Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w01 6/1 kur. 23-27
  • Mwenye Furaha na Shukrani Licha ya Kufiwa na Mpendwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mwenye Furaha na Shukrani Licha ya Kufiwa na Mpendwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mazoezi ya Huduma
  • Jinsi Tulivyopata Kibali cha Kukaa
  • Eneo Jipya
  • Huzuni Kubwa
  • Baraka za Huduma Zinazofurahisha
  • Ninashukuru Sana
  • Mashahidi wa Yehova Ulimwenguni Pote—Bahamas
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Wamishonari Wasukuma Mpanuko wa Ulimwenguni Pote
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Sehemu ya 4—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Tumebarikiwa Sana kwa Kujidhabihu Katika Mambo Madogo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
w01 6/1 kur. 23-27

Simulizi la Maisha

Mwenye Furaha na Shukrani Licha ya Kufiwa na Mpendwa

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA NANCY E. PORTER

Ilikuwa jioni yenye joto, Juni 5, 1947 kwenye visiwa vya Bahamas ambavyo viko karibu na pwani ya kusini-mashariki ya Marekani. Afisa mmoja wa uhamiaji alitutembelea mimi na mume wangu George bila kutarajiwa. Alitupatia barua iliyosema kwamba hatukutakiwa humo visiwani tena, na kwamba ‘tulipaswa kuondoka mara moja!’

MIMI na George tulikuwa wamishonari wa kwanza wa Mashahidi wa Yehova kutumwa huku Nassau, mji mkuu wa Bahamas. Tulipohitimu darasa la nane la shule ya Gileadi, ambayo ni shule ya kuzoeza wamishonari huko New York, tulitumwa Bahamas. Tulikuwa tumefanya nini ili tufukuzwe baada ya miezi mitatu tu? Inawezekanaje niko huku bado, baada ya miaka zaidi ya 50?

Mazoezi ya Huduma

Baba yangu, Harry Kilner, alikuwa na uvutano mkubwa sana katika maisha yangu. Alikuwa kielelezo kizuri sana kwangu. Alijidhabihu sana awe mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ijapokuwa afya yake haikuwa nzuri, alikwenda kuhubiri karibu kila mwisho-juma. Alijitahidi sana kutanguliza masilahi ya Ufalme. (Mathayo 6:33) Hali yetu ya kifedha haikuwa nzuri, hata hivyo katika miaka ya 1930 duka lake la viatu huko Lethbridge, Alberta, Kanada, lilikuwa kituo cha shughuli za kiroho. Ninakumbuka hasa watumishi wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, waitwao mapainia, waliotutembelea na kusimulia mambo waliyoona katika kazi ya kuhubiri.

Katika mwaka wa 1943, nilianza kutumikia kama painia karibu na Fort Macleod na Claresholm, Alberta. Wakati huo kazi yetu ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku nchini Kanada kwa sababu ya habari za uwongo ambazo zilienezwa na wapinzani wakati Vita ya Pili ya Ulimwengu ilipokuwa inaendelea. Eneo letu lilikuwa na umbali wa kilometa 100 kutoka upande mmoja hadi ule mwingine. Hata hivyo, kwa sababu tulikuwa vijana wenye nguvu, hatukuona ugumu wowote kutembea au kuendesha baiskeli kwenda kuhubiri katika vijiji na miji midogo na kuwahubiria wakulima katika eneo hilo. Katika pindi hiyo, nilikuwa na fursa ya kuongea na wahitimu wengine wa shule ya Gileadi. Walioyasimulia yalinivutia na yakaamsha tamaa yangu ya kuwa mishonari.

Niliolewa na George Porter wa Saskatchewan, Kanada, katika mwaka wa 1945. Wazazi wake pia walikuwa Mashahidi wenye bidii tangu 1916, na yeye pia alikuwa ameamua kufanya utumishi wa wakati wote uwe kazi yake. Kwanza tulitumwa Lynn Valley, eneo maridadi la North Vancouver, Kanada. Muda mfupi badaaye tukaitwa kwenda shule ya Gileadi.

