Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ Kwa nini Isaya 11:6, katika New World Translation of the Holy Scriptures, yasema kwamba “jibwa-mwitu kwa kweli litakaa kwa kitambo fulani pamoja na mwana-kondoo mume”? Je! kwani amani hiyo haitakuwa ya kudumu?
Amani yenye kuburudisha katika viumbe-wanyama iliyosemwa kwa unabii kwenye Isaya 11:6-9 itakuwa ya kudumu. Lakini ufasiri wa uangalifu wa Isaya 11:6 waelewesha wazi kwamba wanyama hao hawatakuwa pamoja wakati wote.
Katika New World Translation of the Holy Scriptures, Isaya 11:6 husomeka hivi: “Jibwa-mwitu kwa kweli litakaa kwa kitambo fulani pamoja na mwana-kondoo mume, na pamoja na mwana-mbuzi chui mwenyewe atalala chini, na ndama na simba mchanga aliyeota manyoya ya shingo na mnyama mlishwa-vema wote pamoja; na mvulana mdogo tu atakuwa kiongozi juu yao.”
Msomeko ulio katika fasiri nyingi za Biblia ni kitu kama hiki: “Jibwa-mwitu pia litakaa [au, “litaishi”] pamoja na mwana-kondoo.” Fasiri kama hizo zingeweza kutokeza wazo la jibwa-mwitu na mwana-kondoo wakiwa waandamani wa kuendelea, kana kwamba katika familia mpya au mpango wa maisha.
Hata hivyo, neno la Kiebrania lililotafsiriwa ‘kukaa’ au ‘kuishi’ ni gur. Kulingana na mtunga maneno William Gesenius, lamaanisha “kushinda mahali, kukaa kwa muda, kuishi ni kama si nyumbani, m.y. kama mgeni, mtu wa kigeni, mgeni mwalikwa.” (A Hebrew and English Lexicon of the Old Testament, iliyotafsiriwa na Edward Robinson) Kitabu cha maneno kilichotungwa na F. Brown, S. Driver, na C. Briggs hutoa maana ya “kushinda mahali, kukaa kwa (wakati ulio dhahiri au usio [dhahiri]), kukaa kama mkaaji wa majuzi tu . . . bila haki za asilia.”
Mungu alitumia gur katika kuambia Abrahamu ‘akae kama mgeni’ katika Kanaani. Mzee huyo wa ukoo hangechukua bara hilo liwe lake mwenyewe, bali angeweza kuwa mkaaji mpewa ulinzi huko. (Mwanzo 26:3; Kutoka 6:2-4; Waebrania 11:9, 13, NW) Vilevile, Yakobo alisema kwamba yeye alikuwa ‘akikaa kama mgeni’ katika eneo la Harani, kwa maana angerudi Kanaani.—Mwanzo 29:4; 32:4, NW.
Katika Paradiso ambayo karibuni Mungu atasimamisha, wanyama na wanadamu watakaa kwa amani. Mwana-kondoo hatakuwa hatarini akiwa pamoja na jibwa-mwitu wala ndama akiwa pamoja na chui. Kama kwamba ni kwa kusudi la kuonyesha utofautiano na wakati wa sasa, usemi uliotumika hata waruhusu lile wazo la kwamba jibwa-mwitu lingekuwa mkaaji mwenye kupewa ulinzi na mwana-kondoo.—Isaya 35:9; 65:25.a
Hata hivyo, wanyama hao bado wangeweza kuwa na makao mbalimbali. Wanyama fulani wana umbo la kufaa kukaa misituni, wengine kwenye nyika, na bado wengine kwenye majimbo ya pwani au milimani. Hata wakati wa ile Paradiso ya asilia, Mungu alisema juu ya ‘wanyama wa kufugwa na wanyama wa mwitu.’ (Mwanzo 1:24) Wanyama wa kufugwa kwa wazi walikuwa wale ambao wangeweza kwa kawaida kuwa karibu na wanadamu na makao yao. Mnyama wa mwitu, ajapokuwa si mkatili, kwa wazi alipendelea kuishi mbali na ainabinadamu. Hivyo basi, kama vile unabii wa Isaya utabirivyo, jibwa-mwitu ‘litakaa kwa kitambo fulani pamoja na mwana-kondoo mume,’ lakini halitakuwa karibu-karibu na wanyama hao wa kufugwa kila wakati.
[Maelezo ya Chini]
a The Bible in Living English huyapanga maneno ya Isaya 11:6 hivi: “Na jibwa-mwitu litakuwa mpangishwa-nyumba wa kondoo.”
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 31]
Kitovu cha Utafiti Kuhusu Wanyama, Chuo Kikuu cha Kiebrania kule Tel-Aviv