Kuna Habari Njema Mbele!
SOTE huhuzunishwa wakati wowote tupatapo habari mbaya zenye kutuathiri kibinafsi. Kwa upande ule mwingine, sisi hufurahi habari njema zijapo—habari njema za shangwe kwa ajili yetu na wapendwa wetu. Lakini habari mbaya ziathiripo wengine wala si sisi, mara nyingi watu huwa wadadisi; wengine hata hufurahia kujua kuhusu matokeo mabaya ya wengine. Hili huenda likaeleza kwa sehemu kwa nini habari mbaya zauzwa sana!
Katika sehemu ya mapema ya Vita ya Ulimwengu 2, kulikuwa na kielelezo cha wazi cha upendezi wenye kuogofya katika msiba wa watu wengine. Meli ya kivita ya tani 10,000, Graf Spee, ilikuwa ndiyo fahari ya meli za Ujerumani katika 1939. Kwa majuma kadhaa meli hii ya kivita ilikuwa imesababisha uharibifu mwingi miongoni mwa meli za kibiashara za Mataifa ya Muungano katika bahari kuu za Atlantiki Kusini na Hindi. Hatimaye, manowari tatu za kuvinjari zikafuatia na kushambulia Graf Spee, zikisababisha kupotea kwa uhai na kulazimisha meli hiyo kujikokoteza kuingia bandari ya Uruguai ya Montevideo kwa ajili ya marekebisho. Serikali ya Uruguai iliamuru meli hiyo ya kivita irudi baharini mara moja, sivyo ingefungiwa. Kwa hiyo pigano kali ambalo Uingereza ingeelekea kushinda lilikuwa karibu kutokea.
Kiliposikia hilo, kikundi cha wafanyabiashara katika Marekani kilikodi ndege, kwa gharama ya dola 2,500 hivi kila mmoja, ili kwenda kwa ndege hadi Uruguai kushuhudia pigano hilo lenye kujaa damu. Kwa fadhaiko lao, pigano hilo halikutukia. Adolf Hitler alitoa amri Graf Spee itobolewe ili izame. Maelfu ya watazamaji waliokuja kwa wingi bandarini ili kushuhudia tamasha hiyo ya pigano kali la baharini, badala ya hilo waliona na kusikia, mlipuko mkubwa sana uliozamisha Graf Spee, iliyotobolewa na wafanyakazi wayo yenyewe. Nahodha alijiua kimakusudi kwa kujipiga risasi kichwani.
Licha ya dalili zenye kuogofya katika watu fulani, wengi watakubali kwamba wanapendelea habari njema zaidi ya habari mbaya. Je, wewe huhisi hivyo? Kwa nini basi, historia hurekodi habari nyingi zilizo mbaya na chache sana zilizo nzuri? Je, hali hiyo itapata kubadilishwa?
Visababishi vya Habari Mbaya
Biblia hutueleza juu ya wakati ambapo ni habari njema tu zilizokuwapo. Habari mbaya hazikujulikana wala kusikiwa. Wakati Yehova Mungu alipomaliza kazi zake za uumbaji, sayari Dunia ilikuwa tayari kwa mwanadamu na mnyama kuifurahia. Simulizi la Mwanzo latueleza hivi: “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.”—Mwanzo 1:31.
Baada ya kuumbwa kwa mwanadamu, kutokuwako kwa habari mbaya hakukudumu kwa muda mrefu. Kabla ya Adamu na Hawa kuzaa mtoto yeyote, habari mbaya ya uasi dhidi ya Mungu na mpango wake wa mema wenye utaratibu wa ulimwenguni pote iliripotiwa. Mwana wa kiroho mwenye cheo cha juu akasaliti cheo chake alichokabidhiwa na kufaulu kufanya mume na mke wa kwanza wa kibinadamu kujiunga naye katika mwendo wake wenye uasi na usaliti.—Mwanzo 3:1-6.
Wingi wa habari mbaya zinazoshuhudiwa na wanadamu ulianza wakati huo. Si ajabu kwamba hila, madanganyo, uwongo, ukosefu wa kweli, na kweli-nusu zimeonekana waziwazi sana katika habari mbaya ambazo zimejaa ulimwenguni tangu wakati huo. Yesu Kristo alimwekea lawama waziwazi Shetani Ibilisi kuwa mwanzilishi wa habari mbaya, akiwaambia viongozi wa kidini wa siku Yake hivi: “Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo; wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake. Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe; kwa sababu yeye ni mwongo, na baba wa huo.”—Yohana 8:44.
