Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 5/1 kur. 15-20
  • Semeni Lugha Iliyo Safi Mkaishi Milele!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Semeni Lugha Iliyo Safi Mkaishi Milele!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jinsi ya Kujifunza Lugha Iliyo Safi
  • Machujo ya Uchafu
  • Lugha Iliyo Safi Yasikika
  • Uitumie au Uipoteze
  • Tunabaki Tumeunganishwa
  • Lugha Safi Kwa Ajili Ya Mataifa Yote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Je, Unazungumza Ile “Lugha Safi” kwa Ufasaha?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Unganishweni Na Lugha Iliyo Safi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Namna Lugha Moja Itakavyoleta Umoja kwa Wanadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 5/1 kur. 15-20

Semeni Lugha Iliyo Safi Mkaishi Milele!

“Mtafuteni BWANA [Yehova, NW], . . . itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA [Yehova, NW].”—SEFANIA 2:3.

1. (a) Wanafunzi hutumia njia gani kujifunza lugha ya kigeni? (b) Kwa nini tuseme lugha iliyo safi?

HUENDA wanafunzi wakajifunza lugha mpya kwa kufuata sarufi au kwa kuiga jinsi isemwavyo. Chini ya ile njia ya kufuata sarufi, kwa kawaida wao hutumia vitabu vya mafunzo na hujifunza kanuni za sarufi. Katika ile njia ya kuiga jinsi lugha isemwavyo, wanaiga sauti na violezo vya maneno vinavyosemwa na mwalimu wao. Njia zote mbili hutumika katika kujifunza “lugha iliyo safi.” Na ni muhimu kwamba tuseme lugha hiyo ikiwa tunatumaini ‘kufichwa katika siku ya hasira ya Yehova.’—Sefania 2:1-3; 3:8, 9.

2. Tunaweza kujifunzaje zile zinazoweza kuitwa kanuni za kisarufi za lugha iliyo safi?

2 Kitabu kikuu cha mafunzo kinachotumiwa katika kujifunza lugha iliyo safi ni Biblia. Funzo layo lenye bidii nyendelevu na la vichapo vyenye msingi wa Biblia lakufundisha kile kinachoweza kuitwa kanuni za sarufi za lugha iliyo safi. Funzo la Biblia nyumbani likiongozwa na mmoja wa Mashahidi wa Yehova ni mwanzo mzuri. Kwa wale walio wakfu tayari kwa Mungu, funzo la kawaida lenye bidii nyendelevu la Maandiko ni la lazima. Lakini je, kuna njia hasa zenye matokeo mazuri za kujifunzia lugha iliyo safi? Na kuna manufaa gani kwa kuisema?

Jinsi ya Kujifunza Lugha Iliyo Safi

3. Njia moja ya kujifunza lugha iliyo safi ni ipi?

3 Njia moja ya kujifunza lugha iliyo safi ni kwa kushirikisha kweli unazojifunza na mambo unayojua tayari, kama vile mwanafunzi wa lugha kwa kuendelea aweza kuhusianisha kanuni za kisarufi. Kwa mfano, wakati mmoja huenda ikawa ulijua kwamba Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu, lakini hukujua mengi kuhusu kazi zake. Tangu hapo, huenda funzo la Biblia likawa lilikufunza kwamba Kristo anatawala sasa akiwa Mfalme wa kimbingu na kwamba katika Utawala wake wa Miaka Elfu, ainabinadamu watiifu watainuliwa kwenye ukamilifu. (Ufunuo 20:5, 6) Ndiyo, ufahamu wako wa lugha iliyo safi huendelezwa unaposhirikisha mambo mapya na yale unayojua tayari.

4. (a) Njia nyingine ya kujifunza ‘kanuni za kisarufi’ za lugha iliyo safi ni ipi, na ni simulizi lipi la Biblia linatumiwa kueleza jambo hilo? (b) Ni nini kilichotokea Gideoni na wanaume wake mia tatu walipoanza kutenda? (c) Simulizi juu ya Gideoni linafundisha somo gani?

4 Njia nyingine ya kujifunza ‘kanuni za kisarufi’ za lugha iliyo safi ni kuona akilini mwako matukio yaliyoandikwa katika Biblia. Ili kutoa kielezi: Jaribu ‘kuona na kusikia’ simulizi lililorekodiwa katika Waamuzi 7:15-23. Tazama! Mwamuzi Mwisraeli Gideoni amegawanya jeshi lake kuwa vikosi vitatu vya mia kila kimoja. Kwa kimya, chini ya kisitiri cha giza, washuka Mlima Gilboa na kuzunguka kambi ya Wamidiani wanaolala usingizi. Je! hawa 300 wana silaha za kutosha? Kijeshi, la. Kwani, wangetokeza kicheko cha dhihaka kwa wanajeshi wenye kiburi! Kila mmoja wao ana pembe tu, mtungi mkubwa mmoja wa maji, na mwanga ndani ya mtungi huo. Lakini sikiliza! Kwa ishara waliyopewa, wale wanaume mia moja walio pamoja na Gideoni wapuliza pembe zao na kuvunja mitungi yao ya maji. Ndivyo na wale wengine 200. Wote wainuapo juu mianga yenye kuwaka, unawasikia wakipaaza sauti: “Upanga wa BWANA [Yehova, NW] na wa Gideoni”! Jinsi hilo linahofisha Wamidiani! Watoka katika mahema yao, huku macho yao yaliyojaa usingizi yakiwa yamekodolewa kwa kuogopeshwa na miwako yenye kuruka ambayo yakuza maumbo yenye kivuli na kuwasha hofu za kishirikina. Wamidiani waanzapo kukimbia, wanaume wa Gideoni wanaendelea kupuliza pembe zao, naye Yehova afanya panga za mahasimu hao ziwe dhidi ya mmoja na mwenzake. Ni somo lenye nguvu kama nini katika lugha iliyo safi! Mungu aweza kukomboa watumishi wake bila jeshi la kibinadamu. Zaidi ya hilo, “BWANA [Yehova, NW], hataacha watu wake kwa ajili ya jina lake kuu.”—1 Samweli 12:22.

5. Mikutano ya Kikristo inaweza kusafishaje usemi wetu?

5 Wanafunzi wanapofunzwa lugha mpya kwa ile njia ya kuiga jinsi lugha isemwavyo, wao hujaribu kurudia sauti na violezo vya maneno ya mwalimu kwa usahihi. Kuna fursa nzuri kama nini za kusema lugha iliyo safi kwenye mikutano ya Kikristo! Humo twasikia wengine wakijieleza wenyewe katika lugha hiyo ya ukweli wa Kimaandiko, na huenda tukawa na pendeleo la kutoa maelezo sisi wenyewe. Je! sisi huhofu kwamba huenda tukasema jambo lisilo sahihi? Acheni hilo lisiwe jambo letu kuu la kuhangaikia, kwa kuwa kosa linalosahihishwa kwa fadhili na mzee anayesimamia mkutano kama vile Funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma, laweza kusafisha usemi wetu. Kwa hiyo, hudhuria na ushiriki katika mikutano ya Kikristo kwa ukawaida.—Waebrania 10:24, 25.

Machujo ya Uchafu

6. Kwa sababu gani kuna tofauti kubwa sana kati ya Mashahidi wa Yehova na matengenezo ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo?

6 Wale wanaojulisha wazi kusudi la Yehova na kutangaza Ufalme wake wa kimbingu wanasema lugha iliyo safi wakiwa Mashahidi wake. Wanajulisha jina lake na kumtumikia “kwa nia moja,” au kwa ukubali mmoja. (Sefania 3:9) Ingawa dini za Jumuiya ya Wakristo zina Biblia, hazisemi lugha iliyo safi wala kuita juu ya jina la Mungu kwa imani. (Yoeli 2:32) Hawana ujumbe wenye upatani unaotegemea Maandiko. Kwa nini? Kwa sababu wao huweka mapokeo ya kidini, falsafa za kilimwengu, na ushikamanifu wa kisiasa juu ya Neno la Mungu. Makusudi, matumaini, na njia zao zote ni za ulimwengu mbovu huu.

