu kubwa sana na viti viwili. Mbele kabisa, ndipo alipokuwapo dreva, Overlac Menezes, akiiendesha; katika kiti cha pili alikuwapo mke wake, Maria José. Mwaka wenyewe: 1956.”

Mwandikaji makala hiyo alikuwa mwanamume mmoja jina lake Arisio Maciel, naye alikuwa pia mkurugenzi wa kituo cha kwetu cha redio. Alikutana nasi mara ya kwanza katika 1956 wakati mke wangu na mimi tuliposhiriki sehemu katika ile programu ya Watch Tower Society ya kila juma, Mambo Ambayo Watu Wanafikiria. Katika makala hiyo, yeye alininukuu mimi nikisema kwamba wakati wa kukaa kwetu, “nyumba zote katika Resende zilifanyiwa ziara, barabara kwa barabara.”

Je! wewe ungependa kujua jinsi sisi tulivyopata kujulikana vema sana katika Resende? Na jinsi sisi, tukiwa huko, tuliweza kulea watoto wanane ‘katika nidhamu ya Yehova’ huku tukisaidia kuzuru nyumba zote katika Resende tukiwa na habari njema za Ufalme?—Waefeso 6:4, NW.

Kujifunza Njia za Yehova

Katika Januari 1950, Maria Minc, mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alianza kujifunza Biblia na dada yangu Adeilde katika São Paulo. Mimi nilikuwa na umri wa miaka 16 wakati huo na nilikuwa nimebatizwa nikiwa Mkatoliki lakini nilikuwa sijawa kanisani kwa muda fulani. Hata hivyo, bado niliamini katika Mungu na nilitaka kumtumikia. Kwa hiyo usiku mmoja, nilienda nyumbani kwa Adeilde nikajue habari za dini mpya aliyokuwa akijifunza. Maria Minc alinialika nijiunge katika funzo, na kwa mara ya kwanza katika maisha yangu, nikaona Biblia. Wakati wa mafunzo yaliyofuatana nilistaajabu kujua kutokana na Biblia kwamba jina la Mungu ni Yehova, kwamba karibuni dunia itakuwa paradiso, kwamba moto wa helo na purgatori havipo, na kwamba binadamu hana nafsi isiyokufa. Watu wa ukoo wangu waliniambia hivi: “Wewe utaingiwa na kichaa kwa kusoma sana Biblia kadiri hiyo!”

Nilifanya maendeleo mazuri katika funzo langu la Biblia na nikaanza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme la Kundi la Bélem katika São Paulo. Kwa kutarajia kuona watu wazima tu katika hudhurio, nilipata mshangao wa kupendeza kupata vijana wengi wa umri wangu mwenyewe. Siku ya Februari 5, 1950, nilishiriki katika kazi ya kuhubiri kwa mara ya kwanza, na siku ya Novemba 4 ya mwaka uo huo, nikaonyesha mfano wa wakfu wangu kwa Yehova kwa kubatizwa katika maji.

Muda mfupi baada ya hapo niliwekwa kuwa msemaji wa watu wote. Wakati huo, hiyo ilimaanisha kwamba nilitoa hotuba katika barabara na katika mabustani nikitumia kipaaza-sauti kilichopandishwa juu ya gari. Utendaji mwingine ulikuwa kazi ya magazeti. Siku hizo tulikuwa tukisimama katika kona za barabara tukiwa na mifuko yetu ya magazeti, tukipaaza sauti hivi: “Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Yakitangaza Ufalme wa Yehova!” Sikuangusha magazeti mengi, lakini nilipata moyo mkuu wa kusema mbele ya watu wote.

Utumishi wa Wakati Wote

Ukiwa Mradi

Muda si muda uangalifu wangu ulivutwa kwenye umaana wa utumishi wa painia, au utendaji wa kuhubiri wakati wote. Toleo la Aprili 1, 1950 la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) lilikuwa na makala yenye kichwa “Mapainia Zaidi na Zaidi wa Habari Njema.” Ilitaarifu hivi: “Kutafuta Ufalme kwanza humaanisha kwamba mtu angeweka kwanza kabisa katika akili yake masilahi ya Ufalme nyakati zote. Mtu wa jinsi hiyo angekuwa akitafuta fursa za kutumikia kwa ajili ya huo, wala hangekuwa akitafuta milele mahitaji yake ya kimwili kwanza na kurundika bidhaa za kilimwengu ili kulinda salama wakati ujao wake.” Maneno hayo yalikaza sana roho ya upainia katika moyo wangu.