Kadiri idadi ya wanadamu ilipoongezeka, habari mbaya ziliongezeka pamoja nayo. Bila shaka, hili halimaanishi kwamba hakukuwa na nyakati za shangwe na furaha, kwa kuwa kulikuwa na vitu vingi maishani vilivyosababisha shangwe. Hata hivyo, hali zenye kusikitisha za taabu na huzuni zimedhihirika kote katika kila kizazi cha wanadamu hadi sasa.
Kuna sababu nyingine muhimu inayotokeza hali hii yenye kuhuzunisha. Hiyo ni kuegemea kwetu kulikorithiwa kuelekea kutenda makosa na msiba. Yehova mwenyewe atambulisha kisababishi hiki kisichoepukika cha habari mbaya kwa kusema: “Mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake.”—Mwanzo 8:21.
Kwa Nini Kuna Ongezeko la Habari Mbaya?
Hata hivyo, kuna sababu ambayo imefanya habari mbaya ziongezeke katika karne hii ya 20. Sababu hii yataarifiwa waziwazi katika Biblia, ambayo ilitabiri kwamba wanadamu katika karne ya 20 wangeingia katika kipindi cha kipekee cha wakati kinachoitwa “siku za mwisho” au “wakati wa mwisho.” (2 Timotheo 3:1; Danieli 12:4) Unabii wa Biblia na kronolojia ya Kibiblia hutambulisha hiki “kipindi cha mwisho,” ambacho kilianza katika 1914. Kwa uthibitisho wa Kimaandiko wa jambo hilo, tafadhali ona sura ya 11 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
Siku za mwisho zilipaswa kuanza kwa tukio ambalo moja kwa moja lingesababisha habari mbaya duniani ziongezeke. Hilo lilikuwa nini? Lilikuwa kutupwa chini kwa Shetani Ibilisi na mashetani wake kutoka mbinguni. Unaweza kusoma ufafanuzi huu halisi wa ongezeko lisiloepukika la habari mbaya kwenye Ufunuo 12:9, 12: “Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye. . . . Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.”
Kwa hiyo katika wakati wowote ule ambao bado umebaki hadi siku za mwisho zifikie umalizio wazo, twaweza kutarajia habari mbaya ziendelee na hata kuongezeka zaidi.
Haitakuwa Hivyo Sikuzote
Kwa furaha ya wakazi wa dunia, hali yenye kuhuzunisha ya mambo inayotokeza mweneo wa leo wa habari mbaya haitakuwapo sikuzote. Kwa hakika, twaweza kusema kwa uhakika kwamba mwisho wa habari mbaya uko karibu. Hali haijakosa tumaini, licha ya kuonekana kuwa hivyo. Mwisho wa habari zote mbaya uko karibu sana na utakuja bila kukosa kwa wakati wa Mungu uliowekwa.
Twaweza kuwa na uhakika kuhusu hilo kwa sababu siku za mwisho zatolewa unabii kufikia upeo au kumalizika kwa uharibifu wa Mungu na kuondolewa kwa visababishi vyote vya habari mbaya. Yeye ataondoa wachochezi waovu wa kibinadamu wachocheao mzozo ambao hukataa kubadilika na kugeuka kutoka mwendo wao wenye kosa. Hili hufikia upeo katika ile vita kuu ya Mungu Mweza Yote, ijulikanayo sana kuwa pigano la Har–Magedoni. (Ufunuo 16:16) Mara tu baada ya hilo, Shetani Ibilisi na majeshi yake ya roho waovu watafanywa kuwa wasiotenda. Ufunuo 20:1-3 hufafanua kufungwa kwa Shetani, mwanzilishi wa habari zote mbaya hivi: “Kisha nikaona malaika akishuka kutoka mbinguni mwenye ufunguo wa kuzimu, na mnyororo mkubwa mkononi mwake. Akamshika yule joka, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani, akamfunga miaka elfu; akamtupa katika kuzimu, akamfunga, akatia muhuri juu yake, asipate kuwadanganya mataifa tena.”
Kufuatia matukio haya yenye kutazamisha, wakati wa habari njema zisizo na kifani utakuja kwa ajili ya dunia na wakazi wayo. Wakazi hawa watatia ndani mamilioni ambayo yameokoka vita ya mwisho ya Har–Magedoni na mabilioni yatakayofufuliwa kutoka usingizi wao wa kifo katika makaburi. Habari hizi njema zilizo bora kupita zote zafafanuliwa katika kitabu cha mwisho cha Biblia: “Maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:3, 4.
Je, waweza kuwazia wakati huo wenye furaha? Ni wakati ujao mtukufu kwelikweli ambapo habari mbaya hazitakuwapo tena. Ndiyo, habari zote mbaya zitakuwa zimekwisha na hazitasikiwa tena. Kisha habari njema zitatawala kwa ukuu, na kujaa kwa umilele wote.