“Msiogope, Enyi Kundi Dogo”
“Msiogope, enyi kundi dogo; kwa kuwa Baba yenu ameona vema kuwapa ule ufalme.”—LUKA 12:32.
1. Ni nini ilikuwa msingi wa maneno ya Yesu: “Msiogope, enyi kundi dogo”?
“TAFUTENI ufalme [wa Mungu] kwa kuendelea.” (Luka 12:31, NW) Yesu alipowaambia wanafunzi wake maneno hayo, yeye alitaja kanuni ambayo imeongoza kufikiri kwa Wakristo tangu wakati wake mpaka sasa. Ni lazima Ufalme wa Mungu utangulizwe maishani mwetu. (Mathayo 6:33) Hata hivyo, katika simulizi la Luka, Yesu aliendelea kukiambia kikundi fulani cha kipekee cha Wakristo maneno ya upendo na yenye faraja. Yeye alisema: “Msiogope, enyi kundi dogo; kwa kuwa Baba yenu ameona vema kuwapa ule ufalme.” (Luka 12:32) Akiwa Mchungaji Mwema, Yesu alijua kwamba kulikuwa na nyakati ngumu sana mbele ya wanafunzi wake wa karibu. Lakini hakukuwa na sababu ya wao kuogopa ikiwa wangeendelea kutafuta Ufalme wa Mungu. Kwa hiyo, himizo la Yesu halikuwa amri kali. Badala ya hivyo, lilikuwa ahadi yenye upendo iliyochochea uhakika na moyo mkuu wao.
2. Ni nani wafanyizao kundi dogo, na kwa nini wao wana pendeleo hasa?
2 Yesu alikuwa akisema na wanafunzi wake, naye aliwaita “kundi dogo.” Pia alikuwa akisema na wale ambao Yehova ‘angewapa ule ufalme.’ Kwa kulinganishwa na makundi ya umati mkubwa ambayo yangemkubali Yesu katika nyakati za baadaye, kikundi hiki kwa kweli kilikuwa cha watu wachache. Walionwa pia kuwa wenye thamani kubwa kwa sababu walichaguliwa kwa ajili ya wakati ujao mzuri ajabu, kutumiwa katika utumishi wa kifalme. Baba yao, yule Mchungaji Mkuu, Yehova, aita kundi dogo ili kupokea urithi wa kimbingu kuhusiana na Ufalme wa Kimesiya wa Kristo.
Lile Kundi Dogo
3. Yohana aliona njozi gani tukufu ya kundi dogo?
3 Kwa hiyo, ni nani wafanyizao hili kundi dogo lenye tarajio la ajabu kama hilo? Ni wafuasi wa Yesu Kristo wanaotiwa mafuta kwa roho takatifu. (Matendo 2:1-4) Akiwaona wakiwa waimbaji wa kimbingu walio na vinubi mikononi mwao, mtume Yohana aliandika: “Nikaona, na tazama, huyo Mwana-Kondoo amesimama juu ya mlima Sayuni, na watu mia na arobaini na nne elfu pamoja naye, wenye jina lake na jina la Baba yake limeandikwa katika vipaji vya nyuso zao. Hawa ndio wasiotiwa unajisi pamoja na wanawake, kwa maana ni bikira. Hawa ndio wamfuatao Mwana-Kondoo kila aendako. Hawa wamenunuliwa katika wanadamu, malimbuko kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo. Na katika vinywa vyao haukuonekana uongo. Maana hawana mawaa.”—Ufunuo 14:1, 4, 5.
4. Kundi dogo lina cheo gani duniani leo?
4 Tangu Pentekoste ya 33 W.K., hawa watiwa-mafuta, wenye kuzaliwa kwa roho wametumika wakiwa mabalozi wa Kristo duniani. (2 Wakorintho 5:20) Leo, ni mabaki yao tu wanaobaki, wakitumika pamoja wakiwa jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili. (Mathayo 24:45; Ufunuo 12:17) Tangu mwaka wa 1935 hasa, “kondoo wengine,” ambao ni Wakristo wenye tumaini la kidunia, na ambao sasa wamefikia mamilioni, wameungana nao. Hawa husaidia katika kuhubiri habari njema katika dunia yote.—Yohana 10:16.