Muda si muda, bibi kijana wa kuvutia jina lake Maria José Precerutti alibadili maisha yangu kwa njia ya maana. Yeye alikuwa akifanya maendeleo mema katika funzo lake la Biblia pamoja na mume na mke Mashahidi, José na Dília Paschoal. Siku ya Januari 2, 1954, yeye akawa ndiye mke, mwandamani, rafiki, na msaidiaji wangu mpendwa. Mradi wake, pia, ulikuwa kupainia. Kwa hiyo, kwa kutiwa moyo na vielelezo vya wamisionari kama Harry Black, Edmundo Moreira, na Richard Mucha, sisi tulijaza ombi la kuingia utumishi wa painia. Wazia shangwe yetu—na hangaiko—tulipopokea jibu: “Pendekezo lako la kuwa mwangalizi wa mzunguko limekubaliwa”!

Nilipopokea mgawo wangu wa kwanza wa mzunguko, nilipatwa na babaiko. Mzunguko wangu mpya ulitia ndani makundi kumi katika uliokuwa mji mkuu wa Brazili wakati huo, Rio de Janeiro, kutia na makundi fulani karibu na Betheli. Makao ya kimisionari ya Watchtower Bible School of Gilead yalikuwa katika kundi la kwanza nililogawiwa kuzuru. Nikiwa na umri wa miaka 22, nilihisi sitoshelei sana na nikamwambia Ndugu Mucha, ambaye ndiye wakati huo alikuwa akisimamia kazi katika Brazili: “Mimi naweza kuwafundisha nini watu hawa?” Yeye alijibu hivi: “Ndugu, wewe tumia tu shauri kutokana na Biblia na tengenezo.” Ushauri mwema kweli kweli!

Mwaka mmoja baadaye, Maria José akawa mwenye mimba, nasi tukalazimika kuacha kazi ya mzunguko. Ingawa hivyo, la kufurahisha ni kwamba tulibaki katika utumishi wa wakati wote. Kwa kujibu ombi fulani la familia mbili za Kifinlandi, akina Edvik na akina Leinïos, Sosaiti ilitupa mgawo twende Resende tukiwa mapainia wa pekee, na hilo lilikuwa lakaribia kuwa eneo bikira la wakaaji 35,000. Akina Leiniös ndio waliotupa sisi ile baiskeli yenye viti viwili iliyotajwa katika ile makala Jornal de Resende. Kwa kuitumia, sisi tuliweza kupanda mbegu nyingi za ukweli katika eneo hilo lenye rutuba, nasi tukaendelea kufanya kazi huko kwa miezi kadhaa mpaka binti yetu Alice alipozaliwa katika 1956. Tulipoondoka, dada wawili, Anita Ribeiro na Marian Weiler, walikuja kuzitilia mbegu maji na ‘Mungu akaendelea kufanya zikue.’ Leo, Resende ina makundi tisa na wahubiri zaidi ya 700.—1 Wakorintho 3:7, NW.

Mmoja wa watu wa kwanza niliokutana nao katika Resende alikuwa Manoel Queiroz. Nilipokuwa nikingoja basi, nilimwangushia vitabu viwili mahali alikofanya kazi. Yeye, na baadaye mke wake, Piedade, walifanya maendeleo mema na wote wawili wakabatizwa. Manoel akawa mzee katika kundi na kuendelea kuwa mwaminifu mpaka kifo chake. Pia nilijifunza na Álvaro Soares. Kwenye mkutano wa kwanza aliohudhuria, alishangaa kuona watu sita tu wakiwapo, lakini leo yeye ni mwangalizi wa jiji katika Resende ambako watu zaidi ya elfu moja huhudhuria mikutano katika makundi tofauti. Katika 1978, Carlos mwana wa Álvaro alioa binti yetu Alice. Leo, watu zaidi ya 60 wa familia ya akina Soare ni Mashahidi.

