Je! Uchaji kwa Visalio vya Waonwao Kuwa Watakatifu Humpendeza Mungu?
KIMOJA kati ya visalio vingi vya kidini ni ile damu ya “San Gennaro,” isemwayo kuwa huyeyuka kwa kawaida mara tatu kwa mwaka. Kingine pia ni ile Sanda ya Turin, ambayo yasemwa kwamba ndiyo iliyotumiwa kufungia mwili wa Yesu Kristo. Miongoni mwa visalio vya waonwao kuwa watakatifu ambavyo hufungamanishwa na Yesu ni kile kinachodhaniwa kuwa kitanda cha utoto wake (kilicho katika basilika kubwa huko Roma), kitabu chake cha kuandikia mwendelezo wa maneno, na misumari zaidi ya elfu moja isemwayo kuwa ilitumiwa kwenye kuuawa kwake! Visalio vya kidini vinatia ndani pia vichwa kadhaa vya Yohana Mbatizaji, na miili minne isemwayo kuwa ni ya mwanamke mtakatifu “Santa Lucia” iliyo katika sehemu mbalimbali za Ulaya.
Miongoni mwa majiji yaliyo maarufu hasa kwa ajili ya visalio hivyo ni Trier, katika Ujerumani, ambapo moja kati ya “majoho matakatifu” mengi—lile vazi la ndani lisilo na mshono lililovaliwa na Yesu Kristo—yanahifadhiwa. Katika Jiji la Vatikani lenyewe mna visalio zaidi ya elfu moja katika jumba maalum la kuwekea kumbukumbu za kihistoria. Kwa halisi maelfu ya visalio vya kidini huwekwa katika kanisa la “Mtakatifu Ursula” huko Cologne, katika Ujerumani. Orodha ya visalio hivyo ni ndefu sana. Kwani, katika Italia peke yake, kuna mahali 2,468 paitwapo eti patakatifu penye visalio vya kidini!
Kutoa kicho chenye staha kwa visalio kunadhaniwa kwamba kulianza tangu karne ya nne ya Wakati wa Kawaida wetu, kama kunavyodhaniwa juu ya kutoa kicho cha kiibada kwa “watakatifu.” Kwa sababu za kidini, za kiuchumi, na hata za kisiasa, hesabu ya visalio imeongezeka polepole muda wote wa karne zilizopita, vikiwako kwa maelfu leo. Baraza la Pili la Vatikani lilithibitisha tena kwamba “kulingana na mapokeo yalo, Kanisa hutolea watakatifu kicho cha kiibada na huheshimu visalio vyao asilia na mifano yao.” (Constitution “Sacrosanctum Concilium” sulla sacra Liturgia, katika I Documenti del Concilio Vaticano II, 1980, Edizioni Paoline) “Visalio maarufu, pamoja na vile vinavyoheshimiwa na watu wengi wenye kuvicha,” vyatajwa katika Codex Iuris Canonici (Orodha ya Kanuni za Kanisa) iliyoenezwa na John Paul 2 katika mwaka wa 1983. (Kanuni ya Kanisa ya 1190) Waanglikana na washiriki wa makanisa ya Orthodoksi huheshimu pia visalio vya waonwao kuwa watakatifu.
Kukiwa na misumari mingi inayodhaniwa kuwa ile iliyotumiwa katika kutundikwa kwa Kristo na kukiwa na vichwa vingi vya Yohana Mbatizaji, ni wazi kwamba visalio vya kidini mara nyingi huwa bandia. Kwa mfano, kadirio la tarehe ya kitu kwa kutumia rediokaboni lilithibitisha kwamba Sanda ya Turin ilikuwa bandia. Kwa kupendeza, wakati wa mabishano makali kuhusu sanda hiyo katika 1988, Marco Tosatti mchunguzaji mashuhuri wa Vatikani aliuliza hivi: “Ikiwa mchanganuo wa kisayansi uliotumiwa kwa Sanda hiyo ungetumiwa kwa vitu vingine vinavyotolewa uchaji na watu wengi, uamuzi ungekuwa nini?”
Kwa wazi, hakuna mtu yeyote mwenye hekima ambaye angependa kutoa kicho kwa kisalio bandia. Lakini je! hilo ndilo jambo peke yake linalohitaji kufikiriwa?
Biblia Husema Nini?
Biblia haisemi kwamba watu wenye upendeleo wa Mungu, Waisraeli wa kale, walitoa kicho kwa visalio vya kidini walipokuwa katika utumwa wa Kimisri. Ni kweli, mzee wa ukoo Yakobo alikufa Misri na mabaki yake yakapelekwa nchi ya Kanaani yakazikwe ‘katika pango iliyokuwa shambani mwa Makpela.’ Yusufu mwana wake alikufa Misri pia, na hatimaye mifupa yake ilipelekwa Kanaani ili ikazikwe. (Mwanzo 49:29-33; 50:1-14, 22-26; Kutoka 13:19) Hata hivyo, Maandiko hayaonyeshi hata kidogo kwamba Waisraeli walipata kutoa kicho cha kiibada kwa mabaki ya Yakobo na Yusufu kwa wakati wowote kana kwamba yalikuwa visalio vya kidini.
Fikiria, pia, lile lililotukia kwa habari ya nabii Musa. Chini ya mwelekezo wa Mungu, aliwaongoza Waisraeli kwa miaka 40. Kisha, akiwa na umri wa miaka 120, alikwea Mlima Nebo, akatazama Bara Lililoahidiwa, na kufa. Mikaeli malaika mkuu alibishana na Ibilisi juu ya mwili wa Musa, na Shetani alizuiwa asiweze kabisa kujaribu kuutumia kuwashawishi Waisraeli katika ibada ya visalio. (Yuda 9) Ingawa yaeleweka kwamba waliomboleza kifo cha Musa, wao hawakutoa kamwe kicho cha kiibada kwa mabaki yake. Kwa kweli, Mungu alifanya jambo hilo lisiwezekane kabisa kwa kumzika Musa katika kaburi lisilo na alama mahali pasipojulikana na wanadamu.—Kumbukumbu la Torati 34:1-8.
Watu fulani wanaoshindania utoaji wa kicho cha kiibada kwa visalio hutaja 2 Wafalme 13:21, inayosema hivi: “Ikawa, walipokuwa wakimzika mtu, angalia, waliona kikosi; wakamtupa yule mtu kaburini mwa Elisha; mara yule maiti alipogusa mifupa ya Elisha, alifufuka, akasimama kwa miguu.” Huo ulikuwa muujiza uliohusisha mifupa isiyo na uhai ya mmoja wa manabii wa Mungu. Lakini Elisha alikuwa amekufa naye ‘hakujua neno lo lote’ wakati wa muujiza huo. (Mhubiri 9:5, 10) Kwa hiyo, ni lazima sifa ya ufufuo huo ihesabiwe nguvu ya kufanya miujiza ya Yehova Mungu, aliyeutimiza kupitia roho takatifu, au nguvu ya utendaji yake. Yastahili kuangaliwa pia kwamba Maandiko hayasemi kwamba mifupa ya Elisha ilipewa kicho cha kiibada kwa wakati wowote.
Wengine katika Jumuiya ya Wakristo hushindania kutolea visalio kicho cha kiibada kwa sababu ya lile lisemwalo katika Matendo 19:11, 12, ambapo twasoma hivi: “Mungu akafanya kwa mikono ya [mtume] Paulo miujiza ya kupita kawaida; hata wagonjwa wakaletewa leso na nguo zilizotoka mwilini mwake, magonjwa yao yakawaondokea, pepo wachafu wakawatoka.” Tafadhali ona kwamba Mungu kupitia Paulo ndiye alifanya kazi hizo zenye kupita kawaida. Mtume mwenyewe hakufanya kazi za jinsi hiyo kwa kutegemea nguvu zake mwenyewe, naye hakukubali kupewa kicho cha kiibada na mwanadamu yeyote.—Matendo 14:8-18.
Kinyume cha Mafundisho ya Biblia
Kwa kweli, kutolea visalio vya kidini kicho cha kiibada ni kufanya kinyume cha mafundisho kadhaa ya Biblia. Kwa mfano, jambo la lazima katika kutoa kicho hicho cha kiibada ni imani katika kutoweza kufa kwa nafsi ya kibinadamu. Mamilioni ya washiriki wachaji wa kanisa huamini kwamba nafsi za wote walioorodheshwa na kupewa kicho cha kiibada wakiwa “watakatifu” ziko hai mbinguni. Watu hao wenye mioyo myeupe husali kwa “watakatifu” hao, wakitafuta ulinzi wao na kuwaomba wamsihi Mungu kwa niaba ya waombaji. Kwa kweli, kulingana na kitabu kimoja cha kidini, Wakatoliki huvipa visalio sifa ya “nguvu ya Mtakatifu ya kuomba Mungu kwa niaba ya wengine.”
Hata hivyo, kulingana na Biblia, nafsi ya kibinadamu haina hali ya kutokufa. Wanadamu hawana nafsi ndani yao zisizoweza kufa na zenye uwezo wa kuwako mbali na mwili baada ya kifo. Bali, Maandiko husema hivi: “BWANA [Yehova, NW] akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” (Mwanzo 2:7) Badala ya kufundisha kwamba wanadamu wana nafsi zisizoweza kufa, Biblia husema hivi: “Ile nafsi inayofanya dhambi—hiyo yenyewe itakufa.” (Ezekieli 18:4, New World Translation) Hilo linatumika kwa wanadamu wote—kutia na wale walioorodheshwa baadaye kuwa “watakatifu”—kwa maana sisi sote tumerithi dhambi na kifo kutoka kwa mtu wa kwanza, Adamu.—Warumi 5:12.
Uchaji kwa “watakatifu” wapasa uepukwe kwa sababu wao hawakupewa kamwe mamlaka ya kuomba Mungu kwa niaba ya mtu yeyote. Yehova Mungu ameamuru kwamba Mwana wake tu, Yesu Kristo, ndiye aweza kufanya hivyo. Mtume Paulo alisema kwamba Yesu “hakufa kwa ajili yetu tu—alifufuka kutoka wafu, na hapo penye mkono wa kulia wa Mungu asimama na kusihi kwa ajili yetu.”—Warumi 8:34, The Jerusalem Bible; linganisha Yohana 14:6, 14.
Sababu nyingine ya kuepuka uchaji kwa “watakatifu” na kwa visalio vya kidini vinavyoshirikishwa nao ina msingi katika lile Biblia husema juu ya ibada ya sanamu. Mojawapo ya zile Amri Kumi zilizopewa Waisraeli ilitaarifu hivi: “Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia. Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, BWANA [Yehova, NW], Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu.” (Kutoka 20:4, 5) Karne nyingi baadaye, mtume Paulo aliwaambia Wakristo wenzake hivi: “Wapenzi wangu, ikimbieni ibada ya sanamu.” (1 Wakorintho 10:14) Vilevile, mtume Yohana aliandika hivi: “Watoto wadogo, jilindeni nafsi zenu na sanamu.”—1 Yohana 5:21.
Kwa hiyo, kutoa kicho chenye staha kwa wale walioorodheshwa kuwa “watakatifu” na kwa visalio vya kidini hakuungwi mkono na Biblia. Hata hivyo, watu wengine hutamani kuwa na kitu kionwacho kuwa kitakatifu na ambacho chaweza kuonwa na kuguswa na kinachodhaniwa kuwa na uwezo wa kuokoa. Kwa kweli, wengi huona visalio vya kidini kuwa kiunzi kionekanacho cha ukamatano kati ya mbingu na dunia. Tafadhali fikiria jambo hilo kidogo.
Si kwa kuona na kugusa visalio vya kidini kwamba mtu hutenda kwa upatano na maneno ya Yesu kuhusu ibada ambayo Mungu hutamani. Yesu alisema hivi: “Saa inakuja, nayo saa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.” (Yohana 4:23, 24) Yehova Mungu ni “Roho,” asiyeonekana na macho ya kibinadamu. Kumwabudu “katika roho” kunamaanisha kwamba utumishi wetu mtakatifu kwa Mungu unachochewa na moyo wenye kujaa upendo na imani. (Mathayo 22:37-40; Wagalatia 2:16) Hatuwezi kumtumikia Mungu ‘katika kweli’ kwa kutoa kicho cha kiibada kwa visalio bali ni kwa kukataa tu mambo bandia ya kidini, kujifunza mapenzi yake kama yalivyofunuliwa katika Biblia, na kuyafanya.
Kwa hiyo, haishangazi kwamba mwanachuo James Bentley akiri kwamba ‘Waebrania wa kale hawakuzoea utoaji wa kicho cha kiibada kwa visalio vya waonwao kuwa watakatifu.’ Yeye asema pia kwamba katika zile karne nne kati ya kifo cha Stefano na kuchimbuliwa kwa mwili wake na Lucian, mtazamo wa Wakristo kuelekea visalio vya waonwao kuwa watakatifu ulibadilika kabisa. Hata hivyo, kufikia karne ya tano W.K., Jumuiya ya Wakristo ya uasi-imani ilikuwa tayari imeacha kushikamana na mafundisho ya Biblia ya wazi kuhusu ibada ya sanamu, hali ya wafu, na daraka la Yesu Kristo akiwa yule “anayetuombea.”—Warumi 8:34; Mhubiri 9:5; Yohana 11:11-14.
Ikiwa tunataka ibada yetu impendeze Mungu, ni lazima tuhakikishe kwamba haishirikishwi na namna yoyote ya ibada ya sanamu. Ili ibada yetu ikubalike, ni lazima imwendee Muumba, Yehova Mungu, si kisalio au kiumbe chochote. (Warumi 1:24, 25; Ufunuo 19:10) Ni lazima pia tutwae maarifa sahihi ya Biblia na kujenga imani thabiti. (Warumi 10:17; Waebrania 11:6) Na tukitembea katika njia ya ibada ya kweli, tutatenda kwa upatano na ule ushuhuda mwingi wa Kimaandiko kwamba uchaji wa visalio vya waonwao kuwa watakatifu haumpendezi Mungu.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Mifupa ya Elisha haikutolewa kicho cha kiibada ingawa ilihusika katika ufufuo