5. Wale wanaobakia wa kundi dogo wana mtazamo gani, na kwa nini hawapaswi kuogopa?
5 Wale wanaobaki wa kundi dogo ambao wangali duniani wana mtazamo gani? Wakijua kwamba watapokea ‘Ufalme usioweza kutetemeshwa,’ wao hutoa utumishi wao mtakatifu kwa hofu na kicho cha kimungu. (Waebrania 12:28) Wao watambua kwa unyenyekevu kwamba wana pendeleo lisilokadirika liletalo shangwe nyingi sana. Wao wamepata ile “lulu moja ya thamani kubwa” iliyorejezewa na Yesu aliposema juu ya Ufalme. (Mathayo 13:46) Dhiki kubwa ikaribiapo, watiwa-mafuta wa Mungu wasimama bila kuogopa. Japo kile ambacho kinakaribia kuupata ulimwengu wa wanadamu katika “ile siku ya Bwana iliyo kuu na iliyo dhahiri,” wao hawana woga mbaya juu ya wakati ujao. (Matendo 2:19-21) Kwa nini?
Idadi Yapungua
6, 7. (a) Kwa nini idadi ya kundi dogo ambao wangali hapa duniani ni kidogo sana leo? (b) Kila mtu apaswa kuonaje tumaini lake?
6 Katika miaka ya karibuni idadi ya kundi dogo ambao wangali duniani imekuwa kidogo sana. Hili lilionekana katika ripoti ya Ukumbusho ya 1994. Katika makutaniko yapatayo 75,000 ya watu wa Yehova ulimwenguni pote, ni 8,617 pekee walioonyesha dai lao la kuwa washiriki wa mabaki kwa kula na kunywa mifano. (Mathayo 26:26-30) Kwa kutofautisha, jumla ya hudhurio ilikuwa 12,288,917. Wakristo watiwa-mafuta wajua kwamba hilo latarajiwa. Yehova ameweka idadi kidogo, 144,000, inayofanyiza kundi dogo, naye amekuwa akilikusanya tangu Pentekoste ya 33 W.K. Kwa kupatana na akili, kuitwa kwa kundi dogo kungekwisha wakati idadi hiyo ilipokuwa ikikaribia kutimia, na uthibitisho waonyesha kwamba ukusanyaji wa ujumla wa hao wenye baraka ya kipekee ulikwisha katika 1935. Hata hivyo, kondoo wengine katika wakati wa mwisho walitabiriwa kukua mpaka wawe “mkutano mkubwa sana [“umati mkubwa,” NW] ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.” Tangu 1935 ukusanyaji wa ujumla unaofanywa na Yehova umekuwa wa huu umati mkubwa, ambao wana tumaini la uhai wa milele katika dunia paradiso.—Ufunuo 7:9; 14:15, 16; Zaburi 37:29.
7 Wengi wa wale wa kundi dogo ambao wangali duniani sasa wamo katika miaka yao ya 70, 80, na 90. Wachache wamepita miaka yao ya 100 ya maisha. Wote hawa, hata wawe na umri gani, wajua kwamba kupitia ufufuo wa kimbingu, hatimaye wao wataunganishwa na Yesu Kristo nao watatawala naye katika Ufalme wake wenye utukufu. Wale wa umati mkubwa watakuwa raia wa kidunia wa Kristo Mfalme. Kila mmoja na ashangilie kile ambacho Yehova amewekea wale wampendao. Si juu yetu kuchagua tuwe na tumaini gani. Ni Yehova anayeamua jambo hilo. Vikundi vyote viwili vyaweza kufurahia sana katika tumaini lao la wakati ujao wenye furaha, liwe ni katika Ufalme wa kimbingu au katika dunia paradiso chini ya Ufalme huo.—Yohana 6:44, 65; Waefeso 1:17, 18.