Kuondoka Resende kulimaanisha kwamba utumishi wetu wa wakati wote ulibadilishwa kwa wajibu mwingine wa Kikristo, ‘kuandalia wale walio washiriki wa nyumba yetu.’ (1 Timotheo 5:8, NW) Hata hivyo, sisi tulijitahidi kudumisha roho ya upainia, tukiendelea kuweka utumishi wa wakati wote uwe mradi wetu. Mimi nilipata kazi kwenye shirika fulani katika São Paulo, na kwa mwaka mmoja nikasafiri kila mwisho-juma kilometa 300 kwenda Resende kusaidia kikundi cha huko cha wahubiri 15. Halafu, katika 1960, tulihama tukarudi Resende.

Kulea Watoto

—Pendeleo Lililoongezeka

Kwa kweli sisi hatukupanga kuwa na watoto wengi jinsi hiyo, lakini hata hivyo walikuja, mmoja baada ya mwingine. Baada ya Alice kukawa na Léo, halafu Márcia, Maércio, Plínio, André, na mwisho, katika 1976, wale mapacha, Sônia na Sofia. Kila mmoja alipokewa kwa furaha kuwa “urithi kutoka kwa Yehova.” (Zaburi 127:3, NW) Na kila mmoja alilelewa katika “rekebisho la akilini la Yehova” kwa msaada wake.—Waefeso 6:4, NW.

Hata hivyo, hilo halikuwa furushi jepesi la kazi. Nyakati fulani tulilia machozi kwa sababu ya matatizo. Lakini ilithawabisha. Tuliwaleaje! Kwa funzo la familia, kwa kwenda pamoja nao kwenye mikutano na katika huduma ya shambani kuanzia utoto wao mchanga, kwa kufanya mambo pamoja, kwa kuhakikisha walikuwa na mashirika mema, kwa kuwapa nidhamu thabiti, na kwa kuweka kielelezo chema sisi wenyewe.

Miaka michache iliyopita, katika programu kwenye kusanyiko moja katika Cruzeiro, São Paulo, sisi tulihojiwa na mwangalizi wa mzunguko. Baada ya kuongea juu ya funzo letu la familia, mwangalizi wa mzunguko aliniuliza hivi: “Mke wako alishiriki fungu gani katika jambo hili?” Nakumbuka kwamba machozi yalinilenga-lenga machoni, nami nilikabwa na kitonge kooni hivi kwamba sikuweza kujibu. Kwa nini? Kwa sababu nilithamini kweli kweli fungu la kukata maneno ambalo Maria José alishiriki katika kudumisha familia yetu ya kitheokrasi. Bila utegemezo wake wa uaminifu, ingalikuwa vigumu sana!

Tangu pale pale mwanzoni mwa uchumba wetu, Maria José na mimi tulijifunza Biblia pamoja. Watoto walipotokea, ukawa mwito halisi wa ushindani kuendeleza funzo kwa ukawaida. Ili kusaidia katika jambo hilo, kila juma katika mlango wa friji nilionyesha wakati wa funzo la juma linalofuata na habari zitakazofikiriwa. Pia nilifanya migawo ya pekee kama ilivyohitajiwa. Kwa kielelezo, siku moja Márcia na Plínio walikuwa wakipigana mezani. Kwa hiyo kesho yake, wakakuta juu ya friji mgawo wa “Jinsi ya kuchukuliana na ndugu zako.” Kwenye funzo lililofuata, wote wawili walitoa maoni yao na wakasuluhisha tofauti zao.

Tatizo jingine lilikuwa katika asubuhi za Jumapili ambapo wavulana walikuwa mara nyingi wakisema kwamba walihisi wakiwa wagonjwa mno kutoweza kwenda nje katika utumishi wa shambani. Léo na Plínio walikuwa mabingwa wa kutunga kwamba wana maumivu ya tumbo na magonjwa mengine ili waepuke kuandamana nasi katika kazi ya kuhubiri. Wakati wowote nilipokuwa na mashaka juu ya kama kweli walikuwa wagonjwa, nilisema jambo kama hili: ‘Ikiwa nyinyi ni wagonjwa mno msiweze kwenda katika utumishi, basi bila shaka nyinyi si wazima kiasi cha kutosha kucheza mpira baadaye.’ Kwa kawaida, walipata nafuu ya haraka ajabu.

