Kutumikia kwa Kuhisi Uharaka
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA HANS VAN VUURE
Asubuhi moja katika 1962, Paul Kushnir, mwangalizi wa tawi la Watch Tower Society katika Uholanzi, alikutana nami katika wilaya ya bandari ya Rotterdam. Akinitazama nikiwa upande ule mwingine wa meza katika mkahawa usiokuwa na mwangaza mwingi, alisema hivi: “Je! watambua Hans, kwamba ukikubali mgawo huu, wewe na mke wako mtapata tikiti ya kwenda tu?”
“NAAM, nami nina hakika kwamba Susie atakubali hilo pia.”
“Basi, zungumza hilo pamoja na Susie. Itafaa zaidi mkinijulisha upesi iwezekanavyo.”
Asubuhi iliyofuata alipata jibu letu: “Tutaenda.” Kwa hiyo katika Desemba 26, 1962, tuliwakumbatia watu wa ukoo na marafiki kwenye Uwanja wa Ndege wa Schiphol katika Amsterdam uliokuwa umefunikwa na theluji, tukaruka kwa ndege hadi eneo la mishonari lililo bikira—New Guinea ya Uholanzi (sasa Irian Magharibi, Indonesia)—bara la Wapapua.
Je! tulikuwa na shaka juu ya kukubali mgawo huo mgumu? Sivyo hasa. Tulikuwa tumeweka maisha zetu wakfu kwa moyo wote kufanya mapenzi ya Mungu, nasi tuliamini kwamba yeye angetutegemeza. Tukifikiria yale yaliyotukia maishani mwetu, twaweza kuona kwamba uhakika wetu katika Yehova haujapata kuwekwa mahali pabaya kamwe. Lakini kabla ya kusimulia yale yaliyotukia Indonesia, acheni niwaambie juu ya miaka yetu ya mapema.
Mazoezi ya Wakati wa Vita
Familia yangu ilipotembelewa mara ya kwanza katika 1940 na yule Shahidi mwenye moyo mkuu Arthur Winkler, nilikuwa na miaka kumi tu. Wazazi wangu walishtuka walipogundua yale ambayo Biblia ilisema juu ya mafundisho bandia ya Jumuiya ya Wakristo. Kwa kuwa wakati huo Uholanzi ilikuwa imetwaliwa na Ujerumani ya Nazi na Mashahidi wa Yehova walikuwa wakisakwa, wazazi wangu walilazimika kuamua kama watashirikiana na tengenezo lililopigwa marufuku. Waliamua kufanya hivyo.
Baadaye, moyo mkuu wa mama na nia yake ya kukabili hatari ya kupoteza uhuru na hata uhai ilinivutia. Wakati mmoja aliendesha baiskeli umbali wa kilometa 11 akangoja gizani akiwa na mkoba uliojazwa trakti za Biblia. Kwenye wakati uliowekwa wa kampeni ya pekee kuanza, aliendesha baiskeli kasi kadiri ambavyo angeweza, huku akitia mkono mkobani m̃wake kwa kawaida, akitapanya trakti barabarani. Mwendesha-baiskeli mmoja aliyekuwa akimfuata alimpita hatimaye na, kwa kuhema, alipaaza sauti hivi: “Mama, mama, unapoteza kitu fulani!” Mama aliposimulia tukio hilo tulicheka tukacheka.
Nilikuwa mchanga sana, lakini nilijua kile nilichotaka kufanya na maisha yangu. Katika mmoja wa mikutano yetu katika miaka ya katikati ya 1942, kiongozi alipouliza, “Ni nani atakaye kubatizwa kwenye pindi itakayofuata?” nilinyanyua mkono wangu. Wazazi wangu waliangaliana kwa wasiwasi, wakitia shaka kama nilielewa umaana wa uamuzi kama huo. Lakini hata ingawa nilikuwa na miaka 12 tu, nilielewa kilichomaanishwa na wakfu kwa Mungu.
Kuhubiri nyumba kwa nyumba tukiandamwa na Wanazi kulihitaji hadhari. Ili kuepuka kuzuru nyumba za wale ambao wangeweza kuturipoti, katika siku ambazo wale waliowaunga mkono Wanazi walibandika madirishani mwao karatasi kubwa za utangazaji, niliendesha baiskeli kotekote na kuandika anwani zao. Wakati mmoja mwanamume mmoja aliniona akapaaza sauti: “Vema, mwanangu. Waandike—wote!” Nilikuwa na bidii lakini kwa wazi sikuwa mwenye busara ya kutosha! Vita ilipoisha katika 1945, tulishangilia kwa ajili ya taraja la kuwa na uhuru mwingi zaidi wa kuhubiri.
Mwanzo wa Kazi-Maisha
Katika Novemba 1, 1948, baada ya kumaliza shule, nilipokea mgawo wangu wa kwanza wa kuhubiri wakati wote nikiwa painia. Mwezi mmoja baadaye Ndugu Winkler aliizuru familia niliyokuwa nikikaa nayo. Ni lazima iwe alikuwa amekuja kunichunguza kwa sababu muda mfupi baadaye nilialikwa kufanya kazi kwenye ofisi ya tawi ya Sosaiti katika Amsterdam.
Baadaye niliombwa kuzuru makutaniko ya Mashahidi wa Yehova nikiwa mwangalizi wa mzunguko. Kisha, katika vuli ya 1952, nilipokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la 21 la Watchtower Bible School of Gilead katika New York ili kupokea mazoezi ya mishonari. Kwa hiyo, mwisho-mwisho wa 1952, wanne kati yetu kutoka Uholanzi tulipanda ile meli Nieuw Amsterdam tukaabiri hadi Amerika.
Kuelekea mwisho wa mtalaa wa shule, Maxwell Friend, mmoja wa wafunzi, alisema hivi: “Mtasahau mengi kati ya yale ambayo mmejifunza hapa, lakini twatumaini mambo matatu yatabaki nanyi: imani, tumaini, na upendo.” Pia mambo ambayo yameendelea kuwa akilini na moyoni mwangu ni kumbukumbu za tengenezo la Yehova likifanya kazi kwa kuhisi uharaka.
Baadaye nilipatwa na jambo la kukatisha tamaa sana. Nusu kati ya kikundi chetu cha Waholanzi—kutia na mimi—kilipewa mgawo kurudi Uholanzi. Ingawa nilikuwa nimekata tamaa, sikuwa nimeudhika. Nilitumaini tu kwamba nisingelazimika kungojea miaka 40, kama vile Musa wa zamani, kabla ya kupokea mgawo wa kigeni.—Matendo 7:23-30.
Msaidizi Aliyethaminiwa
Ndugu Fritz Hartstang, rafiki yangu aliye kama baba, aliposikia juu ya mipango yangu ya kuoa, aliniambia hivi kisiri: “Hilo ni chaguo lililo bora zaidi.” Babake Susie, Casey Stoové, alikuwa amekuwa mpiganaji mashuhuri katika Upinzani dhidi ya Wanazi wakati wa Vita ya Ulimwengu 2. Lakini alipotembelewa na Mashahidi katika 1946, alikubali kweli za Biblia kwa utayari. Upesi yeye na watatu kati ya watoto wake sita—Susie, Marian, na Kenneth—walibatizwa. Katika Mei 1, 1947, watoto hao wote walianza huduma ya wakati wote wakiwa mapainia. Katika 1948, Casey aliuza biashara yake, naye pia akaanza kupainia. Baadaye alisema hivi: “Miaka hiyo ilikuwa ndiyo yenye furaha zaidi maishani mwangu!”
Nilifahamiana na Susie katika 1949, alipoalikwa kufanya kazi kwenye ofisi ya tawi ya Amsterdam. Lakini, mwaka uliofuata, yeye na dadake Marian waliondoka kwenda kuhudhuria darasa la 16 la Gileadi wakaabiri hadi mgawo wao wa mishonari—Indonesia. Katika Februari 1957, baada ya miaka mitano ya utumishi wa mishonari huko, Susie alirudi Uholanzi kuolewa na mimi. Wakati huo, nilikuwa nikitumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko, na muda wote wa miaka ya ndoa yetu, mara nyingi yeye ameonyesha nia ya kutoa dhabihu za kibinafsi kwa ajili ya utumishi wa Ufalme.
Baada ya arusi yetu, tuliendelea kuzuru makutaniko katika sehemu tofauti-tofauti za Uholanzi. Miaka ambayo Susie alikuwa amekuwa katika kazi ya mishonari katika migawo migumu ilikuwa imemtayarisha vema kwa ajili ya safari zetu kwa baiskeli kutoka kutaniko moja hadi jingine. Tulipokuwa katika kazi ya mzunguko katika 1962 ndipo Ndugu Kushnir aliponizuru katika Rotterdam na kutualika kuhamia Irian Magharibi, Indonesia.
Utumishi wa Mishonari Katika Indonesia
Tuliwasili mji wa Manokwari—wenye mazingira tofauti kabisa! Kulikuwa na sauti zenye kutia hofu za masiku ya tropiki na joto na mavumbi. Kisha kulikuwa na wale Wapapua kutoka barani waliovaa shuka tu, waliobeba simi, na waliopenda kutembea karibu sana nyuma yetu na kujaribu kugusa ngozi zetu nyeupe—mambo ambayo hayakuwa rahisi kuzoea.
Katika muda wa majuma kadhaa ya kuwasili kwetu, makasisi walisoma barua kutoka mimbari za kanisa wakionya dhidi ya Mashahidi wa Yehova, na kutoa nakala yayo kwa wote waliohudhuria. Hata redio ya mahali hapo ilitangaza juu ya barua hiyo. Kisha makasisi watatu walituzuru na kusisitiza kwamba tuhamie barani tukafanye kazi miongoni mwa wale waliowaita “wapagani.” Ofisa mmoja wa polisi Mpapua mwenye cheo cha juu alituhimiza pia tuondoke, na mshiriki mmoja wa polisi wa siri alituambia kwamba mpango ulikuwa ukifanywa wa kutuua kimakusudi.
Lakini, si wote waliotupinga. Mshauri mmoja wa kisiasa wa Wapapua, raia Mholanzi aliyekuwa karibu kuondoka kwenda Uholanzi, alitujulisha kwa machifu kadhaa Wapapua. “Mashahidi wa Yehova wataleta aina ya dini ya Kikristo iliyo bora zaidi ya zile mmepata kujua,” akawaambia. “Kwa hiyo, mwapaswa kuwakaribisha.”
Baadaye, ofisa mmoja wa serikali alimjia Susie barabarani akanong’ona hivi: “Imeripotiwa kwetu kwamba mmeanza kazi mpya huku, na, kwa hiyo, hatuwezi kuwaruhusu mkae. Lakini, eh, . . . laiti mngalikuwa na kanisa.” Hicho kilikuwa kidokezo! Upesi tulibomoa kuta katika nyumba yetu, tukapanga mabenchi, tukaweka kinara cha msemaji, na kuweka ishara nje kwenye sehemu ya mbele iliyosema “Jumba la Ufalme.” Halafu tukamwalika ofisa huyo azuru. Alikupia kichwa, akatabasamu, na kupiga-piga upande wa kichwa chake kwa kidole chake cha shahada, kana kwamba kusema, ‘Mmetumia akili, mmetumia akili.’
Katika Juni 26, 1964, mwaka na nusu baada ya kuwasili kwetu, Wapapua 12 wa kwanza kati ya wanafunzi wetu wa Biblia walibatizwa. Muda mfupi baadaye, 10 wengine walifuata, na hudhurio letu la mkutano lilikuwa na wastani wa 40. Mapainia wawili Waindonesia walitumwa kutusaidia. Kutaniko lilipokuwa limeimarishwa vizuri katika Manokwari, tawi la Sosaiti la Indonesia lilituandalia mgawo mwingine wa kuhubiri, katika Desemba 1964.
Kabla ya sisi kuondoka, mkuu wa Idara ya Uhusiano ya serikali alituchukua faraghani na kusema: “Nasikitika mwaondoka. Kila juma makasisi walinisihi niwaondoshe kwa sababu walisema kwamba mlikuwa mkiyachuma matunda yao. Lakini niliwaambia: ‘La, bali, wanarutubisha miti yenu.’” Aliongoza hivi: “Kokote mwendako, endeleeni kupiga vita. Mtashinda!”
Katikati ya Mapinduzi
Usiku moja katika Septemba 1965, tulipokuwa tukitumikia katika jiji kuu, Djakarta, waasi Wakomunisti waliua viongozi wengi wa kijeshi, wakachoma moto Djakarta, na kuanza harakati yenye kuenea taifa lote ambayo hatimaye ilimpindua rais wa taifa hilo, Sukarno. Watu 400,000 hivi walipoteza uhai wao!
Wakati mmoja tulikuwa tukihubiri huku risasi zikipigwa na uchomaji wa moto katika barabara ya upande mwingine. Siku iliyofuata tulisikia kwamba jeshi lilikuwa karibu kuharibu jengo la Kikomunisti lililokuwa karibu. Wenye nyumba walionekana wenye kuogopa tulipowajia, lakini waliposikia ujumbe wetu wa Biblia, walistarehe na kutualika ndani. Walihisi salama kuwa nasi. Kipindi hicho kilitufundisha sisi sote kumtegemea Yehova na kudumisha usawaziko chini ya hali mbaya.
Upinzani Zaidi Washindwa
Mwisho-mwisho wa 1966 tulihamia jiji la Ambon kwenye visiwa vya Moluka kusini vyenye kupendeza. Huko, miongoni mwa wakazi wachangamfu, wenye urafiki, tulipata kupendezwa kwingi kwa kiroho. Kutaniko letu dogo lilikua upesi, na hudhurio la mkutano lilikaribia mia moja. Kwa hiyo maofisa wa kanisa la Jumuiya ya Wakristo walizuru Ofisi ya Mambo ya Kidini ili kumsonga mkubwa wayo atulazimishe tuondoke Ambon. Lakini hapo kwenye dawati la chifu huyo, waliona vitabu vya Watch Tower Society vikiwa vimewekwa ili viweze kuonekana wazi! Wakiwa wameshindwa kubadili nia ya chifu huyo waliwasiliana na maofisa wa Wizara ya Dini katika Djakarta, wakijaribu kufanya tufukuzwe si kutoka Ambon pekee bali pia kutoka Indonesia yote.
Wakati huo walionekana wamefanikiwa, kwani Februari 1, 1968, ilikuwa imewekwa kuwa tarehe ya kufukuzwa kwetu. Hata hivyo, ndugu zetu Wakristo katika Djakarta waliwasiliana na ofisa mmoja Mwislamu mwenye cheo cha juu katika Wizara ya Dini, naye akasaidia kupindua uamuzi huo. Kwa kuongezea, sera ya zamani ilibadilishwa, na wamishonari wengine bado wakaruhusiwa waingie nchini.
Hivyo, katika ile miaka kumi iliyofuata, tukiwa katika mandhari ya milima, misitu, na maziwa ya maji yenye fahari kaskazini mwa Sumatra, tulifanya kazi pamoja na wamishonari kutoka Australia, Austria, Ufilipino, Ujerumani, United States, na Uswedi. Kazi ya kuhubiri ilifanikiwa, hasa miongoni mwa kabila kuu la mkoa huo, Wabataki.
Hata hivyo, wala-njama wa kidini walifanikiwa hatimaye kufanya kazi yetu ya kuhubiri ipigwe marufuku katika Desemba 1976, na mwaka uliofuata wengi kati ya wamishonari waliondoka kwenda kwenye migawo katika nchi nyinginezo. Mwishoni, katika 1979, sisi pia tulilazimika kwenda.
Hadi Amerika Kusini
Kufikia sasa tulikuwa na umri wa miaka karibu 50, na tulijiuliza kama tungeweza kujirekebisha na hali ya nchi nyingine bado. “Je! tukubali mgawo mpya au badala ya hivyo tukae mahali fulani hususa?” Susie akauliza.
“Susie,” nikajibu, “kokote ambako Yehova alitualika twende, alitutunza. Ni nani ajuaye ni baraka gani nyinginezo zilizo katika wakati ujao?” Hivyo, tuliwasili katika mgawo wetu mpya, nchi ya Amerika Kusini ya Suriname. Katika muda wa miezi miwili tulikuwa katika kazi ya kusafiri tena na upesi tukahisi tumestareheka.
Tukipitia miaka yetu zaidi ya 45 katika huduma ya wakati wote, Susie na mimi twang’amua jinsi ambavyo utegemezo wa wazazi wetu ulikuwa wa maana ili kutusaidia tuendelee katika kazi ya mishonari. Katika 1969, nilipowaona wazazi wangu tena baada ya miaka sita, baba yangu alinichukua kando akasema: “Mama akitukia kufa kwanza, hamhitaji kuja nyumbani. Kaeni katika mgawo wenu. Nitaweza hali. Lakini ikiwa kinyume, mtapaswa kumwuliza Mama juu ya hilo.” Mama alisema vivyo hivyo.
Wazazi wa Susie walikuwa na mtazamo uo huo usio na ubinafsi. Wakati mmoja Susie alikuwa amekuwa mbali nao kwa miaka 17, lakini hawakumwandikia kamwe neno moja la kuvunja moyo. Bila shaka, ikiwa msaada mwingine usingalipatikana kwa ajili ya wazazi wetu, tungalirudi nyumbani. Jambo ni kwamba, wazazi wetu walikadiria kazi ya mishonari kwa njia iyo hiyo na, hadi kifo chao, walikuwa wamemtumikia Yehova kwa kuhisi uharaka uleule waliokuwa wameingiza mioyoni mwetu.—Linganisha 1 Samweli 1:26-28.
Tumetiwa moyo pia na wenye kutuandikia barua kwa kawaida. Kuna wachache ambao hawajakosa kamwe mwezi mmoja kutuandikia barua katika utumishi wetu wa mishonari wa miaka zaidi ya 30! Lakini zaidi ya yote, twamkumbuka Baba yetu mpendwa wa kimbingu, Yehova, ajuaye namna ya kuwategemeza watumishi wake duniani. Kwa hiyo, tukaribiapo upeo wa matukio ambayo tumekuwa tukitazamia, Susie nami twatamani kuweka “karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova” kwa kuendelea kumtumikia Yehova kwa kuhisi uharaka.—2 Petro 3:12, NW.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Kuoana katika 1957
[Picha katika ukurasa wa 29]
Ni msisimuko ulioje—wachanga sita wakiwa mapainia!