Mashahidi wa Yehova Ulimwenguni Pote—Bahamas
JAMHURI ya Bahamas—kikundi cha visiwa na vijisiwa 3,000—yaenea kwa kilometa 900 kama ushanga wa matumbawe kwenye bahari ya kijani-samawi kati ya Florida na Kyuba. Miongoni mwa wakazi walo 267,000 kuna korasi inayoongezeka ya wapiga mbiu ya Ufalme. Wimbo wao wa sifa watukumbusha Isaya 42:10-12: “Mwimbieni BWANA [Yehova, NW] wimbo mpya, na sifa zake tokea mwisho wa dunia; ninyi mshukao baharini, na vyote vilivyomo, na visiwa, nao wakaao humo. . . . Wapige kelele toka vilele vya milima. Na wamtukuze BWANA [Yehova, NW], na kutangaza sifa zake visiwani.”
Imani Mpya Yakabili Ushindani
Katika Julai 1992, painia mmoja wa kawaida (mhubiri wa Ufalme wa wakati wote) aliangushia mtu aliyemfahamu kibiashara, kile kitabu cha msaada wa kujifunza Biblia Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Baada ya mtu huyo kusoma kitabu hicho, yeye alijiambia mwenyewe hivi, ‘Ni lazima nichunguze dini hii.’ Katika Jumapili mbili zilizofuata, yeye alihudhuria mikutano kwenye Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova mawili tofauti. Halafu, funzo la Biblia likaanzishwa pamoja naye. Hata hivyo, majuma sita tu baada ya yeye kuanza kujifunza Biblia, alikabili ushindani uliotahini imani yake mpya—sherehe za siku ya kuzaliwa.
Familia ya mfanya-biashara huyo ilihusika sana na sherehe hizo, lakini kupenda Neno la Mungu kulimchochea aendelee na masomo yake ya Biblia. Kadiri ujuzi wake wa kweli ya Kimaandiko ulivyoongezeka, ndivyo uelewevu wake wa sherehe za siku ya kuzaliwa na sikukuu za kilimwengu na maoni ya Yehova juu yazo ulivyoongezeka.
Mke wa mtu huyo alipoandaa kikusanyiko cha kirafiki kwa ajili ya Siku ya Baba, yeye alikataa kwa upole kuhudhuria. Hata hivyo, mke huyo alihisi kwamba mume wake hakumpenda tena na alikuwa akiweka dini yake mahali pa kwanza badala ya yeye na familia. Mume huyo alieleza kwa fadhili kwamba kutumia yale aliyokuwa akijifunza kutoka kwa Biblia kulikuwa kukimsaidia kubadilika kuwa mume na baba bora zaidi. Hatimaye, mke huyo alianza kuthamini upendo wa mume wake kwa ajili ya kweli ya Kimaandiko akakubali kujifunza Biblia. Sasa yeye huongoza funzo la Biblia pamoja na familia yake. Na ni furaha iliyoje aliyopata kwenye Mkusanyiko wa Wilaya wa “Ufundishaji wa Kimungu” mwaka uliopita! Mke wake na binti yake walikuwako nao wakamwona akibatizwa.
Wahamiaji Wasikia ule Wimbo Mpya
Maelfu ya wahamiaji kutoka Haiti huishi katika jumuiya ya Wabahama. Wao pia wahitaji kusikia ule wimbo mpya wa kweli ya Ufalme. Mashahidi wanaoishi katika Bahamas washukuru kwamba Waamerika-Wahaiti wawili pamoja na wake zao wamewasili. Watu hao wamesaidia kuimarisha vikundi vya Wahaiti vilivyofanyizwa hivi karibuni katika visiwa vya Grand Bahama na Abaco.
Ukiwa msaada zaidi kwa Wahaiti wanaopendezwa na ujumbe wa Ufalme, mkusanyiko wa wilaya wa kwanza wa Kikreole uliopata kufanywa katika Bahamas ulifanywa kuanzia Julai 31 hadi Agosti 1, 1993. Hudhurio lilifikia 214, huku watatu waliojiweka wakfu hivi karibuni wakibatizwa. Wahaiti wengi waliojifunza kweli katika Bahamas wamerudi kwao au wamehamia kwingineko ili kuongeza sauti zao kwenye zile za Mashahidi wenyeji katika kumwimbia Yehova sifa.
[Sanduku katika ukurasa wa 8]
HABARI ZA NCHI
Mwaka wa Utumishi wa 1993a
KILELE CHA WANAOTOA USHAHIDI: 1,294
UWIANO: Shahidi 1 kwa watu 197
HUDHURIO LA UKUMBUSHO: 3,794
WASTANI WA WAHUBIRI WALIO MAPAINIA: 186
WASTANI WA MAFUNZO YA BIBLIA: 1,715
IDADI YA WALIOBATIZWA: 79
IDADI YA MAKUTANIKO: 22
OFISI YA TAWI: NASSAU
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi, ona 1994 Calendar of Jehovah’s Witnesses.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Jumba la Ufalme la kwanza, likiwa na ofisi ya tawi na makao ya wamishonari
[Picha katika ukurasa wa 9]
Mashahidi hujulisha habari njema kwa bidii
[Picha katika ukurasa wa 9]
Milton G. Henschel na Nathan H. Knorr wakiwa na wamishonari katika Nassau miaka ipatayo 45 iliyopita
[Picha katika ukurasa wa 9]
Ofisi mpya ya tawi, iliyowekwa wakfu Februari 8, 1992