Pindi kwa pindi, tulihitaji kushughulikia hali kwa uangalifu. Léo alipokuwa na miaka 11, alienda mandari (pikniki) pamoja na Mashahidi wenzake, na bila ruhusa akanunua kilogramu moja ya nyama ya nguruwe ili ale. Baadaye, tulipoipokea gharama, Maria José alimwuliza Léo hivi: “Je! ulisahau kwamba ulinunua nyama ya nguruwe?” “La,” yeye akajibu bila kuhisi hatia. “Sikuinunua.” “Haya basi,” Maria akasema, “twende tukaongee na mwenye duka.” Wakiwa njiani kwenda huko, usahaulifu wa Leó ulikwisha. “Sasa nakumbuka,” akaungama, “sikuwa na pesa za kutosha, kwa hiyo nikainunua kwa mkopo na nikasahau kuilipia.” Mimi mwenyewe nililipa gharama hiyo na nikamwomba mwenye duka amwajiri Léo, amwache afanye kazi mpaka achume pesa za kutosha kunilipa mimi. Ilikuwa ndiyo adhabu yake. Kila asubuhi saa kumi asubuhi, Léo alikuwa ndiye wa kwanza kuwasili kazini, na katika muda wa mwezi mmoja akawa amenilipa kiasi kamili.

Sikuzote nyumba yetu ilijaa mapainia, waangalizi wenye kusafiri, wamisionari, na Wanabetheli. Muda mwingi hatukuwa na televisheni ndani ya nyumba, na hiyo ilitusaidia tufanyize mazoea mema ya kujifunza na ya mitazamo ya Kikristo. Katika mazingira ya namna hiyo ndimo tulilea watoto wetu. Baadhi ya barua walizotupelekea baada ya wao kuwa watu wazima zathibitisha kwamba mambo yalienda vema.—Ona sanduku katika ukurasa wa 30.

Kupainia Tena!

Walio wengi wa watoto wetu walipokuwa wamekuwa watu wazima, nilikumbuka makala moja katika toleo la Machi 1, 1955 la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) lenye kichwa “Je! Huduma ya Wakati Wote Yakufaa Wewe?” Kwa sehemu ilisema hivi: “Huenda watu fulani wakawa na mbetuko wa kuiona huduma ya wakati wote kuwa isiyowahusu. Lakini wao wakosea, kwa maana kutokana na nadhiri yake ya wakfu kila Mkristo ana wajibu wa kutumikia wakati wote isipokuwa kama hali asizoweza kudhibiti zafanya jambo hilo lisiwezekane.”

Usiku mmoja nilisali kwa Yehova anifungulie mlango tena ili niingie utumishi wa wakati wote. Familia yangu ilionyesha ushirikiano, na marafiki wakanitia moyo. Nilishangaa sana kwamba mkurugenzi wa shirika ambako nilikuwa nimefanya kazi kwa miaka 26 alikubali kuniacha nifanye kazi ya nusu-wakati ili niweze kutumikia nikiwa painia wa kawaida. Basi nikaanza kwa furaha kazi niliyokuwa nimelazimika kuiacha miaka mingi sana mapema. Na watatu wa watoto wangu walifuata kielelezo changu.

Tulitumikia kwa miaka miwili katika Itatiaia, ambako nilikuwa nimekuwa mzee kwa miaka 15, halafu tukaamua kuhamia mahali ambako uhitaji ulikuwa mkubwa zaidi. Hiyo ilimaanisha kuishi kwa kutegemea malipo ya uzeeni ya kiasi, yaliyo sawa na karibu robo moja ya mshahara mzuri. Hata hivyo, kwa kutumaini katika ahadi ya Yesu katika Mathayo 6:33, tuliiandikia Sosaiti juu ya mipango yetu. Juma moja baadaye, karibu turuke kwa shangwe tulipopokea jibu lao: “Yaonekana ikifaa sisi tudokeze kwamba mhamie jiji la Lages. Lijapokuwa na wakaaji zaidi ya 200,000, kuna wahubiri 100 tu huko katika makundi madogo matatu. Nyinyi mngekuwa msaada mkubwa katika eneo hilo.”

Tulihamia huko Februari 1988. Na tungali hapa, tukiwa kilometa zaidi ya 1,000 kutoka kwa watoto na marafiki wetu. Sasa ndipo tumemaliza msimu wa kipupwe kilicho kibaya zaidi katika muda wa miaka 20. Mimi tu ndiye mzee katika kundi letu, kwa hiyo kuna mengi ya kufanya. Hata hivyo, sisi tumebarikiwa sana sana. Lenye upendezi mwingi zaidi ni eneo lenyewe. Tubishapo hodi kwenye milango ya watu, wao husema: “Ingia ndani tafadhali!” Mafunzo ya Biblia ni rahisi kuanzishwa. Sisi hukubali vitu tofauti kuwa misaada ya upaji wakati fedha ziwapo haba, nasi tumekuja nyumbani na sabuni, marashi, nyembe, nguo za vitoto (kwa ajili ya mjukuu wetu), nafaka za kula, mboga, matunda, maziwa-mtindi, divai, na hata aisikrimu. Wakati mmoja tulikubali vibago vya mbao!

Matunda Ambayo Huleta Thawabu Nyingi

Leo, nikiwa na umri wa miaka 56, nasisimuka wakati wowote nifikiriapo familia yetu. Haikuwa kwamba watoto ‘walizaliwa katika ukweli.’ Walizaliwa katika makao ya Kikristo, na ukweli ulikuwa umekaziwa katika akili na mioyo yao michanga. Wale waliofunga ndoa walifanya hivyo “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39; Kumbukumbu 6:6, 7) Ni kweli kwamba tulifanya vikosa na makosa katika uamuzi. Nyakati fulani tulifanya mambo yasiyo haki. Pindi kwa pindi, mimi nilishindwa kuweka kielelezo bora au nikakosa kujali daraka langu nikiwa baba na mume. Nilipong’amua nililokuwa nimefanya, niliomba msamaha wa Yehova na mke wangu au watoto wangu, nami nikajitahidi kusahihisha kosa hilo.

Tujapokuwa na hali za kutokamilika, familia yetu—ambayo sasa imeongezwa na wana-wakwe, binti-wakwe, na wajukuu—ina washiriki sita katika huduma ya wakati wote, wazee wanne, na mtumishi wa huduma mmoja. Wote isipokuwa wajukuu wamebatizwa. Watoto wadogo watatu ambao wangali pamoja nasi wapanga kufanya utumishi wa wakati wote uwe kazi yao ya maisha. Ni thawabu gani kubwa kuliko hiyo ambayo mtu angeweza kutumainia? Mimi namshukuru Yehova kwa kuwa alituongoza kulea watoto wetu katika nidhamu yake. Twasisimuka kuwaona bado wakifuata mafundisho yake. Nami nasali kwamba sisi, na wao vilevile, wasipate kamwe kugeuka kando kwa kuiacha njia ya uhai.

[Sanduku katika ukurasa wa 30]

Baada ya wao kukua, nyakati fulani watoto wetu walionyesha uthamini katika barua kwa jinsi tulivyowalea. Haya ni machache ya maelezo yao:

“Baba, iweni na uhakika kwamba wewe na Mama mlitufanyia lililo bora kabisa, hata ikiwa mlifanya makosa—jambo ambalo hupata sana Carlos na mimi katika kushughulika na Fabrício mwana wetu.”

Binti Alice, umri 33, mama ya wavulana wawili.

“Ni lazima tukiri kwamba nyinyi mlifanya jitihada ya mwungano kutulea katika rekebisho la akilini la Yehova. Na sasa sisi tunanufaika nalo kama nini!”

Binti Márcia, umri 27, na mume wake, aliye katika kazi ya mzunguko.

“Mimi nang’amua kwamba pendeleo nililo nalo sasa halingaliwezekana bila msaada ambao nyinyi wawili mlinipa kuimarisha msingi thabiti wa kiroho na upendo kwa Yehova na utumishi wake.”

Son Maércio, umri 23, painia wa pekee.

“André, jifaidi kikamili kutokana na uandamani na ujuzi wa Baba. Usipuuze kamwe shauri lake. Mtaweza kusaidiana. Mimi nina furaha sasa kuliko wakati mwinginewo.”

Son Plínio, umri 20, akiwa Betheli.

[Picha of Overlac Menezes’ family katika ukurasa wa 26]

[Hisani]

Foto: MOURA

[Hisani]

Foto: CALINO

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki