Kutoa Ushahidi kwa “Mataifa Yote”
“Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.”—MATHAYO 24:14.
1. Kwa nini ni lazima iwe maneno ya Yesu yaliyorekodiwa kwenye Mathayo 24:14 yaliwashangaza wafuasi wake?
NI LAZIMA iwe maneno ya Yesu yaliyo juu yaliwashangaza kama nini wanafunzi wake wa Kiyahudi! Wazo lenyewe la Wayahudi waliotakaswa kwenda kuongea na Wasio Wayahudi, “Mataifa,” walio ‘wachafu,’ lilikuwa la kigeni kwa Myahudi, hata lenye kuchukiza.a Kwani, Myahudi mwenye kudhamiria asingefikiria kuingia nyumba ya Asiye Myahudi! Wale wanafunzi Wayahudi walikuwa bado na mambo mengi sana ya kujifunza kuhusu Yesu, upendo wake, na utume wake. Na bado walikuwa na mambo mengi ya kujifunza kuhusu kutokupendelea kwa Yehova.—Matendo 10:28, 34, 35, 45.
2. (a) Huduma ya Mashahidi imeenea kadiri gani? (b) Ni mambo gani matatu ya msingi ambayo yamechangia maendeleo ya Mashahidi?
2 Mashahidi wa Yehova wamehubiri habari njema miongoni mwa mataifa, kutia na Israeli ya ki-siku-hizi, na sasa wanapiga mbiu juu yayo katika mataifa mengi zaidi ya wakati mwingine wowote. Katika 1994 Mashahidi zaidi ya milioni nne na nusu wanahubiri katika mabara yapata 230. Wanaongoza mafunzo ya Biblia nyumbani yapata milioni nne na nusu pamoja na watu wenye kupendezwa. Hilo linafanywa huku wakikabili chuki isiyo na sababu ulimwenguni pote, mara nyingi ikiwa na msingi wa kutojua mafundisho na makusudi ya Mashahidi. Kama ilivyosemwa juu ya Wakristo wa mapema, ndivyo iwezavyo kusemwa juu yao: “Katika habari za madhehebu hiyo inajulikana kwetu kwamba inanenewa vibaya kila mahali.” (Matendo 28:22) Basi twaweza kusema ni nini zilizo sababu za huduma yao yenye mafanikio? Kuna angalau mambo matatu yanayochangia maendeleo yao—kufuata miongozo ya roho ya Yehova, kuiga njia za Kristo zenye kutumika, na kutumia vyombo vifaavyo ili kuwa na uwasiliano wenye matokeo.
Roho ya Yehova na Habari Njema
3. Kwa nini hatuwezi kujivuna juu ya yale ambayo yametimizwa?
3 Je! Mashahidi wa Yehova hujivuna juu ya mafanikio yao, kana kwamba yanatokana na uwezo wowote wa pekee ambao huenda wakawa nao? La, kwani maneno haya ya Yesu yawahusu: “Mtakapokwisha kuyafanya yote mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu yaliyotupasa kufanya.” Wakiwa Wakristo waliojiweka wakfu na kubatizwa, Mashahidi wa Yehova wamekubali kwa kujitolea lile daraka la kumtumikia Mungu, hata hali zao za kibinafsi ziwe ni nini. Kwa wengine, hilo lamaanisha utumishi wa wakati wote wakiwa wamishonari au wajitoleaji katika ofisi za tawi na majengo ya kuchapishia vichapo vya Kikristo. Kwa wengine utayari huo wa Kikristo huwaongoza wafanye kazi ya ujenzi wa majengo ya kidini, kuhubiri wakati wote wakiwa wahudumu mapainia, au kuhubiri sehemu ya wakati wakiwa wahubiri wa habari njema katika makutaniko ya makwao. Hakuna yeyote wetu awezaye kwa haki kujigamba juu ya kufanya wajibu wetu, “yaliyotupasa kufanya.”—Luka 17:10; 1 Wakorintho 9:16.
