Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 1/1 kur. 3-5
  • Kwa Nini Sisi Sote Twapaswa Kumsifu Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Sisi Sote Twapaswa Kumsifu Mungu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Ni Yehova Tu Aliyeweza Kunipa Tumaini’
  • ‘Ingawa Mimi Ni Kipofu, Naweza Kuona’
  • Acheni Wote ‘Wamsifu Yah’
  • Unapohisi Umelemewa na Unatamani Kufa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu Wote)—2019
  • Kutoka Mshuko wa Moyo Hadi Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Waambie Unawapenda
    Masimulizi ya Mashahidi wa Yehova
  • Msifu Yah Pamoja Nami
    Mwimbieni Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 1/1 kur. 3-5

Kwa Nini Sisi Sote Twapaswa Kumsifu Mungu?

HALELUYA! Neno hili lajulikana sana na waenda kanisani walio wengi katika Jumuiya ya Wakristo. Baadhi yao hulipaaza kwa sauti katika ibada zao za Jumapili. Lakini, ni wangapi wajuao limaanishwalo kwa kweli na neno hilo? Kwa hakika, hilo ni neno la Kiebrania litumiwalo kwa usemi “Sifuni Yah!” Ni vifijo vya wazi sana, vyenye shangwe juu ya Muumba, ambaye jina lake ni Yehova.a

Neno “Haleluya” hutokea mara nyingi katika Biblia. Kwa nini? Kwa sababu kuna sababu nyingi sana za kumsifu Mungu. Yah (Yehova) ndiye Muumba na Mtegemezaji wa ulimwengu wote mzima ulio mkubwa mno. (Zaburi 147:4, 5; 148:3-6) Ndiye aliyeanzisha mifumikolojia ambayo huwezesha maisha duniani. (Zaburi 147:8, 9; 148:7-10) Naye hupendezwa kipekee na wanadamu. Tukifanya mapenzi yake, yeye hutubariki na hututegemeza katika uhai huu na hututolea lile tumaini hakika la uhai ulio mzuri hata zaidi utakaokuja. (Zaburi 148:11-14) Ni Yah (Yehova) aliyepulizia maneno haya: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:29.

Kwa sababu hiyo, hili himizo la bidii laelekezewa wote: “Haleluya!” “Sifuni Yah, nyinyi watu!” (Zaburi 104:35, NW, kielezi-chini) Lakini, kwa kuhuzunisha, si kila mtu ahisiye kutaka kuitikia. Leo, watu wanateseka. Wengi wana njaa, ni wagonjwa, au wanaonewa. Watu kadhaa huvumilia huzuni nyingi kwa sababu ya matumizi mabaya ya dawa za kulevya au ya alkoholi au matokeo ya ukosefu wao wa adili au ya uasi. Je, kuna sababu yoyote kwa watu hao kumsifu Mungu?

‘Ni Yehova Tu Aliyeweza Kunipa Tumaini’

Ndiyo, kunayo. Yehova hualika kila mtu bila kuacha yeyote, wapate kumjua, kujifunza kufanya mapenzi yake, na kufurahia baraka zinazofanya watu watake kumsifu. Na wengi huitikia. Fikirieni, kwa kielelezo, Adriana katika Guatemala. Adriana alipokuwa na umri wa miaka saba, mamaye alikufa. Punde tu baadaye babaye akaondoka nyumbani. Alipokuwa na umri wa miaka kumi, alianza kufanya kazi ili kujiruzuku. Kwa kuwa mamaye alikuwa amemwambia amtumikie Mungu na kanisa, Adriana alishirikiana na vikundi tofauti-tofauti vya Kikatoliki, lakini alipofikia umri wa miaka 12, alikuwa ametamauka, akajiunga na genge la mtaani. Alianza kuvuta sigareti, kutumia dawa za kulevya, na kuiba. Kwa nini msichana mchanga kama huyo atake kumsifu Mungu?

Dadaye Adriana alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, lakini Adriana akamcheka. Kisha shangazi yao akafa. Kwenye maziko ya shangazi yake, Adriana alisumbuliwa na maswali ya kutatiza. Shangazi yake alikwenda wapi? Je, alikuwa mbinguni? Je, alikwenda kwenye helo yenye moto? Hilo lilitatanisha sana, na Adriana akaenda kwenye kikanisa cha makaburi kusali ili kupata msaada akitumia jina la Mungu Yehova, sawa na vile dadaye alivyokuwa amemfundisha.

Upesi alikuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na kuhudhuria mikutano yao ya Kikristo. Hilo lilimpa mtazamo mpya kabisa juu ya maisha, naye akakomesha kwa moyo mkuu ushirika wake pamoja na magenge ya mtaani. Sasa Adriana, katika miaka yake ya kati ya 20, asema hivi: “Ni kumpenda Yehova tu kulikoniondosha kwenye njia hiyo mbaya ya maisha. Ni Yehova tu katika rehema yake kubwa aliyeweza kunipa tumaini la uhai udumuo milele.” Ujapokuwa mwanzo wake mgumu maishani, Adriana ana sababu bora zaidi sana za kumsifu Mungu.

Hali nyingine iliyo mbaya hata zaidi yaripotiwa kutoka Ukrainia. Mwanamume fulani yumo gerezani akingojea kufishwa. Je, anajihurumia? Je, ameshuka moyo? La, hasha. Akiwa ametembelewa majuzi na Mashahidi wa Yehova na kupata ujuzi juu ya Yehova, aliwaomba wamtembelee mama yake. Sasa anawaandikia kwa sababu amesikia kwamba walitimiza ombi lake. Asema hivi: “Asanteni kwa kumtembelea mamangu. Hiyo ilikuwa habari yenye shangwe zaidi niliyopokea katika mwaka uliopita.”

Akisema juu yake mwenyewe na juu ya wafungwa wenzake ambao amewatolea ushahidi, yeye aandika hivi: “Sasa tuna imani katika Mungu na twajaribu kutenda kulingana na imani yetu.” Amalizia barua yake hivi: “Asanteni kwa kutusaidia kujifunza upendo ni nini na kupata imani. Nikiendelea kuwa hai, nitawasaidia pia. Shukrani kwa Mungu kwamba mko na kwamba mnasaidia wengine wampende Mungu na kumwamini.” Mwanamume huyo amekata rufani ya hukumu yake ya kifo. Lakini kama anafishwa au anakaa gerezani miaka mingi, yeye kwa wazi ana sababu ya kumsifu Mungu.

‘Ingawa Mimi Ni Kipofu, Naweza Kuona’

Sasa, fikiria msichana tineja mwenye nishati apotezaye kwa ghafula uwezo wake wa kuona. Ndilo jambo lililompata Gloria, aishiye Argentina. Gloria akawa kipofu kwa ghafula alipokuwa na umri wa miaka 19, naye hakupata tena uwezo wake wa kuona. Alipokuwa na umri wa miaka 29 alianza kukaa na mwanamume bila kufunga ndoa na upesi akawa mja mzito. Sasa alihisi kwamba maisha yake yalikuwa na maana. Lakini mtoto wake alipokufa, akaanza kujiuliza maswali. Alitaka kujua, ‘Mbona ninapatwa na hili? Nimefanya nini? Je, kwa kweli Mungu yuko?’

Ndipo, Mashahidi wa Yehova wawili wakaja mlangoni pake. Alianza kujifunza Biblia, akajifunza juu ya ahadi yayo kwamba katika ulimwengu mpya, vipofu wataona tena. (Isaya 35:5) Ni tazamio la ajabu kama nini kwa Gloria! Alifurahi sana, hasa mumeye alipokubali kuhalalisha ndoa yao. Halafu mumeye akapatwa na aksidenti akawa asiyejiweza, mwenye kutumia kiti chenye magurudumu sikuzote. Leo mwanamke huyo kipofu hana budi kujitahidi ili kupata riziki. Kwa kuongezea, yeye hufanya kazi zote za nyumbani, na pia kumtunza mumeye kwa uangalifu. Hata hivyo Gloria humsifu Yehova! Kwa msaada wa ndugu na dada zake Wakristo, yeye hujifunza Biblia ya maandishi ya vipofu, naye hutiwa moyo sana na mikutano ya Kikristo kwenye Jumba la Ufalme. Asema hivi: “Ni vigumu kueleza, lakini ingawa mimi ni kipofu, ni kana kwamba naweza kuona.”

Nyakati nyingine watu hunyanyaswa wanapomsifu Mungu. Mwanamke fulani katika Croatia alifurahi alipopata kujifunza juu ya Mungu, lakini mumeye alipinga imani yake mpya akamkatalia mbali na kwenda na binti yao mwenye umri wa mwaka mmoja. Bila makao, kwa sababu ya kuachwa na mumeye na familia, bila nyumba, kazi, wala hata mtoto wake, mwanzoni alikuwa hoi. Lakini kumpenda kwake Mungu kulimtegemeza, ingawa aliweza kumwona bintiye mara chache tu mpaka mtoto huyo alipokua. Mwanamke huyo alikuwa amepata “lulu moja ya thamani ya juu” na asingeweza kuiacha. (Mathayo 13:45, 46) Yeye alidumishaje shangwe yake katika nyakati hizo ngumu? Asema hivi: “Shangwe ni tunda la roho ya Mungu. Yaweza kusitawishwa bila kutegemea hali za nje, sawa na vile mimea iliyopandwa katika jumba la kioo iwezavyo kukua hata halihewa ya nje iweje.”

Katika Finland, Markus mwenye umri wa miaka sita alidodoswa kuwa na maradhi fulani ya misuli yasiyoponyeka. Upesi akaanza kutumia kiti chenye magurudumu. Miaka michache baadaye, mama yake alimpeleka kwa Mpentekoste fulani aliyekuwa akipata umaarufu mwingi kwa kudai kuponya wagonjwa. Lakini hakupata ponyo la kimuujiza. Kwa hiyo Markus akaacha kupendezwa na Mungu akafuatia masomo ya kisayansi na nyanja nyingine za kilimwengu. Halafu karibu miaka mitano iliyopita, mwanamke fulani atumiaye kiti chenye magurudumu aliyeandamana na mwanamume kijana walitembelea nyumba aliyoishi Markus. Walikuwa Mashahidi wa Yehova. Markus alikuwa mwatheisti sasa, lakini hakukataa kuzungumzia dini akawaalika ndani.

Baadaye, wenzi wa ndoa walimtembelea, na funzo la Biblia likaanzishwa. Hatimaye, nguvu za kweli ya Biblia zilibadili maoni ya Markus juu ya mambo, naye akang’amua kwamba kujapokuwa kutojiweza kwake, kwa kweli alikuwa na sababu za kumsifu Mungu. Alisema: “Nafurahi sana kwa sababu nimepata kweli na tengenezo ambalo Yehova anatumia. Sasa maisha yangu yana mwelekezo na maana. Kondoo mwingine aliyepotea amepatikana na hataki kuacha kundi la Yehova!”—Linganisha Mathayo 10:6.

Acheni Wote ‘Wamsifu Yah’

Hayo ni mambo machache tu yaliyoonwa kati ya mengi sana yawezayo kusimuliwa ili kuonyesha kwamba wanadamu leo, hata hali zao ziwe zipi, waweza kuwa na sababu ya kumsifu Mungu. Mtume Paulo alieleza jambo hilo hivi: “Ujitoaji-kimungu ni wenye manufaa kwa mambo yote, kwa kuwa una ahadi ya uhai wa sasa na ule utakaokuja.” (1 Timotheo 4:8) Tukifanya mapenzi ya Mungu, atatimiza “ahadi ya uhai wa sasa.” Bila shaka, katika mfumo huu wa mambo hatawafanya maskini wawe matajiri au wagonjwa wawe na afya. Lakini yeye huwapa roho yake wale wanaomtumikia ili waweze kupata shangwe na uradhi hali zao za nje ziwe zipi. Ndiyo, hata katika “uhai wa sasa,” wagonjwa, wanaoonewa, na maskini waweza kuwa na sababu ya kumsifu Mungu.

Lakini namna gani uhai “utakaokuja”? Kuufikiria kwenyewe kwapaswa kutufanya tumsifu Mungu kwa idili kubwa kupita yote! Twasisimuka kufikiria wakati ambapo umaskini hautajulikana; wakati ambapo “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa”; na wakati ambapo Yehova Mungu “atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Isaya 33:24; Ufunuo 21:3, 4; Zaburi 72:16) Wewe huonaje ahadi hizo kutoka kwa Mungu?

Mwanamume kijana katika El Salvador alikubali trakti ya Biblia iliyoeleza baadhi ya mambo hayo. Alimwambia Shahidi aliyempa hiyo, “Bibi, yanayosemwa na trakti hii ni mazuri mno yasiweze kuaminika.” Wengi huitikia hivyo. Hata hivyo, hizo ni ahadi za yule Mmoja aliyeumba ulimwengu wote mzima, aliyeanzisha duru za kiasili za dunia yetu, na ambaye husaidia hata maskini na wagonjwa wapate shangwe. Twaweza kuamini yale asemayo. Mwanamume kijana aliyetajwa juu alijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova naye akaona hayo kuwa kweli. Ikiwa hujaanza kufanya hivyo bado, twakutia moyo ufanye vivyo hivyo. Kisha, na uweko wakati ambapo mfumo huu wa mambo uliopo umepitilia mbali, na uumbaji wote waungana katika mlio: “Haleluya!” “Sifuni Yah, nyinyi watu!”—Zaburi 112:1, NW; 135:1, NW.

[Maelezo ya Chini]

a Katika Biblia, nyakati nyingine jina “Yehova” hufupizwa kuwa “Yah.”

[Picha katika ukurasa wa 5]

Na uweko wakati ambapo uumbaji wote waungana katika mlio: “Haleluya!”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki