Tegemea Imara ya Kupewa na Mungu
Mambo Makuu Kutokana na Timotheo wa Pili
YEHOVA huwapa watumishi wake nguvu za kuvumilia majaribu na mnyanyaso. Na lo, Timotheo na Wakristo wengine walihitaji kama nini imara ya kupewa na Mungu! Moto fulani uliteketeza Roma katika 64 W.K., na uvumi ulisema kwamba Maliki Nero ndiye aliyeusababisha. Ili kujilinda, aliwalaumu Wakristo, na yaonekana hii ilichochea wimbi la mnyanyaso. Yaelekea wakati huo (karibu 65 W.K.), mtume Paulo alitiwa tena gerezani katika Roma. Ingawa alikuwa akielekeana na kifo, ndipo alipoandika barua yake ya pili kwa Timotheo.
Barua ya Paulo ilimtayarisha Timotheo kukinza waasi-imani na kusimama imara kwa kuelekeana na mnyanyaso. Ilimtia moyo kuzidi kufanya maendeleo ya kiroho na ikaeleza juu ya hali za Paulo gerezani. Pia barua hii husaidia wasomaji kutegemea imara ya kupewa na Mungu.
Upatwe na Uovu na Ufundishe kwa Upole
Mungu hututia imara kuvumilia mnyanyaso tukiwa wapiga mbiu ya habari njema. (1:1-18) Paulo hakumsahau kamwe Timotheo katika sala zake, naye aliikumbuka imani yake isiyo na unafiki. Mungu alimpa Timotheo ‘si roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.’ Hivyo basi yeye asione aibu katika kutoa ushahidi na kupatwa na uovu kwa ajili ya habari njema. Pia alihimizwa ‘ashike kielelezo cha maneno yenye uzima [afya, NW]’ yaliyosikiwa kutoka kwa Paulo, hata kama vile sisi twapaswa kushikamana na ukweli halisi wa Kikristo kwa kuufuatia sana ingawa wengine wajigeuza kutoka kwa huo.
Mambo ambayo Paulo alifundisha yalipasa kukabidhiwa kwa wanaume waaminifu ambao wangefundisha wengine. (2:1-26) Timotheo alihimizwa awe askari mzuri wa Kristo, mwaminifu wakati wa kupatwa na uovu. Paulo mwenyewe aliteseka akiwa katika vifungo vya gerezani kwa kuhubiri habari njema. Alimtia moyo Timotheo afanye yote awezayo ili kujitokeza akiwa mfanya kazi wa Mungu mwenye kukubaliwa, akiepuka maneno matupu yachafuayo kilicho kitakatifu. Na aliambiwa kwamba mtumwa wa Bwana ni lazima afunze wengine kwa upole.
Lihubiri Neno!
Imara ya kupewa na Mungu ingehitajiwa ili kuelekeana na siku za mwisho na kuunga mkono ukweli wa Kimaandiko. (3:1-17) Kutoka kati ya wasiohofu Mungu kungetokea wanadamu “wakijifunza sikuzote, ila wasiweze kabisa kuufikia ujuzi wa kweli.” Hao ‘watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika.’ Hata hivyo, Timotheo alipaswa ‘kukaa katika mambo yale aliyofundishwa.’ Ndivyo na sisi, tukijua kwamba ‘kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.’
Timotheo alipaswa kukinza waasi-imani na kutimiza huduma yake. (4:1-22) Angeweza kufanya hivyo kwa ‘kulihubiri neno’ na kukaa nalo. Hilo lilikuwa jambo muhimu, kwa kuwa kundi lilielekea ‘wakati usiofaa’ kwa sababu watu fulani walikuwa wakifundisha fundisho bandia. Mashahidi wa Yehova pia wanashikamana na Neno la Mungu sasa, wakilihubiri kwa hima katika kundi na kwa watu nje, hata katika hali zisizopendeleka. Paulo ‘alilinda [alishika, NW] imani,’ ingawa aliachwa na watu fulani. Lakini ‘Bwana akamtia nguvu, ili kwa kazi yake ule ujumbe utangazwe kwa utimilifu.’ Sisi pia na tutegemee imara ya kupewa na Mungu na kuendelea kuzihubiri habari njema.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Askari Mzuri: Paulo alimhimiza Timotheo hivi: “Ushiriki taabu pamoja nami, kama askari mwema wa Kristo Yesu. Hakuna apigaye vita ajitiaye katika shughuli za dunia, ili ampendeze yeye aliyemwandika awe askari.” (2 Timotheo 2:3, 4) Askari Mroma wa miguu ‘alivumilia [aliteseka, NW] mabaya’ wakati wa kuchukua silaha nzito, shoka, kikapu, posho za siku tatu, na vitu vingine. (Wars of the Jews cha Josephus, Kitabu 3, sura ya 5) Hakufuatia mapendezi ya kibiashara, kwa maana hiyo haingependeza mkubwa wake, na gharama zake zililipiwa. Vivyo hivyo, Mkristo huteswa na majaribu yenye kuhusiana na kuwa “askari mwema wa Kristo.” Ingawa huenda akafanya kazi kimwili ili kutimiza wajibu fulani wa Kimaandiko, ni lazima asiache mhusiko usiofaa wa vitu vya kimwili umkomeshe kufanya vita vya kiroho. (1 Wathesalonike 2:9) Akitoa ushahidi kutoka nyumba kwa nyumba, yeye hutumia ‘upanga wa roho ambao ni neno la Mungu,’ na husaidia kuweka watu huru kutoka kosa la kidini. (Waefeso 6:11-17; Yohana 8:31, 32) Kwa kuwa maisha yamo hatarini, acha askari wote Wakristo waendelee kumpendeza Yesu Kristo na Yehova Mungu kwa njia hii.