Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 11/1 kur. 22-25
  • “Twatupwa Chini, Bali Hatuangamizwi”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Twatupwa Chini, Bali Hatuangamizwi”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Pigo Kubwa Kwelikweli
  • Familia Yenye Furaha
  • Kushinda Kupooza Kiroho
  • Kukabiliana na Pigo Jingine
  • Kufanya Niwezayo
  • Yehova Amenipa Nguvu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Jinsi Nilivyonufaika Kutokana na Utunzaji wa Mungu
    Amkeni!—1995
  • Nimepooza—Lakini Nafurahia Maisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Nashukuru kwa Ajili ya Utegemezo wa Yehova Usioshindwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 11/1 kur. 22-25

“Twatupwa Chini, Bali Hatuangamizwi”

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ULF HELGESSON

Katika Julai 1983, madaktari wakiegemea juu yangu walipaaza sauti: “Ameamka!” Uvimbe wenye urefu wa sentimeta 12 ulikuwa umeondolewa kutoka kwenye uti wangu wa mgongo katika upasuaji mgumu wa muda wa saa 15. Nilibaki nimepooza kabisa.

SIKU chache baadaye, nilipelekwa hospitali fulani karibu kilometa 60 kutoka mji wa kwetu wa Hälsingborg, kusini mwa Sweden. Huko nilijiunga na programu ya mazoezi ya kurudisha hali ya kawaida. Madaktari wa mazoezi ya mwili walisema yatakuwa yenye kudai mno, hata hivyo, nilitamani sana kuanza. Nilitaka sana kutembea tena. Kwa kufuatia kwa makini programu ya mazoezi ya saa tano kila siku, nilifanya maendeleo haraka.

Mwezi mmoja baadaye mwangalizi wa mzunguko alipotumikia kutaniko letu, yeye pamoja na wazee wengine Wakristo walifanya safari ndefu kuja kufanyia mkutano wa wazee wa kutaniko katika chumba changu cha hospitali. Moyo wangu ulishangilia kama nini uthibitisho huo wa upendo wa kidugu! Baada ya mkutano huo wauguzi katika wodi walitupatia sisi sote chai na sandiwichi.

Mwanzoni madaktari walishangazwa na maendeleo yangu. Baada ya miezi mitatu ningeweza kuketi kwenye kiti changu cha magurudumu na hata kusimama kwa dakika chache. Nilikuwa na furaha nikiazimia kabisa kutembea tena. Familia yangu na Wakristo wenzangu walinipa kitia moyo kingi sana waliponitembelea. Hata niliweza kwenda nyumbani kwa vipindi vifupi.

Pigo Kubwa Kwelikweli

Hata hivyo, baada ya hapo, sikufanya maendeleo zaidi tena. Upesi daktari wa mazoezi ya mwili akanipa ujumbe huu wenye kuumiza: “Hutakuwa nafuu zaidi kuliko ulivyo sasa!” Mradi sasa ulikuwa kuniimarisha nijitembeze nikiwa kwenye kiti changu cha magurudumu. Nilishangaa nini lingenipata. Mke wangu ataiwezaje hali? Yeye mwenyewe alikuwa amefanyiwa upasuaji mkubwa naye alihitaji msaada wangu. Je, ingenibidi kukaa katika makao ya utunzaji daima?

Nilishuka moyo sana. Nguvu zangu, ujasiri wangu, na uwezo wangu zikakwisha polepole. Siku zikapita, nami nikawa sijimudu. Sikupooza kimwili tu bali pia nilikufa ganzi kihisia-moyo na kiroho. ‘Nilitupwa chini.’ Sikuzote nilijiona kuwa mwenye nguvu kiroho. Nilikuwa na imani thabiti sana katika Ufalme wa Mungu. (Danieli 2:44; Mathayo 6:9,10) Nilisadiki ahadi ya Biblia kwamba magonjwa yote na kutojiweza kote kutaponywa katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu na kwamba humo wanadamu wote watarudishwa kwenye uhai mkamilifu. (Isaya 25:8; 33:24; 2 Petro 3:13) Sasa nilihisi nimepooza si kimwili tu bali pia kiroho. Nilihisi ‘kuangamizwa.’—2 Wakorintho 4:9.

Kabla sijaendelea zaidi, ebu nikueleze machache kuhusu maisha yangu.

Familia Yenye Furaha

Nilizaliwa katika 1934, na afya yangu ilikuwa nzuri sikuzote. Mapema katika miaka ya 1950, nilikutana na Ingrid, nasi tukaoana katika 1958 na kuishi katika mji wa Östersund, katika Sweden ya kati. Badiliko kubwa maishani mwetu lilitokea katika 1963 tulipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Wakati huo tulikuwa na watoto wadogo watatu—Ewa, Björn, na Lena. Upesi familia yetu yote ilikuwa ikijifunza na kuendelea vizuri katika ujuzi wa kweli za Biblia.

Muda mfupi baada ya kuanza kujifunza, tulihamia Hälsingborg. Huko, mke wangu na mimi tukajiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa katika 1964. Furaha yetu iliongezeka binti yetu wa kwanza Ewa, alipobatizwa katika 1968. Miaka saba baadaye katika 1975, Björn na Lena pia wakabatizwa, na mwaka uliofuata nikawekwa rasmi kuwa mzee katika kutaniko la Kikristo.

Kazi yangu ya kimwili iliniwezesha kuandalia familia yangu mahitaji ya kimwili vizuri. Nayo furaha yetu ikaongezeka Björn na Lena walipoingia katika huduma ya wakati wote. Upesi Björn akaalikwa kutumikia katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Arboga. Maisha yalituendea vizuri. Kisha, mapema katika 1980, nilianza kuhisi athari za kimwili za uvimbe ulioondolewa mwishowe katika ule upasuaji mkubwa katika 1983.

Kushinda Kupooza Kiroho

Nilipoambiwa kwamba sitatembea tena, maisha yalionekana kutokuwa na tumaini. Nilipataje nguvu za kiroho tena? Ilikuwa rahisi kuliko nilivyofikiri. Nilichukua tu Biblia yangu na kuanza kusoma. Kadiri nilivyosoma, ndivyo nilivyoendelea kupata nguvu za kiroho. Zaidi ya yote, nilikuja kuthamini zaidi Mahubiri ya Yesu ya Mlimani. Niliyasoma tena na tena na kutafakari juu yayo.

Furaha yangu katika maisha ikarudi. Kwa kusoma na kutafakari, nilianza kuona fursa mbalimbali badala ya vizuizi. Tamaa yangu ya kushiriki kweli za Biblia pamoja na wengine ikarudi, nami nilitimiza tamaa hiyo kwa kutolea ushahidi wafanyakazi wa hospitali na wengine niliokutana nao. Familia yangu ilinitegemeza kabisa-kabisa na kupokea mazoezi ya jinsi ya kunitunza. Mwishowe niliweza kutoka hospitali.

Hatimaye nikawa nyumbani. Hiyo ilikuwa siku yenye furaha kama nini kwa sisi sote! Familia yangu ilitayarisha ratiba iliyotia ndani utunzaji wangu. Mwanangu, Björn, aliamua kuacha kazi katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova, akaja nyumbani kusaidia kunitunza. Ilikuwa faraja kama nini kuwa shabaha ya upendo na kujali kwingi kwa familia yangu.

Kukabiliana na Pigo Jingine

Hata hivyo, kadiri muda ulivyopita, afya yangu ilizidi kuharibika, na ikawa vigumu kwangu kujimudu. Mwishowe, zijapokuwa jitihada za kujitoa za familia yangu, hawakuweza kunitunzia nyumbani tena. Hivyo nikafikiri ingekuwa bora nikae katika makao ya kutunzia wagonjwa. Tena, ikamaanisha mabadiliko na kawaida mpya ya kila siku. Lakini sikuruhusu hilo liwe kitu cha kunirudisha nyuma kiroho.

Sikuacha kamwe usomaji wa Biblia na utafiti. Niliendelea kufikiri yale ningeweza kufanya, si yale nisingeweza kufanya. Nilitafakari juu ya baraka za kiroho ambazo Mashahidi wa Yehova wote wanazo. Nilimkaribia Yehova katika sala na kutumia kila fursa kuwahubiria wengine.

Sasa natumia saa zangu za usiku na saa fulani za mchana katika makao ya kutunzia wagonjwa. Alasiri na jioni nazitumia ama nyumbani ama kwenye mikutano yetu ya Kikristo. Utumishi wa jamii hupanga usafiri wa kawaida kwenda na kurudi kutoka mikutanoni na kwenda na kurudi kutoka nyumbani kwangu. Familia yangu iliyojitoa, ndugu kutanikoni, na wafanyakazi kwenye makao ya kutunzia wagonjwa hunitunza kwa njia nzuri ajabu.

Kufanya Niwezayo

Sijioni kuwa asiyejiweza, na familia yangu hainitendei kwa njia hiyo, wala ndugu zangu Wakristo. Ninatunzwa kwa upendo, jambo hilo lanisaidia kuendelea kutumikia vizuri nikiwa mzee. Mimi huongoza Funzo la Kitabu la Kutaniko kila juma, na vilevile funzo la Mnara wa Mlinzi la kutaniko la kila juma kwenye Jumba la Ufalme. Ni vigumu kwangu kugeuza kurasa katika Biblia, hivyo mtu fulani hupewa mgawo wa kunisaidia kufanya hivyo mikutanoni. Mimi huongoza mikutano na kutoa hotuba nikiwa kwenye kiti changu cha magurudumu.

Hivyo bado naweza kufanya mambo mbalimbali niliyothamini kufanya mbeleni, kutia ndani kufanya ziara za uchungaji. (1 Petro 5:2) Mimi hufanya hivyo ndugu na dada wanapokuja kunisaidia au kuomba shauri. Mimi hutumia simu pia, nikichukua hatua ya kwanza kuwapigia wengine simu. Tokeo linakuwa kutiana moyo. (Warumi 1:11, 12) Majuzi rafiki mmoja alisema: “Mara ninapohisi kuvunjika moyo, unanipigia simu kunichangamsha.” Lakini mimi pia hutiwa moyo, nikijua kwamba Yehova anabariki jitihada zangu.

Kabla na baada ya mikutano, nina ushirika mzuri na watoto kutanikoni. Kwa kuwa nimeketi kwenye kiti changu cha magurudumu, sisi huzungumza tukiwa kimo kimoja. Mimi huthamini unyofu wao na kusema kwao mambo wazi. Kijana mmoja mchanga aliniambia hivi wakati mmoja: “Wewe ni asiyejiweza kimwili mwenye sura nzuri!”

Kwa kukazia fikira yale niwezayo kufanya badala ya kuhangaishwa na yale nisiyoweza kufanya, nimekuwa nikifurahia kumtumikia Yehova. Nimejifunza mengi kutokana na yale yaliyonipata. Nimetambua kwamba tunazoezwa na kuimarishwa na majaribu tunayopitia.—1 Petro 5:10.

Nimeona kwamba watu wengi wenye afya nzuri hukosa kufahamu kwamba ni lazima sikuzote tuchukue kwa uzito ibada ya Baba yetu wa mbinguni. Tukikosa kufanya hivyo, ratiba yetu ya funzo, mikutano, na huduma ya shambani yaweza kuwa kawaida tu ya kila siku. Mimi huona maandalizi haya kuwa ya muhimu ili kuokoka kupita mwisho wa ulimwengu huu na kuingia katika Paradiso ya kidunia iliyoahidiwa na Mungu.—Zaburi 37:9-11, 29; 1 Yohana 2:17.

Ni lazima sikuzote tuweke tumaini la uhai katika ulimwengu mpya ujao wa Mungu likiwa hai mioyoni mwetu. (1 Wathesalonike 5:8) Pia nimejifunza kutoshindwa katika vita dhidi ya mwelekeo wowote wa kuvunjika moyo. Nimejifunza kuona Yehova kuwa Baba yangu na tengenezo lake kuwa Mama yangu. Nimekuja kutambua kwamba tukijitahidi, Yehova aweza kutumia yeyote wetu kuwa mtumishi wake mwenye matokeo.

Ingawa nyakati nyingine nimehisi kwamba nilikuwa ‘nimetupwa chini,’ ‘sijaangamizwa.’ Sijaachwa kamwe na Yehova na tengenezo lake, wala na familia yangu na ndugu zangu Wakristo. Kwa sababu ya kuchukua Biblia na kuanza kuisoma, nilipata nguvu za kiroho tena. Namshukuru Yehova Mungu, atoaye “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” tumtumainipo.—2 Wakorintho 4:7, NW.

Natazamia kwa hamu nyingi wakati ujao nikiwa na uhakika na tumaini kamili katika Yehova. Nina hakika kwamba hivi karibuni Yehova Mungu atatimiza ahadi yake ya paradiso iliyorudishwa hapa duniani pamoja na baraka zote za ajabu itakazoleta.—Ufunuo 21:3, 4.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki