Wazee—Kabidhini Wengine Kazi!
YEYE alikuwa mwanamume mnyenyekevu, mwenye saburi, mwenye kufuatilia sana haki iliyotokana na mambo aliyojionea maishani. Hivyo, wanaume, wanawake, na watoto zaidi ya milioni tatu walimtazamia kwa uhakika kupata shauri. Alijaribu asiwatamaushe. Asubuhi hadi jioni, alisikiliza matatizo yao akawasaidia kwa saburi waone jinsi sheria za Mungu zilivyotumika kwa hali yao. Naam, kwa kipindi kifupi, miaka 3,500 hivi iliyopita, makabila 12 ya Israeli yalihukumiwa na mtu mmoja peke yake—Musa.
Hata hivyo, Yethro, baba mkwe wa Musa, alihangaikia jambo hilo. Musa angewezaje kudumisha mwendo wa jinsi hiyo? Kwa hiyo Yethro alijulisha hivi: “Jambo hili ufanyalo si jema. Huna budi utadhoofika wewe, na hawa watu walio pamoja nawe pia; maana jambo hili ni zito mno kwako; huwezi wewe kulitenda peke yako.” (Kutoka 18:17, 18) Suluhisho lilikuwa nini? Yethro alimshauri Musa awakabidhi wengine baadhi ya madaraka yake. (Kutoka 18:19-23) Shauri zuri!
Ndani ya kundi la Kikristo leo, kuna wazee wengi ambao, kama vile Musa, hujaribu kushughulikia mambo mengi zaidi ya vile wawezavyo kutimiza peke yao. Wao hupanga mikutano pamoja na kuitayarisha na kisha kutoa sehemu za programu katika njia ya utaratibu, yenye mafanikio. (1 Wakorintho 14:26, 33, 40; 1 Timotheo 4:13) Wazee pia hushughulikia mahitaji ya washiriki wa kundi mmoja mmoja. (Wagalatia 6:1; 1 Wathesalonike 5:14; Yakobo 5:14) Wao huiongoza ile kazi yenye maana zaidi ya kuhubiri habari njema za Ufalme. (Mathayo 24:14; Waebrania 13:7) Wao hupangia pia, ugavi wa vichapo upatikane kwa kundi ili ugawanywe kwa umma.
Kwa kuongezea, wazee wengine wanagawiwa sehemu kwenye programu za kusanyiko la mzunguko na mkusanyiko wa wilaya. Wao hutumikia katika matengenezo ya kusanyiko na hutumika kwenye halmashauri za uhusiano na hospitali. Wengine husaidia na ujenzi wa Jumba la Ufalme. Na hayo yote ni zaidi ya madaraka yao ya familia na uhitaji wao wa kujilisha wenyewe kiroho. (Linganisha Yoshua 1:8; Zaburi 110:3; 1 Timotheo 3:4, 5; 4:15, 16.) Wanaume hao Wakristo hutimizaje hayo yote? Kama vile Musa ni lazima wapate msaada. Ni lazima wajifunze kukabidhi wengine kazi. Kwa kweli, mtu asiyekabidhi wengine kazi ni mtu asiyeweza kupanga mambo vizuri.
Thamani ya Kuwazoeza Wengine
Kuna sababu nyinginezo za kukabidhi wengine daraka. Katika kielezi cha Yesu cha talanta, kabla ya bwana mkubwa kuondoka kwenda safari ya mbali, aliwaita watumwa wake na kuwakabidhi madaraka yenye viwango mbalimbali. (Mathayo 25:14, 15) Kwa kufanya hivyo, bwana mkubwa aliweza kutimiza miradi kadhaa. Kwanza, alipokuwa ameondoka, watumwa wake walitenda wakiwa mahali pake na kazi ya lazima haikufifia kisha kukoma kabisa alipokuwa ameenda zake. Pili, kwa kuwa matendo ya mtu huonyesha jinsi alivyo zaidi ya maneno yake, bwana mkubwa angeweza kuona uwezo mbalimbali na uaminifu-mshikamanifu wa watumwa wake. Tatu, bwana mkubwa aliwapa watumwa wake nafasi ya kupata uzoefu unaohitajiwa sana.
Kielezi hicho kina maana kwetu leo. Yesu alipoondoka duniani, aliwapa wanafunzi wake wapakwa-mafuta daraka. Wale kati yao waliobaki wangali na daraka la kutunza masilahi ya Ufalme ya ulimwenguni pote. (Luka 12:42) Wakati wa utumishi wa wapakwa-mafuta wa ki-siku-hizi, baraka ya Yehova juu ya tengenezo lake imeonekana wazi. Likiwa tokeo, tengenezo hilo limeongezeka kiajabu. Kwani, katika miaka mitano iliyopita pekee, wapya wengi zaidi ya milioni moja wameonyesha wakfu wao kwa ubatizo wa maji! Hilo limetokeza maelfu ya makundi na mamia ya mizunguko mipya.
Sawa na vile Yesu Kristo alivyomkabidhi madaraka “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” wao nao wamewagawia madaraka ya kundi, wazee na watumishi wa huduma wa “kondoo wengine.” (Mathayo 24:45-47; Yohana 10:16) Hata hivyo, wanaume wengine zaidi waliojiweka wakfu wanahitajiwa ili kushughulikia ule ukuzi mkubwa sana. Watatoka wapi? Ni lazima wazee wawazoeze. Lakini wazee wanawezaje kuwazoeza wanaume hao ikiwa hawawakabidhi madaraka yanayofaa watu mmoja mmoja wanaoonyesha uwezo? Wazee wanaweza kuwa na nafasi gani nyingine ya kuchunguza uwezo na ushikamanifu wa vijana?
Kukabidhi Wengine Kazi Kunamaanisha Nini?
Kwa wengine, “kukabidhi” kunamaanisha kuondoa mizigo, kuepuka, kutojali, au kujiuzulu madaraka yao. Hata hivyo, kunapotumiwa ifaavyo, “kukabidhi” kwa kweli ni njia ya kutimiza madaraka. Neno la kitenzi cha Kiingereza “to delegate” hufasiliwa kuwa, “kumwaminisha mwingine; kuweka rasmi kuwa mwakilishi wa mtu; kugawia daraka au mamlaka.” Hata hivyo, mwenye kukabidhi kazi hubaki mwenye daraka kuu la lile linalofanywa.
Wengine huenda wakasita kukabidhi wengine kazi kwa sababu wanaogopa kwamba watapoteza udhibiti. Hata hivyo, kukabidhi wengine kazi hakumaanishi kupoteza udhibiti. Ingawa haonekani na anatawala kutoka mbingu, Kristo Yesu ana udhibiti mkubwa wa kundi la Kikristo. Yeye, naye, huwaaminisha wanaume wenye ujuzi utunzi wa kundi.—Waefeso 5:23-27; Wakolosai 1:13.
Wengine huenda wasiwe na mwelekeo wa kukabidhi wengine kazi kwa sababu wanahisi kwamba wao wenyewe waweza kufanya kazi hiyo upesi zaidi. Hata hivyo, Yesu aliona thamani ya kuwazoeza wengine. Hakuna yeyote duniani aliyefundisha kwa mafanikio zaidi ya Yesu. (Yohana 7:46) Hata hivyo, baada ya kuwapa 70 kati ya wanafunzi wake maagizo, aliwatuma katika kazi ya kuhubiri. Ingawa hawakuweza kuwa sawa na Yesu katika uwezo wa kuhubiri, walirudi wakiwa na shangwe nyingi mno kwa sababu ya mafanikio yao. Yesu alishangilia pamoja nao akawapongeza, kwani alijua wangeendelea na kazi hiyo muda mrefu baada ya yeye kuondoka na hatimaye wangetimiza mengi zaidi ya yale ambayo angeweza kutimiza kwa wakati wowote akiwa peke yake.—Luka 10:1-24; Yohana 14:12.
Kukabidhi wengine kazi humaanisha pia kupata msaada katika mambo madogomadogo ya lazima. Siku kabla ya Yesu kufa, aliwapa Petro na Yohana mgawo wa kufanya mipango ya lazima kwa ajili ya mlo wake wa mwisho wa Sikukuu ya Kupitwa. (Luka 22:7-13) Yesu hakuhitaji kuhangaika juu ya kununua kondoo, divai, mkate usiotiwa chachu, na mboga chungu; wala hakuhitaji kukusanya vyombo, kuni, na vifaa vya jinsi hiyo. Petro na Yohana walishughulikia mambo hayo madogomadogo.
