Wewe Waweza Kukabiliana na Fadhaiko!
EBU fikiria hali yenye kuhuzunisha ya mwanamume fulani mwenye umri wa miaka 23. Yeye ana elimu kidogo tu na anafanya kazi ya mshahara wa chini kabisa. Ndoa na maisha yenye kuridhisha ni mambo yasiyofikirika kwake. Si ajabu kwamba mama yake asema: “Yeye amehuzunika na kufadhaika sana.” Hali ya kijana huyo ni jambo la kawaida linalowapata mamilioni ya wengine. Kwa sababu moja au nyingine, watu katika tabaka zote za maisha wanafadhaika.
Fadhaiko ni “hisia au hali yenye kudumu sana ya kutokuwa na usalama, kuvunjika moyo, na kutoridhika kunakotokana na tamaa zisizofaulu, mabishano ya kindani, au matatizo mengineo yasiyosuluhishwa.” (Webster’s Third New International Dictionary) Sisi hupatwa na fadhaiko tunapojitahidi sana kutimiza jambo fulani lakini hatufaulu. Twaona tumezuiwa kila upande, kana kwamba twapigisha kichwa chetu kwenye ukuta wa mawe, bila uwezo wa kufaulu. Sisi sote twajua hisia hiyo.
Wale wanaofanya kazi zinazoonekana kutoridhisha huenda wakawa na hisia za kutofaa kitu. Wasipoonyeshwa shukrani, wake au akina mama wanaong’ang’ana na mahangaiko ya kila siku na wajibu mbalimbali wenye kuchosha huenda wakahisi hawakutimiza lolote, na hawathaminiwi. Vijana wanaokabili majaribu shuleni huenda wakahisi kufadhaika wanapojitahidi kupata elimu. Washiriki wa vikundi vinavyobaguliwa huenda wakahisi kuudhika na kukosa furaha, wakisadiki kwamba wanabaguliwa isivyo haki. Wafanya biashara wanaojaribu kwa unyoofu kuandaa bidhaa au utumishi ulio bora huenda wakafilisishwa na washindani wabaya na wasiofuata haki. Maono hayo na mengine yanayofanana na hayo husababisha fadhaiko na huwaacha wengi wakiwa na hisia za kukosa tumaini.
Mwanamume mmoja mwenye hekima aliyeishi karne kadhaa zilizopita aliweza kuonyesha mafadhaiko yake kwa maneno tuwezayo kuelewa. Mfalme wa Waisraeli Sulemani alisema hivi: “Kisha nikaziangalia kazi zote zilizofanywa kwa mikono yangu, na taabu yote niliyotaabika katika kuzitenda; na tazama, yote ni ubatili na kujilisha upepo, wala faida hakuna chini ya jua. Kwa maana mtu hupata nini kwa kazi yake yote, na kwa juhudi ya moyo wake alivyojitahidi chini ya jua? Kwa kuwa siku zake zote ni masikitiko, na kazi yake ni huzuni; naam, hata usiku moyoni mwake hamna raha. Hayo nayo ni ubatili.” (Mhubiri 2:11, 22, 23) Maneno ya Sulemani huonyesha kule kukata tamaa ambako wengi sana huhisi katika kujaribu kukabiliana na mafadhaiko yanayowanyang’anya maisha yenye kuridhisha.
Watu waliofadhaika huenda hata wakakata tamaa. Katika hali mbaya sana baadhi yao wameacha kung’ang’ana, wakiacha kuishi maisha ya jamii ya kawaida na kuishi mtindo-maisha usio wa kawaida. Ili kupata kile wanachohisi wanastahili, wengine wametumia uhalifu na jeuri. Mibano isiyopungua imevunja-vunja ndoa na vifungo vya familia.
Huenda ikawa wengi wetu tumejitahidi sana kupata njia za kukabiliana na fadhaiko. Yajapokuwa yale tunayofanya, mambo huenda yakaonekana kuwa mabaya zaidi. Mithali 13:12 husema hivi: “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua.” Hali njema yetu ya kimwili na ya kiroho huenda ikawa hatarini. Je! hali inakosa tumaini? Je! ni lazima tuishi tukiwa na fadhaiko la daima likiwa adhabu kwa ajili ya kukosa kwetu utoshelevu au makosa yetu? Je! hatua zinazofaa zaweza kuchukuliwa za kukabiliana na fadhaiko ili kuonea shangwe maisha yenye kuridhisha zaidi? Ebu tuone.
Baadhi ya Njia za Kukabiliana na Fadhaiko
Tunapokuwa na tatizo na twahitaji shauri, sisi kwa kawaida humwendea mtu mwenye maarifa, aliye na ujuzi ambaye twaweza kumtumaini. Mithali 3:5, 6 hupendekeza hivi: “Mtumaini BWANA [Yehova, NW] kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” Shauri lifaalo laweza kupatikana katika Neno la Mungu, Biblia. Ebu fikiria baadhi ya mifano ya mwono-ndani inayoandaa.
Fadhaiko huenda ikahusiana na kupata riziki. Kwa mfano, kazi yetu ya kimwili huenda ikaridhisha, lakini mshahara wa chini waweza kuwa chanzo cha mshuko wa moyo. Tunazipenda familia zetu na twataka zipate yaliyo bora kabisa. Hata hivyo, yaonekana hakuna mwisho wa hangaiko juu ya kutimiza wajibu wetu wa kifedha. Huenda tukafanya kazi ya baada ya wakati na hata kuanza kazi ya pili. Baada ya muda fulani maisha yanaonekana kuwa mrudio wenye kuchosha wa kula, kulala, na kufanya kazi. Na bado, gharama zazidi kuwa nyingi, madeni yaongezeka, na fadhaiko lazidi.
Kusudi hasa la kazi ya kimwili ni kuandaa mahitaji yetu. Lakini tunahitaji kiasi gani hasa? Mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu; ila tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo.” Je! tunajaribu kupata zaidi ya hivyo na kupata vilivyo sawa na vya wengine au kufanya mambo wanayoweza kufanya? Ikiwa ndivyo huenda ikawa tunavuna matokeo ya hayo kwa namna ya fadhaiko. “Lakini hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:7-10) Kadirio lenye unyoofu la ufuatiaji wetu mali za kimwili huenda likafunua mambo ambayo hatuhitaji kwa lazima. Marekebisho machache yafaayo kuelekea uwekevu na mtindo-maisha wenye kiasi zaidi huenda yakasaidia sana kupunguza fadhaiko letu.
Tamaa za kiasili zisizotimizwa zimesababisha fadhaiko jingi. Kwa mfano, ni jambo la asili kwa mwanamke kijana kuwa na hamu sana ya kufunga ndoa na kuwa na usalama na shauku yenye uchangamfu inayotokana na maisha ya familia. Huenda akatumia wakati na juhudi nyingi ili kujifanya mwenyewe awe wa kuvutia zaidi kwa mitindo ya karibuni zaidi au vifaa vya kujirembesha na huenda akawa msomaji mwenye bidii wa magazeti yatolewayo kwa kawaida yanayotoa mashauri kwa wasio na wapenzi. Mwanamke huyo huenda akahudhuria kikusanyiko kimoja baada ya kingine akitumaini kukutana na mtu afaaye—bila kufanikiwa. Miaka yapita, na fadhaiko lawa lenye kutovumilika. Kwa kukata tamaa huenda akashawishwa kufunga ndoa na mtu asiyefaa. Vibaya hata zaidi, ili kuridhisha tamaa yake ya kupata shauku, huenda akahusika katika mwenendo unaokosa maadili.
Katika hali kama hiyo, saburi na uamuzi mzuri ni mambo ya muhimu. Kufunga ndoa na mtu asiyefaa—hasa mmoja akosaye imani katika Yehova—kungekuwa kosa zito. (1 Wakorintho 7:39; 2 Wakorintho 6:14, 15) Ukosefu wa maadili bila kuepukika huongoza si kwenye jambo jingine ila uchungu wa moyoni na kukata tamaa. (Mithali 6:32, 33) Kujichunguza mwenyewe kwa unyoofu, pamoja na njia ifaayo ya kushughulika na jambo hilo, kwaweza kusaidia. “Roho ya upole na utulivu” yaweza kuvutia aina ya mwenzi wa ndoa afaaye bora zaidi ya vile mavazi ya kimtindo au virembeshi visivyo vya kawaida viwezavyo. (1 Petro 3:3, 4) Badala ya kutegemea shauri la wastadi wa kilimwengu ambalo mara nyingi hukosa busara au si lenye maana, ni muhimu kumwendea Mwanzilisi wa ndoa ili kujifunza lile linalohitajiwa ili kuwa mke anayependwa na kuthaminiwa. (Mithali, sura 31) Wanaume na wanawake wasiofunga ndoa wanapaswa wajaribu kuonyesha sifa ambazo wangetamani katika mwenzi. Ni jambo la hekima kama nini kutafuta ushirika unaofaa pamoja na watu wanaostahi kanuni za Biblia. Tukizitumia hizo maishani, mataraja yetu kwa ajili ya ndoa yenye furaha yatakuwa mazuri sana. Hata kama ndoa haitokei mara moja, kutenda kulingana na Maandiko kutaleta shangwe na kufanya maisha ya useja kuwa yenye kuthawabisha sana.
Furushi kubwa la wajibu huenda likatufikisha hadi hatua ya kuwa na uchungu mwingi. Huenda kukawa na mbano kutoka pande zote. Tuna mahangaiko juu ya mahitaji makubwa ya familia yetu, na huenda mwajiri wetu asitosheke kamwe. Watu wa ukoo huenda wakatutazamia tuwasaidie kila wakati ambapo kuna tatizo. Kwa sababu ya mibano mingi, orodha ndefu ya mambo ya kibinafsi yanahitaji tuyaelekezee fikira. Huenda ikaonekana kwamba wakati na nishati zetu zinapaswa kuelekezwa kwenye mambo mengi tofauti-tofauti kwa wakati uleule. Fadhaiko laweza kugeuka kuwa uchungu mwingi, na huenda tukahisi kukata tamaa. Kwa hiyo, tufanye nini?
Tungekuwa wenye hekima kukadiria tena mambo tupaswayo kutanguliza. Kwa kuwa twaweza kufanya kiasi fulani tu cha mambo, haiwezekani kufanya kila jambo ambalo wengine wanataka. Tunahitaji kupunguza mambo yawe yale tu “yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:10, NW) Kwa vyovyote vile, “ni afadhali mbwa aliye hai kuliko simba aliyekufa.” (Mhubiri 9:4) Baadhi ya wajibu ni wa lazima na hauwezi kuwekwa kando, huku ule usio wa muhimu sana huenda ukahitaji kungojea. Huenda ikawa tumejitwalia daraka kamili kwa wajibu ambao wapaswa kushirikiwa na wengine. Baadhi ya madaraka huenda yakahitaji kuondolewa kabisa ikiwa si ya lazima. Ingawa hilo huenda mwanzoni likawasababishia wengine usumbufu au kuwatamausha, tunahitaji kujali mipaka yetu wenyewe ya kimwili na ya kihisiamoyo.
Ugonjwa wenye kudhoofisha waweza kusababisha fadhaiko lenye kuumiza sana, kwani waweza kutulaza kitandani kwa siku au majuma kadhaa kwa wakati. Maumivu makali yaweza kutuhuzunisha. Tukitafuta-tafuta tiba, huenda tukamwendea daktari mmoja hadi mwingine au huenda tukameza dawa au vitamini nyingi tukitumaini kwamba zitasaidia. Hata hivyo, huenda tukaendelea kuteseka na huenda tukaanza kushangaa kama kweli maisha yanastahili.
Hilo huenda likawa tatizo liwezalo tu kusuluhishwa katika ulimwengu mpya wa Mungu. (2 Petro 3:13; linganisha Isaya 33:24.) Kwa kuwa wanadamu si wakamilifu, madaktari na dawa zaweza kusaidia kwa kadiri fulani tu. Wakati mmoja huenda tukahitaji kukubali kuteseka kwetu kuwa sehemu ya maisha. Mtume Paulo alikuwa na “mwiba katika mwili,” labda taabu ya macho yake au sehemu nyingine ya mwili wake, yenye kutatiza sana hivi kwamba alisali tena na tena ili kupata kitulizo. (2 Wakorintho 12:7-10) Lakini Mungu hakumponya Paulo, na labda mtume huyo alihitaji kuvumilia taabu hiyo hadi kifo chake. Aliishi na kule kuteseka kwake, na hakuomba asikitikiwe, wala hakupoteza kamwe shangwe yake. (2 Wakorintho 7:4) Ingawa yule mtu mnyoofu Ayubu alipatwa na taabu nyingi, alidumisha imani yake katika Yehova, na hilo liliongoza kwenye thawabu nyingi. (Ayubu 42:12, 13) Ikiwa sisi ni watumishi wa Mungu, twaweza kupata nguvu ya kuendelea kwa kutafakari juu ya mifano hiyo na kusali ili kupata msaada wa Yehova.—Zaburi 41:1-3.
Wenye Nguvu Yajapokuwa Mafadhaiko
Watu wa Yehova waweza kuwa na nguvu kiroho yajapokuwa mafadhaiko mengi. Kwa mfano, ingawa huenda tukahitaji kuvumilia ugonjwa, twaweza kubaki “wazima katika imani” kwa kujinufaisha kikamili kutokana na maandalizi ya Mungu ya kiroho. (Tito 2:1, 2) Ingawa huenda tukawa maskini wa mwisho kimwili, twaweza kuwa tajiri ajabu kiroho.
Kwa kumtegemea Mungu ili kupata hekima na nguvu, twaweza kukabiliana na mafadhaiko ambayo huenda yakatokea katika hali za kinyumbani. Kwa mfano, fikiria Abigaili, mke wa Nabali. Nabali alikuwa “mwovu katika matendo yake,” na jina lake lenyewe humaanisha “-pumbavu; -jinga.” Ni lazima liwe lilikuwa jambo la kufadhaisha kama nini kuishi na mtu kama huyo! Hata hivyo, Abigaili alibaki “mwenye akili njema” na hakukata tamaa. Kwa kweli, maneno na matendo yake yalikuwa yenye busara sana wakati wa tatizo moja hivi kwamba alimsadikisha Daudi asilipe matukano na ukosefu wa shukrani wa Nabali kwa kumwaga damu na kushindwa kutumaini katika Yehova.—1 Samweli 25:2-38.
Hata ikiwa hali inayomhusu mtu fulani anayeshirikiana na kundi la Kikristo inatusababishia fadhaiko, twaweza kuvumilia katika nguvu ambayo Mungu hutoa. Hilo laonyeshwa na uhakika wa kwamba mwenendo wa Diotrefe ambao ungeweza kusababisha fadhaiko haukumzuia yule mtu mwenye kumcha Mungu Gayo asifanye mema na hivyo kuvuna furaha na thawabu nyingi za kiroho.—Matendo 20:35; 3 Yohana 1-10.
Fadhaiko lingeweza kutokea ikiwa tungetamani kuwatumikia waamini wenzetu katika kundi lakini tusichaguliwe wakati wengine wanawekwa rasmi kuwa wazee au watumishi wa huduma. Hata hivyo, badala ya kuruhusu utamausho utushinde, acheni tujaribu kujiimarisha wenyewe kiroho na kuruhusu roho ya Mungu itokeze matunda yayo mema ndani yetu kwa kadiri kubwa zaidi. (Wagalatia 5:22, 23) Wakati wa ile miaka 40 ambayo Musa alitumia akiwa Midiani, Mungu alikuza ndani ya Musa kadiri kubwa zaidi ya upole, saburi, na sifa nyinginezo zilizohitajiwa ili kukabiliana na yale magumu na mafadhaiko ambayo angekabili akiwa kiongozi wa Waisraeli. Vivyo hivyo, huenda ikawa Yehova anatutayarisha kwa ajili ya mapendeleo ya utumishi ya wakati ujao ambayo huenda tukapokea tukibaki imara kiroho na kutoshindwa na fadhaiko.
Kitulizo Kutoka Katika Fadhaiko—Karibuni!
Mafadhaiko yetu yawe ya namna gani, je, yataisha wakati wowote? Kwetu, hali yetu huenda ikaonekana kutokuwa na tumaini lakini sivyo kwa Muumba wetu, Yehova Mungu. Hawezi kufadhaika. Kupitia nabii Isaya, Mungu alisema hivi: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.” (Isaya 55:11) Kwa kuwa Yehova ana uweza na mamlaka yote, hakuna jambo lisilowezekana kwake. (Marko 10:27) Ahadi zake za kuwaletea watu wake baraka zisizo na mwisho zitatimizwa kwa hakika.—Yoshua 21:45.
Shaka na ukosefu wa hakika ni viasili vikuu katika fadhaiko. Hata hivyo tofauti na hilo, “imani ni taraja lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa.” (Waebrania 11:1, NW) Imani katika Mungu huandaa hakikishio la kwamba matumaini yetu yote yenye msingi wa Biblia yatatimizwa kikamili. Kichwa chote cha Biblia hukazia ahadi ya Yehova ya utawala wa Ufalme, ambao chini yao dunia itakuwa paradiso kamilifu ambayo ndani yayo watu wataishi milele kwa shangwe. (Zaburi 37:11, 29) Kila jambo baya—kutia na fadhaiko—litakuwa limeondolewa mbali, kwani Mungu ‘atakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.’—Zaburi 145:16.
Mpaka baraka hizo ziwe halisi, sisi sote tutakuwa na kadiri fulani ya fadhaiko. Lakini tumaini la Kimaandiko laweza kutupa sisi moyo mkuu na imara ya kudumu. Shauri lenye busara tunalopata katika Biblia laweza kutuonyesha jinsi ya kutumia uamuzi mzuri na usababu katika njia itakayoleta usawaziko maishani mwetu na amani mioyoni mwetu. Yajapokuwa mambo yanayotutamausha, twaweza kuona “amani ya Mungu, ipitayo akili zote.” (Wafilipi 4:6, 7) Kwa hiyo lile pigano dhidi ya fadhaiko halikosi tumaini. Kwa msaada wa Yehova twaweza kukabiliana nalo leo na kulishinda wakati ujao.
[Blabu katika ukurasa wa 31]
Mungu aweza kukusaidia ukabiliane na fadhaiko, sawa na alivyowasaidia Ayubu, Musa, Abigaili, na Paulo