Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w90 11/15 kur. 5-7
  • Jinsi ya Kukabiliana na Tatizo la Kiadili la Kuwa Maskini

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi ya Kukabiliana na Tatizo la Kiadili la Kuwa Maskini
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ufuataji Haki—Maoni ya Biblia
  • Utatuzi: Kutumaini Katika Mungu
  • Wabarikiwa kwa Kutumaini Katika Mungu
  • Karibuni, Hakuna Atakayekuwa Maskini!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Je, Umaskini Ni Sababu Halali ya Kuiba?
    Amkeni!—1997
  • Tajiri Ingawa Maskini—Yawezekanaje?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Umaskini Unaoongezeka—Tisho kwa Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
w90 11/15 kur. 5-7

Jinsi ya Kukabiliana na Tatizo la Kiadili la Kuwa Maskini

“WATU ni maskini kwa sababu ni wavivu,” akadai daktari mmoja Mwafrika. “Jiji limejaa wazururaji. Kama wangetaka kazi kikweli, wangeweza kuipata. Hakuna uhitaji wa mtu yeyote kuwa katika umaskini leo.”

Hakuna shaka kwamba watu fulani ni wavivu na kwamba uvivu waweza kuongoza kwenye umaskini. Biblia husema hivi: “Bado kulala kidogo, kusinzia kidogo, bado kukunja mikono upate usingizi! Hivyo, umaskini wako huja kama mnyang’anyi, na uhitaji wako kama mtu mwenye silaha.” (Mithali 24:33, 34) Hata hivyo, maskini wengi si wavivu hata kidogo. Kwa kielelezo, fikiria mwanamume aliyeandika hivi: “Hata saa hii ya sasa, tuna njaa na kiu, tu uchi, twapigwa ngumi, tena hatuna makao.” (1 Wakorintho 4:11) Je! huyo alikuwa mzururaji hoi kabisa? Sivyo kamwe. Maneno hayo yaliandikwa na mtume Paulo. Yeye alichagua kuishi maisha ya riziki kidogo ili aweze kufuatia vizuri zaidi huduma ya Kikristo. Ukosefu wake wa baadhi ya mahitaji ya maisha ulisababishwa pia na hali ambazo hakuweza kuzuia, kama mnyanyaso wa kidini.

Leo, walio wengi wa maskini wa ulimwengu ni wale wapatwao na hali wasizoweza kudhibiti—labda ukosefu wa elimu, uchumi wenye kuzorota katika eneo la kwao, au msukosuko wa kisiasa. Wengi hutoa jasho kuanzia mapema asubuhi hadi usiku sana na kuchakura riziki kidogo tu. Hivyo huenda fursa za kupata fedha kwa njia isiyofuata haki zikaonekana kuwa zenye kuvutia, hata zenye kuhitajiwa kabisa. Kwani, huenda watu fulani wakasababu kwamba Biblia hutetea kuacha maadili pindi kwa pindi! Ingawaje, hiyo husema hivi: “Watu hawamdharau mwivi, akiiba ili kujishibisha, iwapo aona njaa.” Na mwanamume mmoja mwenye hekima alisali hivi: ‘Nisije nikawa maskini sana nikaiba.’—Mithali 6:30; 30:8, 9.

Ufuataji Haki—Maoni ya Biblia

Je! kweli maandiko haya ya Biblia yadokeza wazo la kukubalia ukosefu wa kufuata haki? Acheni tuyachunguze kulingana na habari zinazozunguka. Baada ya kukiri kwamba watu hawadharau mwizi aibaye ili kujaza tumbo lililo tupu, Mithali 6:31 yaendelea kusema hivi: “Lakini akipatikana, atalipa mara saba; atatoa mali yote ya nyumba yake.” Ndiyo kusema, mwizi huyo apatikanapo, yeye hukabili adhabu kamili ya sheria. Hulipia uhalifu wake! Kwa hiyo, badala ya kutia moyo kuiba, maneno haya yawaonya maskini kwamba kuiba kwaweza kutokeza hasara ya kiuchumi, fedheha kwao wenyewe na familia zao, na hasara ya kujistahi.

Lakini namna gani sala ya huyo mwanamume mwenye hekima? Yeye aliomba kwamba asiweze kuja kwenye umaskini na ‘kuiba na kulitaja bure jina la Mungu wake.’ (Mithali 30:9) Ndiyo, ukosefu wa kufuata haki kwa upande wa mtu adaiye kutumikia Yehova waweza kuleta suto juu ya jina la Mungu na juu ya kundi la watu Wake. Mtume Paulo aliandika hivi: “Wewe uhubiriye kwamba mtu asiibe, waiba mwenyewe?” Kama watu fulani wenye kudai kuwa Wakristo wangeiba, hiyo ingeweza kusababisha ‘jina la Mungu litukanwe katika Mataifa.’—Warumi 2:21, 24.

Basi, kwa sababu nzuri Biblia yasema hivi: “Afadhali maskini aendaye katika unyofu wake, kuliko mpotofu wa njia angawa ni tajiri.” (Mithali 28:6) Ingawa yeye mwenyewe alikuwa na maandalizi haba nyakati fulani, mtume Paulo hakukubalia wala hakugeukia kamwe ukosefu wa kufuata haki. Badala ya hivyo, aliandika hivi: “Mwibaji asiibe tena; bali afadhali afanye juhudi, akitenda kazi iliyo nzuri kwa mikono yake mwenyewe, apate kuwa na kitu cha kumgawia mhitaji.”—Waefeso 4:28.

Utatuzi: Kutumaini Katika Mungu

Namna gani wale wanaofanya kazi ngumu lakini wasioweza kuchuma kiasi cha kutosha kutunza familia zao wenyewe? Je! kuwa na ukosefu wa kufuata haki au hata kuiba ni halali katika kisa chao, hasa ikiwa ugonjwa wakumba mshiriki wa familia au dharura nyingine yatukia? Watu fulani hufikiri hivyo. Mkaaji wa bara moja la Afrika alisema hivi: “Katika nchi yetu, ukiwa mfuataji haki, hutaishi. Ukitaka kubaki hai, ni lazima ufuate konakona kadhaa katika njia yako ya maisha.”

Hata hivyo, kotekote katika Afrika mtu huyaona mara nyingi maneno “Tumaini Katika Mungu” yakiwa yamechorwa kwa rangi juu ya magari, yakiwa yameonyeshwa katika vibao vya ukutani, na kupigwa chapa juu ya michoro ya kubandikizwa na kwenye vibandiko vya mabango ya magari. Biblia yenyewe yasema hivi: “Mtumaini BWANA [Yehova, NW] kwa moyo wako wote.” (Mithali 3:5) Ukosefu wa kufuata haki chini ya hali yoyote haungeweza kamwe kupatana na himizo hilo la Kibiblia. Lakini je! kutumaini Mungu ndilo jibu litumikalo kwa lile tatizo la kiadili la kuwa maskini?

Akiwa mhudumu wa Mungu, mtume Paulo alipatwa na magumu kama ‘njaa na kiu; kufunga mara nyingi; baridi na kuwa uchi.’ (2 Wakorintho 11:27) Kwa uhakika, ni lazima Paulo awe alishangaa angebakije akiwa hai! Lakini baada ya miaka kama 25 ya maono ya Kikristo, angeweza kuandika hivi: “Najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote, nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa. Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” (Wafilipi 4:12, 13) Ndiyo, Paulo alitumaini katika Mungu.

Paulo aling’amua kwamba kanuni za Kimaandiko si maneno matupu, ya kuwazia mambo tu. Ni maagizo kutoka kwa Mungu aliye hai ambaye ana hamu ya kuwasaidia na kuwategemeza wale wanaotafuta kuyatumia. Nabii mmoja wa kale alisema hivi: “Kwa maana macho ya BWANA [Yehova, NW] hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.”—2 Nyakati 16:9.

Wabarikiwa kwa Kutumaini Katika Mungu

Kwa nini ni vigumu sana kwa watu walio wengi kutumaini katika Mungu? Bila shaka kwa sababu dini yao imeshindwa kuwapa sababu ya kutosha kufanya hivyo. Makanisa yamefanya Mungu aonekane kuwa asiye na jina, kuwa kitu cha kufikiriwa kimawazo tu, kuwa asiye na utu, asiyeweza kueleweka kwa fikira za kibinadamu. Lakini kupitia funzo la Biblia, Mashahidi wa Yehova wamepata kumjua Mungu, si kama kani ya kuwaziwa tu, bali kama Mtu mwenye jina. (Zaburi 83:18; Waebrania 9:24) Wamejifunza kwamba yeye ana sifa zinazomfanya astahili tumaini letu. Mathalani, kulingana na Kutoka 34:6, Yehova ni “Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli.” Mashahidi hutumaini Mungu na kung’amua kwamba yeye ni ‘mwingi wa kweli.’ Kwa sababu hiyo, wao wana uhakika kamili katika ahadi yake ya kuleta upesi ulimwengu mpya usio na umaskini wenye kuchochota ambao sasa wasumbua sehemu kubwa sana ya jamii ya kibinadamu.—2 Petro 3:13.

Kwa hiyo mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wamethibitisha kwamba kutumaini katika Mungu ni jambo linalofanya kazi. Kwa kielelezo, Rosaline, Shahidi mmoja katika Sierra Leone, hufanya kazi ngumu kuanzia saa kumi na moja asubuhi mpaka usiku sana ili kuandaa chakula na nguo kwa ajili yake mwenyewe na watoto wake sita. Mwanamke huyo ataarifu hivi: “Watu wengi husema kwamba haiwezekani kuishi maisha ya ufuataji haki, lakini mimi najua kwamba hii si kweli. Nyakati fulani mimi huwa na matatizo nisijue jinsi yatakavyotatuliwa. Lakini najua kwamba nikiishi maisha ya ufuataji haki, kila jambo litakuwa sawa kwangu. Kwa hiyo mimi hujaribu sana kutomchukiza Yehova.”

Mwandikaji mmoja alisema hivi: “Mtu maskini asiye na kitu tumboni mwake huhitaji tumaini . . . kuliko mkate.” Ndiyo, kukosa tumaini, kukata tamaa, na kukosa furaha muda wote ni masumbufu yawezayo kuumiza kuliko njaa. Lakini mtu apataye kumjua na kumtumaini Mungu hahitaji kujiacha ashindwe na kukata tamaa. “Mimi nafanya kazi ngumu sasa,” aongezea Rosaline, “lakini nina shangwe kwa sababu najua kwamba wakati unakuja ambapo sitalazimika kutoa jasho kwa njia hii. Sasa mimi nafanya kazi ili nipate chakula kwa ajili yangu na familia yangu, lakini katika ulimwengu mpya wa Yehova, kutakuwa na chakula tele. Hivyo basi sasa mimi nina tumaini na shangwe ambayo sikuwa nayo kamwe kabla sijamjua Yehova.”—Linganisha Isaya 25:6; Ufunuo 21:3, 4.

Ni kweli kwamba huenda wale wanaotumaini katika Mungu wakapatwa bado na misongo ya kiuchumi, kama ilivyompata mtume Paulo. Lakini hawahitaji kamwe kugeukia kuvunja sheria za Mungu ili wabaki hai kiuchumi. Mtunga zaburi Daudi alisema hivi: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa, wala mzao wake akiomba chakula.” (Zaburi 37:25) Ndiyo, Mungu huwajali na kuwabariki wale wawekao masilahi yake kwanza katika maisha zao.—Mathayo 6:25-33.

Hivyo basi ikiwa wewe ni maskini, ‘usikate tamaa katika kutenda mema.’ (2 Wathesalonike 3:13) Usigeukie kamwe kuridhiana kiadili. Jenga uhusiano pamoja na Mungu na umtegemee akusaidie kukabiliana na matatizo na magumu ya maisha. Wale watumikiao Yehova na kumtumaini kweli kweli wahimizwa hivi: “Nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake; huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu.”—1 Petro 5:6, 7.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Mtu maskini asiye na kitu tumboni mwake huhitaji tumaini . . . kuliko mkate.”

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mashahidi wa Yehova husaidia watu watie tumaini lao katika Mungu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki