Mfululizo Utakaotusaidia Katika Huduma Yetu
1. Mfululizo “Mazungumzo Pamoja na Jirani” unatimiza malengo gani mawili?
1 Mara kwa mara, gazeti la Mnara wa Mlinzi toleo la watu wote lina mfululizo wenye kichwa “Mazungumzo Pamoja na Jirani.” Mfululizo huo una malengo mawili, yaani kufafanua mafundisho ya Biblia kwa njia yenye kuvutia na kuonyesha jinsi tunavyoweza kujadiliana mambo kadha wa kadha kwa njia ya busara. (1 Pet. 3:15) Tunawezaje kutumia mfululizo huo vizuri?
2. Tunawezaje kutumia mfululizo “Mazungumzo Pamoja na Jirani” katika huduma yetu?
2 Utumie Katika Huduma: Unaweza kuhifadhi nakala za ziada za Mnara wa Mlinzi zenye mojawapo ya makala katika mfululizo huo. Ikiwa mwenye nyumba, mtu anayependezwa, au mwanafunzi wa Biblia anauliza swali au anazusha jambo ambalo limezungumziwa katika mojawapo ya makala hizo, mpe gazeti lenye makala hiyo na ujitolee kuizungumzia. Ikiwa huna gazeti linalozungumzia jambo hilo, unaweza kulipakua kwenye Tovuti yetu ya jw.org.
3. Tunaweza kutumia njia gani kuzungumzia mojawapo ya makala pamoja na mwenye nyumba?
3 Huenda ukatumia njia gani kuzungumzia mojawapo ya makala hizo na mwenye nyumba? Wengine wamemwalika mtu huyo asome kwa sauti maneno ya jirani, huku wao wakisoma maneno ya Shahidi. Mazungumzo hayo yaliyochapishwa yanaweza kuwa na matokeo mazuri kwa sababu yanampa mwenye nyumba nafasi ya kuchunguza mambo tunayoamini kwa njia ambayo haitazua mabishano.—Kum. 32:2.
4. Tunawezaje kutumia mfululizo huo kujizoeza?
4 Jizoeze na Uwazoeze Wengine: Unaposoma makala hizo, zingatia maandiko, mifano, na njia ya kujadiliana. Tambua jinsi makala ilivyowasilishwa. Halafu jaribu kutumia njia kama hiyo katika huduma. (Met. 1:5; 9:9) Dada mmoja alisema hivi: “Kusoma makala hizi ni kama kujifunza kutoka kwa painia ‘mkamilifu’ ambaye anajua jambo sahihi la kusema kila wakati!”
5. Tunawezaje kuwasaidia wanafunzi wetu wa Biblia wajitayarishe kwa ajili ya huduma?
5 Pia, unaweza kutumia mfululizo huo kuwasaidia wanafunzi wako wa Biblia wajitayarishe kwa ajili ya huduma. Someni habari hiyo pamoja, na umpe nafasi mwanafunzi wako asome sehemu ya Shahidi. Wanafunzi wa Biblia wakifuata njia hiyo, watajizoeza kueleza imani yao kwa busara. (Kol. 4:6) Kwa kweli, makala hizo ni mojawapo ya njia nyingi ambazo Yehova hutusaidia ‘tutimize kwa ukamili’ huduma yetu.—2 Tim. 4:5.