Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 7/1 kur. 14-17
  • Ni Nini Kimepata Mamlaka?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Nini Kimepata Mamlaka?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mamlaka Imo Mashakani
  • Utafutaji wa Mwanadamu wa Mamlaka Halali
  • “Mamlaka Mbili,” “Panga Mbili”
  • Ile Ngano ya Utawala wa Walio Wengi
  • Ngano ya Taifa Kujitawala
  • Jitihada za Wanadamu Zimeshindwa
  • Maoni ya Mkristo Kuhusu Mamlaka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Uzuri wa Enzi Kuu ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Heshima kwa Mamlaka—Kwa Nini Ni Muhimu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Serikali Moja Ile ya Ulimwengu Mmoja Chini ya Enzi Kuu ya Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 7/1 kur. 14-17

Ni Nini Kimepata Mamlaka?

WATU wenye kufikiri huona uhitaji wa kuwa na mamlaka. Bila kuwapo kwa muundo fulani wa mamlaka, upesi jamii ya binadamu ingevurugika. Kwa hiyo, kitabu cha kale cha Kifaransa cha kufundisha sheria za katiba chasema hivi: “Katika kikundi chochote cha wanadamu, kuna matabaka mawili ya watu: wale wanaoamuru na wale wanaotii, wale wanaotoa maagizo na wale wanaoyafuata, viongozi na washiriki, watawala na watawaliwa. . . . Kuna mamlaka katika jamii yoyote ile ya wanadamu.”a

Hata hivyo, mitazamo kuelekea mamlaka imebadilika tangu Vita ya Ulimwengu 2 na hasa tangu miaka ya 1960. Akieleza juu ya kipindi hicho, Encyclopædia Universalis ya Kifaransa yataja kuzuka kwa “tatizo la kupinga utawala na mamlaka.” Tatizo kama hilo halishangazi wanafunzi wa Biblia. Mtume Paulo alitabiri hivi: “Kumbuka, enzi ya mwisho ya ulimwengu huu itakuwa kipindi cha msukosuko! Watu hawatapenda chochote ila wenyewe na fedha; watakuwa wenye maringo, wenye kiburi, na wenye kutukana; wasiotii wazazi . . . ; hawatajizuia katika chuki zao, . . . wasiojidhibiti na wenye jeuri, . . . wakijivuna kwa kujiona kuwa wa maana. Watapenda anasa zao zaidi kuliko Mungu wao.”—2 Timotheo 3:1-4, The Revised English Bible.

Mamlaka Imo Mashakani

Unabii huo wafafanua vema siku zetu na enzi yetu. Mamlaka inabishaniwa katika sehemu zote—familia, shule za umma, vyuo vikuu, biashara, mabaraza ya mitaa na ya taifa. Yale mapinduzi katika ngono, muziki halisi wa rapu, maandamano ya wanafunzi, kususia kazi, migomo ya kazi, na vitendo vya kiharamia vyote ni ishara za kwamba watu wamekoma kustahi mamlaka.

Katika mkutano mmoja uliopangwa kufanywa jijini Paris na Taasisi ya Ufaransa ya Sayansi ya Kisiasa na gazeti la kila siku la Paris Le Monde, Profesa Yves Mény alisema hivi: “Mamlaka yaweza kudumu tu iwapo ni halali.” Sababu moja inayotokeza tatizo la mamlaka ni kwamba wengi hutilia shaka uhalali wa wale wenye mamlaka. Yaani, wanatilia shaka haki yao ya kuwa na mamlaka. Uchunguzi fulani wa maoni ulifunua kwamba katika miaka ya mapema ya 1980, asilimia 9 ya idadi ya watu nchini Marekani, asilimia 10 nchini Australia, asilimia 24 nchini Uingereza, asilimia 26 nchini Ufaransa, na asilimia 41 nchini India waliona serikali zao kuwa si halali.

Utafutaji wa Mwanadamu wa Mamlaka Halali

Kulingana na Biblia, hapo awali mwanadamu alikuwa chini ya mamlaka ya Mungu kwa njia ya moja kwa moja. (Mwanzo 1:27, 28; 2:16, 17) Lakini, mapema wakati huo, wanadamu walitaka wawe huru kimaadili kutokana na Muumba wao. (Mwanzo 3:1-6) Baada ya kukataa theokrasi, au utawala wa Mungu, ilikuwa ni lazima watafute mifumo mingine ya mamlaka. (Mhubiri 8:9) Wengine waliweka mamlaka yao kwa nguvu. Kwa maoni yao, mamlaka iliwapa haki ya kutawala. Ililazimu wawe na uwezo wa kutosha wa kushurutisha mapenzi yao yafuatwe. Ingawa hivyo, wengi wao walihisi uhitaji wa kuhalalisha utawala wao.

Tokea nyakati za mapema watawala walio wengi walifanya hivyo ama kwa kusema kwamba wao ni miungu ama kwamba walikuwa wamepokea uwezo kutoka kwa miungu. Hilo ni wazo bandia la “ufalme mtukufu,” lililodaiwa na watawala wa mapema wa Mesopotamia na wale Farao wa Misri ya kale.

Aleksanda Mkuu, wale wafalme wa Kigiriki waliomfuata, na maliki wengi wa Roma pia walidai kuwa miungu na hata wakashurutisha waabudiwe. Mifumo ya watawala kama hao iliitwa “madhehebu ya watawala,” na kusudi layo lilikuwa ni kuimarisha mamlaka ya mtawala juu ya watu walioshindwa vitani. Kukataa kumwabudu mtawala kulishutumiwa kuwa uhalifu dhidi ya Taifa. Katika kitabu The Legacy of Rome, Profesa Ernest Barker aliandika hivi: “Kuabudiwa kwa maliki [wa Roma], na utii anaopewa kwa sababu ya uungu wake, kwa wazi ndiko msingi, au kishikanisho, cha milki hiyo.”

Jambo hilo liliendelea hata baada ya “Ukristo” kuhalalishwa na Maliki Konstantino (aliyetawala 306-337 W.K.) na baadaye kufanywa na Maliki Theodosia 1 (aliyetawala 379-395 W.K.) kuwa dini ya Taifa ya Milki ya Roma. Baadhi ya maliki “Wakristo” waliabudiwa wakiwa miungu hadi wakati fulani katika karne ya tano W.K.

“Mamlaka Mbili,” “Panga Mbili”

Cheo cha papa kilipokuja kuwa na uwezo zaidi, matatizo kati ya Kanisa na Taifa yakawa mabaya zaidi. Kwa hiyo, kwenye mwisho wa karne ya tano W.K., Papa Gelasio 1 alitokeza kanuni ya “mamlaka mbili”: mamlaka takatifu ya papa ikiwapo pamoja na uwezo wa kifalme wa wafalme—huku wafalme wakitii papa. Kanuni hiyo baadaye ilikuja kuwa fundisho la “panga mbili”: “Ule upanga wa kiroho ambao papa wenyewe walikuwa nao, wakiwaachia watawala wa chini upanga wa kilimwengu, lakini watawala hao bado walilazimika kutumia upanga wao wa kilimwengu kulingana na mielekezo ya papa.” (The New Encyclopædia Britannica) Kwa msingi wa fundisho hilo, katika Enzi za Kati, Kanisa Katoliki lilidai mamlaka ya kutawaza maliki na wafalme ili kuhalalisha mamlaka yao, hivyo wakieneza ngano ya kale ya “umaliki mtakatifu.”

Hata hivyo, tusifikirie hiyo ni ile nadharia iitwayo haki ya kimungu ya wafalme, jambo lililotokea baadaye na lililokusudiwa kuweka huru watawala wa kisiasa wasimtii papa. Nadharia ya haki ya kimungu ya wafalme yasema kwamba wafalme hupata mamlaka yao ya kutawala moja kwa moja kutoka kwa Mungu, wala si kupitia papa wa Roma. New Catholic Encyclopedia yasema hivi: “Katika kipindi ambacho papa alikuwa na mamlaka ya ulimwenguni pote ya kiroho na hata ya kilimwengu juu ya wakuu wa mataifa, wazo la wafalme kuwa na haki ya kimungu liliweka wafalme wa mataifa katika hali ya kuweza kuona mamlaka yao kuwa ya kimungu kama tu ile ya papa.”b

Ile Ngano ya Utawala wa Walio Wengi

Muda ulipozidi kupita, watu walipendekeza vyanzo vingine vya mamlaka. Mojapo ilikuwa ni utawala wa watu. Watu wengi waamini kwamba wazo hilo lilitoka Ugiriki. Hata hivyo, demokrasi ya Ugiriki ya kale ilifuatwa tu katika majiji machache yaliyojitawala, na hata katika majiji hayo ni wakazi wanaume pekee waliokuwa wakipiga kura. Wanawake, watumwa, na wakazi wageni—waliokadiriwa kuwa nusu hadi sehemu nne kwa tano ya idadi ya wakazi—hawakushiriki. Huo haukuwa utawala wa walio wengi hata kidogo!

Ni nani waliotokeza wazo la utawala wa watu? Kwa kushangaza, wazo hilo lilitokezwa katika Enzi za Kati na wanatheolojia wa Roma Katoliki. Katika karne ya 13, Thomas Aquinas alikuwa na maoni ya kwamba ingawa utawala watokana na Mungu, unapewa watu kihalali. Wazo hilo likapendwa sana. New Catholic Encyclopedia yasema hivi: “Wazo hilo la watu kuwa chanzo cha mamlaka lilitegemezwa na wanatheolojia wa Katoliki walio wengi sana wa karne ya 17.”

Ni kwa nini wanatheolojia wa kanisa ambalo watu hawakuruhusiwa kamwe kuchagua papa, askofu, au kasisi waliendeleza wazo la utawala wa watu? Ni kwa sababu baadhi ya wafalme wa Ulaya walikuwa wanazidi kutopendelea mamlaka ya papa. Nadharia ya utawala wa walio wengi ilimpa papa uwezo wa kumpindua maliki au mfalme ikiwa lazima. Wanahistoria Will na Ariel Durant waliandika hivi: “Wayesuiti wengi walikuwa miongoni mwa wale waliotetea utawala wenye kupendwa na walio wengi, nao waliona hilo kuwa njia ya kudhoofisha umaliki dhidi ya mamlaka ya papa. Kardinali Bellarmine alibisha kwamba ikiwa mamlaka ya wafalme yatokana na watu, na kwa hiyo iwategemee, kwa wazi [mamlaka] hiyo iko chini ya papa . . . Luis Molina, Myesuiti Mhispania, alimalizia kwamba watu, wakiwa chanzo cha mamlaka ya kilimwengu, wangeweza kwa haki—lakini kwa taratibu nzuri—kupindua mfalme asiyefuatia haki.”

Bila shaka, hiyo “taratibu nzuri” ingepangwa na papa. Kikithibitisha jambo hilo, kitabu cha Katoliki cha Kifaransa Histoire Universelle de l’Eglise Catholique chanukuu Biographie universelle, kisemacho hivi: “Bellarmine . . . afundisha fundisho la kawaida la Katoliki kwamba wana wa wafalme hupata mamlaka yao kutokana na chaguo la watu, na kwamba watu waweza kutekeleza haki hiyo chini ya uvutano wa papa peke yake.” (Italiki ni zetu.) Hivyo, utawala wa kupendwa na walio wengi ukaja kuwa chombo ambacho papa angetumia kuwa na uvutano juu ya uchaguzi wa watawala na, ikihitajika, kuwapindua. Katika nyakati za karibuni zaidi, huo umefanya utawala wa Katoliki uwe na uvutano juu ya wapiga-kura Wakatoliki katika demokrasi za uwakilishi.

Katika demokrasi za kisasa uhalali wa serikali wategemea lile linaloitwa “kibali cha wanaotawalwa.” Ingawa hivyo, kwa hali nzuri zaidi hicho ni “kibali cha walio wengi,” na kwa sababu ya kutojali kwa wapiga kura pamoja na ujanja, kihalisi “walio wengi” mara nyingi ni wachache wa idadi ya watu. Leo, “kibali cha wanaotawalwa” mara nyingi humaanisha kitu kama “utiifu, au hali ya kujiuzulu, ya wanaotawalwa.”

Ngano ya Taifa Kujitawala

Ngano ya umaliki mtakatifu iliyoendelezwa na papa wa nyakati za mapema ilikigeuka cheo cha papa ilipobadilika kuwa haki ya kimungu ya wafalme. Nadharia ya utawala wenye kupendwa na walio wengi vilevile ililigeukia Kanisa Katoliki. Katika karne za 17 na 18, wanafalsafa wa kilimwengu, kama vile Waingereza Thomas Hobbes na John Locke na Mfaransa Jean-Jacques Rousseau, walifikiria wazo la utawala wenye kupendwa na walio wengi. Wao walisitawisha aina nyingi za nadharia ya “mkataba wa kijamii” kati ya watawala na watawalwa. Kanuni zao hazikutegemea theolojia bali “sheria ya asili,” na nadharia hiyo ilitokeza mawazo yaliyodhuru sana Kanisa Katoliki na cheo cha papa.

Muda mfupi baada ya kifo cha Rousseau, yale Mapinduzi ya Ufaransa yalizuka. Mapinduzi hayo yaliharibu mawazo fulani ya uhalali, lakini yakaleta wazo jipya, wazo la taifa kujitawala. The New Encyclopædia Britannica yaeleza hivi: “Wafaransa walikirihi [wazo la] haki ya kimungu ya wafalme, kutawazwa kupitia jamii ya kifalme, yale mapendeleo ya Kanisa Katoliki la Roma.” Lakini, yasema Britannica, “Mapinduzi hayo yalikuwa yamefanya ule ubuni mpya, wa taifa kujitawala, ukomae.” Wenye mapinduzi walihitaji “ubuni” huo mpya. Kwa nini?

Kwa sababu chini ya ule mfumo ambao Rousseau alikuwa ametetea, wakazi wote wangekuwa na uwezo sawa wa kuchagua watawala. Hilo lingetokeza demokrasi iliyotegemea haki ya kila mtu kupiga kura ulimwenguni pote—jambo ambalo viongozi wa Mapinduzi ya Ufaransa hawakupendelea. Profesa Duverger aeleza hivi: “Ilikuwa hasa kuepuka matokeo hayo, yaliyoonwa kuwa hayafai, kwamba, tokea 1789 hadi 1791, jamii ya tabaka la kati ya waliokuwa washiriki wa Bunge la Mamlaka walibuni nadharia ya taifa kujitawala. Wao walitambua watu kuwa ‘Taifa,’ waliloliona kuwa tofauti, likiwa mbali na visehemu vyalo. Taifa peke yalo, kupitia wawakilishi walo, lina haki ya kutawala . . . Ingawa laonekana kuwa la Kidemokrasi, fundisho la taifa kujitawala si demokrasi kamwe kwa sababu huo unaweza kutumiwa kuhalalisha karibu kila aina ya serikali, hasa utawala wa mtu mmoja.” (Italiki ni zake.)

Jitihada za Wanadamu Zimeshindwa

Kule kukubaliwa kwa Taifa kuwa chanzo halali cha mamlaka kulitokeza utukuzo wa Taifa. The New Encyclopædia Britannica yasema hivi: “Mara nyingi utukuzo wa Taifa hufikiriwa kuwa jambo la kale sana; nyakati nyingine huo huonwa kimakosa kuwa jambo lenye kudumu katika mielekeo ya kisiasa. Mapinduzi ya Amerika na Ufaransa hasa yaweza kutajwa kuwa maonyesho yao ya kwanza yenye nguvu sana.” Tangu mapinduzi hayo, utukuzo wa taifa umeenea katika yale mabara ya Amerika, Ulaya, Afrika, na Asia. Vita zenye ukatili sana zimeonwa kuwa halali kwa sababu tu ya utukuzo wa taifa.

Mwanahistoria Mwingereza Arnold Toynbee aliandika hivi: “Ile roho ya Utaifa ni chachu kali ya divai mpya ya Demokrasi katika chupa za zamani za Ukabila. . . . Upatano huo wa ajabu kati ya Demokrasi na Ukabila umekuwa hatari zaidi katika siasa zinazofuatwa katika Ulimwengu wa Magharibi wa kisasa kuliko Demokrasi yenyewe.” Utukuzo wa Taifa haujatokeza ulimwengu wenye amani. Toynbee alisema hivi: “Vita za Dini zimefuatwa, baada ya kupoa kitambo tu, na Vita za Utaifa; na katika Ulimwengu wa Magharibi wa kisasa ile roho ya ushupavu wa kidini na roho ya ushupavu wa kitaifa kwa wazi ni msukumo mmoja mwovu.”

Kwa kupitia ngano za “umaliki mtakatifu,” “haki ya kimungu ya wafalme,” “utawala wa walio wengi,” na “taifa kujitawala,” watawala wamejaribu kuhalalisha mamlaka yao juu ya wanadamu wenzao. Hata hivyo, baada ya kuangalia rekodi ya watawala wa kibinadamu, Mkristo aweza tu kufikiria lile wazo lililotajwa na Sulemani: “Mwanadamu ametawala mwanadamu mwenzake kwa hasara yake.”—Mhubiri 8:9, NW.

Badala ya kuabudu Taifa la kisiasa, Wakristo huabudu Mungu na kutambua kwamba ni yeye aliye na chanzo halali cha mamlaka yote. Wao wakubaliana na mtunga-zaburi Daudi aliyesema hivi: “Ee, Yahweh, ukuu ni wako, na uweza, na fahari, na wingi wa siku na utukufu, na kila kitu kilichomo mbinguni na duniani ni chako. Enzi kuu yote ni yako, Yahweh; umetukuzwa, u juu ya vitu vyote.” (1 Mambo ya Nyakati 29:11, The New Jerusalem Bible) Lakini, kwa kumheshimu Mungu, wao waonyesha staha kwa mamlaka kwa hali zote za kilimwengu na kiroho. Jinsi wawezavyo kwa shangwe kufanya hivyo hasa itachunguzwa katika makala mbili zifuatazo.

[Maelezo ya Chini]

a Droit constitutionnel et institutions politiques, cha Maurice Duverger.

b The Catholic Encyclopedia yasema: “Hii ‘haki ya kimungu ya wafalme’ (jambo tofauti sana na fundisho la kwamba mamlaka yote, iwe ni ya mfalme au ya jamhuri, ni kutoka kwa Mungu), haijapata kamwe kuungwa mkono na Kanisa Katoliki. Katika wakati wa Mapinduzi ya kidini dhana hiyo ilikuja kupinga sana Ukatoliki, huku maliki kama Henry 8, na James 1, wa Uingereza, wakidai kuwa na mamlaka kamili ya kiroho na ya kiraia.”

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kanisa Katoliki lilidai mamlaka ya kutawaza maliki na wafalme

[Hisani]

Kujitoa kwa Charlemagne: Bibliothèque Nationale, Paris

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki