Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 7/15 kur. 15-20
  • Jitahidi kwa Ajili ya Wokovu wa Nyumba Yako

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jitahidi kwa Ajili ya Wokovu wa Nyumba Yako
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wazazi Wakristo na Mafungu Yao
  • Kutimiza Mahitaji Yao ya Kihisia-Moyo
  • Kutimiza Mahitaji Yao ya Kiroho
  • Kutia Nidhamu kwa Uadilifu
  • Nyumba za Mzazi Mmoja na za Familia za Kambo
  • Endelea Kujitahidi kwa Ajili ya Wokovu wa Nyumba Yako!
  • Zoeza Mtoto Wako Tangu Utoto Mchanga Sana
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Familia za Mzazi Mmoja Zaweza Kufanikiwa!
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Mzazi Mmoja, Matatizo Mengi
    Amkeni!—2002
  • Ubora wa Kutia Adabu katika Upendo
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 7/15 kur. 15-20

Jitahidi kwa Ajili ya Wokovu wa Nyumba Yako

“Waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana.”—WAEFESO 6:4.

1, 2. Ni magumu gani yanayokabili wazazi leo?

GAZETI moja maarufu liliiita mapinduzi. Hiyo ilikuwa katika makala iliyoeleza juu ya mabadiliko ya kushangaza ambayo yametukia katika familia katika miaka ya karibuni. Hayo yalisemwa kuwa “matokeo ya ongezeko kubwa la talaka, ndoa za pili, talaka za pili, kuzaliwa kwa watoto nje ya ndoa, na mikazo mipya katika familia zinazoishi pamoja.” Haishangazi kwamba kuna mibano na mikazo kama hiyo, maana Biblia ilitabiri kwamba watu wangekabili “nyakati za hatari” katika hizi “siku za mwisho.”—2 Timotheo 3:1-5.

2 Kwa hiyo, wazazi leo wanakabili magumu ambayo vizazi vilivyopita havikukabili. Ingawa wazazi fulani miongoni mwetu wamelea watoto katika njia za kimungu “tangu utoto mchanga,” familia nyingi ndipo tu zimeanza ‘kwenda katika kweli.’ (2 Timotheo 3:15, NW; 3 Yohana 4) Huenda watoto wao walikuwa wakubwa wazazi wao walipoanza kuwafundisha njia za Mungu. Isitoshe, idadi inayozidi kuongezeka ya familia za mzazi mmoja na familia za kambo zimo miongoni mwetu. Hata hali zako ziwe zipi, himizo la mtume Paulo latumika: “Waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana.”—Waefeso 6:4.

Wazazi Wakristo na Mafungu Yao

3, 4. (a) Ni mambo gani yamefanya fungu la akina baba lizorote? (b) Kwa nini akina baba Wakristo lazima wafanye zaidi ya kuwa watoa riziki tu?

3 Ona kwamba Paulo alielekeza maneno yake katika Waefeso 6:4 hasa kwa “akina baba.” Mwandikaji mmoja aeleza kwamba katika vizazi vilivyopita “akina baba walikuwa na daraka la kulea watoto wao kiadili na kiroho; akina baba walikuwa na daraka la kuwafundisha watoto wao. . . . Lakini ule Mvuvumko wa Viwanda uliondoa ukaribiano huo; akina baba waliacha mashamba yao na maduka yao, wakaacha nyumba zao ili wakafanye kazi katika viwanda na baadaye katika ofisi. Akina mama walichukua madaraka mengi ambayo zamani yalikuwa ya akina baba. Basi ubaba ukazidi kuwa jambo la kuwaziwa tu lisilotenda kazi.”

4 Wanaume Wakristo: Msiridhike kuwa watoa riziki tu, mkiachia wake zenu kazi zote za kuzoeza na kulea watoto. Mithali 24:27 lilihimiza hivi akina baba wa nyakati za kale: “Tengeneza kazi yako huko nje, jifanyizie kazi yako tayari shambani, ukiisha, jenga nyumba yako.” Na ndivyo ilivyo leo, ikiwa wewe ni mwanaume anayefanya kazi, labda inakubidi ufanye kazi kwa muda mrefu na kwa jasho ili upate riziki. (1 Timotheo 5:8) Hata hivyo, tafadhali baadaye uchukue wakati “jenga nyumba yako”—kihisia-moyo na kiroho.

5. Wake Wakristo waweza kujitahidije kwa ajili ya wokovu wa nyumba zao?

5 Wake Wakristo: Ni lazima nyinyi pia mjitahidi kwa ajili ya wokovu wa nyumba zenu. Mithali 14:1 lasema: “Mwanamke aliye na hekima hujenga nyumba yake.” Mkiwa wenzi wa ndoa, wewe na mume wako mnashiriki daraka la kuzoeza watoto wenu. (Mithali 22:6; Malaki 2:14) Kufanya hivyo kwaweza kutia ndani kutia watoto nidhamu, kuwatayarisha kwa ajili ya mikutano ya Kikristo na kwa ajili ya huduma ya shambani, au hata kuongoza funzo la familia mume wako asipoweza kuliongoza. Waweza kusaidia sana pia katika kufundisha watoto wako kazi za nyumbani, adabu, usafi wa kimwili, na mambo mengine mengi yenye mafaa. (Tito 2:5) Waume na wake wafanyapo kazi pamoja kwa njia hiyo, wao waweza kutimiza mahitaji ya watoto wao kwa njia bora zaidi. Baadhi ya mahitaji hayo ni gani hasa?

Kutimiza Mahitaji Yao ya Kihisia-Moyo

6. Akina mama na baba wana mafungu gani katika ukuzi wa kihisia-moyo wa watoto wao?

6 Mama ‘mlezi atunzapo watoto wake mwenyewe,’ wao huhisi salama salimini na kupendwa. (1 Wathesalonike 2:7; Zaburi 22:9) Mama wengi hawawezi kukinza tamaa ya kuchunga vitoto vyao. Nabii Isaya aliuliza hivi: “Je! mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake?” (Isaya 49:15) Kwa hiyo akina mama wanatimiza fungu kubwa katika ukuzi wa kihisia-moyo wa mtoto. Hata hivyo, akina baba pia wanatimiza fungu kubwa kwa habari hiyo. Mwelimishaji wa mambo ya familia Paul Lewis asema hivi: “Sijapata kamwe kusikia mfanyakazi wa kijamii aliyepata kumsikia mtoto [mtoro] akisema kwamba alikuwa na uhusiano bora pamoja na baba yao. Hakuna hata mmoja kati ya mamia.”

7, 8. (a) Kuna uthibitisho gani kwamba kuna kifungo chenye nguvu kati ya Yehova Mungu na Mwana wake? (b) Akina baba waweza kusitawishaje kifungo cha upendo pamoja na watoto wao?

7 Kwa hiyo, ni jambo muhimu kwa akina baba Wakristo kusitawisha kwa uangalifu kifungo cha upendo pamoja na watoto wao. Kwa kielelezo, fikiria Yehova Mungu na Yesu Kristo. Kwenye ubatizo wa Yesu, Yehova alitangaza hivi: “Wewe ndiwe mwanangu, mpendwa wangu; nimependezwa nawe.” (Luka 3:22) Mambo mengi yaonyeshwa kwa maneno hayo machache! Yehova (1) alimkiri Mwana wake, (2) alionyesha waziwazi upendo wake kwa Yesu, na (3) akajulisha kwamba amependezwa na Yesu. Lakini, hiyo si pindi ya pekee ambapo Yehova alionyesha upendo wake kwa Mwana wake. Baadaye Yesu alimwambia Baba yake hivi: “Ulinipenda kabla ya kuwekwa msingi ulimwengu.” (Yohana 17:24) Lakini, si ni kweli kwamba wana wote na mabinti wote watiifu wahitaji kutambuliwa, kupendwa na kukubaliwa na baba zao?

8 Ikiwa wewe ni baba, yaelekea kwamba unaweza kusaidia sana katika kusitawisha kifungo cha upendo pamoja na watoto wako kwa kuwaonyesha upendo kwa njia halisi na kwa maneno. Ni kweli kwamba ni vigumu sana kwa wanaume fulani kuonyesha upendo wao, hasa kama wao hawakupata kamwe kuonyeshwa upendo waziwazi na baba zao wenyewe. Lakini hata jitihada isiyopendeza ya kuonyesha watoto wako upendo yaweza kuwa na uvutano wenye nguvu. Iwayo yote, “upendo hujenga.” (1 Wakorintho 8:1) Watoto wako wakihisi salama kwa sababu ya upendo wako wa kibaba, wataelekea zaidi kuwa “wana na mabinti halisi” nao hawataogopa kukueleza mambo yao ya kindani.—Mithali 4:3.

Kutimiza Mahitaji Yao ya Kiroho

9. (a) Wazazi Waisraeli wenye kumhofu Mungu waliandaaje mahitaji ya kiroho ya familia zao? (b) Wakristo wana fursa zipi za kufundisha watoto wao kwa njia isiyo rasmi?

9 Watoto wana mahitaji ya kiroho vilevile. (Mathayo 5:3) Musa alihimiza wazazi Waisraeli hivi: “Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.” (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Ikiwa wewe ni mzazi Mkristo, unaweza kufundisha mambo mengi kwa njia isiyo rasmi, kama wakati “utembeapo njiani.” Wakati unaotumiwa mkiwa pamoja katika gari la familia, mwendapo dukani, au mtembeapo na watoto wako mkiwa katika huduma ya Kikristo ya nyumba kwa nyumba huandaa fursa zifaazo za kufundisha katika hali zenye starehe. Pindi za mlo ni wakati mzuri hasa wa familia kuzungumza. “Sisi hutumia pindi za mlo kuzungumzia mambo yaliyotokea mchana,” aeleza mzazi mmoja.

10. Kwa nini nyakati nyingine funzo la familia lawa gumu, na ni lazima wazazi wawe na azimio gani?

10 Hata hivyo, mafundisho rasmi kupitia funzo la Biblia la kawaida pamoja na watoto wako ni muhimu pia. Ni kweli kwamba “ujinga umefungwa ndani ya moyo” wa watoto. (Mithali 22:15) Wazazi fulani wasema kwamba watoto wao waweza kwa urahisi kuvuruga kimakusudi funzo la familia. Kwa njia gani? Kwa kukosa kutulia na kutopendezwa na mambo, na kwa kutokeza vikengeusha fikira vyenye kuudhi (kama kupigana na ndugu zao wachanga), au kwa kujifanya kuwa hawajui kweli za msingi za Biblia. Jambo hilo likiendelea mpaka liwe vita baina ya nia mbili, ni lazima nia ya mzazi iwe yenye nguvu zaidi. Wazazi Wakristo wasichoke na kuacha watoto wao watawale nyumba.—Linganisha Wagalatia 6:9.

11. Funzo la familia laweza kufanywaje lifurahishe?

11 Kama watoto wako hawafurahii funzo la familia, labda waweza kufanya mabadiliko fulani. Kwa kielelezo, je, funzo hilo latumiwa kuwa udhuru wa kuyarudia makosa ya karibuni zaidi ya watoto wako? Labda ingekuwa bora zaidi kuzungumzia matatizo kama hayo kwa faragha. Je! funzo lenu hufanywa kwa ukawaida? Ikiwa unafutilia mbali funzo kwa sababu ya kipindi cha televisheni ukipendacho zaidi au kwa sababu ya michezo, yaelekea kwamba watoto wako hawatachukua funzo kwa uzito sana. Je! unaongoza funzo lako kwa bidii na kwa shauku? (Warumi 12:8) Naam, funzo lapaswa kufurahiwa. Jaribu kuhusisha watoto wote. Uwe mwenye mwelekeo unaofaa na mwenye kujenga, ukiwapongeza watoto wako kwa uchangamfu kwa ajili ya kushiriki kwao. Usipitie tu habari, bali, bila shaka, jaribu kufikia mioyo.—Mithali 23:15.

Kutia Nidhamu kwa Uadilifu

12. Ni kwa nini si lazima nidhamu ihusu adhabu ya kimwili nyakati zote?

12 Watoto huhitaji nidhamu sana pia. Ukiwa mzazi, uwawekee mipaka. Mithali 13:24 lasema hivi: “Yeye asiyetumia fimbo yake humchukia mwanawe; bali yeye ampendaye humrudi.” Hata hivyo, Biblia haimaanishi kwamba ni lazima nidhamu itolewe kwa fimbo nyakati zote. Mithali 8:33 lasema: “Sikieni mafundisho,” na twaambiwa kwamba “lawama [“karipio,” NW] hupenya moyoni mwa mwenye ufahamu, kuliko mapigo mia moyoni mwa mpumbavu.”—Mithali 17:10.

13. Nidhamu ya mtoto yapaswa itoleweje?

13 Huenda nidhamu ya kimwili ikafaa wakati fulani. Hata hivyo ikitolewa kwa hasira, yaelekea kwamba itapita kiasi na isifaulu. Biblia yaonya hivi: “Nyinyi akina baba, msiwachokoze watoto wenu, wasije wakakata tamaa.” (Wakolosai 3:21) Hakika, “jeuri humpumbaza mwenye hekima.” (Mhubiri 7:7) Kijana mwenye uchungu wa moyo aweza hata kuasi dhidi ya viwango vya uadilifu. Hivyo wazazi wapaswa kutumia Maandiko wakitia nidhamu watoto wao kwa uadilifu na kwa njia thabiti lakini yenye kusawazika. (2 Timotheo 3:16) Nidhamu ya kimungu hutolewa kwa upendo na kwa upole.—Linganisha 2 Timotheo 2:24, 25.a

14. Wazazi wafanye nini wahisipo mwelekeo wa kupandwa na ghadhabu?

14 Bila shaka, “twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi.” (Yakobo 3:2) Hata mzazi ambaye kwa kawaida ni mwenye upendo aweza kushindwa na mkazo wakati fulani aseme maneno yasiyo ya fadhili au kuonyesha hasira. (Wakolosai 3:8) Jambo hilo likitukia, jua lisitue kama mtoto wako ana msononeko mkubwa au wewe mwenyewe ukiwa umekasirika. (Waefeso 4:26, 27) Tatua matatizo na mtoto wako, ukiomba msamaha ikiwa inafaa. (Linganisha Mathayo 5:23, 24.) Kuonyesha unyenyekevu kama huo kwaweza kuwafanya mkaribiane na mtoto wako. Ukihisi kwamba huwezi kudhibiti hasira yako na utashindwa na ghadhabu, tafuta msaada kutoka kwa wazee wa kutaniko waliowekwa rasmi.

Nyumba za Mzazi Mmoja na za Familia za Kambo

15. Watoto katika familia za mzazi mmoja waweza kusaidiwaje?

15 Hata hivyo, si watoto wote wana utegemezo wa wazazi wawili. Nchini Marekani, mtoto 1 kati ya 4 analelewa na mzazi mmoja. ‘Wavulana wasio na baba’ walikuwa wengi katika nyakati za Biblia, na Maandiko hutaja kwa ukawaida hali ya kuwahangaikia. (Kutoka 22:22, NW) Leo, nyumba za Kikristo za mzazi mmoja vilevile hukabili mikazo na magumu, lakini wao hufarijika wakijua kwamba Yehova ni “baba wa yatima [“wavulana wasio na baba,” NW] na mwamuzi wa wajane.” (Zaburi 68:5) Wakristo wanahimizwa “kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao.” (Yakobo 1:27) Wenzi wenye kuamini waweza kusaidia sana katika kutoa msaada kwa familia za mzazi mmoja.b

16. (a) Wazazi walio peke yao waweza kufanya nini kwa niaba ya nyumba zao? (b) Kwa nini huenda nidhamu ikawa ngumu kutoa, lakini kwa nini ni lazima itolewe?

16 Ikiwa wewe ni mzazi mmoja, wewe mwenyewe waweza kufanya nini ili unufaishe familia yako? Wahitaji kuwa mwenye bidii kuhusu funzo la Biblia la familia, hudhurio la mikutano, na huduma ya shambani. Hata hivyo, kutoa nidhamu kwaweza kuwa jambo gumu sana. Labda bado waomboleza baada ya kumpoteza mwenzi wako mpendwa kwa kifo. Au huenda bado unang’ang’ana na hisia za hatia au hasira kwa sababu ya kuvunjika kwa ndoa. Ikiwa nyote wawili mna haki ya kisheria ya kulea watoto, huenda hata ukaogopa kwamba mtoto wako atapendelea kuwa pamoja na mwenzi wako mliyetalikiana au kuachana naye. Hali kama hizo zaweza kufanya iwe vigumu kihisia-moyo kutoa nidhamu yenye usawaziko. Hata hivyo, Biblia yatuambia kwamba “mwana aliyeachiliwa humwaibisha mamaye.” (Mithali 29:15) Kwa hiyo, usishindwe na hisia ya hatia, majuto, au mkazo wa kihisia-moyo unaotokana na mwenzi wa ndoa mliyeachana naye. Weka viwango vifaavyo na vyenye kupatana. Usiridhiane kanuni za Biblia.—Mithali 13:24.

17. Mafungu ya washiriki wa familia yaweza kukosa kutambuliwaje katika nyumba za mzazi mmoja, na ni nini laweza kufanywa ili kuepuka tatizo hilo?

17 Hata hivyo, magumu yaweza kutokea ikiwa mama aliye mzazi wa pekee amtendea mwanaye kana kwamba huyo ni mwenzi wake wa badala—mwanaume wa nyumba—au binti yake kuwa msiri wake, akimtwika binti huyo matatizo yake ya siri. Haifai kufanya hivyo kwani mtoto huvurugika tu akili. Wakati mafungu ya mzazi na ya mtoto hayatambuliwi waziwazi, kutia nidhamu kwaweza kuzorota. Acha ijulikane kwamba wewe ndiye mzazi. Ikiwa wewe ni mama anayehitaji shauri la Biblia, litafute kutoka kwa wazee au labda kutoka kwa dada mkomavu mwenye umri mkubwa.—Linganisha Tito 2:3-5.

18, 19. (a) Ni yapi baadhi ya magumu yakabiliwayo na familia za kambo? (b) Wazazi na watoto katika familia za kambo waweza kuonyeshaje hekima na utambuzi?

18 Familia za kambo hukabili magumu vilevile. Mara nyingi, wazazi wa kambo hupata kwamba ni nadra sana waonyeshwe “upendo wa mara hiyo [na watoto].” Kwa kielelezo, watoto wa kambo waweza kuwa na hisia nyepesi kwa tendo lolote linaloonekana kuwa upendeleo kuelekea watoto halisi wa mama huyo. (Linganisha Mwanzo 37:3, 4.) Kwa hakika, huenda watoto wa kambo wakapambana na huzuni kwa sababu ya mzazi aliyekufa nao wahofu kwamba kumpenda mzazi wa kambo kwa njia fulani kungekuwa kukosa uaminifu-mshikamanifu kwa baba yao au mama yao halisi. Majaribio ya kutoa nidhamu ifaayo yaweza kukabiliwa na ukumbusho mkali kwamba, ‘Wewe si mzazi wangu halisi!’

19 Mithali 24:3 lasema hivi: “Nyumba hujengwa kwa hekima, na kwa ufahamu huthibitika.” Naam, hekima na utambuzi huhitajiwa na washiriki wote wa familia za kambo ili zifaulu. Baadaye, ni lazima watoto wakubali ukweli ambao mara nyingi ni mchungu kwamba mambo yamebadilika. Wazazi wa kambo vilevile wanaweza kuhitaji kujifunza kuwa wenye saburi na huruma, bila kukasirika upesi wanapoona ni kama wanakataliwa. (Mithali 19:11; Mhubiri 7:9) Kabla ya kuchukua daraka la kuwa mtoa-nidhamu, kwanza jaribu kusitawisha urafiki pamoja na mtoto wa kambo. Huenda wengine wakaona kuwa bora kumwacha mzazi halisi wa mtoto huyo atoe nidhamu mpaka kifungo hicho kiwe kimesitawishwa. Mikazo itokeapo, ni lazima jitihada za kuwasiliana zifanywe. “Hekima hukaa nao wanaoshauriana,” lasema Mithali 13:10.c

Endelea Kujitahidi kwa Ajili ya Wokovu wa Nyumba Yako!

20. Vichwa vya familia za Kikristo wapaswa kuendelea kufanya nini?

20 Familia za Kikristo zenye nguvu hazitokei tu. Ni lazima nyinyi vichwa vya familia mwendelee kujitahidi kwa ajili ya wokovu wa nyumba zenu. Mwe macho, mkichunguza vitabia au mielekeo ya kilimwengu. Wekeni kielelezo kizuri katika usemi, mwenendo, upendo, imani, na usafi wa maadili. (1 Timotheo 4:12) Onyesheni matunda ya roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22, 23) Sifa za saburi, kuwafikiria wengine, kusameheana, na shauku nyororo zitaimarisha jitihada zako za kufundisha watoto wako njia za Mungu.—Wakolosai 3:12-14.

21. Hali changamfu na yenye furaha yaweza kudumishwaje nyumbani?

21 Kwa msaada wa Mungu, jaribu kudumisha roho changamfu na yenye furaha katika nyumba yako. Tumieni wakati pamoja mkiwa familia, mkijaribu kula angalau mlo mmoja mkiwa pamoja kila siku. Mikutano ya Kikristo, utumishi wa shambani, na funzo la familia ni muhimu sana. Lakini, pia kuna “wakati wa kucheka; . . . na wakati wa kucheza.” (Mhubiri 3:1, 4) Naam, ratibu pindi za kuwa na tafrija zenye kujenga. Kuzuru majumba ya hifadhi, makao ya wanyama, na sehemu nyinginezo kama hizo hufurahisha familia nzima. Au waweza kuzima televisheni na kutumia wakati huo kuimba, kusikiliza muziki, kucheza michezo, na kuzungumza. Hilo laweza kusaidia familia ikaribiane zaidi.

22. Kwa nini mjitahidi kwa ajili ya wokovu wa nyumba yenu?

22 Na nyinyi nyote mlio wazazi Wakristo na mwendelee kujitahidi ili kumpendeza Yehova kikamili “mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifu ya Mungu.” (Wakolosai 1:10) Jengeni nyumba yenu kwenye msingi imara wa utii kwa Neno la Mungu. (Mathayo 7:24-27) Na mwe na hakika kwamba jitihada zenu za kulea watoto wenu “katika adabu na maonyo ya Bwana.” zitampendeza yeye.—Waefeso 6:4.

[Maelezo ya Chini]

a Ona makala “Maoni ya Biblia: ‘Fimbo ya Nidhamu’—Je! Ni ya Kikale?” katika Amkeni! la Septemba 8, 1992, Kiingereza.

b Ona Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1981, kurasa 4-17.

c Ona Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1984, kurasa 21-5, Kiingereza.

Ungejibuje?

◻ Mume na mke waweza kushirikianaje katika kujenga nyumba zao?

◻ Ni nini baadhi ya mahitaji ya kihisia-moyo ya watoto, nayo yaweza kutimizwaje?

◻ Vichwa vya familia waweza kufundishaje watoto wao kirasmi na kwa njia isiyo rasmi?

◻ Wazazi wawezaje kutia nidhamu kwa uadilifu?

◻ Ni nini chaweza kufanywa kwa manufaa ya familia zenye mzazi mmoja na familia za kambo?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Upendo na ukubali wa baba ni muhimu kwa ukuzi wa kihisia-moyo wa mtoto

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki