Dini—Kwa Nini Ukosefu Wa Upendezi?
“BINADAMU asiye na dini ni kama nyumba isiyo na madirisha.” Ndivyo mwanamume mmoja Mjapani alivyoeleza uhitaji wa mwangazio wa maarifa ya kidini kwa mwana wake, Mitsuo. Hata hivyo, Mitsuo hakuchukua maneno ya baba yake kwa uzito. Na hesabu inayoongezeka ya watu katika Japani, kama kwingineko, wanaonekana kuwa na maoni ayo hayo. Wanaridhika kuwa ‘nyumba zisizo na madirisha’ kwa kutopendezwa sana kuacha nuru ya kidini iangaze ndani ya maisha zao.
Hivyo, Japani ilipofanya Uchunguzi wa Hali ya Watu Taifani, asilimia 69 ya raia zayo walidai kwamba hawakujifikiria kuwa watu wa kidini. Kati ya vijana, hesabu ilikuwa kubwa hata zaidi. Vivyo hivyo, katika ile nchi ya Thailand ambayo wakati mmoja ilikuwa ya Kibuddha kweli kweli, asilimia 75 ya wale wanaoishi katika maeneo ya mjini hawaendi tena kwenye mahekalu ya Kibuddha. Katika Uingereza karibu moja kati ya makanisa manane ya Kianglikana yamefungwa kwa miaka zaidi ya 30 kwa sababu ya kutotumiwa.
Ingawa hivyo, katika Japani mapambo ya kidini yangali yanaonekana sana. Lakini kama vile vyombo vya bei kubwa vya china, yanaletwa nje kwa nyakati chache tu—kama vile kwa arusi na maziko. Dini inathaminiwa zaidi kwa fungu layo katika kuhifadhi desturi za mahali na urithi wa kifamilia kuliko kwa mwangazio wa maarifa ya kiroho. Wengi wanaona dini kuwa dawa tu ya kuwatuliza wanyonge na wenye wasiwasi; hawaoni faida nyingine zozote zenye kutokana nayo. ‘Dini ni sawa ikiwa una wakati wa kuifuata au ukiona uhitaji wayo,’ wanasema watu fulani, ‘lakini ni lazima ujitumainie mwenyewe ili upate riziki na kulipia gharama za kufanya hivyo.’
Ni nini kinachoongoza ubaridi huu? Sababu fulani-fulani zingeweza kutolewa. Kwanza, kuna mazingira ya kijamii. Vijana wengi wamepokea mazoezi kidogo ya kidini au hawakupokea yoyote. Si ajabu kwamba wengi wa wale wanaoishi katika jamii inayoweka thamani kubwa juu ya kufuatia vitu vya kimwili wanakuwa watu wazima wanaofuatia vitu vya kimwili.
Katika nchi fulani-fulani mwenendo wenye sifa mbaya sana wa waevanjeli wa TV wenye pupa na ukosefu wa adili na viongozi wengine wa kidini walio na cheo kikubwa umegeuza watu kutoka kwenye dini, hali moja na kuhusika kwa dini katika mambo ya kisiasa na jitihada za vita. Hiyo inaonyeshwa na lililotukia kuhusu ile dini ya Kishinto katika Japani. “Huku vita [Vita ya Ulimwengu 2] ikiwa inamalizika kwa ushinde katika Agosti 1945, visehemu vitakatifu vya Kishinto vilipatwa na shida kubwa,” inasema Encyclopædia of the Japanese Religions. Ushinto, ambao ulipepea moto wa vita na kuahidi ushindi, ulikatisha watu tamaa. Falsafa ya kwamba hakuna Mungu wala Buddha ikaenea upesi.
Hata hivyo, je! kweli tunapaswa kuridhika na maoni ya ubinafsi, ya kuona hapa mbele tu—ya wakati wa sasa hivi tu? Wanadamu walio wengi wana akili ya kutaka kujua mambo. Wangependa kujua walitoka wapi, wanaenda wapi, kwa nini wanaishi, na jinsi ya kuishi. Wao husitawi sana wakiwa na tumaini. Kusukuma kando maswali juu ya maisha, au kuyakandamiza kwa wazo la kwamba “mambo haya hayajulikani,” hakuridhishi. Hata yule mtu asiyeamini kuna Mungu Bertrand Russell aliongea juu ya kuwa na “umivu mkali sana lisiloeleweka—utafutaji wa kitu fulani kilicho ng’ambo ya kile kilichomo katika ulimwengu.” Dini ya kweli ingeweza kumaliza utafutaji huo. Lakini jinsi gani? Kuna uthibitisho gani kwamba dini yoyote inastahili kuchukuliwa kwa uzito kadiri hiyo?