7. Kwenye 1 Yohana 4:4-6 ni tofauti zipi zinazoonyeshwa kati ya Mashahidi wa Yehova na dini bandia?

7 Jumuiya ya Wakristo—kwa hakika, milki nzima ya ulimwengu ya dini bandia—haisemi lugha kama ile Mashahidi wa Yehova husema. Kwa kupendeza, mtume Yohana aliwaandikia wale wanaisema lugha iliyo safi hivi: “Mwatokana na Mungu; nanyi mmewashinda, kwa sababu yeye aliye ndani yenu [aliye katika muungano pamoja na nyinyi, NW] ni mkuu kuliko yeye aliye katika [muungano pamoja na, NW] dunia. Hao ni wa dunia; kwa hiyo wanena ya dunia na dunia huwasikia. Sisi twatokana na Mungu. Yeye amjuaye Mungu atusikia; yeye asiyetokana na Mungu hatusikii.” (1 Yohana 4:4-6) Watumishi wa Yehova wamewashinda walimu bandia kwa sababu Mungu, aliye mmoja na watu wake, “ni mkuu kuliko yeye [Ibilisi, aliye katika muungano pamoja na, NW] dunia,” jamii ya kibinadamu isiyo adilifu. Kwa kuwa waasi-imani “ni wa dunia” na wana roho yayo mbovu, “wanena ya dunia na dunia huwasikia.” Lakini watu walio kama kondoo husikiliza wale ambao hutokana na Mungu, waking’amua kwamba watu wa Yehova husema lugha iliyo safi ya ukweli wa Biblia unaoandaliwa kupitia tengenezo lake.

8. Mtu wa kuasi ni nani?

8 Uasi-imani mkubwa ulitabiriwa, na ‘siri ya uasi’ ilikuwa tayari ikifanya kazi katika karne ya kwanza ya W.K. Wakati ulipopita, wanaume waliokubali—au kunyakua—madaraka ya kufundisha katika kundi walifunza mafundisho mengi bandia. Lugha yao haikuwa safi hata kidogo. Kwa sababu hiyo, alizuka “mtu wa kuasi” mwenye kujumlisha wengi, wale makasisi wa Jumuiya ya Wakristo, waliojifunganisha na mapokeo bandia ya kidini, falsafa ya kilimwengu, na mafundisho yasiyo ya kimaandiko.—2 Wathesalonike 2:3, 7.

Lugha Iliyo Safi Yasikika

Ulimwenguni Pote

9. Ni matukio gani ya kidini yaliyokuwako muda wa karne ya 19?

9 Ni kikundi kidogo tu cha watu wenye kuhofu Mungu ‘kilichoshindania imani waliyokabidhiwa watakatifu.’ (Yuda 3) Waamini kama hao wangepatikana wapi? Kwa karne nyingi, dini bandia iliweka watu wengi katika giza la kiroho, lakini Mungu alijua wale wachache waliokuwa na kibali chake. (2 Timotheo 2:19) Halafu, katikati ya mabadiliko ya kibiashara, kiviwanda, na kijamii ya karne ya 19, kulizuka sauti zilizojitokeza kutoka kwa machafuko yenye mvurugo wa kidini. Vikundi vidogo vilijaribu kusoma ishara za nyakati na kutabiri kuja kwa pili kwa Yesu Kristo, lakini si wote waliokuwa wakisema lugha iliyo safi.

10. Ni kikundi gani cha “kuja kwa pili” kilichochaguliwa na Mungu kusema lugha iliyo safi, na kwa nini ni dhahiri kwamba mkono wa Yehova umekuwa nao?

10 Hata hivyo, katika 1879, ilipata kuwa wazi ni sauti gani ya “kuja kwa pili” ilikuwa ikichaguliwa na Yehova iseme lugha iliyo safi ikiwa Mashahidi wake. Kufikia wakati huo, kikundi kidogo cha funzo la Biblia kikiongozwa na Charles Taze Russell kilikuwa kikikutania Pittsburgh, Pennsylvania, U.S.A. Walikuwa wamekuwa na uhakika kwamba kuja kwa pili kwa Yesu kungeanza kuwapo kwake kusikoonekana, kwamba wakati wa taabu ya ulimwengu ulikuwa mbele, na kwamba ungefuatwa na Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo ambao ungetokeza kurudishwa kwa Paradiso duniani, pamoja na uhai wa milele kwa wanadamu watiifu. Katika Julai 1879 hao Wanafunzi wa Biblia walianza kuchapisha lile gazeti linalojulikana sasa kuwa Mnara wa Mlinzi. Nakala 6,000 tu za toleo lalo la kwanza ndizo zilizogawanywa. Lakini “mkono wa Yehova” ulikuwa pamoja na Mashahidi hao, kwa maana jarida hili linachapishwa sasa kwa lugha 111 likiwa na wastani wa kuchapa wa zaidi ya nakala 15,000,000 kwa kila toleo.—Linganisha Matendo 11:19-21, NW.

11, 12. Ni zipi baadhi ya kweli za Kimaandiko ambazo wale wanaosema lugha iliyo safi huelewa?

11 Kupitia Biblia na vichapo vya Mashahidi wa Yehova, na hasa kwa upigaji mbiu wa hawa Wakristo wenye bidii wa habari njema, lugha iliyo safi imekuja kujulikana duniani pote. Na ni manufaa kubwa kama nini zinazoonewa shangwe na wale wanaoisema! Badala ya kusema kwamba ‘Mungu ni Mungu, Kristo ni Mungu, na Roho Mtakatifu ni Mungu’ katika ile lugha ya kifumbo isiyoeleweka ya Utatu, wanakubaliana na msimamo wa Biblia kwamba Yehova ndiye Mungu Aliye Juu Zaidi, Yesu Kristo aliye mdogo zaidi ni Mwana Wake, na roho takatifu ni kani ya utendaji ya Mungu yenye kustaajabisha. (Mwanzo 1:2; Zaburi 83:18; Mathayo 3:16, 17) Wasemaji wa lugha iliyo safi wajua kwamba mwanadamu hakugeuka-geuka kutoka namna ya chini zaidi ya uhai bali aliumbwa na Mungu mwenye upendo. (Mwanzo 1:27; 2:7) Wanang’amua kwamba nafsi hukoma kuwako wakati wa kufa—uhakika ambao huondolea mbali kuhofu wafu. (Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4) Helo hueleweka kuwa kaburi la kawaida la ainabinadamu, si mahali penye moto wa mateso palipobuniwa na mungu mkatili. (Ayubu 14:13) Wanajua pia kwamba ufufuo ndio tumaini la wafu lililotolewa na Mungu.—Yohana 5:28, 29; 11:25; Matendo 24:15.

12 Wale wanaosema lugha iliyo safi huonyesha staha kwa damu na uhai. (Mwanzo 9:3, 4; Matendo 15:28, 29) Wanang’amua kwamba uhai wa kidunia wa Kristo ndio ukombozi uliolipwa kwa ajili ya wanadamu watiifu. (Mathayo 20:28; 1 Yohana 2:1, 2) Hawasali kamwe kwa “watakatifu,” wakijua kwamba ni lazima sala zao zielekezwe kwa Yehova Mungu kupitia Yesu Kristo. (Yohana 14:6, 13, 14) Kwa kuwa Neno la Mungu linalaumu ibada-sanamu, sanamu hazitumiwi katika ibada yao. (Kutoka 20:4-6; 1 Wakorintho 10:14) Nao huepuka hatari za uhusiano na roho waovu kwa sababu wanakataa uwasiliani-roho, ambao pia umelaumiwa katika Biblia.—Kumbukumbu 18:10-12; Wagalatia 5:19-21.

13. Kwa nini wale ambao husema lugha iliyo safi hawatataniki?

13 Watumishi wa Yehova, ambao husema lugha iliyo safi, hawatataniki wasijue wako wapi katika mkondo wa wakati. Yehova amewafundisha kwamba wako katika “wakati wa mwisho,” Yesu Kristo akiwepo akiwa roho mtukufu asiyeonekana. (Danieli 12:4; Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5; 1 Petro 3:18) Akifuatwa na majeshi ya kimbingu yenye uweza, Kristo yuko karibu kupanda aingie katika pigano kutekeleza hukumu ya Mungu dhidi ya mfumo huu wa mambo. (Danieli 2:44; Ufunuo 16:14, 16; 18:1-8; 19:11-21) Ndiyo, na wale wanaosema lugha iliyo safi wana shughuli sana wakijulisha wazi zile habari njema kwamba karibuni Ufalme wa Mungu chini ya Yesu Kristo utaleta mibaraka mitukufu kwa ainabinadmu wote watiifu katika dunia-paradiso. (Isaya 9:6, 7; Danieli 7:13, 14; Mathayo 6:9, 10; 24:14; Luka 23:43) Yote hayo, na bado tumegusia-gusia kijuujuu tu! Kwa hakika, lugha iliyo safi ndiyo lugha yenye utajiri zaidi, yenye thamani zaidi duniani!

14. Ni manufaa gani nyingine zinazoonewa shangwe na wale wanaosema lugha iliyo safi?

14 Manufaa yanayoonewa shangwe na wale wanaosema lugha iliyo safi, yanatia ndani “amani ya Mungu” inayolinda mioyo na nguvu za kufikiri. (Wafilipi 4:6, 7) Wanatii she-ria za Biblia, ambazo huendeleza afya, furaha, na uradhi ambao hutokana na kumpendeza Yehova. (1 Wakorintho 6:9, 10) Ndiyo, na wasemaji wa lugha iliyo safi wana tumaini la kupata uhai wa milele katika ulimwengu mpya alioahidi Mungu.—2 Petro 3:13.

Uitumie au Uipoteze

15. Wewe utanufaikaje kutokana na ufahamu mzuri wa lugha iliyo safi?

15 Ikiwa utasema lugha iliyo safi katika ulimwengu mpya, ni lazima uijue vizuri sana hivi kwamba inakuwa ndiyo lugha ambayo katika hiyo wewe wafikiri. Wakati mtu anapokuwa akijifunza lugha, kwanza anafikiri katika lugha yake ya kienyeji na kufasiri mawazo yake katika ile mpya. Lakini apatapo kuwa stadi zaidi katika ile lugha mpya, anaanza kufikiri katika hiyo bila kuhitaji kuitafsiri. Vivyo hivyo, kupitia funzo la bidii nyendelevu, waweza kupata ufahamu mzuri wa lugha iliyo safi hivi kwamba utajua jinsi ya kutumia sheria na kanuni za Biblia ili kutatua matatizo na kubaki katika “kile kijia cha uhai.”—Zaburi 16:11, NW.

16. Ni jambo gani ambalo laweza kutokea ikiwa wewe husemi lugha iliyo safi kwa kawaida?

16 Ni lazima uitumie lugha iliyo safi kwa ukawaida, au sivyo utapoteza uwezo wa kuisema kwa ustadi. Kwa kielelezo: Miaka kadhaa iliyopita, baadhi yetu tulijifunza lugha ya kigeni. Huenda tukakumbuka maneno machache katika lugha hiyo lakini yaelekea kwamba tumepoteza ustadi wetu wa kuisema kwa kuwa hatuitumii daima. Jambo ilo hilo laweza kutukia kwa lugha iliyo safi. Tusipoitumia kwa ukawaida, twaweza kupoteza ustadi wetu wa kuisema, na hiyo ingeleta matokeo yenye kuhuzunisha kiroho. Kwa hiyo acheni tuiseme kwa ukawaida kwenye mikutano na katika huduma ya Kikristo. Utendaji huo, pamoja na funzo la kibinafsi, utatuwezesha kusema mambo kwa usahihi katika lugha iliyo safi. Na hilo ni jambo la maana kama nini!

17. Ni nini kinachotoa kielezi kwamba usemi waweza kuwa wenye kuokoa uhai au wenye kuleta kifo?

17 Usemi waweza kuwa wenye kuokoa uhai au kuleta kifo. Hiyo ilionyeshwa wakati wa pigano kati ya kabila la Waisraeli la Waefraimu na Mwamuzi Yeftha wa Gileadi. Ili kuwatambulisha Waefraimu waliokuwa wakijaribu kutorokea ng’ambo ya Mto Yordani, Wagileadi walitumia neno la siri “Shibolethi,” ambalo lilikuwa na sauti “sh” ya kuanzia. Wanaume wa Efraimu walijisaliti wazi kwa askari wa Gileadi kando ya Yordani kwa kusema “Sibolethi” badala ya “Shibolethi,” wakiwa wanatamka vibaya sauti ya kuanzia ya neno hilo. Kama tokeo, Waefraimu 42,000 waliuawa! (Waamuzi 12:5, 6) Vivyo hivyo, yale yanayofundishwa na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo huenda yakasikika kuwa karibu na lugha iliyo safi kwa wale ambao hawafahamu vizuri ukweli wa Biblia. Lakini kusema katika njia bandia ya kidini kutathibitika kuwa na msiba wa kifo katika siku ya hasira ya Yehova.

Tunabaki Tumeunganishwa

18, 19. Maana ya Sefania 3:1-5 ni nini?

18 Kwa kurejezea Yerusalemu wa kale usio mwaminifu na kifani chake cha ki-siku-hizi, Jumuiya ya Wakristo, inasemwa kwenye Sefania 3:1-5 hivi: “Ole wake yeye aliyeasi na kutiwa unajisi, mji wa udhalimu! Hakuitii sauti; hakukubali kurudiwa [nidhamu, NW]; hakumwamini BWANA [Yehova, NW]; hakumkaribia Mungu wake. Wakuu wake walio ndani yake ni simba wangurumao; makadhi wake ni mbwa-mwitu wa jioni; hawasazi kitu cho chote hata siku ya pili. Manabii wake ni watu hafifu, wadanganyifu; makuhani wake wamepatia unajisi patakatifu, wameifanyia sheria udhalimu. BWANA [Yehova, NW] kati yake ni mwenye haki; hatatenda uovu; kila asubuhi hudhihirisha hukumu yake, wala hakomi; bali mtu asiye haki hajui kuona haya.” Ni nini maana ya maneno hayo?

19 Yerusalemu ya kale na pia Jumuiya ya Wakristo ya ki-siku-hizi waliasi dhidi ya Yehova na kujichafuza kwa ibada bandia. Utendaji kosa wa viongozi wao ulitokeza udhalimu. Yajapokuwa maonyo ya Mungu yaliyorudiwa-rudiwa, hawakusikiliza wamkaribie. Wakuu wao wamekuwa kama simba wenye pupa, wakipuuza uadilifu kwa kiburi. Mahakimu wao wamchana-chana haki kama mbwa-mwitu wenye njaa kuu. Makuhani wao ‘wamenajisi kilicho kitakatifu na kufanya jeuri kwa sheria’ ya Mungu. Kwa hiyo, Yehova yuko karibu ‘kukusanya mataifa na kuzikutanisha falme, ili kuzimwagia ghadhabu yake, ukali wote wa hasira yake.’—Sefania 3:8.

20. (a) Ni nini lazima kifanywe ili kuokoka siku ya hasira ya Yehova? (b) Unaweza kupataje tumaini la kuonea shangwe mibaraka ya milele kutoka kwa Mungu?

20 Siku ya hasira ya Yehova inakaribia kwa haraka. Kwa hiyo, ili kuokoka na kuingia ndani ya ulimwengu mpya wa Mungu, jifunze na uiseme lugha iliyo safi bila kukawia. Ni kwa kufanya hivyo tu ndio utapata ulinzi kutokana na msiba wa kiroho sasa na kutokana na afa la tufe lote linalokaribia kwa kasi. Mashahidi wa Yehova wanatangaza rasmi siku ya hasira ya Mungu na ujumbe wenye kutia moyo wa Ufalme wake. Wao hupendezwa kama nini kuongea juu ya umaliki wake wenye utukufu! (Zaburi 145:10-13) Unganishwa nao, nawe waweza kutumaini kuonea shangwe uhai wa milele na mibaraka mingineyo kutoka kwa Mwanzishi wa lugha iliyo safi, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.

Wewe Ungejibuje?

◻ Ni zipi njia mbalimbali za kujifunza lugha iliyo safi?

◻ Kwa nini inanufaisha kusema lugha iliyo safi?

◻ Ni jambo gani linaloweza kutokea ikiwa hutumii lugha iliyo safi kwa ukawaida?

◻ Mtu aweza kuokokaje siku ya hasira ya Yehova na kuonea shangwe mibaraka ya milele?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Gideoni na wanaume wake wapuliza pembe zao na kuinua mianga yao

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kuanzia 1879 na kuendelea ilifanywa iwe wazi kwamba Charles Taze Russell na washirika wake walikuwa wakitumiwa na Mungu kueneza lugha iliyo safi

[Picha katika ukurasa wa 20]

Je! wewe umeunganishwa pamoja na Mashahidi wa Yehova katika kusema lugha iliyo safi?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki