Jihadharini na Manabii Wawongo!
WENZI wa ndoa Wabrazili walikuwa wameenda kulala waliposikia wevi wakivunja na kuingia nyumbani mwao. Wenzi hao wa ndoa wenye hofu nyingi walifaulu kuepa kupitia dirisha la chumba cha malazi na kuita polisi. Lakini baadaye mke alikuwa amefadhaishwa sana na jambo hilo hivi kwamba hangeweza kulala katika nyumba hiyo na akalazimika kwenda kwa mama yake.
Yeyote ambaye amewahi kuvunjiwa nyumba yake au ambaye amepokonywa katika njia yoyote ile atamhurumia. Mwono kama huo waweza kuwa wenye kusumbua, na, kwa kuhuzunisha, watu wengi zaidi wanaumia katika njia hiyo. Hata hivyo, kuna aina ya wivi yenye matokeo mabaya zaidi.
Ni nini aina hiyo ya wivi ulio mbaya zaidi, na ni nani walio wevi? Yesu Kristo alitupa habari fulani juu ya hiyo wakati, alipokuwa akizungumza juu ya siku yetu, alisema: “Na manabii wengi wa uongo watatokea, na kudanganya wengi.” (Mathayo 24:11) Manabii wawongo ni wevi. Kwa njia gani? Wanaiba nini? Kuiba kwao kunalinganishwa na kutoa kwao unabii. Kwa hiyo ili kuelewa jambo hilo vizuri, twahiji kwanza kujua kutoa unabii ni nini kulingana na Biblia.
Linalomaanishwa na Kutoa Unabii
Unapofikiria juu ya kutoa unabii, labda jambo la kwanza linalokujia akilini ni kule kutabiri juu ya wakati ujao. Huku kwa kweli kulikuwa sehemu ya kazi ya manabii wa Mungu wa zamani, lakini haikuwa kazi yao ya msingi. Kwa mfano, nabii Ezekieli alipoambiwa katika njozi ‘atabirie upepo,’ alipaswa tu atoe amri kutoka kwa Mungu. (Ezekieli 37:9, 10) Yesu alipokuwa katika jaribu mbele ya makuhani, alitemewa mate na kupigwa makofi na wanyanyasi wake wakasema kwa mzaha: “Tabiri kwa sisi, wewe Kristo; Ni nani aliyekupiga?” Hawakuwa wakimuuliza Yesu awatabirie wakati ujao. Walikuwa wanamjaribu Yesu atambulishe kwa uwezo wa Mungu wale ambao walikuwa wamempiga.—Mathayo 26:67, 68, ZSB
Kwa kweli, linalotokezwa na maneno ya lugha ya Biblia ya kwanza yanayotafsiriwa ‘kutoa unabii’ au “unabii” kwa msingi ni kusema mawazo ya Mungu kuhusu jambo au, kama vile kitabu cha Matendo kielezavyo, kusema “matendo makuu ya Mungu.” (Matendo 2:11) Ni katika njia hiyo kwamba watu wengi wanapokonywa na manabii wawongo.
Ni nani, basi, walio manabii wawongo, na wanaiba nini? Ili kujibu swali hilo, acheni tuangalie nyuma katika historia ya taifa la Israeli hadi wakati wa Yeremia.