Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 1/1 kur. 8-17
  • Kumpenda Yehova Huchochea Ibada ya Kweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumpenda Yehova Huchochea Ibada ya Kweli
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ripoti Yenye Kutokeza
  • Utumishi wa Upendo kwa Ainabinadamu
  • Wapendao Uhuru wa Kimungu
  • Upendo Mwingi kwa Yehova
  • Kutembea kwa Nafsi Yote katika Njia ya Uzima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Baraka za Huduma ya Painia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 1/1 kur. 8-17

Kumpenda Yehova Huchochea Ibada ya Kweli

“Huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake.”—1 YOHANA 5:3.

1, 2. Ni nini chapasa kuwa kichocheo cha kumtumikia Yehova?

KIKUNDI kimoja cha wageni 80 kutoka Japani kilikuwa kikitalii Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova katika California, U.S.A. Mazingira yenye kupendeza kutia ndani shamba lililojaa ndege kama kunguru wenye rangi ya buluu, hua, na ndege wadogo sana wafanyao uvumi kwa mabawa yao, liliwafanya wahisi kuwa karibu zaidi na Muumba wao Mtukufu, Yehova Mungu. Mtembezi wao alitambua kwa upesi kwamba karibu kila mmoja katika kikundi hicho alikuwa akitumikia wakati wote akiwa painia. Kwa hiyo, baadaye, kikundi hicho kiliulizwa swali ambalo limetokezwa mara nyingi: “Ni kwa nini kuna mapainia wengi sana Japani? Kulikuwa kimya kwa kitambo kidogo. Kisha mwanamke kijana mmoja akaitikia kwa hiari: “Ni kwa sababu tunampenda Yehova.”

2 Kumpenda Yehova—huko kunatusukuma kama nini kuwa wenye bidii katika utumishi wake! Ni kweli, si kila mmoja awezaye kupainia. Kwa kweli, walio wengi wa wahubiri wetu wa Ufalme milioni nne hawajaweza kupanga ratiba zao ili kuweza kuonea shangwe pendeleo hilo. Lakini wengi wanaoruhusiwa na hali zao hulifikilia hilo. Na sisi wengine twaweza pia ‘kumtumaini Yehova na kutenda mema,’ tukionyesha upendo wetu kwa kuwa na sehemu fulani katika kazi ya kufanya wanafunzi. (Zaburi 37:3, 4) Na waabudu wote wa Yehova waliojiweka wakfu wanaweza kushiriki katika kukuza roho ya upainia, kwa kutoa utegemezo wenye upendo kwa wale wanaopainia.—Mathayo 24:14; 28:19.

3. Ni tofauti gani yapasa kuonwa kati ya wengi wanaodai kuwa Wakristo na Mashahidi wa Yehova?

3 Tofauti na wengi wanaodai kuwa Wakristo, ambao kwa faida yao huona dini kuwa jambo la ziada tu maishani mwao, Mashahidi wa Yehova huonyesha upendo mwingi kwa Mungu ambao huwachochea waendelee ‘kutafuta kwanza ufalme wake na haki yake.’ Hilo limehitaji kudhabihu, lakini kudhabihu huko kumefaa kama nini! (Mathayo 6:33; 16:24) Imepatana na amri ya kwanza iliyo kubwa zaidi, iliyotaarifiwa kwanza na Musa na kurudiwa na Yesu Kristo: “Bwana [Yehova, NW] Mungu wetu ni Bwana [Yehova, NW] mmoja; nawe mpende Bwana [Yehova, NW] Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote.”—Marko 12:29, 30; Kumbukumbu la Torati 6:4, 5.

4, 5. Ni nani wapaswao kuonwa kuwa waaminifu, na uaminifu wapasa kuonyeshwaje?

4 Mfanya kazi mmoja wa makao makuu ya Mashahidi wa Yehova hivi karibuni alimwambia F. W. Franz, msimamizi wa Watch Tower Society mwenye umri wa miaka 98 ambaye ametumia miaka zaidi ya 70 katika utumishi wa wakati wote: “Umekuwa mfano mzuri wa uaminifu, Ndugu Franz.” Na Ndugu Franz akajibu: “Naam! ni lazima uwe mwaminifu.” Hilo latoa muhtasari wa jambo hilo. Katika sehemu yoyote ya utendaji wa Ufalme tunapotumikia, twaweza kuwa waaminifu.—1 Wakorintho 4:2; Wagalatia 3:9.

5 Ni kweli, wengi wangependa kufanya zaidi sana katika utumishi wa Yehova, lakini madaraka ya Kimaandiko au matatizo ya afya huenda yakawazuia kwa njia fulani. Hata hivyo, wale wasioweza kupainia hawapaswi kuonwa kuwa si waaminifu sana. Wengine wamebaki waaminifu chini ya hali zenye kujaribu sana na mara nyingi kwa miaka mingi sana. Naam, wao wamekuwa waaminifu! Wamempenda Yehova na kutumikia kwa bidii katika utegemezo wa moyo wote wa mipango yake ya kitheokrasi. Wamependezwa sana na utendaji wa mapainia na kuwapa kitia-moyo wale wawezao kuwa mapainia, mara nyingi watoto wao wenyewe, wajitahidi kufanya upainia kazi-maisha inayopita zote nyinginezo.—Linganisha Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.

6, 7. Mfano uliowekwa kwenye 1 Samweli 30:16-25 unatumikaje leo?

6 Utendaji wa umoja wenye upendo wa watu wote wa Mungu huenda ukatolewa kielezi na ule usimulizi kwenye 1 Samweli 30:16-25. Katika vita dhidi ya Waamaleki, “Daudi akawapiga tangu ukungu wa jioni hata jioni ya siku ya pili” na kutwaa nyara nyingi. Waliporudi kwenye kambi, wanaume wengine wa Daudi wa vita waliomba kwamba wale ambao hawakwenda nao katika vita kali wasipewe sehemu yoyote ya nyara. Lakini Daudi akajibu hivi: “Ni nani atakayewasikiliza ninyi katika jambo hili? kwa kuwa kama lilivyo fungu lake yeye ashukaye vitani, ndivyo litakavyokuwa na fungu lake huyo akaaye karibu na vyombo; watagawiwa sawasawa.”

7 Kanuni iyo hiyo yatumika leo. Mapainia wako mbele kabisa katika vita yetu ya kiroho. Lakini wote wengine kundini hutoa utegemezo wenye uaminifu-mshikamanifu wa moyo wote. Na tokeo kuu la utendaji wao wa pamoja katika 1991 umeonyeshwa katika chati ifuatayo.

Ripoti Yenye Kutokeza

8. (a) Ripoti ya ulimwenguni pote inaonyesha nini kuhusu jumla ya wahubiri na saa walizotumia katika utumishi wa Yehova? (b) Wewe unaona mambo gani ya kupendeza kwa nchi zilizotokea kwa mara ya kwanza katika ripoti?

8 Naam, kurasa nne zifuatazo za gazeti hili zinaonyesha jinsi jitihada za umoja za waabudu wote wa Yehova wenye bidii zimechangia upanuzi wenye kusisimua wa ulimwenguni pote katika 1991. Kilele kipya kizuri sana cha wahubiri wa Ufalme 4,278,820 kinarekodiwa—ongezeko la asilimia 5.9. Hao walitoa saa 951,870,021 (zaidi ya bilioni moja kwa mara ya kwanza!) kwa utumishi. Na ebu ona jitihada kubwa iliyowekwa na ndugu zetu katika nchi zilizokuwa na vizuizi lakini sasa zinatokea kwa mara ya kwanza katika ripoti ya ulimwenguni pote—Angola, Bulgaria, Chekoslovakia, Romania, Urusi na nyingine nyingi.

9, 10. (a) Mapainia wameitikiaje jaribu la nyakati zilizo ngumu? (b) Ni kitia-moyo gani kinachoandaliwa kwa ajili ya kuingia utumishi wa painia?

9 Katika miaka ya karibuni roho ya upainia imeenea kotekote ulimwenguni. Hata katika nchi ambapo uhuru wa ibada umepewa hivi karibuni tu, idadi ya mapainia inaongezeka. Hali ngumu za kiuchumi haziwazuii Mashahidi hawa walio thabiti wasitoe kila kitu walicho nacho kwa ibada ya Yehova. (Linganisha 2 Wakorintho 11:23, 27.) Kwa wastani wa kila mwezi, asilimia 14 ya wahubiri wote wa Ufalme wamekuwa wakipainia. Kilele cha mapainia ni 780,202 ambacho ni asilimia bora sana ya 18 ya wahubiri wote.

10 Waonapo shangwe ambazo mapainia hupata, wengine pia hutiwa moyo wachukue utumishi huo. Ikiwa wewe haupainii bado, je, upendo wako kwa Yehova waweza kukusukuma useme, kama tunavyosoma kwenye Isaya 6:8, “Mimi hapa, nitume mimi”? Au kupitia funzo lako la Biblia lenye bidii, je, Neno la Mungu laweza kuamsha tamaa yenye kuchoma moyoni mwako, ili kwamba ni lazima tu uchukue hatua ya zaidi ya kuingia katika utumishi wa upainia? Hata katika wakati wa jaribu, neno la Yehova lilimchochea Yeremia hivi kwamba hakuweza kujizuia.—Yeremia 20:9.

Utumishi wa Upendo kwa Ainabinadamu

11. Utendaji wa funzo la Biblia nyumbani limesitawije?

11 Moja kati ya sehemu zenye kutokeza za ripoti ya mwaka ni ongezeko katika idadi ya mafunzo ya Biblia nyumbani yasiyo ya malipo, 3,947,261, yakiongozwa kwa ukawaida kila mwezi ulimwenguni pote. Huo ni mpango wa upendo ambapo Mashahidi wa Yehova hutoa msaada wa ziada kwa watu wenye kupendezwa wanaokuta katika kazi yao ya nyumba kwa nyumba. Tunafurahi kuongoza mafunzo ya Biblia pamoja na watu wa mataifa na malezi yote ya rangi, tukifanya kazi na bidii ile ile ambayo mtume Paulo alionyesha. ‘Kutoa ushahidi kwake kikamili kwa Wayahudi na kwa Wagiriki pia’ bila shaka kulihitaji saa nyingi za kufundisha kweli. (Matendo 20:20, 21, NW) Ni vivyo hivyo leo. Mashahidi wa Yehova husaidia “watu wote [wa aina zote, NW] waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli.”—1 Timotheo 2:4.

12-14. Ni ripoti gani za shangwe zinazotoka Ulaya?

12 Ripoti za ongezeko la utendaji wa funzo la Biblia katika Ulaya Mashariki ni zenye kusisimua kama nini! Kwa miongo mingi ndugu zetu huko walilazimika wakutane katika vikundi vidogo, wakiwa labda na nakala moja iliyochakaa ya Mnara wa Mlinzi ya zamani iliyonakiliwa itumiwe na wote katika kikundi. Lakini sasa Biblia na vichapo vingi vya Biblia vinapelekwa nchi hizo kwa wingi. Inakumbusha mtu juu ya Wimbo Ulio Bora 2:4, King James Version: “Yeye [Yesu Kristo] alinileta kwenye nyumba [ya kiroho] ya karamu, na bendera yake juu yangu ilikuwa upendo.” Wakiwa na nakala zao za kibinafsi za magazeti, wengi wanatayarishwa vizuri kulitumia “kwa halali neno la kweli.”—2 Timotheo 2:15.

13 Kundi la wahubiri 103 katika St. Petersburg, Urusi, hivi karibuni waliripoti mafunzo ya Biblia nyumbani zaidi ya 300. Kama mazao ya jitihadi hiyo ya funzo la Biblia, Mashahidi wapya 53 walibatizwa katika miezi minane tu. Zaidi ya nusu ya kundi hilo wamekuwa katika kweli miezi minane au michache zaidi! Na hawana wazee wowote—wana mtumishi wa huduma mmoja tu wa kushughulikia maendeleo yao ya kiroho.

14 Mhubiri wa Ufalme katika Estonia aliulizwa na mwanafunzi wa Biblia kama angeweza kukaribisha rafiki zake wengine kwenye funzo. Shahidi alipowasili nyumba hiyo juma lifuatalo, alipata watu zaidi ya 50 wakiwa wamekusanyika! Bila shaka, mipango ya pekee ilihitajiwa ili kuendelea kutunza kupendezwa huko kote.

15. Ni nini chaweza kusemwa kuhusu hudhurio la Ukumbusho na ubatizo?

15 Wengi wanaojifunza hupata mwonjo wao wa kwanza wa ushirika wa Kikristo kwa kuhudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Mwaka huu uliopita, hudhurio lilipita 10,000,000 kwa mara ya kwanza, 10,650,158 wakihudhuria ulimwenguni pote katika makundi 66,207 kwa ajili ya pindi hiyo yenye shangwe. Katika nchi kadhaa za Amerika ya Kilatini, Afrika, na Ulaya Mashariki, kulikuwako mahudhurio ya mara tatu au nne zaidi ya idadi ya wahubiri wa Ufalme. Sasa ni lazima tuanze kujitayarisha kwa ajili ya Ukumbusho utakaofanywa mwaka huu Ijumaa Aprili 17. Inatumainiwa kwamba hesabu kubwa ya wanafunzi wa Biblia wapya watakaohudhuria Ukumbusho wataendelea kufanya maendeleo kuelekea ubatizo. Kwa habari ya ubatizo, katika 1991 kilele kipya cha 300,945 walifananisha wakfu wao kwa Yehova Mungu kwa kuingizwa majini. Hilo lilikuwa ongezeko la asilimia X zaidi ya 1990.

Wapendao Uhuru wa Kimungu

16. Ni ripoti gani zenye kusisimua zitokazo kwenye “Wapendao Uhuru” Mikusanyiko ya Wilaya?

16 Sehemu inayostahili kuangaliwa ya mwaka wa utumishi wa 1991 imekuwa ule mfululizo wa “Wapendao Uhuru” Mikusanyiko ya Wilaya, ulioisha sasa katika kizio cha Kaskazini lakini unaoendelea hadi 1992 katika kizio cha kusini. Kwa mara ya kwanza, programu kamili ya mkusanyiko ilitolewa katika nchi kadhaa za Ulaya Mashariki, ambako ndugu zetu wanashangilia kutumia huru zao zilizopatikana karibuni kwa sifa ya Yehova. Hudhurio la jumla ambalo limeripotiwa hadi sasa kwenye mikusanyiko 705 katika nchi 54 ni 4,774,937.

17, 18. (a) Ni uhuru gani mbalimbali unaoonewa shangwe na kutazamiwa na waabudu wa Yehova? (b) Uhuru wa kimungu unatofautianaje na uhuru mbalimbali wa kilimwengu?

17Yesu Kristo aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Kweli itawaweka huru.” (Yohana 8:32) Leo, kweli ya Biblia imeweka mamilioni huru na mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo. Mamilioni haya wamejifunza kwamba maandalizi ya Yehova ya fidia ya dhabihu ya Yesu itawezesha ainabinadamu ‘iwekwe huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata iingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.’ (Warumi 8:19-22) Huo utakuwa uhuru mtukufu kama nini—kuishi milele katika dunia paradiso ndani ya mipaka inayofaa ambayo Yehova ataamua kwa upendo!—Isaya 25:6-8; linganisha Matendo 17:24-26.

18 Uhuru mbalimbali ambao Mashahidi wa Yehova wanaonea shangwe leo, na wanaotazamia kuonea shangwe kwa wingi katika mfumo mpya wa mambo wa Mungu, hutoka kwa Mungu wetu, Yehova. (2 Wakorintho 3:17) Hautegemei harakati yoyote ya kisiasa au ya kimapinduzi. (Yakobo 1:17) Kujilinda dhidi ya kutoelewana kokote juu ya jambo hilo, beji za mkusanyiko wa 1991 zilizovaliwa na Mashahidi wa Yehova katika nchi nyingine za Mashariki mwa Ulaya zilikuwa na maneno: “Wapendao Uhuru wa Kimungu Mkusanyiko wa Wilaya.”

Upendo Mwingi kwa Yehova

19. Ushirika wa kindani wa sala pamoja na Yehova unatutegemezaje?

19 Kumpenda kwetu Yehova na kumtumaini kwetu kutatuwezesha tukae karibu naye katika sala. Ni ushirika huo wa kindani pamoja na Yehova ambao umesaidia ndugu zetu wavumilie magumu na minyanyaso mingi. (Zaburi 25:14, 15) Katika saa yake ya kujaribiwa sana, Yesu alidumisha ushirika wa kindani pamoja na Baba yake kupitia sala. (Luka 22:39-46) Ukaribu wa jinsi hiyo pamoja na Yehova kupitia sala ulimtegemeza Stefano katika maumivu makali ya kufia-imani kwake. Akitazama mbinguni alipokaribia kupigwa kwa mawe hadi kifo, alisema hivi: “Tazama! naona mbingu zimefunguka, na Mwana wa Adamu amesimama mkono wa kuume wa Mungu.”—Matendo 7:56.

20-22. Ono moja linaonyeshaje kwamba Mungu husikia sala?

20 Kama vile Mashahidi wa Yehova wameona mara nyingi sana, Yehova hujibu sala zinazopatana na mapenzi yake. Kwa mfano, katika nchi ya Afrika ambako kazi ya Mashahidi imepigwa marufuku, painia wa pekee aliyekuwa akisafiri kwenda kaskazini kwa basi alikuwa na gunia kubwa la vichapo vya Ufalme na barua za kukabidhi. Mtumishi aliyekuwa akiweka vyombo kwenye basi alimwuliza ndugu hivi: “Gunia hili lina nini?” Ndugu alisema jambo la kwanza lililokuja akilini mwake: “Barua.”

21 Njiani, basi hilo lilipita kasi kituo cha uchunguzi wa kawaida cha magari, na mapolisi wa kusimamisha magari wakaanza kulifukuza basi hilo na wakalisimamisha, wakishuku kwamba lilikuwa limebeba bidhaa zilizopigwa marufuku. Waliamuru kwamba maabiria wote watoke kwenye basi na kwamba mizigo yote ichunguzwe. Hilo lilikuwa tatizo! Ndugu alitembea mwendo mfupi kutoka kwa umati wenye kunung’unika na, akipiga magoti, alisali kwa Yehova. Alipojiunga na umati, mzigo wa kila abiria ulikuwa ukifunguliwa na kuchunguzwa kwa uangalifu mwingi sana. Gunia la ndugu lilipokuja kufunguliwa, alimwomba Yehova msaada kwa kimya.

22 “Gunia hili ni la nani, nalo lina nini?” polisi akasema kwa sauti. Kabla ya ndugu kuweza kusema lolote, mtumishi wa basi akajibu na kusema: “Ni barua kutoka ofisi ya posta ya _ kwenda ofisi ya posta ya _.” “Vema,” ofisa akasema. Aliinua gunia hilo na kumpa mtumishi huyo. “Hakikisha unaliweka mahali palipo salama sana kwa ajili ya safari,” akamwamuru. Painia huyo wa pekee akapiga magoti tena kumshukuru Msikiaji wa sala.—Zaburi 65:2; Mithali 15:29.

23. Yehova ameonyesha nini, na bado ni kwa nini nyakati nyingine anaacha mnyanyaso uendelee hadi mwisho?

23 Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba waabudu wa Yehova wako huru kabisa na matukio ya maafa. Katika hali fulani, katika nyakati za Biblia na leo pia, Yehova ameonyesha kwamba yeye aweza kuwakomboa watu wake. Lakini kwa kupatana na kusuluhisha swala la uaminifu wa kimaadili, yeye nyakati nyingine huonekana kana kwamba aacha mnyanyaso uendelee hadi mwisho. (Linganisha Mathayo 26:39.) Zaidi ya hayo, Yehova hawalindi watu wake na aksidenti, ugomvi wa wenyewe kwa wenyewe, au uhalifu, kivivi hivi tu ingawa kuzoea hekima yenye kutumika ya msingi wa Biblia kwaweza kuwa kwenye thamani. (Mithali 22:3; Mhubiri 9:11) Lakini, twaweza kuwa na uhakika kwamba tukombolewe au tusikombolewe katika hali zenye kujaribu, uaminifu wetu utathawabishwa hata kwa ufufuo ukihitajiwa.—Mathayo 10:21, 22; 24:13.

24. Yehova ameandaa zawadi gani zenye upendo, na twaweza kuitikiaje upendo wake?

24 Zawadi za Yehova zenye upendo ni nzuri ajabu kama nini! Zawadi yake kwa ainabinadamu ya dunia hii na kila kitu kilicho juu yake ni wonyesho wenye kutokeza wa upendo wake. (Zaburi 104:1, 13-16; 115:16) Na zawadi ya Mungu yenye huruma ya Mwana wake, Yesu Kristo, ili kufidi ainabinadamu kutoka dhambi na kifo ni zawadi yenye upendo zaidi iliyopata kutolewa kwa wakati wowote. “Katika hili pendo la Mungu lilionekana kwetu, kwamba Mungu amemtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa yeye. Hili ndilo pendo, si kwamba sisi tulimpenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu.” (1 Yohana 4:9, 10) Kwa kuitikia upendo huo, na tusadikishwe “kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”—Warumi 8:38, 39.

Kupitia Makala Hii

◻ Inamaanisha nini kuwa mwaminifu?

◻ Twaweza kuonyesha upendo kwa Yehova katika sehemu gani za utendaji?

◻ Ni sehemu gani za ripoti ya mwaka wa utumishi zilizokupendeza zaidi?

◻ Twaweza kuonyeshaje uthamini wetu kwa zawadi za Yehova zenye upendo?

[Sanduku katika ukurasa wa 15]

KWA NINI KUNA MAPAINIA WENGI JINSI HIYO?

Kulingana na ripoti, kwa miaka 2,600 Wajapani walikuwa waabudu wenye bidii sana wa maliki wao. Katika vita vya karne hii ya 20 pekee, wanaume wa vita Wajapani zaidi ya milioni tatu walidhabihu maisha zao, kwani walifikiri hakukuwa heshima kubwa zaidi ya kufa kwa ajili ya mungu-maliki. Lakini tabia ya kutaka vita ya Kibuddha na Kishinto ilishindwa katika Vita ya Ulimwengu 2, na baada ya hapo maliki alikana uungu wake. Ni nini kingejaza hali hiyo ya kidini iliyo wachwa wazi? Kwa furaha, mafunzo ya Biblia nyumbani yaliyoongozwa na wamisionari wa Mashahidi wa Yehova na baadaye na Mashahidi wa huko yalisaidia wengi wapate Mungu wa kweli, Yehova, na waweke maisha zao wakfu kwake. Wakfu huo una maana sana kwa Mashahidi hao Wajapani. Ikiwa katika nyakati za zamani wangalidhabihu maisha zao kwa mungu-maliki, sasa wanatoa nishati zao kwa bidii kubwa zaidi kadiri gani wakiwa mapainia katika kumwabudu Mungu na Muumba wa ulimwengu wote mzima aliye hai—Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova!

[Chati katika ukurasa wa 10-13]

1991 SERVICE YEAR REPORT OF JEHOVAH’S WITNESSES WORLDWIDE

(Ona buku lililojalidiwa)

[Picha katika ukurasa wa 16]

Wapendao uhuru wa kimungu —Waabudu wa Yehova kwenye mkusanyiko katika Prague, Agosti 9-11, 1991

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki