Uhalifu Katika Ulimwengu Wenye Machafuko
UHALIFU si tukio la ki-siku-hizi. Uuaji wa kwanza ulitokea maelfu ya miaka iliyopita wakati Kaini alipomwua ndugu yake Habili. Kulalwa kinguvu na usodoma [ulawiti] zinatajwa katika Maandiko ya Kiebrania ya kale. (Mwanzo 3:8; 19:4, 5; 34:1-4) Watu walikuwa wakiviziwa katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida, kama vile mfano wa Yesu wa Msamaria mwema unavyoonyesha. (Luka 10:29-37) Lakini kuna tofauti leo.
Maoni ya watu katika miji mikuu mingi ya ulimwengu, iwe ni New York, London, Calcutta, au Bogotá, ni kwamba uhalifu umeenea zaidi na unatisha zaidi. Ripoti kutoka India Today yenye kichwa kikuu “Madhehebu ya Machafuko” yataarifu hivi: “Hali yenye kusumbua inayotisha kuvunja mfumo wa kimaadili na kijamii ulio mwororo unaounganisha nchi pamoja ni kupandisha cheo uhalifu, uasi usio na nidhamu, na kutotii sheria kufikia kuwa madhehebu.” Katika pigano lao dhidi ya uhalifu, hata polisi nyakati nyingine wanashawishwa kupita mipaka ya kutekeleza sheria na wao wenyewe hutumia njia za uhalifu. Ripoti iliyotangulia kutoka India inataarifu hivi: “Vifo chini ya usimamizi wa polisi vinaendelea kutangazwa katika habari.” Na hiyo ni kweli katika nchi nyinginezo.
Uwezekano wa kuwa mwenye kupatwa na uhalifu unaonekana kuwa unaongezeka. Ripoti kutoka United States inasema kwamba “moja kati ya nyumba nne za Kiamerika iligusiwa na uhalifu wa jeuri au wizi katika 1988.” Tena, watu sasa wanatenda uhalifu wenye jeuri wakiwa wenye miaka michanga zaidi. Gazeti Visión la Amerika ya Latini linataarifu kwamba “tisa kati ya sicarios [wauaji wanaolipwa] kumi ni watoto. [Wao ni] ‘watoto’ katika maana ya hali ya kuzaliwa na wako chini ya ulinzi wa kisheria.” Tena, utendaji wa uhalifu wenye jeuri na watoto ni mwelekeo wa ulimwenguni pote.
Biblia ilitoa unabii hivi karibu miaka 2,000 iliyopita: “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari [zilizo ngumu kushughulika nazo, NW]. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, . . . wasio safi, wasiowapenda wa kwao, . . . wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna . . . Watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika.”—2 Timotheo 3:1-4, 13.
Tangu 1914 kuna ushuhuda mwingi kwamba tunaishi katika hizo siku za mwisho zenye hatari. Ulimwengu, ukiwa umeteseka na vita vya ulimwengu viwili na mapigano mengineyo makuu, katika njia nyingi umekuwa usioweza kutawalika na wenye machafuko. Uhalifu umeenea. Katika maeneo mengi ya miji, wahalifu wametwaa utawala, wakibadilisha mitindo-maisha ya wengi wenye kutii sheria. Ni kama vile seneta mashuhuri wa U.S. alivyotaarifu: “Kuna mambo mengi sana ya kuhangaikia sasa, mambo ambayo hatukuwa tukihofia kamwe. Nyakati nyingine tunaogopa sana hivi kwamba tunakuwa wafungwa, huku wale ambao wanapaswa kufungwa wakienda huru.”
Kama tokeo, watu leo wanajihadhari kwa njia ambayo haikuhitajiwa miaka 20 au 30 iliyopita. Milango inakuwa na makufuli mawili au matatu na inaimarishwa kwa chuma cha pua. Watu katika mahali pengi huchukua pesa za kutosha ili kuridhisha mnyang’anyi kwa kutarajia wataepuka kupigwa kwa kukosa kuwa na chochote cha kuwapa wezi. Baada ya jua kushuka barabara nyingi zinaachwa karibu tupu, zikiendewa mara kwa mara na wajinga wa mambo, wenye ujasiri wa kipumbavu, na wale ambao wamelazimishwa na hali kuwa huko—shabaha rahisi kwa wenye kunyang’anya ambao huzunguka-zunguka pori la mji.
Tunaweza kufanya nini ili tuepuke kuwa wenye kudhulumiwa isivyo haki kwa uhalifu katika ulimwengu huu wenye machafuko na vuruguvurugu? Tunaweza kukabilianaje?