Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Kustahi Utakatifu wa Uhai
BIBLIA huonyesha kwamba damu ni yenye thamani kubwa machoni pa Mungu na kwamba yeye hushutumu kuitumia vibaya. (Mambo ya Walawi 17:14; Matendo 15:19, 20, 28, 29) Kwa sababu ya mielekezo hiyo ya Biblia, Mashahidi wa Yehova hawakubali kutiwa damu mishipani.
Ili kuwasaidia madaktari na wafanyakazi wa hospitali kuelewa msimamo wa kidini wa Mashahidi wa Yehova kuhusu jambo hilo na kuthamini kwamba Mashahidi watakubali matibabu mengineyo, Watch Tower Society imepanga Halmashauri za Uhusiano na Hospitali (HLC) katika mabara tofauti-tofauti. Washiriki wa halmashauri hizo huzuru mahospitali ili kusema na wafanyakazi wa tiba. Hivi karibuni, katika majiji 12 katika Polandi, mikutano zaidi ya 200 ilifanywa, iliyohusisha madaktari wa tiba zaidi ya 500, hasa wasimamizi wa kliniki au wa wadi za hospitali. Jambo lifuatalo lilitukia wakati wa ziara moja ya jinsi hiyo:
“Mkutano mmoja kwenye Kliniki ya Upasuaji wa Moyo katika Zabrze ulikuwa wenye mafanikio zaidi. Tangu 1986 kikundi [hicho] kwenye kliniki hiyo kimekuwa kikiwafanyia ndugu zetu upasuaji bila damu. Kufikia sasa, upasuaji wa jinsi hiyo wa visa 40 umefanywa. Kliniki hiyo iko tayari kuwatibu wagonjwa kutoka kotekote Polandi na kutoka ng’ambo pia. Baada ya mazungumzo ya muda wa dakika 50, makamu mmoja wa msimamizi wa wadi moja alijulisha washiriki wa HLC kwa kikundi cha wagonjwa na kusema hivi: ‘Watu hawa ni Mashahidi wa Yehova. Wao hushirikiana na kliniki yetu, nao hutusaidia. Si waamini wenzao tu bali pia wagonjwa wote wengine hunufaika na msaada wao. Kwa sababu ya Mashahidi wa Yehova, tumekuja kusadiki kwamba upasuaji mkubwa wa moyo waweza kufanywa bila damu.
“‘Kwa kielelezo, tulimfanyia upasuaji mwanamke huyu [akielekeza kidole kwa mmoja kati ya wagonjwa wake] bila damu, naye anarudi nyumbani Jumatatu. Ningependa kusema kwamba sisi hutumia damu mara chache zaidi kuliko hapo mbele kwa sababu ni hatari. Inashirikishwa na HIV, mchochota wa ini, na kuchukua muda mrefu kupona.
“‘Mimi ni Mkatoliki, lakini katika nyumba yetu tumekuwa wenye kuvumilia maoni ya wengine sikuzote. Siku moja nilitembea huku na huku katika Stediamu ya Slaski pamoja na watoto wangu. Hapo mbele, stediamu hiyo ilikuwa imeachiliwa bila kutunzwa, lakini tuliona kwamba sasa ilikuwa imebadilika isiweze kutambuliwa. Nilimwuliza mfanyakazi mmoja jinsi badiliko hilo lilivyotokea. Alisema kwamba wasimamizi wayo walikuwa karibu wamepoteza tumaini la kutengeneza stediamu hiyo, lakini ilikodishwa Mashahidi wa Yehova, nao wakaijenga upya.
“‘Kwa hiyo hawa ni watu ambao sisi sote twaweza kujifunza mengi kutoka kwao. Nafikiri kwamba katika wadi hii twapaswa kuvumilia maoni ya wengine.’ Halafu, akielekeza tena kidole kwa Shahidi mmoja ambaye angefanyiwa upasuaji baada ya siku chache, akasema hivi: ‘Mwanamke huyu ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, naye atafanyiwa upasuaji bila damu.’”
Ingawa Mashahidi wa Yehova hawajaribu kulazimisha wengine waamini itikadi zao, wao wenyewe hufuata kielelezo cha mitume na “kumtii Mungu kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29) Hilo latia ndani kustahi damu. Wanathamini wakati wengine wanapostahi masadikisho yao ya kidini juu ya suala hili.