Neno la Mungu Hufanya “Miujiza”
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA THÉRÈSE HÉON
Siku moja mwaka wa 1965, niliingia jengo fulani la biashara, nikawatolea wafanyabiashara nakala za magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Nilipogeuka ili kuondoka, nilisikia kishindo. Risasi ilipiga sakafu karibu na miguu yangu. “Hiyo ndiyo njia ya kushughulika na Mashahidi wa Yehova,” akadhihaki mmoja wa wafanyabiashara hao.
ONO hilo liliniogopesha—lakini si vya kutosha kunifanya niache huduma ya wakati wote. Kweli za Biblia nilizokuwa nimejifunza zilikuwa zenye thamani mno kuruhusu chochote kinifanye niache huduma yangu. Acha nieleze ni kwa nini nasema hivyo.
Baada ya kuzaliwa kwangu Julai 1918, wazazi wangu walikaa Cap-de-la-Madeleine, kijiji kidogo katika Quebec, Kanada, kinachojulikana kama Mahali pa Miujiza. Wageni walimiminika hapa ili kutolea heshima kwenye kihekalu cha Bikira Mariamu. Ingawa ile iliyodaiwa kuwa miujiza ya kufanywa na Mariamu haiwezi kuthibitishwa, Neno la Mungu limefanya jambo lililo la kimuujiza kihalisi maishani mwa watu wengi sana kadiri ambavyo hiki kijiji kimeongezeka kikawa mji wenye wakazi zaidi ya 30,000.
Nilipokuwa mwenye umri wa miaka ipatayo 20, baba yangu aliona kupendezwa kwangu na mambo ya kidini naye akanipa Biblia yake. Nilipoanza kuisoma, nilishangaa kujifunza kutoka (kitabu cha) Kutoka sura ya 20 kwamba ibada ya sanamu inalaumiwa waziwazi. Mara moja nikakosa uhakika katika mafundisho ya Kanisa Katoliki nami nikaacha kuhudhuria Misa. Sikutaka kuabudu sanamu. Ningali naweza kumsikia baba akisema, “Thérèse, je, huendi kanisani?” “La,” nikajibu, “naisoma Biblia.”
Kusoma Biblia kuliendelea kuwa sehemu ya maisha yangu hata baada ya kuolewa mwezi wa Septemba 1938. Kwa kuwa mara nyingi mume wangu, Rosaire, alifanya kazi usiku, nilifanya zoea la kusoma Biblia alipokuwa kazini. Upesi nikakata kauli kwamba ni lazima Mungu awe ana watu fulani, nami nikaanza kuwatafuta.
Jitihada Yangu ya Kuwatafuta Watu wa Mungu
Kwa sababu ya yale niliyokuwa nimejifunza kanisani, nilipokuwa mchanga, niliogopa kulala usingizi kwa kuhofu kuamka na kujikuta katika helo. Ili kushinda hofu hiyo, nilikuwa nikijiambia kwamba Mungu wa upendo asingeruhusu jambo baya hivyo litendeke. Nikiwa na uhakika, niliendelea kuisoma Biblia, nikijitahidi kutafuta kweli. Nilikuwa kama yule towashi Mwethiopia aliyesoma bali hakuelewa.—Matendo 8:26-39.
Ndugu yangu André na mke wake, walioishi katika nyumba iliyo chini yetu katika jengo lenye orofa, walianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova mwaka 1957 hivi. Nilimwambia dada-mkwe wangu anionye kwa kupiga-piga dari, Mashahidi walipokuja kuhubiri katika hilo jengo. Kwa njia hiyo ningejua ili nisifungue mlango. Siku moja alisahau kunionya.
Siku hiyo niliufungua mlango nikakutana na Kay Munday, aliye painia, kama waitwavyo wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Aliongea nami kuhusu jina la Mungu, akieleza kwamba Mungu ana jina la kibinafsi, Yehova. Baada ya yeye kuondoka, nilichunguza Biblia yangu ili kuhakikisha kwamba yale aliyokuwa amesema kwa kweli yaliungwa mkono na maandiko ya Biblia. Utafiti wangu ulinifurahisha sana.—Kutoka 6:3, Douay Version, kielezi-chini; Mathayo 6:9, 10; Yohana 17:6.
Kay alipotembelea tena, tulizungumzia fundisho la Katoliki la Utatu, linalodai kwamba Mungu ni watu watatu katika Mungu mmoja. Baadaye nilichunguza kwa uangalifu Biblia yangu mwenyewe ili kujiridhisha kwamba haifundishi Utatu. (Matendo 17:11) Uchunguzi wangu ulithibitisha kwamba Yesu si mwenye ukuu ulio sawa na Mungu. Yeye aliumbwa. Alikuwa na mwanzo, hali Yehova hakuwa na mwanzo. (Zaburi 90:1, 2; Yohana 14:28; Wakolosai 1:15-17; Ufunuo 3:14) Nikiwa nimeridhika na yale niliyokuwa nikijifunza, nilifurahi kuendelea na mazungumzo ya Biblia.
Siku moja katika 1958, wakati wa dhoruba ya theluji ya mwezi wa Novemba, Kay alinialika nihudhurie kusanyiko la mzunguko lililokuwa lifanywe jioni iyo hiyo katika jumba lililokodiwa. Nilikubali mwaliko huo nami nikaifurahia programu. Baadaye, nikizungumza na Shahidi fulani aliyenijia, niliuliza, “Je, ni lazima Mkristo wa kweli ahubiri nyumba hadi nyumba?”
“Ndiyo,” akasema, “ni lazima habari njema itangazwe, na Biblia hufunua kwamba kuwatembelea watu nyumbani kwao ni njia ya maana ya kuhubiri.”—Matendo 20:20.
Nilipendezwa kama nini na jibu lake! Lilinisadikisha kwamba nilikuwa nimewapata watu wa Mungu. Kama angalisema, “La, si lazima,” ningalishuku kama nimeipata kweli, kwani nilijua yale Biblia ilisema kuhusu kuhubiri nyumba hadi nyumba. Tangu wakati huo na kuendelea, nilifanya maendeleo ya kiroho upesi.
Baada ya hilo kusanyiko la mzunguko, nilianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova iliyofanywa katika mji wa jirani wa Trois-Rivières. Kay na mwenzake, Florence Bowman, walikuwa ndio Mashahidi pekee waliokuwa wakiishi Cap-de-la-Madeleine wakati huo. Siku moja nikasema, “Kesho nitakuja kuhubiri pamoja nanyi.” Walifurahi kuandamana nami.
Kuhubiri Katika Mji wa Nyumbani Kwangu
Nilifikiri kwamba kila mtu angeukubali ujumbe wa Biblia, lakini upesi nikapata kujua kwamba sivyo ilivyokuwa. Kay na Florence walipopewa mgawo wa kwenda kwingineko, ni mimi tu niliyekuwa nikihubiri kweli za Biblia nyumba hadi nyumba katika mji huo. Kwa ujasiri, niliendelea kuhubiri nikiwa peke yangu kwa muda wa miaka ipatayo miwili mpaka ubatizo wangu Juni 8, 1963. Siku hiyohiyo nilijiandikisha katika huduma iliyoitwa wakati huo utumishi wa upainia wa likizo.
Niliendelea kuwa painia wa likizo kwa mwaka mmoja. Kisha, Delvina Saint-Laurent akaahidi kwamba angekuja Cap-de-la-Madeleine na kuhubiri pamoja nami mara moja kwa juma ikiwa ningekuwa painia wa kawaida. Kwa hiyo nilijaza ombi langu la upainia. Lakini, kwa kuhuzunisha, majuma mawili tu kabla sijaanza huduma ya wakati wote, Delvina akafa. Ningefanya nini? Nilikuwa nimelijaza ombi na sikutaka kubadili mipango yangu. Kwa hiyo katika Oktoba 1964, nilianza kazi-maisha yangu katika huduma ya wakati wote. Kwa miaka minne iliyofuata, nilienda nyumba hadi nyumba nikiwa peke yangu.
Mara nyingi wale Wakatoliki wa kidini wa Cap-de-la-Madeleine walikuwa wenye uhasama. Baadhi yao waliwaita polisi wakijaribu kunizuia nisihubiri. Siku moja, kama nilivyotaja mwanzoni, mwanabiashara mmoja alijaribu kunitia hofu kwa kupiga risasi kwenye miguu yangu. Hilo lilisababisha mazungumzo mengi mjini. Stesheni ya televisheni ya mahali hapo ililiita kampeni dhidi ya Mashahidi wa Yehova. Hilo tukio lote lilitokeza ushahidi mzuri. Miaka kumi baadaye, mtu wa ukoo wa mwanabiashara huyo aliyekuwa amepiga risasi kunielekea akawa Shahidi mwenyewe.
“Miujiza” Iliyofanywa na Neno la Mungu
Muda wa miaka yote, nimeona ukuta wa upinzani dhidi ya kweli za Biblia ukiporomoka kidato kwa kidato katika Cap-de-la-Madeleine. Mwaka 1968 hivi, Mashahidi wengine walihamia hapa, na wakazi wa hapa wakaanza kuitikia kweli za Biblia. Kufikia miaka ya mapema ya 1970, kwa kweli, kulikuwa na ongezeko kubwa katika idadi ya mafunzo ya Biblia. Wakati ulifika ambapo nilihitaji kuwaomba Mashahidi wengine waongoze mafunzo kadhaa ya Biblia niliyokuwa nikiongoza ili niweze kuendelea kuwa na wakati wa kufanya huduma ya nyumba hadi nyumba.
Siku moja mwanamke kijana alikubali kutoka kwangu ule msaada wa kujifunza Biblia Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Mwandamani wake wakati huo alikuwa mwanamume kijana aitwaye André, mhalifu mwenye sura ya kuwa mjeuri aliyejiunga katika mazungumzo. Mazungumzo pamoja na André yaliamsha kupendezwa kwake, na funzo la Biblia likaanzishwa. Upesi baadaye alianza kusema na marafiki wake kuhusu yale aliyokuwa akijifunza.
Wakati mmoja, nilikuwa nikijifunza Biblia pamoja na wahalifu wanne, mmoja wao ambaye hakusema mengi sana lakini alisikiliza sana. Jina lake lilikuwa Pierre. Usiku mmoja karibu saa nane, mume wangu nami tulisikia mlango ukibishwa. Ebu wazia mandhari hii: Wahalifu wanne walikuwa wamesimama hapo wakiwa na maswali ya kuniuliza. Kwa uzuri, Rosaire hakulalamika kamwe kuhusu ziara hizo za wakati usiofaa.
Mwanzoni hao wanaume wanne waliihudhuria mikutano. Hata hivyo, ni André na Pierre pekee waliodumu. Walipatanisha maisha zao na viwango vya Mungu wakabatizwa. Kwa miaka zaidi ya 20 sasa, wanaume hao wawili wamemtumikia Yehova kwa uaminifu. Walipoanza kujifunza, walijulikana sana kwa utendaji wao wa uhalifu nao walichunguzwa na polisi. Nyakati nyingine polisi walikuja kuwatafuta baada ya mojapo mafunzo yetu ya Biblia au wakati wa mkutano wa kutaniko. Ninafurahi kwamba niliwahubiri “watu wa namna zote,” na kwa njia hiyo nikajionea mwenyewe jinsi Neno la Mungu hutokeza mabadiliko yanayoonekana kwa kweli kuwa ya kimuujiza.—1 Timotheo 2:4, NW.
Ikiwa ningalikuwa nimeambiwa mwanzoni mwa huduma yangu kwamba hatimaye kungekuwa na Jumba la Ufalme katika Cap-de-la-Madeleine na kwamba lingalijaa watu wa Yehova, nisingaliamini hilo. Kwa furaha yangu lile kutaniko dogo moja katika jiji la jirani la Trois-Rivières limeongezeka hadi makutaniko sita yenye kusitawi yanayokutana katika Majumba ya Ufalme matatu, kutia na lile katika Cap-de-la-Madeleine.
Mimi binafsi nimekuwa na shangwe ya kusaidia watu wapatao 30 wafikie hatua ya wakfu na ubatizo. Sasa, nikiwa na umri wa miaka 78, naweza kwa kweli kusema kwamba ninafurahi kwamba niliweka wakfu maisha yangu kwa Yehova. Hata hivyo, ni lazima nikiri kwamba nimekuwa na nyakati fulani-fulani za kushuka moyo. Ili kushindana na vipindi hivyo kwa mafanikio, sikuzote ninafungua Biblia yangu na kusoma mafungu fulani yanayoniburudisha sana. Haiwezekani kwangu kuruhusu siku moja ipite bila kusoma Neno la Mungu. Lenye kutia moyo hasa ni Yohana 15:7, mahali lisemapo: “Ninyi mkikaa ndani yangu, na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa.”
Ni tumaini langu kumwona Rosaire katika ulimwengu mpya ulio karibu sana. (2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4) Kabla tu ya kifo chake katika 1975, alikuwa akifanya maendeleo mazuri kuelekea ubatizo. Kwa sasa, nimeazimia kudumu katika huduma ya wakati wote na kuendelea kushangilia katika kazi ya Yehova.