Katika miaka iliyopita nimeongea na wahitimu wa shule za theolojia na kuona jinsi ambavyo masomo yao ya kitheolojia yameharibu imani yao katika Mungu na Neno Lake, Biblia. Kinyume cha hilo, shule ya Gileadi ilitusaidia kutumia akili, na zaidi ya yote iliimarisha imani yetu katika Yehova Mungu na Neno lake. Wanafunzi wenzetu walitumwa China, Singapore, India, nchi za Afrika, Amerika Kusini, na penginepo. Bado ninaweza kukukumbuka jinsi tulivyosisimuka tulipojua kwamba tungetumwa katika visiwa vyenye joto vya Bahamas.

Jinsi Tulivyopata Kibali cha Kukaa

Safari yetu ya kwenda Bahamas ilikuwa fupi ikilinganishwa na safari za wanafunzi wenzetu kwenda mahali walipotumwa. Baada ya muda mfupi tulifurahia joto, anga na maji ya baharini yenye rangi ya samawati, majengo yenye rangi nyeupe-nyeupe, na baiskeli nyingi zisizohesabika. Hasa ninawakumbuka wale Mashahidi watano waliotulaki meli yetu ilipowasili. Muda si muda tulijifunza kwamba utamaduni wa huku ni tofauti sana na ule ambao tulikuwa tumezoea. Kwa mfano, mume wangu aliombwa asiniite mpenzi hadharani, kwa kuwa usemi huo hutumiwa hasa kuhusu uhusiano wa nje ya ndoa.

Baada ya muda mfupi makasisi walitushtaki kuwa Wakomunisti. Yaelekea walifanya hivyo kwa sababu walituona kuwa tisho kwao walipoona jinsi tulivyoshirikiana na watu bila vizuizi. Kwa sababu hiyo, tuliamuriwa tuondoke nchini. Lakini Mashahidi wa visiwani ambao idadi yao ilipungua 20 siku zile, mara moja walipata maelfu ya watu waliotia sahihi ombi la kuturuhusu kukaa nchini. Kwa hiyo, amri ya kutufukuza nchini ikabatilishwa.

Eneo Jipya

Watu wa Bahamas wanampenda Mungu. Kwa hiyo, walikubali bila kusita kweli ya Biblia, na mishonari wengine waliohitimu Gileadi wakatumwa huku. Kisha, katika mwaka wa 1950, ofisi ya tawi ikaanzishwa. Miaka kumi baadaye, Milton Henschel ambaye anafanya kazi kwenye makao makuu huko Brooklyn, New York, alitembelea Bahamas na kuuliza ikiwa mishonari yeyote angekuwa tayari kwenda kuanzisha kazi ya kuhubiri kwenye kisiwa kingine cha Bahamas. Mimi na George tulijitolea kwenda kisiwani Long Island, tukaishi huko kwa muda wa miaka 11.

Kisiwa hicho ni mojawapo ya visiwa vya Bahamas na kina urefu wa kilometa 140 na upana wa kilometa 6. Hakukuwapo miji katika kisiwa hicho siku hizo. Makao makuu ya Bahamas yaitwayo Clarence Town yalikuwa na nyumba 50 hivi. Maisha yalikuwa ya kizamani—hakuwa na umeme, maji ya mifereji, wala chumba cha kupikia, wala maji ndani ya nyumba. Kwa hivyo, tulihitaji kuzoea kile kinachoitwa maisha ya kisiwa cha mbali. Huko watu walipenda sana kuzungumzia hali ya afya. Tulizoea kuwasalimu watu bila ya kuuliza, “Habari yako?” kwa kuwa mara nyingi walijibu swali hilo kwa kueleza kwa urefu matatizo yao yote ya afya ambayo wamewahi kupata.

Tulifanya kazi ya kuhubiri kwa kwenda jikoni hadi jikoni kwa sababu kwa kawaida watu walipatikana jikoni. Walipikia katika nyumba ya nyasi yenye jiko la kuni. Watu wa vijiji walikuwa wakulima na wavuvi wa samaki wenye urafiki lakini maskini. Wengi wao walikuwa wafuasi wa dini lakini waliamini sana ushirikina pia. Mara nyingi matukio yasiyo ya kawaida yalionwa kuwa dalili ya jambo fulani.

