Maisha na Huduma ya Yesu
MAKALA “Yesu Amaliza Yote Ambayo Mungu Amwomba Afanye,” kwenye kurasa zifuatazo ndiyo sehemu ya mwisho ya mfululizo wetu ulioendelea kwa muda mrefu wa “Maisha na Huduma ya Yesu.” Habari hii ya kuvutia imetokea katika Mnara wa Mlinzi kwa zaidi ya miaka sita, katika matoleo ya kufuatana 149, kuanzia na toleo la Agosti 1, 1985.
Ni tumaini letu kwamba mfululizo huu katika Mnara wa Mlinzi umekusaidia kufuata onyo la upole la mtume Paulo ‘kumtazama Yesu’ na kutii amri ya Mungu ‘kumsikia yeye.’ (Waebrania 12:2, 3; Mathayo 17:5) Miaka iliyopita, wengi wameandika kusema kwamba wamesaidiwa kufanya hivyo. “Ni kama tu nilikuwa huko nikimsikiza na kutazama anayoyafanya,” akaandika msomaji mmoja.
“Nimekuja kumpenda zaidi kwa sababu ya makala hizo.” Msomaji mwingine aliandika hivi: “Kila toleo laonekana kuwa na jambo ambalo nilikuwa nimekosa nilipokuwa nikisoma usimulizi wa Biblia. Nimeonea shangwe kufahamu matukio tofauti-tofauti katika maisha ya Yesu katika utaratibu mzuri zaidi wa jinsi yalivyofuatana kwa kusoma kila makala.” Wengi wameonyesha uthamini kama huo kwa kujifunza ni wakati gani na mahali gani Yesu alifunza na kufanya mambo wakati wa huduma yake.
Mwanamke mmoja katika Hispania alisema hivi: “Nimeweka makala zote tangu mwanzo. Ni zenye kufunza sana kwa watu wazima na kwa watoto pia. Nina miaka 44, nami nasisimuka ninaposoma masimulizi hayo. Ni kama tu nilikuwapo katika kila tukio la kihistoria.”
Mama mmoja katika United States aliandika hivi: “Kwa sababu ya ufupi wa makala hizo na urahisi wazo wa kueleza, mume wangu amejiunga nasi katika funzo letu la familia. Mwana wangu wa umri wa miaka minane aliniomba niandike kuwashukuru kwamba baba yake sasa ajifunza Biblia. Aomba kwamba siku moja makala hizo zichapishwe katika kitabu ili aweze kuzishiriki pamoja na wanashule wenzake.”
Labda washiriki maoni ya msomaji ambaye karibuni aliomboleza hivi: “Nahisi kuhuzunika kidogo nifikiriapo kwamba mfululizo huu utaisha karibuni wakati siku za mwisho za maisha ya Kristo zinaposimuliwa. Kwa kweli nitakosa sehemu yazo sana katika Mnara wa Mlinzi.” Twatumaini kwamba wewe utaonea shangwe sehemu hii ya mwisho ya mfululizo wetu “Maisha na Huduma ya Yesu.”