4. Upinzani wa huduma ya Kikristo ulimwenguni pote umeshindwaje?
4 Mafanikio yoyote tunayokuwa nayo yaweza kusemwa yanatokana na roho ya Yehova, au kani ya utendaji. Ni halali kusema leo kama ilivyosemwa katika siku za nabii Zekaria: “Hili ni neno la BWANA kwa Zerubabeli, kusema, Si kwa uwezo, wala kwa nguvu, bali ni kwa roho yangu, asema BWANA wa majeshi.” Hivyo, upinzani ulimwenguni pote kwa kazi ya kuhubiri ya Mashahidi umeshindwa, si kwa jitihada za kibinadamu, bali kwa mwelekezo na ulinzi wa Yehova.—Zekaria 4:6.
5. Yehova ana fungu jipi katika kule kuenezwa kwa ujumbe wa Ufalme?
5 Kwa habari ya wale waitikiao ujumbe wa Ufalme, Yesu alisema hivi: “Imeandikwa katika manabii, Na wote watakuwa wamefundishwa na Mungu. Basi kila aliyesikia na kujifunza kwa Baba huja kwangu. . . . Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa amejaliwa na Baba yangu.” (Yohana 6:45, 65) Yehova aweza kusoma mioyo na akili, naye awajua wale ambao huenda wakaitikia upendo wake hata ingawa huenda wasimjue bado. Yeye hutumia pia malaika wake kuelekeza huduma hii isiyo na kifani. Ndiyo sababu katika njozi Yohana aliona malaika wakishiriki akaandika hivi: “Nikaona malaika mwingine, akiruka katikati ya mbingu, mwenye Injili [“habari njema,” NW] ya milele, awahubiri hao wakaao juu ya nchi, na kila taifa na kabila na lugha na jamaa.”—Ufunuo 14:6.
Kufahamu Uhitaji wa Kiroho
6. Ni mtazamo upi wa msingi unaohitajiwa ili mtu aitikie habari njema?
6 Jambo jingine lihusikalo katika Yehova kumpa mtu fursa ya kukubali habari njema ni lile lionyeshwalo na Yesu: “Wenye furaha ni wale wenye kufahamu uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbingu ni wao.” (Mathayo 5:3, NW) Mtu anayeridhika na hali yake au ambaye hajitahidi kutafuta kweli hatafahamu uhitaji wa kiroho. Yeye afikiria mambo ya kimwili tu. Kutosheka na hali kunakuwa kizuizi. Kwa hiyo, wakati wengi tunaokutana nao tuendapo nyumba kwa nyumba wanapokataa ujumbe, ni lazima tufikirie zile sababu zote tofauti-tofauti ambazo huenda zikawafanya watu waitikie hivyo.
7. Kwa nini wengi hawaitikii kweli?
7 Wengi hukataa kusikiliza kwa sababu wao hushikamana kwa ushupavu na dini waliorithi nao hawako tayari kushiriki katika mazungumzo. Wengine wamevutiwa na dini inayofaana na utu wao—watu fulani hutaka dini ya mafumbo, wengine huitikia hali ya kihisiamoyo, wengine bado hutafuta shughuli za kijamii kanisani kwao. Watu wengi leo wamechagua mtindo-maisha unaopingana na viwango vya Mungu. Labda wanaishi maisha yasiyo ya kiadili, ambayo ndiyo sababu yao ya kusema, “Mimi sipendezwi.” Hata hivyo wengine, ambao huenda wakadai kuwa na elimu na kuwa watu wa kisayansi, huikataa Biblia kuwa ni sahili mno.—1 Wakorintho 6:9-11; 2 Wakorintho 4:3, 4.
8. Kwa nini kukataa ujumbe kwa watu hakupunguzi bidii yetu? (Yohana 15:18-20)
8 Je! kukataa kwa walio wengi kupunguze imani na bidii yetu katika ile huduma ya kuokoa uhai? Twaweza kupata faraja kutokana na maneno ya Paulo kwa Warumi: “Ni nini, basi, ikiwa baadhi yao hawakuamini? Je! kutokuamini kwao kutaubatili uaminifu wa Mungu? Hasha! Mungu aonekane kuwa amini na kila mtu mwongo; kama ilivyoandikwa, ili ujulike kuwa una haki katika maneno yako, ukashinde uingiapo katika hukumu.”—Warumi 3:3, 4.
9, 10. Kuna uthibitisho upi kwamba upinzani umeshindwa katika mabara mengi?
9 Twaweza kupata kitia-moyo kutokana na vile vielelezo vingi kotekote ulimwenguni vya nchi ambazo zimeonekana kuwa haziitikii sana na hata hivyo, baadaye, zimethibitika kuwa tofauti kabisa. Yehova na malaika wamejua kwamba kulikuwa na wale wenye mioyo myema ambao wangeweza kupatikana—lakini Mashahidi wa Yehova walilazimika kuwa wenye udumifu na kuvumilia katika huduma yao. Kwa kielelezo, chukua baadhi ya nchi ambako Ukatoliki ulionekana kutokeza kizuizi kisichoshindika miaka 50 iliyopita—Argentina, Brazili, Hispania, Ireland, Italia, Kolombia, Mexico, na Ureno. Mashahidi walikuwa wachache huko nyuma katika 1943, 126,000 pekee ulimwenguni pote, kukiwa na 72,000 kati ya hao katika Marekani. Ukosefu wa ujuzi pamoja na chuki isiyo na sababu iliyowakabili Mashahidi ilionekana kuwa kama ukuta wa matofali ambao haungeweza kuvunjwa. Hata hivyo, leo baadhi ya matokeo ya kuhubiri yenye mafanikio zaidi yamekuwa katika nchi hizo. Ndivyo ilivyo na nchi nyingi zilizokuwa za Kikomunisti hapo awali. Katika 1993 ubatizo wa watu 7,402 kwenye mkusanyiko katika Kiev, Ukrania, waonyesha uthibitisho wa hili.
10 Mashahidi wametumia njia zipi ili kuwasilisha habari njema kwa majirani wao? Je! wametumia mivutio ya kimwili ili kupata waongovu, jambo ambalo wengine wamedai? Je! wamewatembelea tu wale walio maskini na wasio na elimu, kama vile wengine wamedai?
Njia Zenye Mafanikio za Kupitisha Habari Njema
11. Yesu aliweka kielelezo kipi chema katika huduma yake? (Ona Yohana 4:6-26.)
11 Yesu na wanafunzi wake walianzisha kigezo ambacho Mashahidi hufuata hadi leo katika kazi yao ya kufanya wanafunzi. Yesu alienda popote ambapo palikuwa na watu, matajiri kwa maskini—nyumbani, hadharani, kando ya maziwa ya maji, kwenye pande za milima, hata katika masinagogi.—Mathayo 5:1, 2; 8:14; Marko 1:16; Luka 4:15.
12, 13. (a) Paulo aliandaaje kigezo kwa ajili ya Wakristo? (b) Mashahidi wa Yehova wamefuataje kielelezo cha Paulo?
12 Kuhusu huduma yake mwenyewe, mtume Paulo angeweza kusema hivi kwa haki: “Ninyi wenyewe mnajua tangu siku ya kwanza nilipokanyaga hapa Asia, jinsi nilivyokuwa kwenu wakati wote nikimtumikia Bwana . . . , ya kuwa sikujiepusha katika kuwatangazia neno lo lote liwezalo kuwafaa bali naliwafundisha waziwazi, na nyumba kwa nyumba.”—Matendo 20:18-20.
13 Mashahidi wa Yehova wanajulikana kotekote ulimwenguni kwa kufuata kwao kigezo cha kimitume, huduma ya nyumba kwa nyumba. Badala ya kukazia fikira huduma ya televisheni iliyo ghali, ya kijuujuu tu, na isiyowasiliana na watu kibinafsi, Mashahidi huwaendea watu, matajiri kwa maskini, na kukutana nao uso kwa uso. Wanajaribu kuzungumza kuhusu Mungu na Neno lake.b Hawajaribu kufanya watu wawe Wakristo kwa kuwapa vitu. Kwa wale walio tayari kusababu, wao huonyesha kwamba suluhisho pekee la kweli kwa matatizo ya wanadamu ni utawala kupitia Ufalme wa Mungu, utakaobadili hali juu ya dunia yetu kuwa bora.—Isaya 65:17, 21-25; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:1-4.
14. (a) Wamishonari na mapainia wengi wamewekaje msingi thabiti? (b) Twajifunza nini kutokana na ono la Mashahidi wa Yehova katika Japani?
14 Ili kazi itimizwe katika mabara mengi kadiri iwezekanavyo, wamishonari na mapainia wametanguliza kazi katika mataifa mengi. Wameweka msingi, na kisha Mashahidi wa mahali hapo wameongoza. Hivyo, idadi kubwa za Mashahidi wa kigeni hawajahitajiwa ili kuendeleza kazi ya kuhubiri na kuiendeleza ikiwa imepangwa vema kitengenezo. Kielelezo kimoja chenye kutokeza ni kile cha Japani. Huko nyuma katika miaka ya mwisho-mwisho ya 1940, hasa wamishonari Waaustralasia na Waingereza walienda huko, wakajifunza lugha, wakajipatanisha na hali za enzi baada ya vita zilizokuwa za kikale kwa kadiri fulani, wakaanza kutoa ushahidi nyumba kwa nyumba. Katika Vita ya Ulimwengu 2, Mashahidi walikuwa wamepigwa marufuku na kunyanyaswa katika Japani. Kwa hiyo wamishonari waliwasili wakapata Mashahidi Wajapani wachache tu waliokuwa wakitenda. Lakini leo wameongezeka kufikia zaidi ya 187,000 katika makutaniko zaidi ya 3,000! Ni nini iliyokuwa siri ya mafanikio yao ya mapema? Mishonari mmoja mwenye miaka ya utumishi zaidi ya 25 akiwa huko alisema hivi: “Lilikuwa jambo la maana zaidi kujifunza kuzungumza na watu. Kwa kujua lugha yao, tuliweza kushirikiana nao, kuelewa na kuthamini njia yao ya maisha. Tulilazimika kuonyesha kwamba tuliwapenda Wajapani. Tulijaribu kwa unyenyekevu kuwa sehemu ya jumuiya ya hapo bila kuridhiana kanuni zetu za Kikristo, bila shaka.”
Mwenendo wa Kikristo Ni Ushahidi Pia
15. Mashahidi wameonyeshaje mwenendo wa Kikristo?
15 Hata hivyo, watu hawajaitikia ujumbe wa Biblia pekee. Wameona pia Ukristo katika matendo. Wameona upendo, upatano, na kuungana kwa Mashahidi hata wakiwa chini ya hali zenye kujaribu sana, kama vile vita vya wenyewe kwa wenyewe, ugomvi wa kikabila, na uadui wa kijamii. Mashahidi wamedumisha msimamo dhahiri wa kutokuwamo kwa Kikristo katika mapigano yote na wametimiza maneno haya ya Yesu: “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.”—Yohana 13:34, 35.
16. Ni ono jipi lionyeshalo upendo wa Kikristo wenye kutumika?
16 Upendo wa jirani ulionyeshwa katika kisa cha mtu fulani mzee-mzee aliyeandikia gazeti la mahali hapo juu ya “Bw. na Bi. Jamaa Mwema.” Yeye alieleza kwamba majirani wake walikuwa wamekuwa wenye fadhili kwake wakati mkewe alipokuwa akifa. “Tangu afe . . . wamekuwa supa [wazuri] sana,” yeye akaandika. “Tangu wakati huo ‘wamenilea’ . . . , wakinifanyia kazi zozote zile na kusaidia kusuluhisha matatizo ya mstaafu mwenye umri wa miaka 74. Jambo lifanyalo hili lisiwe la kawaida ni kwamba wao ni weusi, nami ni mweupe. Wao ni Mashahidi wa Yehova, mimi ni Mkatoliki aliyeacha kushiriki.”
17. Twapaswa kuepuka mwendo upi?
17 Ono hili laonyesha kwamba twaweza kutoa ushahidi katika njia nyingi, kutia na mwenendo wetu wa kila siku. Kwa kweli, isipokuwa mwenendo wetu ni wa mfano wa Kristo, huduma yetu ingekuwa ya Kifarisayo, bila matokeo. Hatutaki kuwa kama wale ambao Yesu alieleza hivi: “Yo yote watakayowaambia, myashike na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi.”—Mathayo 22:37-39; 23:3.
Jamii ya Mtumwa Huandaa Vyombo Vifaavyo
18. Fasihi za Biblia hututayarishaje ili kusaidia watu wenye mioyo ifuatayo haki?
18 Jambo jingine muhimu katika kuhubiri habari njema kwa mataifa yote limekuwa kule kupatikana kwa fasihi za Biblia zinazotokezwa na Watch Tower Bible and Tract Society. Tuna vitabu, broshua, trakti, na magazeti yawezayo kuridhisha karibu kila mtu mwenye moyo mweupe aulizaye maswali. Tukikutana na Mwislamu, Mhindu, Mbuddha, Mtao, au Myahudi, twaweza kutumia kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu au trakti na vijitabu mbalimbali ili kuanzisha mazungumzo na labda funzo la Biblia. Mtu asiyeamini kuwako kwa Mungu akiuliza kuhusu uumbaji, twaweza kutumia kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? Kijana akiuliza, ‘Ni nini kusudi la uhai?’ twaweza kumrejezea kwenye kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi. Ikiwa mtu fulani anaathiriwa sana na matatizo ya kibinafsi—mshuko wa moyo, uchovu, unajisi, talaka—sisi tuna magazeti ambayo yameshughulikia habari hizo kwa njia yenye kutumika. Kwa kweli, jamii ya mtumwa mwaminifu ambayo Yesu alitoa unabii kwamba ingekuwa ikitoa “chakula kwa wakati wake” inatimiza fungu layo.—Mathayo 24:45-47.
19, 20. Kazi ya Ufalme imeongezaje mwendo katika Albania?
19 Lakini ili kufikia mataifa, imekuwa lazima kutokeza fasihi hizi katika lugha nyingi. Imewezekanaje kutafsiri Biblia na fasihi za Kimaandiko katika lugha zaidi ya 200? Kufikiria kifupi kielelezo kimoja, Albania, kwaonyesha jinsi jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili imeweza kuendeleza habari njema yajapokuwa magumu makubwa na bila kuwa na Pentekoste ya kisasa kuwezesha lugha zijulikane mara iyo hiyo.—Matendo 2:1-11.
20 Miaka michache tu iliyopita, Albania ilionwa bado kuwa nchi pekee ya Kikomunisti isiyoamini kuwako kwa Mungu kwelikweli. Gazeti National Geographic lilisema hivi katika 1980: “Albania hukataza [dini], ikipiga mbiu katika 1967 juu ya kuwa ndiyo ‘nchi ya kwanza ulimwenguni isiyoamini kuwako kwa Mungu.’ . . . Kizazi kipya cha Albania chajua tu imani ya kwamba Mungu hayuko.” Sasa kwa kuwa Ukomunisti umefifia, Waalbania wanaotambua uhitaji wao wa kiroho wanaitikia kule kuhubiri kunakofanywa na Mashahidi wa Yehova. Timu ndogo ya utafsiri inayotia ndani vijana Mashahidi wanaojua Kiitalia na Kiingereza ilifanyizwa katika Tiranë 1992. Ndugu wenye sifa za kustahili waliotembelea kutoka mabara mengine waliwafundisha kutumia kompyuta ndogo ili kuingiza habari katika Kialbania. Walianza kwa kutafsiri trakti na gazeti Mnara wa Mlinzi. Wapatapo uzoefu, wanajitahidi kutafsiri vichapo vinginevyo vya Biblia vyenye thamani. Kwa sasa kuna Mashahidi wenye kutenda wapata 200 katika nchi hiyo ndogo sana (idadi ya watu ikiwa 3,262,000), na 1,984 walihudhuria Ukumbusho katika 1994.
Sisi Sote Tuna Daraka
21. Tunaishi katika kipindi cha aina gani?
21 Matukio ya ulimwengu yanafikia upeo. Kukiwa na ongezeko la uhalifu na ujeuri, machinjo na unajisi katika vita vya mahali fulani-fulani, ulegevu wa kiadili unaoenea na matunda yao ya magonjwa yanayopitishwa kingono, kutostahi mamlaka ya kisheria, ulimwengu waonekana kuwa wenye mchafuko, usioongozeka. Tumo katika kipindi kifananacho na nyakati za kabla ya Gharika zinazosimuliwa katika Mwanzo: “BWANA akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote. BWANA akaghairi kwa kuwa amemfanya mwanadamu duniani, akahuzunika moyo.”—Mwanzo 6:5, 6; Mathayo 24:37-39.
22. Mashahidi wa Yehova wote wana daraka jipi la Kikristo?
22 Kama vile katika siku ya Noa, Yehova atachukua hatua. Lakini katika haki na upendo wake, yeye ataka habari njema na ule ujumbe wenye kuonya uhubiriwe kwanza kwa mataifa yote. (Marko 13:10) Kwa habari hiyo Mashahidi wa Yehova wana daraka—kutafuta wale wanaostahili amani ya Mungu na kuwafundisha njia zake za amani. Karibuni, wakati wa Mungu uwadiapo, utume wa kuhubiri utakamilishwa kwa mafanikio. “Ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 10:12, 13; 24:14; 28:19, 20.
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate habari zaidi juu ya Wasio Wayahudi, ona kichwa cha habari “Mataifa” katika Insight on the Scriptures, Buku 2, kurasa 472-4, lililotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Ili upate madokezo yenye kutumika juu ya huduma ya Kikristo, ona Mnara wa Mlinzi, Januari 15, 1985, ukurasa 12, “Namna ya Kuwa Wahudumu Wenye Matokeo,” na ukurasa 18, “Huduma Yenye Matokeo Inayoongoza Kwenye Wanafunzi Zaidi.”
Je! Wakumbuka?
◻ Mashahidi wa ki-siku-hizi wamekuwa na mafanikio gani katika huduma yao?
◻ Kwa nini wengi hukataa ujumbe wa Kikristo?
◻ Mashahidi hutumia njia gani ya kuhubiri ya kimitume?
◻ Sisi tuna vyombo vipi kwa ajili ya huduma yenye matokeo?
◻ Ni lazima sisi sote tufanye nini kwa kupatana na Marko 13:10?
[Sanduku katika ukurasa wa 19]
NCHI MASHAHIDI WENYE KUTENDA KATIKA 1943 KATIKA 1993
Argentina 374 102,043
Brazili 430 366,297
Chile 2 44,668
Hispania Hakuna rekodi ya utendaji 97,595
Ireland 150? 4,224
Italia Vita ya Ulimwengu 2-hakuna rekodi 201,440
Kolombia ?? 60,854
Mexico 1,565 380,201
Peru Hakuna rekodi ya utendaji 45,363
Poland Vita ya Ulimwengu 2-hakuna rekodi 113,551
Ufaransa Vita ya Ulimwengu 2-hakuna rekodi 122,254
Ufilipino Vita ya Ulimwengu 2-hakuna rekodi 116,576
Ureno Hakuna rekodi ya utendaji 41,842
Uruguai 22 9,144
Venezuela Hakuna rekodi ya utendaji 64,081
[Picha katika ukurasa wa 17]
Mashahidi wa Yehova wanaongezeka katika nchi nyingi za Katoliki, kama vile Hispania
[Picha katika ukurasa wa 18]
Mashahidi wa Yehova wanatenda katika mataifa kotekote duniani