Makasisi hawakuona aibu kuingia nyumbani mwa watu bila kualikwa na kuvirarua vichapo vya Biblia ambavyo tulikuwa tumewaachia wenye nyumba. Watu waoga walirudi nyuma, lakini si wote. Kwa mfano, mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 70 hakutishwa. Alitaka kuelewa Biblia, na hatimaye akawa Shahidi na vilevile watu kadhaa wengine. Wengi walipoanza kupendezwa George alihitaji kuendesha gari lake kilometa 300 Jumapili kadhaa, ili kuwasaidia wenye kupendezwa kuhudhuria mikutano.

Miaka ya mapema, wakati ambapo sisi tulikuwa Mashahidi pekee katika kisiwa hicho, mimi na George tulidumisha hali nzuri ya kiroho kwa kufanya mikutano yote ya Kikristo. Mbali na hilo tulijitahidi kujifunza somo la gazeti la Mnara wa Mlinzi na kusoma Biblia kila Jumatatu jioni. Tulisoma pia kila nakala ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! mara tulipoyapokea.

Baba yangu alikufa tulipoishi Long Island. Majira ya kiangazi ya mwaka wa 1963, tukapanga mama yangu aje kuishi karibu nasi. Hata ingawa alikuwa mzee alizoea maisha ya Long Island kwa kadiri fulani, akaishi huko hadi kifo chake mwaka wa 1971. Kwenye kisiwa cha Long Island kuna kutaniko na Jumba la Ufalme jipya siku hizi.

Huzuni Kubwa

Katika mwaka wa 1980, George alitambua kwamba afya yake ilianza kuharibika. Hiyo ilikuwa pindi ngumu sana maishani mwangu. Mume wangu mpendwa, mfanyi-kazi mwenzangu, na rafiki yangu, alikuwa anaugua ugonjwa wa Alzheimer (hali ya upungufu wa uwezo wa akili). Utu wake ulibadilika kabisa. Afya yake ikaharibika kabisa katika miaka yake minne ya mwisho. Alikufa mwaka wa 1987. Aliandamana nami kwenye utumishi na kwenye mikutano hadi aliposhindwa kabisa, ijapokuwa nililia machozi mara nyingi nilipoona jitihada zake. Upendo wa ndugu Wakristo umenifariji sana tangu kifo chake, hata hivyo ninamkosa sana.

Mimi na George tulikuwa na mazungumzo ya ukawaida yenye kufurahisha na nilithamini jambo hilo sana. Sasa, kwa kuwa George amekufa, nashukuru sana kwamba Yehova anawaalika watumishi wake ‘wasali bila kukoma,’ ‘wadumu katika sala,’ na kutoa “kila namna ya sala.” (1 Wathesalonike 5:17; Waroma 12:12; Waefeso 6:18) Ni faraja kubwa kujua kwamba Yehova anatujali. Ninakubaliana kabisa na mtunga-zaburi aliyeimba hivi: “Na ahimidiwe Bwana, siku kwa siku hutuchukulia mzigo wetu.” (Zaburi 68:19) Kutohangaikia ya kesho, kukubali hali yangu, na kushukuru kwa baraka za kila siku, kama vile Yesu alivyosema, ni njia bora ya maisha.—Mathayo 6:34.

Baraka za Huduma Zinazofurahisha

Kuwa na shughuli nyingi katika huduma ya Kikristo kumenisaidia kutozingatia kupita kiasi mambo yaliyopita. Kwa njia hiyo nimeshinda hisia zinazosababisha kuvunja moyo. Kuwafundisha wengine kweli ya Biblia kumeniletea furaha ya kipekee. Shughuli hizo zote zimenisaidia kuwa na taratibu ya kiroho ambayo imeimarisha maisha yangu.—Wafilipi 3:16.

Wakati mmoja nilipata simu kutoka kwa mwanamke ambaye nilikuwa nimemtolea ujumbe wa Ufalme miaka 47 hivi awali. Alikuwa binti ya mmoja wa wanafunzi wetu wa kwanza wa Biblia tulipowasili Bahamas katika mwaka wa 1947. Mama yake, baba, na ndugu na dada zake wote na vilevile wengi wa watoto na wajukuu wao, wakawa Mashahidi wa Yehova. Zaidi ya washiriki 60 wa jamaa ya mwanamke huyo ni Mashahidi. Lakini yeye mwenyewe hakukubali kweli ya Biblia. Hata hivyo, sasa alikuwa tayari kuwa mtumishi wa Yehova Mungu. Mimi na George tulipowasili huku Bahamas, kulikuwa na Mashahidi wachache sana. Ni furaha kama nini kuona Mashahidi zaidi ya 1,400 leo!

