Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 2/1 kur. 30-31
  • Je, Ni “Yehova” au Ni “Yahweh”?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Ni “Yehova” au Ni “Yahweh”?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Penye Chanzo cha Ubishi Huo
  • Ni Nini Kinachoweza Kupatikana Katika Jina?
  • Kwa Nini Tulitumie Jina la Mungu Ikiwa Hatujui Linavyopaswa Kutamkwa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Jina la Mungu—Maana Yalo na Linavyotamkwa
    Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
  • Yehova Ni Nani?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Kumtambua Mungu wa Pekee wa Kweli
    Amkeni!—1999
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 2/1 kur. 30-31

Je, Ni “Yehova” au Ni “Yahweh”?

“MCHANGANYIKO,” “-sio ya asili” “-enye kupotosha.” Ni nini ambacho kingesababisha wasomi wa Kiebrania cha Biblia watumie maneno hayo yenye mkazo? Jambo linalobishaniwa ni kama “Jehovah” ni matamshi sahihi ya Kiingereza ya jina la Mungu. Ubishi huu umeendelea bila kudhibitiwa, kwa muda unaozidi miaka mia moja. Leo, wasomi wengi wanapendelea neno lenye silabi mbili “Yahweh.” Lakini je, kwa kweli matamshi “Yehova” ni “yenye kupotosha” kwa kiasi hicho?

Penye Chanzo cha Ubishi Huo

Kulingana na Biblia, Mungu mwenyewe aliwafunulia wanadamu jina lake. (Kutoka 3:15) Uthibitisho wa Kimaandiko waonyesha kwamba watumishi wa Mungu wa kale walitumia jina hilo kwa uhuru. (Mwanzo 12:8; Ruthu 2:4) Mataifa mengine pia yalijua jina la Mungu. (Yoshua 2:9) Hili lilikuwa hivyo hasa baada ya Wayahudi waliorudi kutoka utumwani Babiloni kuchangamana na watu wa mataifa mengi. (Zaburi 96:2-10; Isaya 12:4; Malaki 1:11) Kichapo The Interpreter’s Dictionary of the Bible chasema: “Kuna uthibitisho wa kutosha kwamba katika kipindi cha baada ya utekwa wageni wengi walivutiwa na dini ya Wayahudi.” Hata hivyo, kufikia karne ya kwanza W.K., ushirikina uliohusisha jina la Mungu ulikuwa umesitawi. Hatimaye, taifa la Kiyahudi halikuacha kutumia jina la Mungu waziwazi tu bali wengine hata walikataza lisitamkwe kabisa. Hivyo matamshi yake sahihi yakapotea—au je, yalipotea?

Ni Nini Kinachoweza Kupatikana Katika Jina?

Katika lugha ya Kiebrania, jina la Mungu linaandikwa kwa herufi hizi יהוה. Herufi hizi nne, zinazosomwa kuanzia kulia hadi kushoto, kwa kawaida zinajulikana kuwa Tetragramatoni. Majina mengi ya watu na ya mahali yanayotajwa katika Biblia yana ufupisho wa hilo jina la kimungu. Je, inawezekana kwamba majina haya ya kibinafsi yaweza kuandaa vidokezi fulani kuhusu jinsi ambavyo jina la Mungu lilitamkwa?

Kulingana na George Buchanan, profesa wa heshima kwenye Semina ya Theolojia katika Wesley, Washington, D.C., Marekani, jibu ni ndiyo. Profesa Buchanan aeleza hivi: “Katika nyakati za kale, mara nyingi wazazi waliwapa watoto wao majina ya miungu yao. Hilo lamaanisha kwamba wangetamka majina ya watoto wao namna ambavyo wangetamka jina la mungu wao. Tetragramatoni ilitumiwa katika majina ya watu, na sikuzote walitumia vokali ya katikati.”

Fikiria mifano michache ya majina ya kibinafsi yanayopatikana katika Biblia yanayotia ndani namna iliyofupishwa ya jina la Mungu. Yonathani, linaloonekana kuwa Yoh·na·thanʹ au Yehoh·na·thanʹ katika Biblia ya Kiebrania, lamaanisha “Yaho au Yahowah ametoa,” asema Profesa Buchanan. Jina la nabii Eliya ni ʼE·li·yahʹ au ʼE·li·yaʹhu katika Kiebrania. Kulingana na Profesa Buchanan, jina hilo lamaanisha: “Mungu wangu ni Yahoo au Yahoo-wah.” Vivyo hivyo, jina Yehoshafati kwa Kiebrania ni Yehoh-sha·phatʹ, linalomaanisha “Yaho amehukumu.”

Matamshi yenye silabi mbili ya Tetragramatoni kama “Yahweh” hayangetia ndani mvumo wa vokali o katika jina la Mungu. Lakini katika majina mengi ya Kibiblia yanayohusisha jina la kimungu, mvumo huu wa vokali ya katikati hupatikana katika namna ya awali na namna iliyofupishwa kama vile katika Jehonathan na Jonathan. Hivyo, Profesa Buchanan asema hivi kuhusu jina la kimungu: “Haiwezekani hata kidogo kukosa kutia ndani vokali oo au oh. Nyakati nyingine neno hilo lilifupishwa kuwa ‘Ya,’ lakini si ‘Ya-weh’ kamwe. . . . Wakati Tetragramatoni ilipotamkwa katika silabi moja ilikuwa ‘Yah’ au ‘Yo.’ Ilipotamkwa kwa silabi tatu ingekuwa ‘Yahowah’ au ‘Yahoowah.’ Ikiwa ilipata kufupishwa kuwa na silabi mbili ingekuwa ‘Yaho.’”—Biblical Archaeology Review.

Maelezo haya hutusaidia kuelewa taarifa iliyotolewa na msomi wa Kiebrania wa karne ya 19 Gesenius katika kichapo chake Hebrew and Chaldee Lexicon to the Old Testament Scriptures: “Wale wanaofikiria kwamba יְהוָֹה jina [Ye-ho-wah] lilikuwa matamshi halisi ya [jina la Mungu] wana msingi wa kutetea maoni yao. Katika njia hii silabi zilizofupishwa יְהוֹ [Ye-ho] na יוֹ [Yo], ambazo majina mengi ya kibinafsi huanza nazo, zaweza kuelezwa kwa njia yenye kusadikisha.”

Hata hivyo, katika utangulizi wa tafsiri yake ya hivi karibuni ya The Five Books of Moses, Everett Fox ataja kwamba: “Jitihada za kale na za kisasa za kupata tena matamshi ‘sahihi’ ya jina [la Mungu] kwa Kiebrania hazijafua dafu; wala jina ‘Yehova,’ linalosikika nyakati fulani wala lile la kiwango cha wasomi, ‘Yahweh,’ haliwezi kuthibitishwa kabisa.”

Bila shaka mjadala wa wasomi utaendelea. Wayahudi waliacha kutamka jina la Mungu wa kweli kabla Wamasora hawajaunda mfumo wa kutofautisha vokali. Hivyo, hakuna njia hakika ya kuthibitisha ni vokali zipi zilizoandamana na zile konsonanti YHWH (יהוה). Na bado, majina hasa ya watu mashuhuri katika Biblia—ambayo matamshi yake sahihi hayakupotezwa kamwe—huandaa kidokezi thabiti cha matamshi ya kale ya jina la Mungu. Kwa sababu ya uhakika huo, angalau wasomi fulani hukubali kwamba matamshi “Yehova” si yenye “kupotosha” kwa vyovyote.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Jina “Yehova” limekuwa matamshi yanayopendwa zaidi ya jina la Mungu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki