Kuwavuna Waabudu
MTUME Yohana alipewa njozi ya matukio yenye kuutetemesha ulimwengu ambayo yangetukia “siku ya Bwana.” Alimwona Bwana Yesu Kristo wa kimbingu akipanda farasi kuelekea vita ya uadilifu, inayotolewa mfano wa farasi dume mweupe—“akishinda tena apate kushinda.” Jambo la kwanza analofanya ni kumvurumisha adui mkubwa zaidi wa Mungu, Shetani, kutoka mbinguni hadi ujirani wa dunia. Shetani aitikia kwa kuipiga ainabinadamu na mauaji, njaa, na magonjwa yasiyo na kifani, yanayotolewa mfano wa wapandaji-farasi wa ufananisho na farasi zao—wa rangi nyekundu, nyeusi, na nyeupe-nyeupe. (Ufunuo 1:10; 6:1-8; 12:9-12) Ole hizo zililipuka kwanza katika mwaka wa 1914 na zimeongezeka tangu wakati huo. Karibuni, zitafikia upeo kwa ile ambayo Yesu alieleza kuwa “dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.”—Mathayo 24:3-8, 21.
Waabudu wa Yehova watapatwa na nini wakati huo? Ufunuo sura 7, mistari 1 hadi 10, husema juu ya majeshi ya kimalaika “wakizizuia” pepo za uharibifu mpaka waabudu hao wawe wamekusanywa. Katika kipindi tangu 1914, wale wa mwisho duniani wa Israeli ya kiroho, wanaohesabika kuwa 144,000, wanakusanywa. Na kisha “tazama, mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.” Hesabu ya mkutano huo mkubwa tayari imefika mamilioni. Wanasimama wakiwa na kibali mbele ya kiti cha enzi cha Mungu kwa sababu ya kujizoeza imani katika damu ya Yesu ya fidia, aliyechinjwa kama mwana-kondoo asiye na hatia. “Wakilia kwa sauti kuu wakisema, Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.” Waabudu hao wenye bidii huendelea kusema “Njoo!” kwa wengine bado, ambao nao hukusanywa kwa ajili ya wokovu kupitia “dhiki ile iliyo kuu.”—Ufunuo 7:14-17; 22:17.
“Duniani Mwote”
Kwaweza kusemwa hivi juu ya waabudu hao wenye kujitoa: “Sauti yao imeenea duniani mwote, na maneno yao hata miisho ya ulimwengu [dunia, NW].” (Warumi 10:18) Juhudi yao imebarikiwa na mazao ya ajabu. Kwa mfano:
Meksiko sasa inaripoti waabudu wa Yehova watendaji 335,965, ongezeko la elfu mia moja katika miaka mitatu tu! Kwa nini kuna ongezeko kubwa kama hilo? Kisa kifuatacho kitasaidia kueleza hilo. Mwanamume kijana aitwaye Aurelio alikuwa msakristi (Mtunza chumba cha vyombo na mavazi matakatifu) katika kanisa moja la Katoliki. Kila mara Mashahidi wa Yehova walikuja katika kijiji hicho, alizipiga kengele ili kuwazuia watu wasiwasikilize. Baadaye alinunua Jerusalem Bible ya Katoliki akaanza kuisoma, lakini hakuielewa. Halafu siku moja alimwona rafiki na nakala ya New World Translation mkononi mwake. Aurelio alimkaripia rafiki yake na, akimwambia kwamba Biblia yake ilikuwa ya uwongo, alimpeleka nyumbani kwake mwenyewe kumwonyesha Biblia ya “kweli.” Rafiki yake akasema: “Soma Kutoka 20,” kisha akaondoka.
Akianza na sura 1 msakristi huyo alisoma kitabu cha Kutoka mpaka alipofika sura 20, mistari 4 na 5. Alishangazwa na lile ambalo Biblia yake ya Kikatoliki ilisema juu ya sanamu. Baada ya misa Jumapili iliyofuata, alimkabili padri na maandiko hayo juu ya sanamu. Kwanza padri alisema kwamba yeye alizipa sanamu kicho tu; hakuziabudu. Akiona kwamba hilo halikumtosheleza Aurelio, padri alimshtaki kuwa alikuwa anajifunza na Mashahidi wa Yehova. Aurelio alikana hilo lakini akaongeza, “Sasa nitafanya hivyo!”
Mashahidi waliporudi kijijini mara ifuatayo, Aurelio alikutana nao akaanza kujifunza Biblia pamoja nao. Aliacha kufanya kazi kanisani na katika miezi mitatu akastahili kushiriki katika huduma ya peupe pamoja na Mashahidi wa Yehova. Nyumba ya kwanza aliyotembelea ilikuwa ya padri, ambaye hakuweza kuamini aliyoona alipomwona yule aliyekuwa msakristi zamani katika daraka la mhubiri wa Ufalme. Padri alimtisha na kuondolewa katika ushirika wa kanisa, lakini Aurelio akamwambia kwamba hilo lisingekuwa jambo la lazima kwa kuwa yeye tayari alikuwa ameacha kanisa. Mwendo wake wenye ujasiri uliwatia moyo wengi wa kijiji hicho ambao tayari walikuwa wakijifunza na Mashahidi wa Yehova. Aurelio pamoja na wengine 21 kutoka kijiji hicho walibatizwa kwenye mkusanyiko wa wilaya uliofauta. Ongezeko katika eneo hilo ni la haraka sana hivi kwamba kulikuwako mzee mmoja tu wa kupitia maswali ya wataka kubatizwa na kikundi hicho.
‘Sauti Yao Ilienea’
Hakuna kuepa kuhubiri Ufalme. Mkatoliki Mwitaliano mmoja alikuwa akikasirika kila wakati Mashahidi wa Yehova walipomtembelea. Kwa hiyo kampuni yake ilipomhamisha Singapore, alihisi kwamba hatimaye asingesumbuliwa nao. Lakini kwa mshangao wake, Mashahidi walikuwa huko pia. Kwa hiyo alipata mbwa wakali wawili ili washambulie Mashahidi wafuatao ambao wangekuja. Mashahidi walipotembelea nyumba yake, mbwa hao waliruka nje. Wakiwa na hofu nyingi, wanawake hao walikimbia kuokoa maisha zao, wakielekea pande tofauti kwenye njia panda. Mbwa mmoja alipokaribia kumpata mmoja, kwa kukata tamaa Shahidi huyo alinyakua broshua mbili kutoka mkoba wake na kuzisukuma katika kinywa cha mbwa kilichokuwa wazi. Kisha, mbwa akaacha kumfuata, akageuka, na kukimbia nyumbani.
Juma lifuatalo, Mashahidi hao hao wawili walikuwa wakifanya ziara ya kurudia kwenye nyumba iliyokuwa upande ule mwingine wa barabara. Mwenye wale mbwa alikuwa katika shamba lake, na kwa mshangao, aliwasalimu wanawake hao na kuwaalika nyumbani mwake. Aliwaambia kwamba hakuwa kamwe amesema na Mashahidi wa Yehova au kusoma vichapo vyao vyovyote. Lakini alikuwa ameshangaa kupata broshua hizo katika kinywa cha mbwa wake mmoja. Jioni hiyo alikuwa amezisoma broshua hizo na kuvutiwa sana nazo. Ingawa alikuwa amekuwa Mkatoliki maisha yake yote, alionyesha tamaa ya kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova.
Kwa kuwa mwanamume huyo alikuwa anahamishwa Italia tena, mipango ilifanywa ili Mashahidi wa Yehova wajifunze pamoja naye huko. Yeye na mke wake walipoanza kuhudhuria mikutano, padri wa parishi aliwakabili kwa hasira na matisho. Mtu fulani alipowasha shamba lao moto, wenzi hao walivunja uhusiano wote na kanisa. Mtu huyo asema sasa: “Tayari nimekuwa nikitoa ushahidi kwa washiriki wengi wa familia yangu kwa sababu nataka kuwajulisha kwamba Yehova ni Mungu wa pekee wa kweli.”
‘Hata Miisho ya Dunia’
Ono jingine kutoka miisho ya dunia linaonyesha jinsi ujumbe wa Ufalme unavyothaminiwa na unavyosaidia kubadili maisha. Alipokuwa akihudhuria masomo ya kabla ya kuzaa, Shahidi katika Australia alikutana na mwanamke aliyekuwa na mazoea mengi mabaya, hata kukataa kuacha kuvuta sigareti wakati wa kuwa mja mzito. Shahidi huyo alisumbuliwa sana na mwelekeo wake. Ilitukia kwamba walipata watoto wao wakati mmoja na katika wadi moja, kwa hiyo walikuwa na nafasi ya kuongea. Ilionekana kana kwamba mwanamke huyo alikuwa amekuwa na matatizo mengi wakati wa utoto wake, na sasa ndoa yake ilikuwa karibu kuvunjika. Kwa hiyo, baada ya kuondoka hospitali, Shahidi huyo alimtembelea mwanamke huyo na kuanza funzo la Biblia pamoja naye, akitumia kitabu Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha.
Mume wa mwanamke huyo alikuwa amesali kwa Mungu kwamba angepata dini ya kweli, akiongeza sharti hili: “Maadamu si Mashahidi wa Yehova!” Hata hivyo, alipopata kujua kwamba mke wake alikuwa akijifunza na Mashahidi, alianza kuuliza maswali na akaalikwa ajiunge katika funzo. Alifanya hivyo, na upesi akaanza kuhudhuria mikutano ya kundi. Sasa, mume na mke pia wamebatizwa, na kwa wazi hali yao ya ndoa imekuwa bora sana.
Mafunzo ya Biblia nyumbani yenye msingi wa vichapo kama hivyo yametokeza kukusanywa kwa waabudu wapya wengi. Katika nchi ambako Mashahidi wa Yehova wamelazimika wavumilie mapinduzi, vita vya wenyewe kwa wenyewe, au vizuizi vya Kiserikali, utendaji wa mafunzo ya Biblia nyumbani umeongezeka. Vita ya wenyewe kwa wenyewe ilikuwa kali katika Angola kwa miaka mingi, na Mashahidi wakapatwa na mnyanyaso na magumu. Mapema mwaka uliopita, wahubiri zaidi ya 14,000 walikuwa wakiripoti mafunzo ya Biblia nyumbani zaidi ya 40,000, lakini wahubiri walikuwa na vichapo vichache vya Biblia. Waangalizi wasafirio walitembelea kikundi kidogo kila siku, wakipanga utumishi wa shambani wakati wa mchana na mikutano kila jioni! Ilikuwa shangwe kama nini wakati uadui ulipoisha na tani 42 za vichapo vya Biblia vilivyohitajiwa sana viliwasili kutoka Afrika Kusini! Kwa hakika, upendo wa ndugu hao ‘utazidi zaidi na zaidi pamoja na maarifa sahihi na ufahamu kamili,’ wakiweza sasa “kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:9, 10, NW) Ni kichocheo kilichoje kwa wale walio na misaada mingi ya kujifunza Biblia ili kujifaidi zaidi na maandalizi ambayo Yehova anafanya kwa neema nyingi!—1 Timotheo 4:15, 16.
Furaha ya waabudu hao waaminifu inatukumbusha maneno ya Yesu katika Mahubiri ya Mlimani: “Wenye furaha ni wale waonao uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbingu ni wao. . . . Wenye furaha ni wale ambao wamenyanyaswa kwa minajili ya uadilifu, kwa kuwa ufalme wa mbingu ni wao. . . . Shangilieni na kuruka-ruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa katika mbingu.” (Mathayo 5:3-12, NW) Ni mavuno yaliyoje ambayo tayari yanakusanywa katika Angola!
Katika maeneo mengine ya ulimwengu, vizuizi kwa utendaji wa Mashahidi wa Yehova vinalegezwa na kuondolewa pia. Yesu alieleza katika siku yake: “Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache.” (Mathayo 9:37) Hilo ni kweli kama nini leo! Uhitaji wa watenda kazi zaidi uko sikuzote. Tunafurahi kwamba ibada yetu inatia ndani kukusanya katika mavuno. Hakuna shangwe kubwa zaidi iwezayo kupatikana duniani leo kuliko utumishi wetu wa kujitoa kwa Yehova ulio na mazao.
Lakini, ni nini kinachochochea watumishi wa Yehova kuonyesha shangwe na bidii kama hiyo? Tutaona.