Wazee leo waweza kufurahia manufaa izo hizo wakiiga mfano wa Yesu. Kwa mfano, yule anayetunza vichapo huenda akaombwa aagize ugavi unaohitajiwa kwa ajili ya kampeni inayokuja. Huenda akaagizwa achanganue rekodi zake ili kuamua jinsi vifaa kama hivyo vilivyotumiwa katika kampeni zilizopita. Huenda pia akafikiria hali za eneo la kundi kabla ya kutayarisha fomu ifaayo ya kuagizia. Kisha ampe mwandishi wa kundi fomu hiyo ili aichunguze. Mtumishi wa vichapo akiisha kujifunza kazi yake, lisingekuwa jambo la lazima kwa mwandishi kuchunguza tena rekodi za wakati uliopita maadamu jumla za vichapo kwenye fomu ya kuagizia zaonekana kuwa sawa. Kwa wazi, tendo hilo sahili la kukabidhi wengine kazi lingefanya kupeleka agizo la vichapo kuwa jambo rahisi na sahili zaidi kwa wote wanaohusika.
Kwa sababu ya uwezekano huo wa kupata manufaa, mtu aweza kukabidhije wengine kazi kwa mafanikio?
Jinsi ya Kukabidhi Wengine Kazi
Fafanua kazi. Kwanza, elewesha wazi matokeo yanayotazamiwa. “Fanyeni biashara hata nitakapokuja” ndivyo yule “mtu mmoja, kabaila” katika kielezi cha Yesu cha mina alivyowaambia watumwa wake kumi. (Luka 19:12, 13) Bwana mkubwa aliwatazamia watumwa wafanye biashara na mina zao kwa njia ya kupata faida na kisha kuripoti faida zao wakati aliporudi. Walijua yale waliyohitajiwa wafanye. Kanuni hiyo ingetumikaje kwa habari ya mradi wa ki-siku-hizi wa Jumba la Ufalme? Kwa mfano, ndugu aliyepewa mgawo wa kurekebisha paa kwa kawaida angeambiwa vifaa vya kutumia, mahali pa kuvipata, na wakati wa kuanza kazi hiyo, ikiwa hali ya hewa yaruhusu. Miongozo hiyo hususa hutokeza utaratibu mzuri.
Ni jambo la maana kufafanua si lile tu linalohusika katika kazi hiyo bali pia maamuzi ambayo mtu aruhusiwa kufanya na ni mambo gani yapaswayo kurejezewa kwa mtu mwingine. Musa aliwaambia wale alioweka rasmi kwamba walipaswa kuhukumu kesi ndogo, lakini kesi ngumu zilipaswa kuletwa kwake.—Kutoka 18:22.
Unapogawa madaraka, uwe mwangalifu kuepuka kuwapa watu wawili daraka moja. Watu zaidi ya mmoja wanapogawiwa madaraka yale yale, mchafuko hutokea. Ebu fikiria lile ambalo lingeweza kutokea ikiwa kwenye mkusanyiko mkubwa wa Mashahidi wa Yehova, Idara ya Usafi na Idara ya Utumishi wa Chakula zote mbili zingepewa daraka la kusafisha vibanda vya chakula, au ikiwa Idara ya Ukaribishaji na Idara ya Kuzamisha zote mbili zingepewa mgawo wa kuwaelekeza watazamaji wakati wa ubatizo.
Wape migawo wanaume wenye uwezo. Yethro alimshauri Musa hivi: “Ni lazima wewe mwenyewe uwatafute wanaume wenye uwezo, wamchao Mungu miongoni mwa watu wote, wanaume wanyoofu na wasiofisidika, na kuwaweka rasmi juu ya watu.” (Kutoka 18:21, The New English Bible) Kwa wazi, ni lazima kwanza mtu awe na sifa za kiroho. Ili kuamua ikiwa mtu ni ‘mwenye uwezo’ wa kufanya kazi iliyoko, ni lazima ufikirio utolewe kwa mambo kama vile vitabia vya kibinafsi, ujuzi, mazoezi, na stadi. Hivyo, hasa Mkristo mwenye mwelekeo wa upole, wa kupendeza, wenye kutaka kusaidia yaelekea angefanya kazi vizuri kwenye kaunta ya magazeti au akiwa mkaribishaji. Vivyo hivyo, mtu anapochaguliwa ili kumsaidia mwandishi wa kundi, kwa kufaa ufikirio ungetolewa jinsi alivyo mwenye utaratibu. Je! yeye hukazia fikira mambo madogoma-dogo, je, anategemeka, na je, aweza kuweka siri? (Luka 16:10) Kufikiria mambo hayo pamoja na sifa za kiroho za lazima kwaweza kusaidia kumweka mtu afaaye kwenye kazi fulani.
Toa vifaa vya kutosha. Mtu anayetumikia atahitaji kuwa na vifaa fulani ili akamilishe kazi aliyogawiwa. Labda atahitaji vyombo, fedha, au msaada. Toa vifaa vya kutosha. Kwa mfano, ndugu huenda akaombwa afanye marekebisho ya lazima kwenye Jumba la Ufalme. Kwa wazi, angeambiwa lile linalohitajiwa kufanywa, lakini huenda pia akahitaji fedha za matumizi madogo-madogo ili anunue vifaa ambavyo huenda vikahitajiwa. Labda atahitaji msaada. Kwa hiyo wazee wanaweza kuwaomba wengine wamsaidie au kutolea kundi tangazo kama vile ‘Ndugu fulani atakuwa akifanya kazi fulani kwenye jumba, na huenda akawaomba baadhi yenu msaada.’ Kufikiria kimbele huko kutamzuia mtu asigawe kazi bila kuandaa vifaa vya kutosha. “Usikabidhi kazi nusu-nusu” ndivyo mshauri mmoja wa kazi ya usimamizi alivyoeleza jambo hilo.
Unapogawa madaraka, waarifu wengine kwamba mtu huyo anafanya kazi badala yako. Mamlaka ya kufanya kazi badala yako ni kifaa cha kazi pia. Yoshua alipewa utume akiwa kiongozi mpya wa Israeli mbele ya “mkutano wote.” Musa aliagizwa ‘aweke juu yake sehemu ya heshima yake.’ (Hesabu 27:18-23) Katika mpango wa kundi, jambo ilo hilo huenda likatimizwa kwa kuweka tu kwenye ubao wa matangazo orodha ya wale waliopewa migawo ya kazi.
Unga mkono maamuzi yao. Sasa yule aliyepewa mgawo aweza kufanya kazi iliyoko. Lakini kumbuka, waweza kuwa chanzo kweli kweli cha kitia-moyo kwake ikiwa unaunga mkono maamuzi mazuri anayofanya. Kwa mfano, wewe ukiwa mzee huenda ukawa na upendeleo wako mwenyewe juu ya jinsi ya kuweka vikuza sauti na fanicha kwenye jukwaa la Jumba la Ufalme, labda kwa njia tofauti ya jinsi ndugu aliyepewa mgawo wa kazi hiyo afanyavyo. Hata hivyo, ikiwa ndugu anayeshughulikia jukwaa anaruhusiwa uhuru wa kadiri fulani katika kazi yake, yaelekea atapata uhakika na ujuzi. Isitoshe, huenda pia akafanya mambo yawe mazuri zaidi. Mshauri mmoja wa biashara alitaarifu hivi: “Kabidhi wengine kazi, si jinsi ifanywavyo. . . . Mara nyingi, uwezo wa kubuni huonyeshwa.”
Zaidi ya hayo, ndugu afanyaye kazi hiyo hasa, huwa mara nyingi karibu na hali fulani hususa na hivyo huenda akaelewa vema zaidi matatizo yanayohusika nayo. Yaelekea atatatua matatizo kwa kutumia masuluhisho yafanyayo kazi kweli kweli. Huenda pia akashughulika na mambo yasiyoonekana waziwazi kwa watazamaji. Kwa hiyo, mwangalizi mmoja Mkristo alisema hivi juu ya msaidizi mmoja mwenye ujuzi: “Akisema kuna matatizo fulani, mimi huamini lile asemalo.”
Naam, kifaa chenye thamani kubwa zaidi kipatikanacho kwa wazee Wakristo ni wanaume na wanawake waliojiweka wakfu walio na nia na uwezo wa kusaidia katika njia yoyote wanayoelekezwa. Wazee, tumieni kwa faida yenu kifaa hicho bora sana! Kukabidhi wengine kazi ni ishara ya kuwa na kiasi na kwaweza kupunguza mkazo na fadhaiko. Kwa njia hiyo, hutawezeshwa kufanya mengi zaidi tu bali pia utawapa wengine nafasi ya kupata uzoefu unaohitajiwa.