Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Uhuru wa Kiroho Katika Kolombia
TANGU wakati wa wale mashujaa wa vita Wahispania, Ukatoliki umekuwa dini yenye uvutano katika Amerika Kusini. Katika Kolombia hiyo imekuwa dini rasmi ya Serikali kwa muda mrefu. Kwa miaka 105 ambayo imepita, Vatikani imekuwa na mapatano pamoja na serikali ya Kolombia ambayo yalilinda kanisa na kulipatia mapendeleo ya pekee katika shughuli za elimu na ndoa.
Katika Desemba 1990 watu wa Kolombia walichagua tume ili ifanyize katiba mpya, iliyotimizwa kufikia katikati ya 1991. Katiba hiyo mpya inabadili hali ya kidini katika Kolombia. Sasa dini zote zina haki sawa mbele ya sheria, na mafundisho ya kidini hayawezi kulazimishwa kwa watoto katika shule za umma. Mapatano pamoja na Vatikani yanakaribia kupitiwa upya kwa kufuatia mabadiliko hayo mapya ya kikatiba.
Uhuru huo mkubwa zaidi wa dini utapunguza uvutano wa Kanisa Katoliki, ukifanya iwe rahisi zaidi kwa watu wenye mioyo myeupe kupata maarifa ya Biblia na kupata uhuru wa kiroho.
Wakitazamia uhuru wa kiroho, Mashahidi wa Yehova 51,000 katika nchi hiyo walikuwa wakifanya matayarisho ili kuwatunza wakimbizi wa kiroho. Majengo yao mapya ya tawi yaliyopanuliwa, yanayotia ndani matbaa yenye mwendo kasi inayochapisha katika rangi kamili, karibu yakamilishwe. Mapainia wa pekee wa muda wametumwa kwenye miji midogo zaidi ili kutafuta kondoo wa Yehova waliopotea nao wametimiza kazi ya kielimu ya Biblia nzuri ajabu. Katika miji 63, kila mmoja ukiwa na wakazi 10,000, makundi na vikundi vipya 47 vimefanyizwa.
Roho ya Yehova iendeleapo kusukuma watu wenye mioyo myeupe, vijana wengi wanaitikia pia. Kichapo Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi kimethibitika kuwa msaada wenye thamani kubwa kwa vijana hao na kwa wazazi wao pia. Alipokuwa akienda nyumba kwa nyumba, Shahidi mmoja alikutana na mwanamume mmoja aliyekuwa amesoma sehemu-sehemu za kitabu hicho, ambacho alikuwa amekopeshwa nakala moja yacho na jirani. Alivutiwa sana na ile hekima inayotumika ambayo kitabu hicho kinaonyesha katika kuzungumzia matatizo ya familia. Sura ya 4, “Kwa Nini Baba na Mama Waliachana?” ilimvutia hasa, kwa kuwa yeye na mke wake walikuwa karibu sana kutengana. Alisema kitabu hicho kilimwokoa kutoka msiba mkubwa. Sasa yeye na familia yake wanajifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na wanahudhuria mikutano yote ya kundi. Wanashukuru sana kwa ajili ya ile hekima inayotumika ambayo Yehova huandaa kupitia Biblia na tengenezo lake.
Ono hilo laonyesha ule uhuru wa kiroho unaotukia katika Kolombia huku Mashahidi wa Yehova wakiwasaidia wale wenye njaa kiroho wajifunze juu ya makusudi ya Yehova ya ajabu na ulimwengu wake mpya, ulio karibu sasa.—2 Petro 3:13.