Mashahidi wa Yehova Ulimwenguni Pote—Jamhuri ya Ufilipino
VILE visiwa 7,083 vyenye mawe-mawe vya kitropiki vinavyofanyiza Jamhuri ya Ufilipino ni sehemu ya juu zaidi ya mfululizo wa milima uliozama baharini kwa sehemu.a Na wale wakazi 62,000,000 wa Ufilipino hupenda kuongea juu ya karibu habari yoyote. Roho hiyo ya upole hutokeza shamba lenye rutuba kwa ajili ya ushahidi wa Ufalme.
Kutoa Ushahidi Shuleni
Kwenye kisiwa cha Masbate, mwanafunzi mchanga mmoja wa shule ya upili aliweza kutoa ushahidi kwa mwalimu wake na darasa lake katika mtihani mmoja wa kujibu kweli au si kweli. Yeye aripoti hivi:
“Taarifa ilikuwa, ‘Ikiwa Mungu anipenda mimi, yeye hatanipa matatizo au kuniruhusu niteseke.’ Mwalimu wangu alipochunguza karatasi zetu [za mtihani], aliona kwamba wote isipokuwa mimi walijibu kweli. Mwalimu wangu aliniruhusu nieleze darasa kwa nini nilijibu si kweli. Nilisema kwamba si Mungu ambaye hutupa sisi matatizo, ingawa yeye huruhusu mateso na kuturuhusu tutahiniwe. Nikitumia Biblia yangu, ambayo mimi hupeleka shuleni sikuzote, nilisababu na darasa juu ya maneno kwenye 1 Yohana 4:8, ‘Mungu ni upendo.’ Baada ya elezo langu, mwalimu wangu alisadikishwa, akagonga dawati lake, na kusema: ‘Marilou amesema kweli.’ Mimi pekee ndiye niliyepata jibu sahihi kwa swali hilo na nilipokea maksi za juu zaidi.”
Ujumbe wa Ufalme Uko Kotekote
Alipokuwa akishiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba katika sehemu nyingine ya Ufilipino, painia mmoja wa kawaida (mpiga mbiu ya habari njema wa wakati wote) alikutana na mama wa watoto wadogo watatu. Mwanamke huyo alionyesha kupendezwa sana na ujumbe wa Ufalme, na hilo likafanya iwe rahisi kuanzisha funzo la Biblia pamoja naye. Ingawa mume wake hakupendezwa kwamba alikuwa akipokea masomo ya Biblia, hasa kutoka kwa Mashahidi wa Yehova, funzo liliendelea.
Mtu huyo alihamisha familia yake hadi jiji jingine, akifikiri kwamba hilo lingekomesha ushirika wa mke wake pamoja na Mashahidi. Hata hivyo, haukuwa muda mrefu kabla yao kumpata mwanamke huyo, na alianzisha tena funzo lake la Biblia. Bila shaka, mume wake aliudhika sana. Alipeleka hasira yake kazini, ambako alieleza hisia zake kwa mteja mmoja ambaye alikuwa akimtengenezea gari lake. Mtu huyo hakujua kwamba mteja huyo alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
Shahidi alimweleza kwamba ikiwa mke wake angeendelea na masomo yake ya Biblia hilo lingeinufaisha sana familia nzima. Yeye angeweza kuanza kutumia kanuni za Biblia humohumo nyumbani. Ilidokezwa pia kwamba mume mwenyewe angeweza kunufaika kwa kujifunza juu ya Ufalme wa Mungu.
Matokeo ya mazungumzo hayo yalikuwa nini? Mke wa mtu huyo alikuwa na uhuru zaidi wa kujifunza Biblia, na mtu huyo akaamua kurudisha familia yake nyumbani ilikokuwa hapo awali. Huko mwanamke huyo alifanya maendeleo ya kiroho hadi kufikia hatua ya kuwa mhubiri wa Ufalme asiyebatizwa. Mume wake pia alikubali funzo la Biblia, na familia nzima ikaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi, ona 1994 Calendar of Jehovah’s Witnesses.
[Sanduku katika ukurasa wa 8]
HABARI ZA NCHI
Mwaka wa Utumishi wa 1993
KILELE CHA WANAOTOA USHAHIDI: 116,576
UWIANO: Shahidi 1 kwa Watu 549
HUDHURIO LA UKUMBUSHO: 357,388
WASTANI WA WAHUBIRI WALIO MAPAINIA: 22,705
WASTANI WA MAFUNZO YA BIBLIA: 94,370
IDADI YA WALIOBATIZWA: 7,559
IDADI YA MAKUTANIKO: 3,332
OFISI YA TAWI: MANILA
[Picha katika ukurasa wa 9]
Kutoa ushahidi sokoni huleta matokeo mazuri
[Picha katika ukurasa wa 9]
Ofisi ya tawi ya Watchtower Society katika Manila