Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Ukweli wa Biblia Unashinda Mapokeo
MAPOKEO ya kidini yanaweza kuwa na mizizi ya ndani sana. Mamilioni wana maoni ya kwamba ni kosa mtu kubadili dini yake. Sauli, ambaye akawa mtume Paulo, kwa wazi alikuwa na maoni ayo hayo, kwa kuwa alisema hivi: “Nikajitahidi sana katika kuyashika mapokeo ya baba zangu [kuliko wengi walio hirimu zangu].” Lakini alipoonyeshwa ukweli, alibadilika kutoka Dini ya Kiyahudi kuwa Mkristo. (Wagalatia 1:13-16) Wengi leo wamekuja kufahamu kwamba ukweli wa Biblia unatoka kwenye chanzo kilicho juu kuliko mapokeo. Angalia jinsi ukweli wa Biblia ulivyoshinda katika Italia.
Mwanamke mmoja anaeleza hivi: “Dada yangu na mimi tulikulia katika familia kubwa yenye mapokeo ya Kikatoliki yaliyo ya muda mrefu, nasi tulikuwa Wakatoliki wenye kujitoa sana. Kadiri wakati ulivyopita, nilifunga ndoa. Halafu nikafiwa na mume wangu, nami nikaishi nikiwa mjane kwa miaka mingi nikiwa peke yangu pamoja na watoto wangu. Mpwa wangu wa kike alifundisha katekisimu, naye aliendelea kumwuliza padri maswali ya Biblia, lakini hakupokea majibu ya kutosheleza.”
“Nilipokuwa nikitembelea mji wa nyumbani kwetu, nilionana mara ya kwanza na Mashahidi wa Yehova na nikakubali funzo la Biblia. Wote waliokuwa waandamani wangu Wakatoliki walinidhihaki kwa kujifunza Biblia. Hata hivyo, sikuvunjika moyo. Kwa mara ya kwanza, nikawa na Biblia, na hakuna mtu angeninyang’anya hiyo kamwe. Dada yangu pia akachukua msimamo wake upande wa Yehova, na katika muda unaopungua miaka miwili, sisi wote wawili tukabatizwa.
“Nililia nilipovunja uhusiano mara ya kwanza kutoka kanisani kwa sababu nilihofu kuacha mapokeo yaliyokuwa yametia mizizi ndani yangu kwa miaka 76. Lakini sasa nafurahia kutembea katika njia za Yehova na kufanya yote niwezayo ili kusaidia wengine watoke katika giza la kiroho!”—Linganisha 1 Petro 2:9.
Mkata Nywele Anasahihisha Fikira Yenye Makosa
Mkata nywele katika Japani alipenda sana kuongea juu ya roho waovu na ma-UFO (vitu visivyotambulikana vyenye kuruka angani) alipokuwa akikata nywele za waliozoea kumjia. Hata hivyo, baada ya yeye kuanza kujifunza Biblia, alifahamu jinsi zoea hili lilivyokuwa hatari. Hivyo basi badala yalo alialika waliozoea kumjia kwamba wajiunge naye katika funzo lake la Biblia. Kwa vijana waliozoea kumjia alitoa ushahidi juu ya uumbaji. Kila juma aliagiza Biblia na nakala za kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani kutoka kwa Shahidi aliyekuwa akijifunza naye ili aweze kuwaangushia wateja wake.
Ingawa alikuwa bado si Shahidi, aliangusha miunganisho zaidi ya 30 ya Biblia na vitabu Kuishi Milele katika mwaka wake wa kwanza wa kujifunza. Watu zaidi ya 25 walianza kujifunza Biblia kutokana na ushahidi wake wa vivi hivi. Nyakati fulani watu wanaofika kumi wangeshiriki katika kikundi chake cha funzo la Biblia. Sasa saba kati ya wale aliowatolea ushahidi akiwanyoa nywele wamesahihishwa fikira yao yenye makosa nao ni Mashahidi waliobatizwa wa Yehova!yy