Mara kwa mara watu huniuliza ikiwa ninasikitika kwamba sina watoto wangu mwenyewe. Bila shaka, watoto wanaweza kuwa baraka. Hata hivyo, huenda wazazi waliozaa watoto wasipate kuonyeshwa upendo ambao ninaonyeshwa na watoto, wajukuu, na vitukuu wangu wa kiroho. Kwa kweli wale ‘wanaofanya mema’ na walio “matajiri katika kazi zilizo bora” ni watu wenye furaha. (1 Timotheo 6:18) Kwa hiyo ninajitahidi kuwa na shughuli katika huduma kwa kadiri niwezavyo.

Siku moja tulipokuwa kwa daktari wa meno, mwanamke mmoja mchanga alianza kuongea nami na kusema, “Wewe hunijui, lakini ninakujua, na ninataka tu kukuambia kwamba nakupenda.” Kisha akaeleza jinsi alivyopata kujua kweli ya Biblia na jinsi anavyoshukuru kwamba sisi mishonari tulikuja huku Bahamas.

Wakati mmoja nilipotoka likizoni na kurudi kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huku Nassau ninakoishi sasa, nilipata waridi moja kwenye mlango wangu. Lilikuwa na ujumbe huu, “Tunafurahi kuwa umerudi nyumbani.” Ninampenda Yehova na kumshukuru sana ninapoona watu wazuri ambao Neno na tengenezo lake, na vilevile roho yake imetokeza! Naam, mara nyingi Yehova hutumia wale walio karibu nasi kututegemeza.

Ninashukuru Sana

Maisha yangu hayakuwa rahisi, na mpaka leo nina matatizo fulani. Lakini nina sababu nyingi ya kushukuru—furaha ya huduma, upendo wa ndugu na dada wengi Wakristo, utunzaji wenye upendo wa tengenezo la Yehova, kweli nzuri ajabu ya Biblia, tumaini la kuwa pamoja na wapendwa waliokufa watakapofufuliwa, na kumbukumbu za miaka 42 ya ndoa pamoja na mtumishi mwaminifu wa Yehova. Kabla hatujaoana, niliomba kwamba niweze daima kumsaidia mume wangu kudumu katika utumishi wa wakati wote ambao alipenda mno. Yehova alijibu sala hiyo. Kwa hiyo ninataka kuonyesha shukrani yangu kwa Yehova kwa kuendelea kudumisha uaminifu wangu kwake.

Watalii wanapenda kuja huku Bahamas kufurahia mambo yenye kupendeza katika sehemu hii ya joto na wanalipa maelfu ya dola za Marekani ili kufanya hivyo. Kwa kuwa nilichagua kumtumikia Yehova popote ambapo tengenezo lake linanielekeza, nimefurahia kusafiri kotekote katika visiwa hivi nikitangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Lakini jambo muhimu ni kwamba, nimekuja kujua na kuthamini upendo wa watu bora wenye urafiki wa Bahamas.

Ninawashukuru sana wale ambao waliwafundisha wazazi wangu kweli. Nilipokuwa mchanga wazazi wangu walisitawisha katika akili na moyo wangu tamaa ya kutanguliza Ufalme wa Mungu. Watumishi wachanga wa Yehova wa siku hizi wanaweza vilevile kupokea baraka nyingi wakiingia kupitia “mlango mkubwa” ambao huelekeza kwenye fursa nyingi ya kupanua huduma. (1 Wakorintho 16:9) Wewe pia utakuwa mwenye shukrani nyingi ukitumia maisha yako kumstahi “Mungu wa miungu,” Yehova.—Kumbukumbu la Torati 10:17; Danieli 2:47.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kutoa ushahidi barabarani huko Victoria, B.C., katika mwaka wa 1944

[Picha katika ukurasa wa 24]

Mimi na George tulihudhuria Shule ya Gileadi mwaka wa 1946

[Picha katika ukurasa wa 25]

Mimi na George mbele ya nyumba ya wamishonari Nassau, Bahamas, katika mwaka wa 1955

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nyumba ya wamishonari huko Deadman’s Cay, ambapo tulitumikia kuanzia mwaka wa 1961 hadi 1972

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki