Kanisa la Amerika ya Latini Katika Hali ya Kufadhaika—Kwa Nini Mamilioni Wanaondoka?
KUTOKA mpaka wa kaskazini mwa Meksiko hadi ncha ya kusini mwa Chile, hakuna jiji au kijiji cha Amerika ya Latini ambacho hakionei fahari kanisa la Roma Katoliki katikati yacho. Hata hivyo, “badiliko kubwa linatukia katika Amerika ya Latini,” akiri Joseph E. Davis, mkurugenzi wa programu ya taasisi moja inayoendeleza utendaji mbalimbali wa Kikatoliki. Alikiri pia kwamba Amerika ya Latini, eneo ambalo kwa muda wa zaidi ya karne tatu limekuwa chini ya uvutano wa Kanisa la Roma Katoliki, sasa iko karibu kubadilika sana.
Si siri kwamba utawala wa Kanisa Katoliki unadhoofika kwa kasi. Hivi karibuni, idadi ya Wakatoliki wenye bidii ilikadiriwa kuwa asilimia 15 tu ya wakaaji wote katika Amerika ya Latini. 1991 Britannica Book of the Year kiliripoti hivi: “Maaskofu wa dini ya Roma Katoliki na papa mwenyewe walionyesha hofu kwamba Amerika ya Latini ya kihistoria yenye kufuata dini ya Katoliki ilikuwa ikigeuka kwa njia ya hatari kutoka katika ile imani ya zamani.” Kwa nini hilo linatukia? Kwa nini wengi sana wanaacha zizi la Kikatoliki? Ni nini kinachowapata wale wanaopotea?
Jitihada ya Kutafuta Elezo
Viongozi wakatoliki wanalaumu ongezeko kubwa la “mfarakano” kuwa ndicho chanzo cha matatizo yao. Padri mmoja wa Ulaya anayefanya kazi Bolivia alilalamika hivi: “Kanisa ni kama mti ambao nguvu zao zinaondolewa na mafarakano yaliyo kama magugu.”
Katika Argentina, dini mpya 140 zinaripotiwa kila mwaka, jambo liwezalo kusaidia kueleza sababu kwa nini idadi ya washiriki wa Kanisa Katoliki imeshuka kutoka asilimia 90 hadi asilimia 60 au 70 tangu miaka ya katikati ya 1970. Katika Tijuana, Meksiko, asilimia 10 ya wale wakaaji milioni mbili wamehamia zile dini 327 za huko ambazo si za Kikatoliki. Gazeti Time liliripoti hivi: “Kwa kustaajabisha, kwa hakika kuna karibu Waprotestanti Wabrazili wengi kuliko Wakatoliki kanisani Jumapili.” Haishangazi kwamba, kama vile gazeti moja la habari lilivyosema, “makadinali wa Amerika ya Latini walipokutana pamoja na papa katika Jiji la Vatikani ili kuzungumzia mambo mawili ya maana zaidi kwa kanisa la leo,” mojawapo lilikuwa “lile tatizo la mafarakano.”
Katika mkutano mmoja pamoja na maaskofu wa Meksiko, papa alisema kwamba mafanikio ya zile dini mpya nyingi “ni kwa sababu ya uvuguvugu na kutojali kwa wana wa kanisa wasiotunza utume wao wa kievanjeli.” Kwa nini “wana wa kanisa” hawajali kutimiza mahitaji ya kiroho ya Wamerika wa Latini hali wengi sana wanaistahi Biblia? Safu moja ya mhariri katika Última Hora, gazeti La Paz, Bolivia, yaeleza hivi: “Kanisa limeingia ulimwenguni kwa kadiri wa sana hivi kwamba kila siku laonekana laacha mazingira yalo. Haipasi itushangaze kuona, kama vile inavyotukia, kwamba mapadri ni wanasoshiolojia, wanauchumi, waandishi wa habari, au wanasiasa zaidi ya kuwa makasisi.”
Wanasiasa Zaidi ya Kuwa Wahubiri?
Kuhusika kwa kanisa katika siasa wakati wa miaka ya 1970 na ya 1980 bila shaka kulichangia lile chukizo ambalo Wamerika wa Latini wengi huhisi kwa Ukatoliki. Uchunguzi uliotangazwa kwa chapa katika 1985 uliona jambo hili kuhusu Maryknoll, lile shirika la Catholic Foreign Mission Society of America, pamoja na misheni zalo nyingi za Amerika ya Latini: “Maryknoll limeleta kwa mafanikio ule ujumbe wa Umaksi-Ulenini wa mapinduzi yenye jeuri ili likubaliwe na umma kwa sababu hasa limeruhusiwa kutenda likiwa sehemu ya Kanisa Katoliki. Ujumbe walo umemfikia si mhudhuriaji-kanisa wa kawaida tu, bali pia, watungaji-sera Wamerika walio mashuhuri.”
Ebu fikiria pia ile iitwayo eti vita chafu, ambamo, kwa kustaajabisha, Waargentina kutoka 10,000 hadi 30,000 walichukuliwa kwa nguvu na kuuawa bila kuhukumiwa katika miaka ya mwisho-mwisho ya 1970. Safu moja ya mhariri katika National Catholic Reporter, chini ya kichwa “Damu Yatia Mawaa Kanisa Katika Argentina,” ilisema hivi: “Ono la Argentina linafanana sana na yale matendo ya kanisa Katoliki katika Ujerumani ya Nazi, linatokeza tena lile swali juu ya kama nguvu za mamlaka ni zenye umaana zaidi kwa kanisa kuliko ile amri ya Gospeli ya kushuhudia kweli.”
Tamaa ya kanisa ya kupata nguvu za mamlaka katika serikali za ulimwengu huonyesha kwa wazi kwamba kanisa si rafiki ya Mungu. Biblia husema hivi: “Je! hamjui kwamba kuwa rafiki wa ulimwengu ni kuwa adui wa Mungu? Yeyote anayetaka kuwa rafiki wa ulimwengu anajifanya adui wa Mungu.” (Yakobo 4:4, Jerusalem Bible ya Kikatoliki) Haishangazi basi, kwamba wengi hawaendei Kanisa Katoliki ili kupata mwongozo wa kiroho. Lakini ni nini limewapata wale ambao wameondoka zizi la Kikatoliki?
Kondoo Wasio na Mchungaji
Wao wanafanana sana na wale watu ambao viongozi wa kiroho wa dini ya Kiyahudi walishindwa kuwatunza. Biblia husema kwamba Yesu “aliwaonea huruma kwa sababu walikuwa hoi na wenye wasiwasi kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36, JB) Wengi wameacha Kanisa Katoliki kwenda dini ziitwazo eti za kievanjelisti. Je! hizo zimewatunza vema zaidi kondoo hao waliopotea? Je! Waprotestanti wanaelekea zaidi kuwa kama vile Yesu alivyowaambia wafuasi wake wa kweli: “Wao si wa [sehemu ya, NW] ulimwengu, kama mimi nisivyo wa [si sehemu ya, NW] ulimwengu”?—Yohana 17:14.
Dini nyingi zisizo za Kikatoliki hujaribu kuonyesha mfano wa kuwa watiifu kwa Biblia kuliko kuwa wafuasi wa mapokeo ya kidini. Mara nyingi hiyo ni wonyesho wa kijuujuu tu. Mafundisho ya msingi ya matengenezo ya Kiprotestanti yanafanana sana na yale ya Kanisa Katoliki hivi kwamba watazamaji wengi wangeweza kwa urahisi kutumia ile methali ya Kiandea: “Es la misma cholita con otra pollera” (Ni yuleyule mwanamke mdogo Mhindi akiwa na skati tofauti).
Kwa kielelezo, karibu vikundi vyote vya Kiprotestanti vinafundisha kwamba Mungu ni Utatu, hata hivyo hilo si fundisho la Biblia. The Encyclopedia of Religion yakiri hivi: “Wafafanuzi wa maandiko na wanatheolojia leo huafikiana kwamba Biblia ya Kiebrania haina fundisho la Utatu . . . Agano Jipya pia halina fundisho dhahiri la Utatu.”a
Kwa wazi Waprotestanti wamejifungamanisha na ulimwengu huu na siasa zao kadiri ile ile ambavyo Wakatoliki wamejifungamanisha. Encyclopedia of Latin America yasema hivi: “Uprotestanti katika Amerika ya Latini umejipatanisha pia na . . . siasa za uchaguzi zinazopendwa na wengi. Mara nyingi mapasta wenyeji huwa wateja wa wafadhili wa kisiasa nao huandaa kura ili kupata mapendeleo ya kiserikali kwa ajili ya makanisa yao.” Latin American Research Review yasema hivi: “Uprotestanti umefunga ndoa na siasa katika Guatemala tangu ulipowasili nchi hiyo mara ya kwanza,” ikiongeza kwamba “umekuwa njia ya kuwasilisha tabia za kisiasa na za kijamii zikiwa namna ya dini.”
Ushiriki wa dini ya Protestanti katika siasa mara nyingi umeongoza kwenye ushiriki wa dini ya Protestanti katika vita. Hayati Harry Emerson Fosdick, aliyeonwa kuwa mmoja wa makasisi Waprotestanti aliye mashuhuri zaidi katika historia ya Amerika, alikiri hivi: “Historia yetu ya Magharibi imekuwa yenye vita moja baada ya nyingine. Tumewalea watu kwa ajili ya vita, tumewazoeza watu kwa ajili ya vita; tumetukuza vita; tumewafanya wapiga vita kuwa mashujaa wetu na hata ndani ya makanisa yetu tumeziweka bendera za vita . . . Kwa pembe moja ya mdomo wetu tumemsifu Mwana-Mfalme wa Amani na kwa pembe ile nyingine tukatukuza vita.”
Wapaswa Kufanya Nini?
Baada ya kusimulia dini bandia kuwa malaya wa ufananisho anayefanya uasherati pamoja na serikali za dunia, kitabu cha Biblia cha Ufunuo chasema hivi: “Watu wangu, ondokeni kwake, ili msishirikiane naye katika uhalifu wake, msije mkaipata adhabu yake.”—Ufunuo 18:4, JB.
Wengi hutambua kwamba kuna ufisadi mwingi kanisani, bado wao wanasita kuliacha kwa sababu Kanisa la Roma limekuwa na historia ya kale sana. Hata hivyo, kumbuka kwamba mfumo wa ibada ya Kiyahudi ulikuwa wa zamani sana; hata hivyo Mungu aliwakatalia mbali Wayahudi wasiwe watu wake wateule walipoasi imani kutoka katika mafundisho yake ya kweli. Watumishi waaminifu wa Mungu waliacha dini ya Kiyahudi walipotambua kwamba Mungu alikuwa sasa akitumia kundi la Kikristo badala yayo. Unaweza kutambuaje kundi la Kikristo la kweli leo?
Karibu Wamerika wa Latini milioni moja wamekuwa Mashahidi wa Yehova katika miongo miwili ambayo imepita. Kwa nini walifanya badiliko hilo? Gazeti moja la habari katika Martínez de la Torre, Veracruz, Meksiko, lilichunguza swali hilo. Lilisema hivi: “Wanafunzi hao wa Biblia wamefanyizwa na karibu asilimia 100 ya wale waliokuwa wachaji wa dini tofauti-tofauti, hasa Wakatoliki, ambao wameona dini ikipeperuka kuelekea siasa na kukubali na kupendelea kwayo mazoea yasiyo ya kibiblia kama vile kuchanganya imani pamoja, ukosefu wa maadili, na jeuri. Kujipatanisha na kanuni za Kimaandiko za mwenendo bila kushiriki katika ibada ya sanamu au mapokeo yenye vyanzo visivyo wazi, kumekuwa chanzo cha uradhi kwao. Hilo limewapa umoja wa imani unaostahili sifa ambao huonekana kuwatofautisha popote wawezapo kupatikana.”
Gazeti jingine la habari la Amerika ya Latini lilisema hivi: “Mashahidi wa Yehova ni watu wenye bidii, wenye kufuatia yaliyo haki, wenye kumhofu Mungu. Ni wenye kufuata mambo ya zamani na wenye kupenda mapokeo na dini yao hutegemea mafundisho ya Biblia.” Tunakualika ujifunze Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova popote unapoishi. Utajifunza kwamba tumaini lao na njia yao yote ya maisha inategemea Biblia. Naam, utajifunza jinsi ya kumwabudu Mungu kwa “roho na kweli.”—Yohana 4:23, 24.
[Maelezo ya Chini]
a Ona kijitabu Je! Uamini Utatu? kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Chati katika ukurasa wa 21]
MASHAHIDI WA YEHOVA KATIKA NCHI NYINGINE ZA AMERIKA YA LATINI
1971 1992
Nchi Wahubiri Wahubiri
Argentina 20,750 96,780
Bolivia 1,276 8,868
Brazili 72,269 335,039
Chile 8,231 44,067
Colombia 8,275 55,215
Ekwedori 3,323 22,763
El Salvador 2,181 20,374
Guadeloupe 1,705 6,830
Guatemala 2,604 13,479
Hondurasi 1,432 6,583
Jamhuri ya Dominika 4,106 15,418
Kosta Rika 3,271 14,018
Meksiko 54,384 354,023
Panama 2,013 7,732
Paraguay 901 4,115
Peru 5,384 43,429
Puerto Riko 8,511 25,315
Uruguay 3,370 8,683
Venezuela 8,170 60,444
JUMLA 212,156 1,143,175