Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 1/1 kur. 5-8
  • Uumbaji Mpya Watokezwa!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uumbaji Mpya Watokezwa!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uumbaji wa “Mbingu Mpya na Dunia Mpya”
  • “Mjawe na Furaha Milele”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Namna “Mbingu Mpya na Dunia Mpya” Zitakavyoanza
    Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
  • Kufanya Vitu Vyote Kuwa Vipya
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Taratibu Mpya Inayokuja Inayotegemezwa na Roho Takatifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 1/1 kur. 5-8

Uumbaji Mpya Watokezwa!

MFALME Sulemani mwenye hekima alisema hivi wakati mmoja: “Jambo jipya hakuna chini ya jua.” (Mhubiri 1:9) Hilo ni kweli kuhusu ulimwengu wa asili tunamoishi, lakini namna gani yale makao makubwa mno ya uumbaji wa kiroho wa Yehova? Katika makao hayo, mmoja aliye mkuu zaidi ya Sulemani, kwa kweli, aliye mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi, alikuja kuwa uumbaji mpya wenye kutokeza. Hilo lilitukiaje?

Katika mwaka 29 wa Wakati wa Kawaida wetu, yule mwanamume mkamilifu, Yesu, alijitokeza mwenyewe abatizwe na Yohana kwenye Mto Yordani. “Baada ya kubatizwa mara hiyo Yesu alitoka katika maji; na, tazama! mbingu zilifunuka, na akaona roho ya Mungu ikishuka kama njiwa ikija juu yake. Tazama! Pia, kulikuwako sauti kutoka katika mbingu iliyosema: ‘Huyu ndiye Mwanangu, mpendwa, ambaye mimi nimekubali.’” (Mathayo 3:16, 17, NW) Hivyo, yule mtu Kristo Yesu alikuwa uumbaji mpya wa kwanza, aliyepakwa mafuta kufanya mapenzi ya Mungu. Baadaye, kwa msingi wa kifo chake cha kidhabihu, Yesu alikuja kuwa Mpatanishi wa agano jipya kati ya Mungu na kikundi kiteule cha watu. Kila mmoja wao amekuja kuwa “kiumbe kipya [uumbaji mpya, NW],” aliyezaliwa kwa roho ya Mungu kwa tumaini la kimbingu, akiwa na taraja la kutawala pamoja na Yesu katika Ufalme wake wa kimbingu.—2 Wakorintho 5:17; 1 Timotheo 2:5, 6; Waebrania 9:15.

Kwa muda wa karne ambazo zimepita, Wakristo hao wapakwa-mafuta, wenye kuzaliwa kwa roho wamekusanywa katika muungano pamoja na Kristo wakiwa kundi la Kikristo la kweli, hilo lenyewe likiwa kiumbe kipya. Mungu aliliita kutoka katika ulimwengu huu kwa kusudi fulani, kama vile mtume Petro anavyotaarifu: “Ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu.” (1 Petro 2:9) Kama vile Kristo Yesu, uumbaji mpya wa Mungu wa kwanza, uumbaji mpya huo wa baadaye una wajibu wa msingi wa kuhubiri habari njema. (Luka 4:18, 19) Ni lazima washiriki wao mmoja mmoja, wanaofikia idadi ya 144,000 hatimaye, ‘wavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.’ (Waefeso 4:24; Ufunuo 14:1, 3) Hilo lataka wasitawishe “tunda la Roho,” linalosimuliwa kwenye Wagalatia 5:22, 23, na kutunza utumishi wao kwa uaminifu.—1 Wakorintho 4:2; 9:16.

Ikoje kuhusu uumbaji mpya huo katika nyakati za ki-siku-hizi? Katika mwaka wa 1914, kama vile jedwali ya wakati ya Biblia inavyoonyesha, maneno ya Ufunuo 11:15 yalitimizwa: “Ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu [Yehova] na wa Kristo wake, naye atamiliki hata milele na milele.” Tendo la kwanza la Kristo akiwa Mfalme aliyetawazwa karibuni lilikuwa kuvurumisha Shetani na malaika zake wa kishetani kutoka mbinguni hadi kwenye ujirani wa dunia. Hilo lilileta “Ole wa nchi,” katika namna ya vita ya ulimwengu ya kwanza na taabu zilizoambatana nayo.—Ufunuo 12:9, 12, 17.

Hilo lilitumika pia likiwa ishara kwa mabaki ya uumbaji mpya duniani ya kwamba ni lazima washiriki katika kutimiza unabii wa Yesu: “Habari njema ya ufalme [uliosimamishwa] itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.” Ule “mwisho” ni nini? Yesu aendelea kueleza: “Wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe. Na kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu ye yote; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo.”—Mathayo 24:3-14, 21, 22.

Roho ya Yehova iliwasukuma wale wapakwa-mafuta wa uumbaji mpya wake waanze kujishughulisha katika kampeni ya kuhubiri yenye kuenea sana iliyopata kutendeka kwenye dunia hii. Kutoka maelfu machache katika 1919, idadi ya hao wapiga mbiu ya Ufalme wenye bidii iliongezeka hadi 50,000 hivi kufikia miaka ya katikati ya 1930. Kama ilivyotolewa unabii, “sauti yao imeenea duniani mwote, na maneno yao hata miisho ya ulimwengu.”—Warumi 10:18.

Je! mabaki ya uumbaji mpya peke yao ndio wangekusanywa kwa ajili ya wokovu? La, kwani unabii ulikuwa umetaarifu kwamba malaika wa Mungu wangezuia zile pepo za dhiki kubwa mpaka kukusanywa kukamilishwe si tu kwa Waisraeli hao wa kiroho wenye kwenda mbinguni bali pia kwa wengine, “mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.” Mwisho wao ungekuwa nini? Wangetoka “dhiki ile iliyo kuu” bila kudhurika ili kufurahia uhai wa milele katika dunia-paradiso!—Ufunuo 7:1-4, 9, 14.

Kwa furaha, huo mkutano mkubwa, unaokusanywa kutoka nchi 229 hivi, umeongezeka kuwa Mashahidi watendaji karibu 4,500,000. Wengi zaidi wanakuja, kama inavyoonyeshwa na hudhurio la 11,431,171 kwenye Ukumbusho wa kifo cha Yesu katika Aprili 17 mwaka jana. Kati ya mamilioni hayo yote, ni 8,683 tu, wanaodai kuwa mabaki ya kiumbe kipya duniani, walioshiriki mifano ya Ukumbusho. Wale walio katika kikundi hicho kidogo wasingeweza kamwe peke yao, kuitimiza ile kazi kubwa mno ya kuhubiri leo. Mamilioni wanaojumlika kuwa mkutano mkubwa sasa wanafanya kazi bega kwa bega pamoja nao katika kuitimiza kazi hiyo. (Sefania 3:9) Isitoshe, washiriki wenye kuzoezwa vema wa huo mkutano mkubwa sasa wanafanya kazi ya usimamizi na kazi nyinginezo zenye daraka pamoja na Baraza Linaloongoza la wapakwa-mafuta la Israeli wa kiroho, kama vile Wanethini wasio Waisraeli walivyofanya kazi pamoja na makuhani wakirekebisha kuta za Yerusalemu.—Nehemia 3:22-26.

Uumbaji wa “Mbingu Mpya na Dunia Mpya”

Ni shangwe iliyoje inayoandamana na kukusanywa huko! Ni kama vile Yehova alivyosema ingekuwa: “Mimi naumba mbingu mpya na nchi [dunia, NW] mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo; maana, tazama, naumba Yerusalemu uwe shangwe, na watu wake wawe furaha. Nami nitaufurahia Yerusalemu, nitawaonea shangwe watu wangu; sauti ya kulia haitasikiwa ndani yake tena, wala sauti ya kuomboleza.” (Isaya 65:17-19) Mbingu mpya ya uumbaji wa Yehova itajumuika hatimaye kuwa ya Kristo Yesu na wale washiriki waliofufuliwa 144,000 wa uumbaji mpya ambao wamenunuliwa kutoka kwa ainabinadamu kwa muda wa karne 19 ambazo zimepita. Serikali hiyo ni tukufu zaidi, tena zaidi, ya serikali yoyote ya kidunia iliyopata kutawala katika Yerusalemu halisi, hata ile ya siku ya Sulemani. Inatia ndani Yerusalemu Mpya, mji wa kimbingu, unaosimuliwa katika uzuri wao wote wa kumetameta katika Ufunuo sura 21.

Yerusalemu mpya ni bibi-arusi wa kiroho wa Kristo, wafuasi wake wapakwa-mafuta 144,000, wanaoungana na Bwana-arusi wao mbinguni baada ya kifo chao na ufufuo wao wa kiroho. Wanaonyeshwa kwenye Ufunuo 21:1-4, “[wa]kishuka kutoka mbinguni kwa Mungu,” yaani, wakitumiwa naye katika kuelekeza baraka kwa ainabinadamu hapa duniani. Kwa njia hiyo unabii huu unatimizwa: “Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye, Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”

Twaweza kushukuru kama nini kwa ajili ya uumbaji wa Mungu wa hiyo mbingu mpya! Tofauti na zile tawala za muda tu, zenye ufisadi ambazo zimeikumba ainabinadamu kwa muda mrefu sana, mpango huo wa kiserikali wa Mungu utakuwa wa kudumu. Uumbaji mpya na watoto wao wa kiroho, mkutano mkubwa, unashangilia ahadi hii ya Mungu ya ziada: “Kama vile mbingu mpya na nchi [dunia, NW] mpya nitakazofanya, zitakavyokaa mbele zangu, asema BWANA [Yehova, NW], ndivyo uzao wenu na jina lenu litakavyokaa.”—Isaya 66:22.

“Dunia mpya” yaanza na wazao wa wapakwa-mafuta wa ule uumbaji mpya. Ni jamii mpya ya ainabinadamu duniani yenye kumhofu Mungu. Chuki, uhalifu, jeuri, ufisadi, na ukosefu wa maadili katika jamii ya kibinadamu leo kwa hakika yakazia uhitaji wa badiliko kamili ili kutokeza jamii mpya ya dunia, yenye kuendeshwa chini ya mwelekezo wa mbingu mpya wenye ukarimu. Ndivyo Yehova anavyokusudia. Jinsi ambavyo ameumba mbingu mpya, ndivyo anavyoiumba dunia mpya kwa kukusanya mkutano mkubwa ukiwa kiini cha jamii ya ulimwengu mpya yenye amani. Jamii hiyo pekee ndiyo itakayookolewa ikiwa hai ‘kutoka katika ile dhiki iliyo kuu.’—Ufunuo 7:14.

Tunaweza kutazamia nini baada ya dhiki kubwa? Akisema na mitume wake, waliokuwa wa kwanza wa wale wanaojumuika kuwa mbingu mpya itakayotawala dunia mpya, Yesu aliahidi hivi: “Amin, nawaambia ya kwamba ninyi mlionifuata mimi, katika ulimwengu mpya, [uumbaji mpya NW], atakapoketi Mwana wa Adamu [binadamu, NW] katika kiti cha utukufu wake, ninyi nanyi mtaketi katika viti kumi na viwili.” (Mathayo 19:28) Wote 144,000 wa huo Yerusalemu Mpya watashiriki pamoja na Yesu katika kuhukumu ainabinadamu. Wakati huo upendo utachukua mahali pa ubinafsi na chuki ukiwa msingi ambao jamii ya kibinadamu unajengwa juu yao. Matatizo ya kikabila, ya rangi, na ya kitaifa yataondolewa kabisa. Ufufuo utawarudisha wapendwa kidato kwa kidato. Mabilioni ya ainabinadamu yenye uaminifu watakuja kuwa familia moja kubwa, yenye umoja, iliyoinuliwa kwenye uhai wa milele kwenye dunia iliyogeuzwa kuwa paradiso.

Huo utapita kwa mbali ile hali kamilifu inayowaziwa na wanadamu. Utakuwa uumbaji wa kudumu—“mbingu mpya na dunia mpya ambayo imejaa uadilifu”! (2 Petro 3:13, Habari Njema kwa Watu Wote) Kwa hakika, hilo ni taraja zuri ajabu, ahadi tukufu ya yeye aliyesema, “Tazama, nayafanya yote kuwa mapya,” na aliyeongeza taarifa hii yenye kuchochea imani: “Andika ya kwamba maneno hayo ni amini na kweli.”—Ufunuo 21:5.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki