Dunia—Kwa Nini Iko Hapa?
Kuna swali upaswalo kufikiria: Je, sayari yetu nzuri ilitokezwa na Muumba mwenye akili ambaye ana kusudi fulani kwa dunia na kwa wanadamu wanaoishi juu yake? Kutatua suala hilo kwa kukuridhisha kwaweza kukusaidia uelewe wakati ujao una nini kwa ajili ya sayari yetu.
WANASAYANSI wengi ambao wamechunguza ulimwengu na dunia yetu kwa undani, wameona uthibitisho mbalimbali wenye kuonyesha kuwako kwa Muumba, kwamba Mungu ndiye aliyeiumba. Fikiria maelezo kutoka kwa mwanasayansi mmoja tu:
Profesa Paul Davies aandika katika kitabu The Mind of God: “Kuwako kwa ulimwengu wenye utaratibu, na upatano, wenye miundo imara iliyo na utaratibu na utata, kwahitaji sheria na hali za aina ya pekee sana.”
Baada ya kuzungumzia “sadfa” kadhaa ambazo waastrofizikia na wengineo wamezifahamu, Profesa Davies aongeza kusema hivi: “Mtu afikiriapo sadfa hizi kwa pamoja, hizo huandaa uthibitisho wenye kuvutia kwamba, uhai kama tuujuavyo hutegemea kwa njia nyetivu sheria muhimu za fizikia, na pia aksidenti ambazo huonekana kutokea bila kutarajiwa katika takwimu halisi ambazo ulimwengu umeteua ili kutokeza uzito mbalimbali wa mata zilizo ndogo zaidi, kani ya uwezo, na kadhalika. . . . Yatosha kusema kwamba, kama tungejifanya kuwa Mungu na kuteua takwimu za uzito huo mbalimbali vile tupendavyo kwa kugeuza seti ya vifundo, tungepata kwamba namna ambavyo tumegeuza vifundo hivyo vyote, ingefanya ulimwengu uwe usioweza kukalika. Katika visa fulani yaonekana kana kwamba vifundo tofauti-tofauti lazima viwekwe katika hali nzuri kabisa ikiwa ulimwengu utakuwa katika hali itakayofanya uhai usitawi. . . . Uhakika wa kwamba hata mabadiliko madogo ya namna mambo yalivyo, yaweza kufanya ulimwengu usiweze kufanyiwa uchunguzi, bila shaka ni jambo la hakika, lenye umaana mkubwa.”
Kwa watu wengi matokeo ya uchunguzi ulio hapo juu yamaanisha kwamba, dunia yetu pamoja na ulimwengu wote, ulitokezwa na Muumba mwenye kusudi. Ikiwa ndivyo ilivyo, twahitaji kwanza kabisa kujua ni kwa nini aliiumba dunia. Twahitaji pia kuhakikisha, tukiweza, kusudi lake kwa dunia ni nini. Kwa habari hii, jambo lisilo la kawaida hutokea. Licha ya kupendwa kwa uatheisti kulikoenea pote, idadi ya watu yenye kushangaza bado huamini katika Muumba mwenye akili. Makanisa yaliyo mengi ya Jumuiya ya Wakristo husema tu juu ya Mungu mweza yote na Muumba wa ulimwengu wetu. Hata hivyo, ni mara chache dini hizi husema kwa uhakika na usadikisho juu ya wakati ujao wa dunia katika kusudi la Mungu.
Biblia Husema Nini?
Ni jambo la akili kutegemea chanzo cha habari ambacho kimekubaliwa na wengi kuwa kimetoka kwa Muumba. Chanzo hicho ni Biblia. Mojawapo ya taarifa zake iliyo rahisi na wazi zaidi kuhusiana na wakati ujao wa dunia yetu, yapatikana kwenye Mhubiri 1:4. Twasoma hivi: “Kizazi huenda, kizazi huja; nayo dunia hudumu daima.” Biblia hueleza waziwazi ni kwa nini Yehova Mungu aliiumba dunia. Yaonyesha pia kwamba aliiweka katika mahali paifaapo kabisa katika ulimwengu na kuhusiana na jua letu, ili kutegemeza uhai juu yake. Mungu Mweza Yote alimpulizia nabii wa kale, Isaya, aandike hivi: “Maana BWANA, aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni BWANA, wala hapana mwingine.”—Isaya 45:18.
Lakini vipi njia anazositawisha mwanadamu za kuharibu uhai wote duniani? Katika hekima yake isiyolinganika, Mungu atangaza kwamba ataingilia kabla ya wanadamu kuweza kuharibu uhai wote kwenye sayari yetu. Ona ahadi hii yenye kutumainisha katika Ufunuo, kitabu cha mwisho cha Biblia: “Mataifa wakawa na hasira ya kisasi, na hasira ya kisasi yako mwenyewe ikaja, na wakati uliowekwa rasmi kwa ajili ya wafu kuhukumiwa, na kuwapa thawabu yao watumwa wako hao manabii na watakatifu na wale wanaohofu jina lako, wadogo na wakubwa, na kuwaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia.”—Ufunuo 11:18.
Yehova hutufunulia lile lililokuwa kusudi lake la awali la kuiumba dunia, kito hiki katika anga, kama vile mwanaanga mwenye kuzunguka dunia alivyoifafanua. Mungu aliikusudia iwe paradiso ya tufeni pote, ikiwa imekaliwa na wanadamu kwa furaha—wanaume kwa wanawake—wote wakiishi kwa amani na upatano. Alipanga kujaza watu kwenye sayari hatua kwa hatua kwa kuwaruhusu wanadamu wawili wa kwanza wazae watoto. Ili awafurahishe wenzi wawili wa kwanza wa kibinadamu, Yehova alikuwa ameifanya sehemu ndogo ya dunia iwe paradiso. Kwa vile uzazi wa familia za kibinadamu ungeendelea kwa miaka na karne nyingi, bustani ya Edeni ingepanuka hatua kwa hatua hadi wakati ambapo andiko la Mwanzo 1:28 lingetimizwa: “Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha.”
Tuonapo sasa hali yenye kusikitisha ya dunia na ya wakazi wake, je, hilo humaanisha kwamba kusudi la Mungu la awali kwa dunia limeshindwa? Au je, amebadili kusudi lake na kuamua kwamba kwa sababu ya upotovu wa wanadamu, ataruhusu sayari iangamizwe kabisa na kuanza mambo upya? La, twaweza kuwa na uhakika kwamba hakuna yoyote ya hali hizo za mambo itakuwa hivyo. Biblia hutuambia kwamba chochote ambacho Yehova hukusudia ni lazima hatimaye kitukie, kwamba chochote aamuacho hakiwezi kuzuiwa na mtu yeyote au hata jambo lisilotarajiwa. Yeye atuhakikishia hivi: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”—Isaya 55:11.
Kusudi la Mungu Lilikatizwa, Si Kubadilishwa
Kwa sababu ya uasi wa Adamu na Hawa na kufukuzwa kwao kutoka katika bustani ya Edeni, ilikuwa wazi kwamba kusudi la Mungu la kuwa na dunia iliyo paradiso lingetimizwa bila wao kuwako. Hata hivyo, Yehova alionyesha papo hapo kwamba baadhi ya watoto wao wangetekeleza amri yake ya awali. Ni kweli, hilo lingechukua wakati, hata karne nyingi, lakini hakuna jambo lionyeshalo ni wakati mwingi kadiri gani ambao ungalihusika katika kutekeleza amri hiyo ya awali, hata kama wote wawili, Adamu na Hawa wangaliendelea kuishi wakiwa wakamilifu. Jambo la hakika ni kwamba, kufikia mwisho wa Utawala wa Milenia wa Kristo Yesu—miaka zaidi ya elfu moja kuanzia sasa—hali za Kiparadiso za Edeni zitaenea duniani pote na sayari Dunia itakaliwa na wazao wenye amani na furaha wa wanadamu wawili wa kwanza. Kwa kweli, uwezo wa Yehova akiwa Mkusudiaji asiyeweza kukosea utatetewa kwa umilele!
Kisha kutakuwa na utimizo wa unabii mbalimbali wenye kusisimua ambao Mungu alipulizia muda mrefu uliopita. Maandiko kama vile Isaya 11:6-9 yatatimizwa kwa utukufu: “Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza. Ng’ombe na dubu watalisha pamoja; watoto wao watalala pamoja; na simba atakula majani kama ng’ombe. Na mtoto anyonyaye atacheza penye tundu la nyoka, na mtoto aliyeachishwa atatia mkono wake katika pango la fira. Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”
Afya mbaya na ugonjwa wenye kuleta kifo yatakuwa mambo ya wakati uliopita kama vile kifo chenyewe kitakavyokuwa. Je, kuna jambo lolote liwezalo kuwa dhahiri zaidi ya maneno hayo sahili yapatikanayo katika kitabu cha mwisho cha Biblia? “Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa vikundi vya watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:3, 4.
Naam, twaweza kujipa moyo—sayari yetu Dunia iliyo nzuri itadumu. Na liwe pendeleo lako kuokoka mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo pamoja na mazoea yake yenye kuangamiza dunia. Ulimwengu mpya ulio safi wenye kutokezwa na Mungu uko karibu. Na wapendwa wengi wataamka kutoka katika kifo kupitia muujiza wa ufufuo. (Yohana 5:28, 29) Kwa kweli, dunia yetu itadumu, nasi twaweza kudumu pamoja nayo na kuifurahia.