Katayarishwa kwa Utumishi wa Kimisionari Katika Miaka ya 1990
KIPINDI cha pekee kinaanza kwa utumishi wa kimisionari. Huku milango ya nafasi ikifunguka katika maeneo mengi mapya, Mashahidi wote waaminifu wa Yehova wana hamu ya kusonga mbele kwenye utendaji mkubwa hata zaidi.
Hivyo basi ilikuwa ni kwa tazamio kubwa kwamba wale wanafunzi 24 wa darasa la 89 la Watchtower Bible School of Gilead walihudhuria programu yao ya uhitimu katika Septemba 9, 1990. Wasikilizaji waliokuwa jumla ya wageni walioalikwa zaidi ya 5,000 na washiriki wa familia ya Betheli walikusanyika kwa ajili ya uhitimu wa wamisionari wapya hawa, ambao tayari walikuwa wamepokea migawo kwenda nchi kumi. Ikitoka Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova katika Jiji la Jersey, New Jersey, programu nzima ilisikiwa pia na wale waliokusanyika kwenye Betheli ya Brooklyn, Mashamba ya Watchtower, na kwenye Kitovu cha Elimu cha Watchtower kule Patterson, New York.
Saa 4:00 kamili ya asubuhi, Theodore Jaracz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova na mwenyekiti wa siku hiyo, aliomba wimbo wa kufungua. Kufuata hili, sala ikatolewa na Arthur Worsley wa familia ya Betheli ya Brooklyn. Ndipo mwenyekiti akaelekeza kwenye Matendo 10:33, ambapo Kornelio amiri-mia Mroma aliambia Petro hivi: “Sisi sote tupo hapa mbele za Mungu, tupate kuyasikiliza maneno yote uliyoamriwa na Bwana [Yehova, NW].” Ilisemwa kwamba matukio ya kihistoria yenye kutukia katika siku ya Petro yangefungua njia ya habari njema kujulishwa rasmi kwa mataifa yote.
Philip D. Wilcox, kutoka Mashamba ya Watchtower, alitoa ya kwanza ya hotuba saba zenye kusisimua. Akitumia maneno ya Wafilipi 4:7, alichukua kichwa chake kuwa “Amani ya Mungu na Iwasaidie Katika Mgawo Wenu.” Alisema hivi: “Yehova Mungu ndiye Chanzo cha amani yote ya kweli. Yeye anafurahia amani katika maana ya ujumla, au kamili, naye hawi na wasiwasi, hangaiko, wala usumbufu wowote wa akili. Kwa hiyo, kuna utulivu na amani yenye kuzunguka kuwapo kutukufu kwa Yehova katika kiti chake cha ufalme, kama inavyoonyeshwa na ule upinde wa rangi ya zumaridi-kijani ulioonwa na Yohana katika njozi. (Ufunuo 4:2, 3) Amani yake inaelekea nje zaidi ya alipo yeye mwenyewe kufikia wale wote ambao wataruhusu iwasaidie. Je! nyinyi mtaiacha ifanye hivyo?” Ndugu Wilcox alitaja misaada miwili muhimu, sala na nia ya kumngojea Yehova. (Mika 7:7; Wafilipi 4:6) Hakuna jambo lolote ambalo Mungu anaruhusu linaloweza kusababisha umizo la kudumu, akasema.
Lloyd Barry, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alifuata juu ya kichwa “Endelea Kutabasamu.” Alianza kwa usemi, “Kicheko ni dawa nzuri.” Alikumbuka usemi huo kwa sababu huko nyuma katika 1955 kilikuwa ndicho kichwa cha toleo lililokuwa la kwanza la gazeti Amkeni! kutokea katika Kijapani. Lakini kicheko cha aina gani? Si kile “kicheko cha mpumbavu” chenye makelele mengi, kisicho cha akili. (Mhubiri 7:6) Bali, ni kile kicheko chenye uchangamfu na ustarehe cha wamisionari na wengine wanaoitikia mwaliko wa Daudi wa ‘kushangilia katika Yehova’ sikuzote. (Zaburi 32:11) Ndugu Barry alisema kwamba kujapokuwa na majaribu makali, Ayubu angeweza kuendelea kutabasamu, kwa maana alijua alikuwa akishika uaminifu wa kimaadili kwa Mungu. Wamisionari walio thabiti ijapokuwa wanapatwa na majaribu kama ya Ayubu watapokea ile baraka kubwa zaidi mwishowe. (Ayubu 29:24; 42:12) Msemaji alimalizia hivi: “Endeleeni kuwa wenye shughuli, endeleeni kutabasamu, nanyi mtavuna tabasamu ya kibali cha Yehova cha milele.”
Msemaji aliyefuata alikuwa Richard E. Abrahamson, aliyechagua kichwa “Acheni Kiasi Chenu Kijulikane kwa Watu Wote,” msingi wacho ukiwa Wafilipi 4:5, NW. Kulingana na Kigiriki cha msingi, neno ‘-a kiasi’ linaweza kuwa na maana ya “-kuachia nafasi.” Wamisionari fulani wamekuwa na matatizo kwa sababu tu ya mapendezi ya kibinafsi. Mmoja alishtuka kwa jinsi misionari mwenzake alivyokata kwa nguvu kipande cha jibini mezani. Baada ya miaka 22 ya utumishi wa misionari, yule aliyekuwa ameshtuka aliona kwamba matata yaliyo mengi yanaanza kuhusiana na mambo yasiyo na maana sawasawa na jinsi mtu anavyokata jibini. Msemaji alishauri hivi: “Jifunzeni kujirekebisha, kama mti katika dhoruba. Kuna faida nyingi za kuwa wenye kuachia nafasi, kama vile mtu kuweza kuvumilia majaribu na kubaki kwenye mgawo wake akiwa na amani ya akili.”
Milton G. Henschel, wa Baraza Linaloongoza, alizungumzia kichwa “Mlango Mkubwa Unaoongoza Kwenye Utendaji Umefunguka.” Ndugu Henschel alisema kwamba Yesu alipenda watu, akawasikitikia, na kuwafundisha mambo mengi. Akiwa Efeso mtume Paulo aliwaandikia Wakorintho hivi: “Nimefunguliwa mlango mkubwa wa kufaa sana, na wako wengi wanipingao.” (1 Wakorintho 16:8, 9) Kujapokuwa na upinzani huu, Paulo alifundisha katika jumba la usikilizaji la Tirano kwa miaka miwili, hivi kwamba ujumbe wa Ufalme ulipata kujulikana kotekote katika wilaya ya Esia. (Matendo 19:9, 10) Mlango huo uliofunguka uliongoza kwenye mafanikio katika kuhubiri kwake. Kundi la Efeso lilikuwa bado likifanya kazi mwishoni mwa karne ya kwanza.—Ufunuo 2:1-7.
Jack D. Redford, mfunzi wa Gilead, aliongea juu ya kichwa ‘Endeleeni Kujijaribu Nyinyi Ni Nini.’ (2 Wakorintho 13:5) Wamisionari wa Gilead wamefungua mashamba mapya na kuimarisha makundi yaliyofanyizwa tayari, wakivumilia mengi na kukinza kitafuno cha kuwatega ambacho Ibilisi amewanyooshea ili kuwageuza kando. Na wapya wanaendelea kujiunga nao. Kwa maono mawili ya wazi sana, mfunzi alitoa mfano jinsi ilivyo muhimu mtu kujaribu imani yake. Misionari mmoja wa kiume alipoteza mapendeleo yake baada ya kupuuza shauri lenye kumwonya juu ya mwendo mbaya. Tofauti na hivyo, mwingine wa kike alibaki katika mgawo wake akiwa na shangwe, ingawa katika miezi yake mitatu ya kwanza huko, alikuwa amebaki akiwa ngozi na mifupa tu kutokana na ugonjwa uliofanya pia apoteze nywele zake na kusikia kwake. Angali huko baada ya miaka 42 na, kupitia mafunzo ya Biblia, amesaidia watu 156 kufikia ubatizo. Ndugu Redford alimalizia hivi: “Kinzeni Ibilisi, naye atawakimbia. Msichukue kamwe kitafuno chake. Endeleeni kuthibitisha nyinyi wenyewe ni nini. Yehova atawatunza.”
Halafu, mfunzi mwingine, Ulysses V. Glass, akasema juu ya kichwa “Hekima Iko Pamoja na Wenye Kiasi.” (Mithali 11:2, NW) Alitumia saa ya mkono yenye betri ya nguvu za jua kutoa mfano kwamba nuru ya Neno la Mungu inaweza kuendelea ‘kututilia nguvu.’ “Lakini,” akaonyesha, “maarifa pekee hayatoi hekima. Kiasi pia kinatakwa na Mungu.” (Mika 6:8) Kiasi kitatuongoza kuogopa Mungu, na “woga wa BWANA [Yehova, NW] ni mwanzo wa hekima.” (Mithali 9:10, ZSB) Ni kweli, ni lazima tujifikirie kwa kadiri fulani; kujilaumu-laumu kunaweza kuharibu. Yehova amewapa watu fulani uwezo wa pekee, kama vile alivyofanya wakati wa ujenzi wa hema takatifu, lakini ni lazima kujitahidi kuwa na uaminifu katika kiasi. “Wakati wa kipindi cha masomo,” Ndugu Glass akaliambia darasa, “nyinyi mlitoa ushuhuda wa kutegemeka na heshima. Onyesheni uaminifu uu huu katika mgawo wenu, na Mungu atawabariki.”
Albert D. Schroeder, wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ya kichwa cha makala hii “Katayarishwa kwa Utumishi wa Kimisionari Katika Miaka ya 1990.” Alianza hivi: “Miaka ya 1990 tayari imeanza kwa kishindo. Mataifa mengi ya Ulaya ya Mashariki yametikiswa. Miezi kadhaa iliyopita Ukuta wa Berlin ulifunguliwa. The New York Times lilikuwa na kichwa kikubwa hiki: ‘Agosti 1990, Mwezi Uliotikisa Ulimwengu.’ Hivyo basi, nyinyi wahitimu mnaishi katika wakati wa mtikiso. Je! miezi yenu mitano ya funzo imewatayarisha kwa ajili yake? Ndivyo kabisa!” Halafu akataja mengine ya mambo yenye msaada ya New World Translation of the Holy Scriptures—With References na jinsi kujifunza hiyo kumefanya Neno la Mungu liwe hai. Chombo kingine chenye nguvu ambacho kimetayarisha wanafunzi ni “All Scripture Is Inspired of God and Beneficial,” ambacho sasa kimo katika chapa yacho iliyosahihishwa ya 1990. Kile kichapo cha hivi majuzi Mankind’s Search for God kinapasa pia kuwa msaada wenye nguvu kwa wamisionari. Ndugu Schroeder alimalizia hivi: “Hivyo basi, akina ndugu, mpeni Yehova asante kwa elimu ya ajabu yenye thamani isiyohesabika ambayo mmepata—moja iliyo imara na isiyoweza kutikiswa. Songeni mbele mkiwa na baraka ya Yehova na mwe na uhakika kamili katika yeye na Kiongozi wetu wa ajabu, Yesu Kristo. Maneno tuliyo nayo katika Maandiko yamevuviwa kikweli na yatawaongoza na kuwaelekeza nyinyi katika kazi ya kimisionari.”
Salamu kutoka nchi 11 zilisomwa. Wanafunzi walipokea diploma zao, na mmoja wao akasomea Baraza Linaloongoza na familia ya Betheli barua iliyo na maono ya kutoka moyoni.
Kipindi cha alasiri kilitia ndani funzo lililofupishwa la Mnara wa Mlinzi, likiongozwa na David L. Walker, mshiriki wa Halmashauri ya Mashamba ya Watchtower. Halafu wanafunzi wakatumia kichwa kile chenye kutia moyo “Nguvu ya Sala Katika Kuhubiri” katika kuigiza maono ya shambani. Kundi moja la hapo lilionyesha drama yenye kusisimua Kawekwa Huru Kuendeleza Ibada ya Kweli, ikitegemea kurudi kwa Ezra kwenda Yerusalemu ili kuendeleza ibada ya kweli. Ndugu Frederick W. Franz, msimamizi wa Shule ya Gilead, alimalizia kwa sala yenye kugusa moyo.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Darasa la 89 Lenye Kuhitimu la Watchtower Bible School of Gilead
Katika orodha iliyo chini, safu zimepewa namba kutoka mbele kwenda nyuma, na majina yamepangwa katika orodha kutoka kushoto kwenda kulia katika kila safu. (1) Ahr, K.; Johnston, L.; Ng Ying Kin, V.; Sukkau, A.; Rodriguez, A.; Myklebust, N. (2) Ahr, H.; Verbeek, P.; Verbeek, K.; DeBolt, S.; DeBolt, S. (3) Sukkau, W.; Ayala L; Ayala, S.; Jenson, R.; Ng Ying Kin, J.; Myklebust, T. (4) Rodriguez, C.; Ferlisi, G.; Ferlisi, L.; Tank, J.; Jenson, K.; Tank, J.; Johnston, P.