8. Kutiwa muhuri kwa wale 144,000 kumefikia hatua gani, na ni nini kitakachotendeka kukimalizika?
8 Kundi dogo la 144,000 kamili hufanyiza “Israeli wa Mungu,” ambao wamechukua mahali pa Israeli wa asili katika makusudi ya Mungu. (Wagalatia 6:16) Kwa hiyo, mabaki hufanyiza wale wanaobaki wa taifa hilo la kiroho ambao wangali duniani. Hao wanaobaki wanatiwa muhuri ili kupata kibali cha Yehova cha mwisho. Katika njozi, mtume Yohana aliona jambo hilo likitendeka, naye aliripoti hivi: “Nikaona malaika mwingine, akipanda kutoka maawio ya jua, mwenye muhuri ya Mungu aliye hai; akawapigia kelele kwa sauti kuu wale malaika wanne waliopewa kuidhuru nchi na bahari, akisema, Msiidhuru nchi, wala bahari, wala miti, hata tutakapokwisha kuwatia muhuri watumwa wa Mungu wetu juu ya vipaji vya nyuso zao. Nikasikia hesabu yao waliotiwa muhuri katika kila kabila ya Waisraeli [wa kiroho], watu mia na arobaini na nne elfu.” (Ufunuo 7:2-4) Kwa kuwa kazi hii ya kutia muhuri Israeli wa kiroho yaonekana yaendelea kwisha, matukio ya kusisimua yatakayotendeka karibuni yanatazamiwa. Kwanza, “dhiki kubwa,” wakati pepo nne za uharibifu ziachiliwapo juu ya dunia, lazima iwe iko karibu sana.—Ufunuo 7:14, NW.
9. Kundi dogo laonaje idadi inayozidi kuongezeka ya umati mkubwa?
9 Wale wa umati mkubwa ambao tayari wamekusanywa wamefikia mamilioni. Hili huchangamsha mioyo ya mabaki kama nini! Ingawa wale wa kundi dogo ambao wangali duniani waendelea kupungua, wao wamezoeza na kuwatayarisha wanaume wanaostahili wa ule umati mkubwa kuchukua madaraka kuhusiana na tengenezo la Mungu la kidunia linalopanuka. (Isaya 61:5) Kama Yesu alivyoonyesha, kutakuwa na waokokaji wa dhiki kubwa.—Mathayo 24:22.
“Msiogope”
10. (a) Ni shambulio gani litakalofanywa karibuni dhidi ya watu wa Mungu, nalo litaongoza kwenye nini? (b) Kila mmoja wetu aulizwa maswali gani?
10 Shetani pamoja na roho waovu wake wameshushwa hadi duniani. Yeye na vikosi vyake wanaongozwa ili wafanye shambulio lao la kufa na kupona dhidi ya watu wa Yehova. Shambulio hilo, lililotabiriwa katika Biblia, lafafanuliwa kuwa shambulio la Gogu wa Magogu. Ibilisi huelekeza shambulio lake kwa akina nani hasa? Je, si kwa washiriki wa mwisho wa kundi dogo, wale Israeli wa Mungu wa kiroho, wanaoishi kwa amani “katikati ya dunia”? (Ezekieli 38:1-12) Ndiyo, lakini mabaki ya jamii ya watiwa-mafuta waaminifu, pamoja na waandamani wao waaminifu-washikamanifu, wale kondoo wengine, watajionea jinsi shambulio la Shetani litakavyoanzisha ghafula itikio la kutazamisha kutoka kwa Yehova Mungu. Yeye ataingilia mambo akihami watu wake, na hilo litatokeza “siku ya BWANA iliyo kuu na itishayo.” (Yoeli 2:31) Leo, mtumwa mwaminifu mwenye akili anatimiza utumishi muhimu, wenye kuokoa uhai, akionya juu ya hali inayokuja ya Yehova kuingilia mambo. (Malaki 4:5; 1 Timotheo 4:16) Je, unaunga mkono kwa bidii utumishi huo, ukishiriki katika kuhubiri habari njema za Ufalme wa Yehova? Je, utaendelea kufanya hivyo ukiwa mtangazaji wa Ufalme asiyeogopa?
11. Kwa nini mtazamo wenye moyo mkuu ni muhimu leo?
11 Kwa sababu ya hali iliyopo ya ulimwengu, huu ni wakati ufaao kama nini kwa kundi dogo kutii maneno ambayo Yesu alielekeza kwao: “Msiogope, enyi kundi dogo”! Mtazamo huo wenye moyo mkuu ni muhimu kwa sababu ya yale yote yanayotimizwa kwa kupatana na kusudi la Yehova. Wakiwa mmoja-mmoja, kila mmoja wa wale wa kundi dogo hutambua uhitaji wa kuvumilia hadi mwisho kabisa. (Luka 21:19) Kama vile Yesu Kristo, aliye Bwana na Bwana-Mkubwa wa kundi dogo, alivyovumilia na kuthibitika kuwa mwaminifu hadi mwisho wa uhai wake wa kidunia, ndivyo ilivyo lazima kwa kila mmoja wa mabaki avumilie na kuthibitika kuwa mwaminifu.—Waebrania 12:1, 2.
12. Paulo, kama Yesu, aliwahimizaje Wakristo watiwa-mafuta wasiogope?
12 Lazima watiwa-mafuta wote wawe na mtazamo uleule kama wa mtume Paulo. Akiwa mtiwa-mafuta aliye mtangazaji wa peupe, ona jinsi maneno yake juu ya ufufuo yanavyopatana na himizo la Yesu la kutoogopa. Paulo aliandika hivi: “Mkumbuke Yesu Kristo, aliyefufuka katika wafu, wa uzao wa Daudi kama inenavyo injili yangu. Nami katika hiyo nimeteswa hata kufungwa kama mtenda mabaya; lakini neno la Mungu halifungwi. Kwa ajili ya hilo nastahimili mambo yote, kwa ajili ya wateule, ili wao nao waupate wokovu ule ulio katika Kristo Yesu, pamoja na utukufu wa milele. Ni neno la kuaminiwa. Kwa maana, kama tukifa pamoja naye, tutaishi pamoja naye pia; kama tukistahimili, tutamiliki pamoja naye; kama tukimkana yeye, yeye naye atatukana sisi; kama sisi hatuamini, yeye hudumu wa kuaminiwa. Kwa maana hawezi kujikana mwenyewe.”—2 Timotheo 2:8-13.
13. Washiriki wa kundi dogo wana masadikisho gani ya ndani, nayo huwasukuma kufanya nini?
13 Kama mtume Paulo, washiriki wanaobaki wa kundi dogo lililotiwa mafuta wako tayari kuvumilia mateso watangazapo ule ujumbe wenye nguvu ulio ndani ya Neno la Mungu. Masadikisho yao yana msingi thabiti waendeleapo kutumaini zile ahadi za kimungu za wokovu na za kupewa kwao “taji ya uzima” wakithibitika kuwa waaminifu hadi kifo. (Ufunuo 2:10) Kwa kupata ufufuo na badiliko la mara iyo hiyo, wao wataingizwa katika muungano pamoja na Kristo, ili watawale pamoja naye wakiwa wafalme. Huo ni ushindi ulioje kwa ajili ya mwendo wao wa kushika uaminifu-maadili wakiwa washindi wa ulimwengu!—1 Yohana 5:3, 4.
Tumaini la Kipekee Sana
14, 15. Tumaini la ufufuo la kundi dogo ni la kipekee sana kwa njia gani?
14 Tumaini la ufufuo la kundi dogo ni la kipekee sana. Kwa njia zipi? Kwanza, huo watangulia ule ufufuo wa ujumla wa “waadilifu na wasio waadilifu.” (Matendo 24:15, NW) Kwa kweli, ufufuo wa watiwa-mafuta unafuata utaratibu fulani kulingana na umashuhuri, kama inavyothibitishwa kwa wazi na maneno haya yanayopatikana kwenye 1 Wakorintho 15:20, 23, (NW): “Kristo ameinuliwa kutoka kwa wafu, matunda ya kwanza kati ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo. Lakini kila mmoja katika daraja lake mwenyewe: Kristo aliye matunda ya kwanza, baadaye wale walio wa Kristo wakati wa kuwapo kwake.” Kwa kuwa na aina ya uvumilivu na imani ambayo Yesu alionyesha, wale wa kundi dogo wanajua yale yanayowangojea wamalizapo mwendo wao wa kidunia, hasa tangu Bwana wa kweli alipokuja kwenye hekalu lake ili kuhukumu katika 1918.—Malaki 3:1.
15 Paulo atupa sisi sababu nyingine ya ziada ya kuona ufufuo huo kuwa wa kipekee sana. Kama ilivyorekodiwa kwenye 1 Wakorintho 15:51-53, yeye aliandika hivi: “Angalieni, nawaambia ninyi siri [“siri takatifu,” NW]; hatutalala sote, lakini sote tutabadilika, kwa dakika moja, kufumba na kufumbua, wakati wa parapanda ya mwisho. . . . Maana sharti huu uharibikao uvae kutokuharibika, nao huu wa kufa uvae kutokufa.” Maneno haya yatumika kwa wale wa kundi dogo wanaokufa wakati wa kuwapo kwa Kristo. Bila kulazimika kulala usingizi katika kifo kwa kipindi kirefu, wao huvishwa hali ya kutokufa, “kwa dakika moja, kufumba na kufumbua.”
16, 17. Kuhusu tumaini lao la ufufuo, Wakristo watiwa-mafuta leo wamebarikiwaje hasa?
16 Kulingana na uelewevu huu, twaweza kuona maana ya maneno ya mtume Yohana yapatikanayo katika Ufunuo 14:12, 13. Yeye aliandika hivi: “Hapa ndipo penye subira ya watakatifu, hao wazishikao amri za Mungu, na imani ya Yesu. Nikasikia sauti kutoka mbinguni ikisema, Andika, Heri wafu wafao katika Bwana tangu sasa. Naam, asema Roho, wapate kupumzika baada ya taabu zao; kwa kuwa matendo yao yafuatana nao.”
17 Ni thawabu ya kipekee sana kama nini waliyowekewa mabaki ya kundi dogo! Ufufuo wao utakuja upesi, punde tu baada ya wao kulala usingizi katika kifo. Ni badiliko lenye kutazamisha kama nini wanalopata wachukuapo mgawo wao katika makao ya roho! Utukuzo huo wa kundi dogo ukiwa waendelea sasa hivi na utimizo wa unabii mwingi mkuu wa Biblia ukiwa karibu kutimia, washiriki wa mwisho wanaobaki wa kundi dogo kwa kweli hawahitaji ‘kuogopa.’ Na kutoogopa kwao kwawatia moyo wale wa umati mkubwa, wanaopaswa kusitawisha mtazamo huo wa kutoogopa watazamiapo kukombolewa katika ule wakati wenye taabu kubwa zaidi ambayo dunia imewahi kupata.
18, 19. (a) Kwa nini wakati tunamoishi ni wa hima? (b) Kwa nini watiwa-mafuta pamoja na kondoo wengine hawapaswi kuogopa?
18 Kukumbuka utendaji mbalimbali wa kundi dogo huwawezesha wao na umati mkubwa kuendelea kumhofu Mungu wa kweli. Saa ya hukumu yake imewasili, na wakati ufaao unaobaki ni wenye thamani kubwa. Wakati ni mfupi kwelikweli kwa wengine kuchukua hatua. Lakini, kwa upande wetu, sisi hatuogopi kwamba kusudi la Mungu litashindwa. Kwa hakika litafanikiwa!
19 Tayari, zile sauti kubwa za kimbingu zimesikika zikisema: “Ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atamiliki hata milele na milele.” (Ufunuo 11:15) Kwa hakika, yule Mchungaji Mkuu, Yehova, anaongoza kondoo zake zote katika “njia za haki kwa ajili ya jina lake.” (Zaburi 23:3) Kundi dogo linaongozwa kwa hakika kwenye thawabu yalo ya kimbingu. Na kondoo wengine watahifadhiwa kwa usalama kupitia dhiki kubwa ili kufurahia uhai wa milele katika makao ya kidunia ya Ufalme mtukufu wa Mungu chini ya utawala wa Kristo Yesu. Kwa hiyo, ingawa maneno ya Yesu yalielekezwa kwa kundi dogo, hakika watumishi wote wa Mungu walio duniani wana sababu ya kusikiliza maneno yake: “Msiogope.”
Je, Unaweza Kueleza?
◻ Kwa nini tutazamie idadi inayobaki ya kundi dogo kupungua?
◻ Ni nini hali ya watiwa-mafuta leo?
◻ Kwa nini Wakristo hawapaswi kuogopa, lijapokaribia shambulio la Gogu wa Magogu?
◻ Kwa nini tumaini la ufufuo la 144,000 ni la kipekee sana, hasa leo?