Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ Mtu anapokufa, je, inafaa kwa Wakristo kuipa familia hiyo maua au kupeleka maua kwenye nyumba ya maziko?
Katika nchi fulani ni jambo la kidesturi kufanya hivyo, Lakini kutumia maua kwenye maziko mara nyingi kumekuwa na maana ya kidini. Kwa hiyo acheni tuchunguze jambo hilo zaidi, hasa kwa kuwa kuna desturi nyinginezo ambazo huenda zikaonekana kuhusika vivyo hivyo na dini bandia. Ona maelezo kutoka The Encyclopedia of Religion (1987):
“Maua yanahusika na makao matakatifu kupitia ushirikiano wayo na miungu na miungu-wake. Flora, mungu-mke wa Kiroma wa masika na wa maua, huleta uzuri na manukato kwa maua yachanuayo. . . Miungu wanaweza kutulizwa na kuabudiwa . . . kupitia matoleo ya chakula na maua.
“Ushirikiano wa maua na kawaida za ibada za kifo hutukia kotekote ulimwenguni. Wagiriki na Waroma walifunika wafu na makaburi yao kwa maua. Nafsi za Wabuddha wanaokufa katika Japani hubebwa juu kwenye yungiyungi (ua pana ambalo huelea majini), na mawe ya makaburi katika maziara huenda yakawekwa kwenye mayungiyungi yaliyochongwa . . . Watahiti huacha mashada ya maua yaliyofungiliwa makangaga karibu na mwili baada ya kifo na kisha humwaga marashi ya maua juu ya maiti ili kufanya iwe rahisi kwayo kuingia maisha matakatifu ya baada ya kifo . . . Maua yaweza pia kuwako kwa nyakati takatifu kwa namna ya uvumba au manukato.
Wakitambua kwamba maua yametumiwa kuhusiana na dini bandia, Wakristo fulani wamehisi kwamba hawapaswi kutoa au kupeleka maua kwa ajili ya maziko. Hisia yao huenda pia ikaonyesha tamaa yao ya kuepuka desturi za kilimwengu, kwa kuwa wafuasi wa Yesu wapaswa wasiwe “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19, NW) Hata hivyo, maandiko ya Biblia yenye kuhusika na hayo, na maoni ya watu wa mahali fulani huhusika pia katika jambo hilo.
Maua ni sehemu ya zawadi nzuri za Mungu kwa walio hai kufurahia. (Matendo 14:15-17; Yakobo 1:17) Uumbaji wake wa maua mazuri umetumiwa katika ibada ya kweli. Kile kinara cha taa katika tabenakulo (hema) kilipambwa na “maua ya mlozi . . . na maua.” (Kutoka 25:31-34) Michoro iliyochongwa katika hekalu ilitia ndani mashada ya maua na miti ya minazi. (1 Wafalme 6:18, 29, 32) Kwa wazi, matumizi ya kipagani ya maua au mashada ya maua hayakumaanisha kwamba waabudu wa kweli walipaswa sikuzote kuepuka kuyatumia.—Matendo 14:13.
Lakini, vipi lile swala lenye kutia ndani mengi zaidi la kufuata desturi, kama vile desturi za maziko? Biblia hurejezea desturi nyingi, fulani zisizofaa kwa waabudu wa kweli, nyingine zilizofuatwa na watu wa Mungu. Wafalme wa Kwanza 18:28 hutaja ile “desturi” ya waabudu wa Baali ya ‘kupiga kelele, na kujikata-kata’—desturi ambayo waabudu wa kweli wasingefuata. Kwa upande mwingine, Ruthu 4:7 haionyeshi kutokubali kokote kuhusu ile “desturi [ya] zamani za kale katika Israeli, kwa habari ya [jinsi ya kuzoea] kukomboa.”
Desturi zilizokubaliwa na Mungu huenda hata zikasitawi katika mambo yaliyo ya kidini tu. Mungu alipopangilia mwadhimisho wa Kupitwa, yeye hakutaja matumizi ya divai, lakini kufikia karne ya kwanza, ilikuwa desturi kutumia vikombe vya divai. Yesu na mitume wake hawakukataa desturi hiyo ya kidini. Hawakuiona kuwa jambo baya, nao waliifuata.—Kutoka 12:6-18; Luka 22:15-18; 1 Wakorintho 11:25.
Ni vivyo hivyo na desturi nyinginezo za maziko. Wamisri walikuwa wakipaka maiti dawa kidesturi zisioze. Yusufu mzee wa ukoo aliye mwaminifu hakuwa na tendo-mwitikio la kusema moja kwa moja bila kufikiri kwamba, ‘Hii ni desturi ya kipagani, kwa hiyo ni lazima sisi Waebrania tuiepuke.’ Badala ya hivyo, ‘aliwaagiza watumishi wake waganga [matabibu, NW], kwamba wampake babaye dawa asioze,’ kwa wazi ili Yakobo aweze kuzikwa katika Bara Lililoahidiwa. (Mwanzo 49:29–50:3) Baadaye Wayahudi walisitawisha desturi tofauti za maziko, kama vile kuuosha mwili na kuuzika siku ya kifo. Wakristo wa mapema walikubali desturi za Kiyahudi kama hizo.—Matendo 9:37.
Hata hivyo, vipi ikiwa desturi ya maziko inaonwa kuwa na maana inayotegemea kosa la kidini, kama vile imani katika nafsi isiyoweza kufa? Kumbuka kutokana na ile ensaiklopedia kwamba wengine “huacha mashada ya maua yaliyofungiliwa makangaga karibu na mwili baada ya kifo na kisha humwaga marashi ya maua juu ya maiti ili kufanya iwe rahisi kwayo kuingia maisha matakatifu ya baada ya kifo.” Hata ingawa huenda desturi kama hiyo iwepo hiyo haimaanishi kwamba ni lazima watumishi wa Mungu waepuke jambo lolote linalofanana na hiyo. Ingawa Wayahudi hawakuamini “kuingia maisha matakatifu ya baada ya kifo,” Biblia husema hivi: “Wakautwaa mwili wake Yesu, wakaufunga sanda ya kitani pamoja na yale manukato, kama ilivyo desturi ya Wayahudi katika kuzika.”—Yohana 12:2-8; 19:40.
Wakristo wapaswa kuepuka mazoea yanayopingana na kweli ya Kibiblia. (2 Wakorintho 6:14-18) Bado, vitu, mapambo, na mazoea ya aina mbalimbali yameweza, kwa wakati mmoja au mwingine, kupewa maana bandia au kuhusianishwa na mafundisho yasiyo ya kimaandiko. Miti imeabudiwa, umbo la moyo limeonwa kuwa takatifu, na uvumba umetumiwa katika sherehe za kipagani. Je, hilo linamaanisha kwamba ni lazima Mkristo asitumie kamwe uvumba, asiwe na miti katika mapambo yoyote, au asivae vito vyenye umbo la moyo?a Hiyo si ndiyo sababu ya kukata uamuzi hivyo.
Mkristo wa kweli apaswa afikirie hili: Je! kufuata desturi fulani kungeonyesha wengine kwamba nimechagua imani au mazoea yasiyo ya kimaandiko? Kipindi cha wakati na mahali vingeweza kuongoza jibu la hilo. Desturi (au pambo) huenda ikawa ilikuwa na maana ya kidini bandia mamileani yaliyopita au huenda ikawa na maana hiyo leo katika nchi ya mbali. Lakini bila kuchukua wakati mwingi katika kuchunguza hilo, jiulize mwenyewe hivi: ‘Maoni ya kawaida mahali ninapoishi ni gani?’—Linganisha 1 Wakorintho 10:25-29.
Ikiwa inajulikana sana kwamba desturi fulani (au pambo, kama vile msalaba) ina maana ya kidini bandia, iepuke. Hivyo Wakristo wasingepeleka maua kwa namna ya msalaba, au moyo mwekundu ikiwa huo huonwa kuwa na maana ya kidini. Au katika mahali maalum huenda kukawa njia fulani rasmi iliyo na maana ya kidini ambayo katika hiyo maua hutumiwa penye maziko au penye mahali pa kaburi. Mkristo apaswa aepuke hiyo pia. Lakini hiyo haimaanishi kwamba kuandaa shada la maua kwenye maziko tu au kumpa rafiki maua hospitalini kunapasa kuonwa kuwa kitendo cha kidini kipasacho kuepukwa.b
Tofauti na hilo, katika nchi nyingi desturi ya kuandaa maua imeenea sana na huonwa kuwa fadhili inayofaa. Maua yaweza kuchangia uzuri na kufanya pindi yenye huzuni iwe yenye kupendeza zaidi. Yaweza pia kuwa wonyesho wa huruma na ufikirio. Mahali penginepo desturi huenda ikawa kuonyesha maoni kama hayo kwa kitendo cha ukarimu, kama vile kuandaa chakula kwa mgonjwa au kwa watu wenye majonzi. (Kumbuka ile shauku aliyoonewa Dorkasi kwa sababu alionyesha kupendezwa na ufikirio kwa wengine. [Matendo 9:36-39]) Wakati kufanya hivyo hakuhusiani kwa wazi na imani bandia, Mashahidi wa Yehova fulani huwa na zoea la kuandaa maua yenye uchangamfu kwa rafiki aliyelazwa hospitalini au wakati kifo kimetukia. Na wakiwa mmoja mmoja huenda wakaonyesha kupendezwa kwao na hisia zao zaidi kwa vitendo vinavyofaa.—Yakobo 1:27; 2:14-17.
[Maelezo ya Chini]
a Wapagani wametumia kwa muda mrefu uvumba wa maua katika sherehe zao, lakini halikuwa jambo baya kwa watu wa Mungu kutumia uvumba katika ibada ya kweli. (Kutoka 30:1, 7, 8; 37:29; Ufunuo 5:8) Ona pia “Je, Hayo Ni Mapambo ya Ibada ya Sanamu?” katika Amkeni! ya Desemba 22, 1976 (ya Kiingereza).
b Matakwa ya familia yapasa kufikiriwa, kwa kuwa wengine huarifu kwamba yeyote atakaye kupeleka maua apaswa badala yake kufanya mchango kwa kundi au kwa shirika lingine la kihisani.