Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ “Lile jema” ambalo mtume Paulo hakuweza kufanya kama alivyotaja kwenye Warumi 7:19, lilikuwa nini?
Kwa msingi, Paulo alikuwa akirejezea hali yake ya kutoweza kufanya mambo yote mema yaliyopangiliwa katika Sheria ya Musa. Hilo lilikuwa jambo lisilowezekana kwa Paulo na wengine wote, kutia na sisi, kwa sababu ya kutokamilika na udhambi. Lakini si lazima tukatishwe tamaa. Dhabihu ya Kristo ilifungua njia kwa ajili ya msamaha kutoka kwa Mungu na msimamo mzuri pamoja Naye.
Warumi 7:19 husomwa hivi: “Kwa maana lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo.” Muktadha unaonyesha kwamba Paulo alikuwa akisema hasa juu ya “lile jema” kulingana na yale yaliyotajwa waziwazi katika Sheria. Katika mstari wa 7 alikuwa amesema hivi: “Tusemeje, basi? Torati ni dhambi? Hasha! Walakini singalitambua dhambi ila kwa sheria; kwa kuwa singalijua kutamani, kama torati isingalisema, Usitamani.” Naam, Sheria ilionyesha wazi kwamba kwa kuwa wanadamu hawakuweza kuifuata kikamili, wanadamu wote walikuwa wenye dhambi.
Paulo aliendelea kutaja kwamba alikuwa “hai hapo kwanza bila sheria.” Huo ulikuwa wakati gani? Wakati alipokuwa katika viuno vya Abrahamu kabla ya Yehova kuandaa Sheria. (Warumi 7:9; linganisha Waebrania 7:9, 10.) Ingawa Abrahamu hakuwa mkamilifu, Sheria haikuwa imetolewa bado, kwa hiyo hakuwa akikumbushwa juu ya udhambi wake kwa kukosa kufuata amri zayo nyingi sana. Je, hilo lamaanisha kwamba Sheria ilipokwisha kutolewa na ikaonyesha kutokamilika kwa mwanadamu, ilikuwa na matokeo mabaya? La. Paulo aliendelea hivi: “Basi torati ni takatifu, na ile amri ni takatifu, na ya haki, na njema.”—Warumi 7:12.
Ona kwamba Paulo alisimulia Sheria kuwa “takatifu” na “njema.” Katika mistari ifuatayo, alieleza kwamba “lililo jema”—Sheria—lilionyesha wazi kwamba alikuwa mtenda dhambi, na dhambi hiyo ilimfanya astahili kifo. Paulo aliandika hivi: “Lile jema nilipendalo silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo. Basi kama lile nisilolipenda ndilo nilitendalo, si mimi nafsi yangu nilitendaye, bali ni ile dhambi ikaayo ndani yangu.”—Warumi 7:13-20.
Katika muktadha huo, basi, Paulo hakuwa akisema juu ya wema kwa ujumla, au vitendo vyema tu. (Linganisha Matendo 9:36; Warumi 13:3.) Alikuwa akirejezea hasa juu ya kufanya (au kutofanya) mambo yaliyokuwa yakipatana na Sheria njema ya Mungu. Mbeleni alikuwa amezoea dini ya Kiyahudi kwa bidii na—alipolinganishwa na wengine—‘hakuwa na hatia.’ Hata hivyo, hata ingawa akilini mwake alikuwa amekuwa mtumwa mwenye kudhamiria wa ile Sheria njema, bado hakuitii kikamili. (Wafilipi 3:4-6) Sheria ilionyesha viwango vya Mungu vikamilifu, ikionyesha mtume kwamba katika mnofu wake bado alikuwa mtumwa wa sheria ya dhambi na kwa hiyo akawa mwenye kuhukumiwa kifo. Hata hivyo, Paulo angeweza kushukuru kwamba kwa dhabihu ya Kristo alitangazwa rasmi kuwa mwadilifu—akaokolewa kutoka kwa sheria ya dhambi na matokeo yayo yastahiliyo, yaani, hukumu ya kifo.—Warumi 7:25.
Leo Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa, kwa maana ilitundikwa kwenye mti wa mateso. (Warumi 7:4-6; Wakolosai 2:14) Hata hivyo twafanya vyema kutambua kwamba haikuwa sheria yenye kulemeza ambayo haipasi kufikiriwa. La, kwa msingi Sheria ilikuwa njema. Kwa hiyo tuna sababu ya kusoma vitabu vya Biblia vilivyo na Sheria na kujifunza matakwa yayo kwa Israeli. Mashahidi wa Yehova kotekote duniani watafanya hivyo karibuni, wakiendelea na usomaji wao wa Biblia wa kila juma.
Tusomapo Sheria, twapaswa tuzifikirie kanuni za msingi za amri zayo mbalimbali na manufaa ambayo watu wa Mungu walipata walipojaribu kufuata amri hizo njema. Twapaswa kuthamini, pia, kwamba sisi si wakamilifu na kwa hiyo hatuwezi kufuata kikamili yale mema tujifunzayo kutoka kwa Neno la Mungu. Lakini tunapopigana dhidi ya sheria ya dhambi, twaweza kushangilia juu ya taraja la kuponyoshwa kupitia dhabihu ya Kristo itakayotumiwa kwetu.