Kwa Nini Muda Mrefu Sana Kulijibu Suala
MIAKA 6,000 hivi iliyopita, enzi kuu ya Mungu haikuwa imeshindaniwa. Alipomaliza kazi zake za ajabu za uumbaji, “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.” (Mwanzo 1:31) Ndipo aliingia kipindi kirefu cha ‘kupumzika’; bila shaka, si kwamba alikuwa amechoka kimwili. Bali, alipumzika kwa kuacha kazi yake ya uumbaji duniani, akiwa na uhakika kwamba kusudi lake zuri kuhusu kazi hizo lingefanikiwa kikamili.—Mwanzo 2:1-3, NW; Isaya 55:11.
Hilo lilikuwa kusudi gani? Yehova aliweka wenzi wa kwanza wa kibinadamu katika mahali palipoitwa bustani la Edeni. Daraka lao la kwanza lilikuwa kutunza makao yao ya kiparadiso, kutia ndani wanyama wayo wa namna mbalimbali. Pia, wangezaa na kulea watoto. Halafu, familia yao ilipoongezeka, wangetakiwa wapanue Paradiso mpaka miisho ya dunia kwa kutii amri ya Mungu ‘kutiisha dunia.’ Hivyo, hatimaye dunia ingekuwa makao mazuri kabisa, iliyojazwa na familia yenye furaha na yenye umoja ikimtumikia Baba yao wa kimbingu. Hilo lilikuwa kusudi la Mungu la kwanza.—Mwanzo 1:27, 28; 2:8, 15, 20-22.
Je, Adamu na Hawa wangeshiriki kutimiza kusudi hilo tukufu hadi mwisho walo? Hilo lilitegemea kama wangeendelea kushirikiana nalo kwa kumtii Muumba wao. Kutii kwao hakungekuwa kwa kizembe, bila kufikiri. Wao walipewa hiari, kwa ajili Mungu aliwataka wamtumikie kwa moyo wenye kuthamini. Aliandaa jaribu rahisi, kuwa ukumbusho wenye kuonekana wa enzi yake kuu ya haki. Wangeweza kula maandalizi yoyote ya bustani isipokuwa moja. Kulikuwako mti wa matunda ambao Mungu alisema hivi kuuhusu: “Siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.”—Mwanzo 2:16, 17.
Maneno hayo hutuambia kwamba Adamu na Hawa hawakuumbwa wazeeke na kufa. Kifo kingekuja ikiwa tu walikosa kutii amri hiyo rahisi. Ikiwa Adamu na Hawa wangalibaki kuwa watiifu kwa Mungu, leo wangalikuwa bado hai duniani wakiwa wazazi wa familia ya wazao wakamilifu wa ulimwenguni pote.—Ona kanuni inayoelezwa katika Zaburi 37:29.
Hata hivyo, mmoja wa viumbe vya kimalaika wa Mungu, anayeitwa Shetani sasa, akawa mchambuzi wa njia ya Mungu ya kutawala. Yeye alimhimiza Hawa kula tunda lililokatazwa, akidokeza kwa udanganyifu kwamba kwa kutokutegemea enzi kuu ya Mungu, Hawa angekuwa na hali njema zaidi. Lakini, kusudi la kweli la Shetani lilikuwa tamaa ya kuwa mungu wa familia ya ainabinadamu ambayo ingekuwako.—Mwanzo 3:1-5; Mathayo 4:8, 9; Yohana 8:44.
Kwa kuwa Yehova alikuwa amewapa wenzi wa kwanza wa kibinadamu kila kitu walichohitaji, Hawa angalipaswa atetee enzi yake kuu na akatae dokezo la uwongo la Shetani. Lakini, kwa huzuni, yeye alisonga mbele kuvunja sheria ya Mungu. Baadaye, Adamu alichagua kuungana na mke wake katika mwenendo huo usio wa hekima. Hivyo wenzi hao wenye ushupavu, na Shetani pia, waliasi dhidi ya Mungu, na suala la enzi kuu ya kimungu likatokezwa.—Mwanzo 3:6.
Wakati Wahitajiwa Kujibu Masuala Muhimu
Yehova angaliweza kuharibu wale waasi watatu hapo hapo. Lakini hilo lisingalijibu maswali yaliyotokezwa na uasi wao. Je, binadamu angeweza kujitawala mwenyewe kwa kufanikiwa bila Mungu? Je, ilikuwa haki Mungu kudai utii kwa enzi yake kuu? Tena, kwa sababu ya mwenendo wa wenzi wa kwanza, je, wanadamu wowote wangechagua bila ubinafsi kumtumikia Mungu kwa hiari yao wenyewe—hata walipojaribiwa na Shetani? (Ayubu 1:7-11; 2:4) Ingechukua wakati kujibu maswali hayo. Ingechukua wakati, pia, kushinda matokeo ya uasi huo wa kwanza na kutimiza kusudi la Mungu kufanya dunia iwe paradiso iliyokaliwa na jamii ya binadamu isiyo na dhambi. Sisi bado tunangojea mchanganuo wa mwisho wa masuala hayo.
Kupatana na sheria yake, Mungu aliwaondolea Adamu na Hawa pendeleo la kuishi milele. Hawakustahili tena kushiriki katika timizo la kusudi lake kubwa. Hata hivyo, kabla ya wao kufa, walikubaliwa kuzaa na kulea wazao. Ni kweli, Adamu na Hawa hawangeweza tena kupitishia wazao wao uhai wenye nguvu usio na dhambi. (Warumi 5:12) Lakini ingawa vizazi waliofuata walizaliwa wasio wakamilifu na wenye hukumu ya kifo, watu wengi walikuwa na nafasi ya kuonyesha waliposimama kuhusiana na suala kubwa la enzi kuu.
Kuchanganua Suala
Mungu ataamuaje mambo haya kuhusu enzi yake kuu? Maswali yaliyotokezwa nyuma Edeni yamejibiwa katika maana moja. Maelfu ya miaka ya historia ya kibinadamu yamefunua wazi kwa uchungu kwamba hoja ya Shetani kwamba Hawa angekuwa na hali njema zaidi bila kumtegemea Mungu ilikuwa uwongo. Utawala wa binadamu ambao unampuuza Mungu umeendelea kushindwa. Ni kama vile Biblia inavyosema: “Mwanadamu ametawala mwanadamu kwa kumwumiza.”—Mhubiri 8:9, NW.
Kwa upande mwingine, mambo mengi mazuri yamekatibiwa wakati wa miaka mirefu tangu Adamu na Hawa walipotenda dhambi. Wengi wa aina ya binadamu wameonyesha ushikamano usioweza kuvunjwa kwa enzi kuu ya Yehova, mfano wenye kutokeza zaidi ukiwa ule wa “Mwana wa binadamu,” Yesu Kristo mwenyewe. (Mathayo 20:18, NW; Waebrania 11:1–12:3) Wale ambao wamefuata amri za Mungu na kukiri enzi yake kuu wameona kwamba hiyo kwa kweli ndiyo njia bora zaidi. Wamejionea ukweli wa mithali hii: “Baraka ya BWANA [Yehova, NW] hutajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo.” (Mithali 10:22) Tena, wao hatimaye watashiriki katika timizo la kusudi tukufu la Mungu, kwa sababu ya uandalizi wa ufufuo.—Yohana 5:28, 29.
Yehova hajasahau kusudi lake la kwanza. Wale wanaokataa enzi yake kuu hawatakubaliwa watawale duniani kwa wakati wote, na Biblia inaonya kwamba karibuni Mungu atatenda dhidi yao. Tunasoma hivi: “Ghadhabu ya Mungu imedhihirishwa kutoka mbinguni juu ya uasi wote.” (Warumi 1:18) Wonyesho huo unaokuja wa kasirani ya Mungu, ambao Biblia inauita Har–Magedoni, utaonyesha bila shaka lolote kwamba yeye kwa kweli yuko. Wale tu ambao hukubali enzi yake kuu ndio watakaookoka tokeo hilo. “Wanyofu watakaa katika nchi [dunia, NW], na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi [dunia, NW], nao wafanyao hila watang’olewa.”—Mithali 2:21, 22.
Lile Suala Kubwa na Wewe
Kwa sababu ya mambo hayo ya hakika, ni lazima kila mmoja wetu—kama Adamu na Hawa—afanye uchaguzi. Je, tutajaribu kuishi bila kumtegemea Mungu? Au, tutajitiisha chini ya enzi yake kuu? Kumbuka, hili ndilo suala kubwa zaidi ambalo linakukabili leo. Ingawa masuala mengine yaonekana kuwa yenye maana, yanahusu uhai wako wa sasa. Suala hili linahusu uhai wa milele. Uamuzi utakaofanya utaathiri wakati wako ujao wa milele.
Unaweza kuonyeshaje kwamba unakubali enzi kuu ya Mungu? Kwa kujifunza Neno lake, Biblia, kwa bidii, na kujitahidi kutii mapenzi yake katika kushiriki na Wakristo wengine wa kweli. (Sefania 2:2, 3) Ukifanya hivyo, utakuwa na tumaini lenye furaha la kuona timizo la kusudi tukufu la Mungu. Utapata kuona uhalisi wa ahadi hii ya ajabu: “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo . . . Bali wenye upole watairithi nchi [dunia, NW], watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:10, 11) Ni tokeo zuri kama nini kwa wote wajitiishao kwa enzi kuu ya Mungu! Ni sababu nzuri kama nini ya kuamua kwa hekima katika jambo hili lenye maana zaidi!