Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 10/15 kur. 4-7
  • Je, Waweza Kuiamini Biblia?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Waweza Kuiamini Biblia?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Biblia au Mapokeo?
  • Umuhimu wa Maandiko
  • Manufaa ya Kuishi Kulingana na Biblia
  • Ukweli Kuhusu Helo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Imani Yako Katika Ufufuo Ni Yenye Nguvu Kadiri Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Je! Nafsi Huendelea Kuishi Baada ya Kifo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Jizoeze Imani Ili Upate Uhai wa Milele
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 10/15 kur. 4-7

Je, Waweza Kuiamini Biblia?

ITIKADI katika Biblia huendelea kuenea sana, hata katika ulimwengu wa kisasa. Kwa mfano, katika uchunguzi wa Gallup uliofanyiwa Wamarekani hivi majuzi, asilimia 80 walikuwa na itikadi ya kwamba Biblia ni Neno la Mungu. Iwe katika eneo lenu kuna asilimia kubwa kama hiyo au la, waweza kuelewa kwamba waumini hao hutarajia kufundishwa Biblia kanisani. Lakini, mara nyingi hawafundishwi. Chukua kwa kielelezo, lile fundisho la kuteseka kwa nafsi baada ya kifo.

Je, purgatori au helo yenye moto hufundishwa mahali popote katika Biblia? Leo, wasomi wengi katika Jumuiya ya Wakristo wangejibu la. New Catholic Encyclopedia hutaarifu hivi: “Katika mchanganuo wa mwisho kabisa, fundisho la Kikatoliki la purgatori lina msingi wa kimapokeo, wala si wa Andiko Takatifu.” Kwa habari ya helo, A Dictionary of Christian Theology hueleza hivi: “Katika A[gano] J[ipya] hatupati moto wa helo ukiwa sehemu ya mahubiri ya kale.”

Kwa hakika, tume ya mafundisho ya Kanisa la Uingereza hivi karibuni ilikuwa habari motomoto kwenye magazeti, ilipopendekeza kukataliwa katakata kwa fundisho la moto wa helo. Dakt. Tom Wright mkuu wa Kanisa Kuu la Litchfield, ataarifu kwamba taswira ya zamani juu ya helo “ilimfanya Mungu kuonekana kama dubwana na hilo liliwaacha watu wengi wakiwa na makovu yenye kuumiza sana kisaikolojia.” Ripoti ya tume hiyo huifafanua helo kuwa “hali ya kutokuwako kabisa.”a Vivyo hivyo, New Catholic Encyclopedia hutaarifu hivi kuhusu maoni ya Kikatoliki: “Elimu ya dini leo huliona tatizo la helo kuwa hali ya kutenganishwa na Mungu.”

Kwa kweli, yale ambayo Biblia hufundisha juu ya nafsi hupingana na fundisho la purgatori na moto wa helo. Mara nyingi Biblia husema juu ya kufa kwa nafsi. “Nafsi inayofanya zambi itakufa.” (Ezekieli 18:4, Zaire Swahili Bible; linganisha tafsiri ya King James na Douay ya Katoliki). Kulingana na Biblia, wafu hawana fahamu, hawawezi kuumia. “Kwa sababu walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lolote.” (Mhubiri 9:5) Tumaini ambalo Biblia huwatolea wafu ni ufufuo wa wakati ujao. Rafiki ya Yesu Lazaro alipokufa, Yesu alilinganisha kifo na kulala usingizi. Dada ya Lazaro Martha alionyesha tumaini linalofundishwa katika Biblia alipojulisha hivi: “Najua atafufuliwa katika ufufuo siku ya mwisho.” Kwa kumfufua Lazaro kutoka katika kifo, Yesu alihakikishia wanadamu tumaini hilo.—Yohana 5:28, 29; 11:11-14, 24, 44.

Wanahistoria huonyesha kwamba lile fundisho la kwamba mwanadamu ana nafsi iliyotenganishwa, na isiyoweza kufa halitokani na Biblia bali latokana na falsafa ya Kigiriki. New Catholic Encyclopedia husema kwamba Waebrania wa kale hawakumfikiria mtu kuwa aliyefanyizwa kwa mwili na nafsi isiyo na umbo. Hiyo hutaarifu hivi juu ya itikadi ya Waebrania: “Pumzi ya uhai ilipoingia ndani ya mtu wa kwanza aliyefanyizwa na Mungu kwa mavumbi ya ardhi, yeye alikuja kuwa kiumbe ‘kilicho hai.’ (M[wanzo] 2.7). Kifo hakikuonekana kuwa mtengano wa vitu viwili tofauti vilivyo ndani ya mtu, sawa na ilivyo katika falsafa ya Kigiriki; ile pumzi ya uhai hutoka naye mtu huachwa akiwa ‘kiumbe aliyekufa’ (M[ambo ya Walawi] 21.11; H[esabu] 6.6; 19.13). Katika kila kisa neno ‘kiumbe’ lingekuwa [neʹphesh] ya Kiebrania, litafsiriwalo mara nyingi kuwa ‘nafsi’ lakini, kwa hakika, ikilingana kwa ukaribu sana na mtu huyo.”

Ensaiklopedia hiyohiyo hutaarifu kwamba wasomi Wakatoliki hivi karibuni “wameendelea kukazia kwamba A[gano] J[ipya] halifundishi kwamba nafsi haiwezi kufa katika maana ya utamaduni wa Kiyunani [Kigiriki].” Yamalizia hivi: “Makisio ya kifalsafa hayawezi kutoa utatuzi wa msingi juu ya uhai baada ya kifo, kama ule utatuzi upatikanao kutokana na ile zawadi ya Ufufuo ipitayo nguvu za kawaida.”

Biblia au Mapokeo?

Lakini, mawazo yasiyo ya Kibiblia yalipataje kuwa sehemu ya fundisho la kanisa? Makanisa mengi hudai kwamba Biblia ndiyo mamlaka yake ya juu zaidi. Kwa kielelezo, hivi karibuni Papa John Paul wa Pili alisema juu ya uhitaji wa Andiko “kukubaliwa na Wakatoliki kuwa la kweli kabisa, na kuwa kanuni kuu kuliko zote za imani yetu.” Hata hivyo, ni jambo lenye kukubalika kwa ujumla kwamba mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo leo si kama yale ya Wakristo wa karne ya kwanza. Makanisa mengi huona mabadiliko hayo kuwa sehemu ya maendeleo ya hatua kwa hatua ya fundisho la kanisa. Isitoshe, Kanisa Katoliki huchukulia kwamba mapokeo ya kanisa yana mamlaka sawa na Maandiko. Kichapo New Catholic Encyclopedia husema kwamba kanisa “haliamini fundisho lolote kwa msingi wa Andiko pekee, pasipo kutegemea mapokeo, wala hakuna msingi wa mapokeo peke yake, pasipo kutegemea Andiko.”

Kihistoria, makanisa yamebadili mafundisho ya Kimaandiko, kwa yale yenye msingi tu wa mapokeo. Kwa hakika makanisa mengi sasa huyaona mafundisho ya Biblia kuwa yenye makosa. Kwa kielelezo, New Catholic Encyclopedia hutaarifu kwamba ni “wazi kwamba taarifa nyingi za Biblia si za kweli zinapoangaliwa kwa msingi wa ujuzi wa sayansi na historia ya kisasa.” Likizungumzia juu ya fundisho la Biblia kwamba wafu hawana fahamu, hiyo huongeza hivi: “Hata katika mambo ya kidini, A[gano] la K[ale] hutoa ushuhuda wa ujuzi usio kamili juu ya . . . uhai baada ya kifo.” Ensaiklopedia hiyo hunukuu Zaburi 6:5 (mstari 6 katika Biblia fulani) kuwa kielelezo cha hili: “Maana mautini hapana kumbukumbu lako; katika kuzimu ni nani atakayekushukuru?” Seminari fulani za Kiprotestanti na vyuo vingine havifundishi tena kwamba Biblia haikosei. Kwa upande mwingine, Kanisa Katoliki huamini kwamba lina mamlaka ya kufundisha, ambayo kwayo, hilo hufasiri kinachofundishwa katika Biblia. Hata hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Vipi ikiwa fasiri mbalimbali kama hizo zaonekana kupingana na Maandiko?’

Umuhimu wa Maandiko

Kwa kurudia-rudia, Yesu alinukuu maandiko kuwa yenye mamlaka, mara nyingi akitanguliza hoja zake kwa kusema hivi: “Imeandikwa.” (Mathayo 4:4, 7, 10; Luka 19:46) Kwa kweli, Yesu alipozungumzia juu ya hali ya ndoa ya mtu fulani, yeye hakusema kutokana na makisio ya falsafa za Kigiriki, bali kutokana na simulizi la Mwanzo juu ya uumbaji. (Mwanzo 1:27; 2:24; Mathayo 19:3-9) Kwa wazi, Yesu aliyaona Maandiko kuwa yamepuliziwa na Mungu na ya kweli. Katika sala kwa Mungu, yeye alisema hivi: “Neno lako ni kweli.”—Yohana 17:17.b

Biblia hurekodi jinsi Yesu alivyowachambua vikali viongozi wa kidini wa wakati wake: “Kwa ustadi mwaweka kando amri ya Mungu kusudi mhifadhi mapokeo yenu. . . . Hivyo mwalibatilisha neno la Mungu kwa mapokeo yenu.” (Marko 7:6-13) Vivyo hivyo, mtume Paulo alikinza mkazo wa kufyonza ama falsafa ya Kigiriki ama mapokeo yenye makosa katika kufundisha kwake. “Jihadharini,” akaonya. “Labda huenda kukawa na mtu fulani ambaye atawachukua nyinyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyo mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu.” (Wakolosai 2:8; 1 Wakorintho 1:22, 23; 2:1-13) Kulikuwa na mapokeo fulani, au mafundisho, ambayo Paulo aliwahimiza Wakristo wadumishe, lakini haya yalitegemea Maandiko, nayo yalipatana kabisa na Maandiko. (2 Wathesalonike 2:13-15) “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa,” Paulo akaandika, “ili mtu wa Mungu apate kuwa hodari, aliyeandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 Timotheo 3:16, 17.

Paulo alitangulia kuona kimbele kule kuchukuliwa pole kwa pole mbali na Maandiko. Yeye alimwonya Timotheo hivi: “Kutakuwako kipindi cha wakati ambapo hawatachukuliana na fundisho lenye afya, . . . nao watageuzia mbali masikio yao kuacha kweli.” Alimhimiza Timotheo hivi: “Ingawa hivyo, wewe tunza akili zako katika mambo yote.” (2 Timotheo 4:3-5) Lakini kwa njia gani? Njia moja ni kuwa mwenye “akili ya uelekevu.” Kamusi moja ya Kigiriki hufasili neno hili la Biblia kuwa “utayari wa kujifunza na kukagua jambo bila kupendelea.” Luka alitumia usemi huu kuwafafanua Waberoya wa karne ya kwanza waliomsikiliza Paulo. Mafundisho ya Paulo yalikuwa mapya kwao, nao hawakutaka kupotoshwa. Akiwapongeza, Luka aliandika hivi: “[Waberoya] walikuwa wenye akili ya uelekevu bora zaidi kuliko wale katika Thesalonike, kwa maana walilipokea neno kwa hamu ya akili iliyo kubwa zaidi sana, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku juu ya kama mambo hayo yalikuwa hivyo.” Kuwa wenye akili ya uelekevu hakukuwafanya Waberoya wawe wenye kutia shaka, wenye mibetuko ya kuamini kitu chochote. Bali, “wengi kati yao wakawa waamini” kwa sababu ya uchunguzi wao wa moyo mnyofu.—Matendo 17:11, 12.

Manufaa ya Kuishi Kulingana na Biblia

Wakristo wa mapema walijulikana kwa ajili ya kushikamana kwao na Biblia na kwa upendo wao wa kujidhabihu. Hata hivyo, watu wengi leo wana “namna ya ujitoaji-kimungu lakini wa[na]thibitika kuwa si kweli kwa nguvu ya hiyo.” (2 Timotheo 3:5) Namna yoyote ya Ukristo leo ambayo haipatani na Ukristo wa awali, hauwezi kuwa na nguvu halisi za wema wowote katika maisha ya watu. Je, hili lingeweza kusaidia kueleza kwa nini twaona ongezeko la jeuri, ukosefu wa adili, kuvunjika kwa familia, na ufuatiaji wa vitu vya kimwili katika sehemu kubwa ya Jumuiya ya Wakristo? Katika nchi fulani ya “Kikristo,” vita mbaya za kikabila hupiganwa na washiriki wa dini moja.

Je, ile roho ya akili yenye uelekevu ya Waberoya ilitoweka? Je, kuna kikundi chochote cha watu leo kinachoamini na kuishi kulingana na Biblia?

Kitabu Encyclopedia Canadiana husema hivi: “Kazi ya Mashahidi wa Yehova ndio urudishaji na uanzishaji-upya wa Ukristo wa kale uliozoewa na Yesu na wanafunzi wake katika karne ya kwanza na ya pili za wakati wetu wa kawaida.” Ikiwarejezea Mashahidi, New Catholic Encyclopedia hutaarifu hivi: “Wao huiona Biblia kuwa chanzo pekee cha imani yao, na kanuni ya mwenendo wao.”

Bila shaka hii ndiyo sababu kubwa ya Mashahidi wa Yehova kujulikana ulimwenguni pote kwa ufanisi wao wa kiroho, amani, na furaha. Hivyo basi, twawatia moyo wasomaji wetu wajifunze mengi juu ya mafundisho ya Biblia yenye afya kiroho. Ujuzi mkubwa zaidi waweza kuongoza kwenye kuitumainia Biblia hata zaidi na imani yenye nguvu zaidi katika Mungu. Manufaa ya milele ya imani hiyo yastahili jitihada hiyo.

[Maelezo ya Chini]

a National Public Radio—“Morning Edition”

b Ili kupata habari zaidi juu ya kutegemeka kwa Biblia, ona broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, iliyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Mtume Paulo na wengine walihubiri sokoni

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mashahidi wa Yehova “huiona Biblia kuwa chanzo pekee cha imani yao, na kanuni ya mwenendo wao”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki