Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 2/1 kur. 25-29
  • Kushangilia Katika Yehova Kujapokuwa Majaribu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kushangilia Katika Yehova Kujapokuwa Majaribu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mwanzo Usio na Makuu
  • Majaribu Zaidi na Shangwe
  • Maendeleo ya Kitheokrasi Kisiwani
  • Ubatizo na Ukuzi Thabiti
  • Kusanyiko Lenye Kusisimua la Mapenzi ya Kimungu
  • Nafikia Mradi wa Utumishi wa Wakati Wote
  • Baraka Nyingi Wakati Uliopita na Wakati Ujao
  • “Kazi Nzuri!”
    Amkeni!—1994
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kitabu-mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1990
    1990 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 2/1 kur. 25-29

Kushangilia Katika Yehova Kujapokuwa Majaribu

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA GEORGE SCIPIO

Katika Desemba 1945, nililala katika wadi ya hospitali, nikiwa nimepooza kabisa isipokuwa mikono na miguu. Nilifikiri hali yangu ilikuwa ya muda tu, lakini wengine walishuku kama ningeweza kutembea tena. Lilikuwa jaribu kama nini kwa kijana mtendaji mwenye umri wa miaka 17! Nilikataa kukubali ubashiri huo. Nilikuwa na mipango mingi sana, kutia ndani safari ya kwenda Uingereza pamoja na mwajiri wangu mwaka ambao ungefuata.

NILIKUWA nimeshikwa na ugonjwa wa kupooza ambao ulikuwa umekikumba kisiwa chetu cha nyumbani cha St. Helena. Uliua watu 11 na kulemaza makumi yao. Nilipokuwa nimelala kitandani, nilikuwa na wakati mwingi wa kutafakari kuhusu maisha yangu mafupi na kuhusu wakati wangu ujao. Nilipokuwa nikifanya hivyo, nilianza kung’amua kwamba, zijapokuwa taabu zangu, nilikuwa na sababu ya kushangilia.

Mwanzo Usio na Makuu

Katika mwaka wa 1933 nilipokuwa na umri wa miaka mitano, baba yangu, Tom, aliyekuwa polisi na shemasi katika Kanisa la Baptisti, alijipatia vitabu viwili vilivyojalidiwa kutoka kwa Mashahidi wa Yehova wawili. Walikuwa waeneza-evanjeli wa wakati wote, au mapainia, waliokuwa wamekizuru kisiwa hicho kwa muda mfupi.

Mojawapo wa vitabu hivyo kiliitwa The Harp of God. Baba yangu alikitumia kujifunzia Biblia pamoja na familia yetu na watu kadhaa wenye kupendezwa. Kilikuwa na habari ngumu, na nilielewa mambo machache sana. Lakini nakumbuka nikitia alama kila andiko tulilozungumzia kwenye nakala yangu ya Biblia. Punde si punde baba yangu aling’amua kwamba habari tuliyokuwa tukijifunza ilikuwa kweli na kwamba ilitofautiana na yale aliyokuwa akihubiri katika Kanisa la Baptisti. Alianza kuwaeleza wengine juu yake na kuhubiri kutoka mimbari kwamba hakuna Utatu, moto wa helo, na hakuna nafsi isiyoweza kufa. Hili lilisababisha mjadala mkubwa kanisani.

Hatimaye, katika jitihada za kutatua suala hilo, mkutano wa kanisa ulifanywa. Swali liliulizwa, “Ni nani anayeunga mkono Wabaptisti?” Wengi walikubali. Swali lililofuata lilikuwa, “Ni nani anayemuunga mkono Yehova?” Watu wapatao 10 au 12 walikubali. Waliombwa waache kushiriki katika kanisa hilo.

Huu ulikuwa mwanzo usio na makuu wa dini mpya katika kisiwa cha St. Helena. Baba yangu aliwasiliana na makao makuu ya Watch Tower Society katika Marekani na kuomba mashine ya kunakili kwa ajili ya kuchezea umma mihadhara ya Biblia iliyorekodiwa. Aliambiwa kwamba mashine hiyo ilikuwa kubwa sana kuweza kupelekwa hadi St. Helena. Kinanda cha gramafoni kidogo zaidi kilipelekwa, na baadaye akina ndugu wakaagiza viwili zaidi. Walitembea kotekote katika kisiwa hicho kwa miguu na kwa kutumia punda, wakipelekea watu ujumbe.

Kadiri ujumbe ulivyoenea ndivyo na upinzani. Shuleni kwetu, watoto wangeimba: “Kila mtu na aje asikie, kikosi cha Tommy Scipio chenye kinanda cha gramofoni!” Hili lilikuwa jaribu kali kwangu, kijana wa shule aliyetaka kukubaliwa na marika wake. Ni nini kilichonisaidia kuvumilia?

Familia yetu kubwa—ya watoto sita—ilikuwa na funzo la Biblia la familia la kawaida. Pia tulisoma Biblia tukiwa pamoja kila asubuhi kabla ya kiamsha kinywa. Bila shaka hili limechangia fungu kubwa sana katika kusaidia familia yetu iendelee kwa uaminifu katika kweli kwa miaka iliyopita. Mimi binafsi nilisitawisha upendo kwa Biblia nilipokuwa na umri mchanga, na kwa miaka ambayo imepita, nimedumisha zoea la kusoma Biblia kwa ukawaida. (Zaburi 1:1-3) Kufikia wakati nilipoacha shule nikiwa na umri wa miaka 14, nilikuwa nimeimarika sana katika kweli, na nilimhofu Yehova kutoka moyoni. Hili liliniwezesha kushangilia katika Yehova kujapokuwa majaribu hayo.

Majaribu Zaidi na Shangwe

Nilipokuwa nimelala kitandani nikiwa mgonjwa nikifikiri juu ya miaka hiyo na mataraja yangu ya wakati ujao, kutokana na funzo langu la Biblia nilijua kwamba ugonjwa huu haukuwa jaribu fulani au adhabu kutoka kwa Mungu. (Yakobo 1:12, 13) Hata hivyo, ugonjwa wa kupooza ulikuwa jaribu lenye kuhuzunisha, na ningebaki na madhara yake kwa muda wote wa maisha yangu.

Nilipopona, nilihitaji kujifunza kutembea tena. Pia misuli fulani ya mikono yangu iliacha kufanya kazi. Siwezi kuhesabu mara nilizoanguka kila siku. Hata hivyo, kwa sala yenye bidii na jitihada zenye kuendelea, kufikia mwaka wa 1947, niliweza kutembea tena kwa kutumia bakora.

Wakati huo nilimpenda mwanamke fulani mchanga, Doris, aliyekuwa na usadikisho wa kidini kama wangu. Tulikuwa wachanga sana kufikiria kufunga ndoa, lakini nilichochewa kufanya maendeleo ya kutembea zaidi. Pia niliacha kazi yangu kwa sababu mshahara haukutosha kuruzuku mke, na nilianzisha maabara yangu ya meno, ambayo ilifanya kazi kwa miaka miwili iliyofuata. Tulioana katika mwaka wa 1950. Kufikia wakati huo nilikuwa nimechuma pesa za kutosha za kununua gari dogo. Sasa ningeweza kuwapeleka akina ndugu mikutanoni na katika utumishi wa shambani.

Maendeleo ya Kitheokrasi Kisiwani

Katika mwaka wa 1951 Sosaiti ilitutumia mwakilishi wao wa kwanza. Alikuwa Jacobus van Staden, mwanamume mchanga kutoka Afrika Kusini. Tulikuwa tu tumehamia nyumba iliyokuwa kubwa, hivyo tungeweza kumwandalia mahali pa kulala kwa mwaka mzima. Kwa kuwa nilikuwa nimejiajiri mwenyewe, tulitumia muda mwingi pamoja katika kazi ya kuhubiri, na nilipokea mazoezi mengi yenye thamani kutoka kwake.

Jacobus, au Koos kama tulivyomwita, alipanga mikutano ya kutaniko ya kawaida, ambayo sisi sote tulishiriki kwa furaha. Tulikuwa na tatizo la usafiri kwa sababu kulikuwako magari mawili tu miongoni mwa wote wenye kupendezwa. Mandhari ilikuwa yenye mawemawe na milima mingi, na kulikuwako barabara chache zilizokuwa nzuri wakati huo. Hivyo, ilikuwa kazi kubwa kupeleka kila mtu mikutanoni. Wengine walianza kutembea asubuhi mapema. Nilibeba watatu katika gari langu na kuwashukisha mahali fulani barabarani. Walishuka na kuanza kutembea. Nilirudi, nikachukua wengine watatu kwa umbali fulani, nikawashukisha, na kurudi. Hatimaye, wote walifika mikutanoni kwa njia hii. Baada ya mikutano, tulifuata utaratibu huo huo kurudisha kila mtu nyumbani.

Pia Koos alitufundisha jinsi ya kuwa na utoaji wenye matokeo milangoni. Tulijionea mambo mengi mazuri na mengine hayakuwa mazuri sana. Lakini shangwe tuliyopata katika huduma ilipita majaribu yote yaliyosababishwa na wapinzani wa kazi yetu ya kuhubiri. Asubuhi moja nilikuwa nikihubiri na Koos. Tulipoukaribia mlango, tulisikia sauti kutoka ndani. Mwanamume fulani alikuwa akisoma Biblia kwa sauti kubwa. Tungeweza kusikia waziwazi maneno yanayojulikana sana ya Isaya sura ya 2. Alipofika kwenye mstari wa 4, tulibisha mlango. Mwanamume mzee mwenye urafiki alitukaribisha ndani, na tulitumia Isaya 2:4 kumweleza habari njema za Ufalme wa Mungu. Tulianza kujifunza Biblia pamoja naye hata ingawa aliishi mahali pasipoweza kufikika kwa urahisi. Tulihitaji kuteremka mlima, kuvuka kijito kwa kukanyaga mawe ya kuvukia, kupanda mlima mwingine tena, na kisha kuteremka kwa nyumba yake. Lakini jitihada hizo zilikuwa na matokeo. Mwanamume huyu msikivu alikubali kweli na akabatizwa. Kusudi afike mikutanoni, alitembea kwa kutumia bakora mbili hadi kufikia mahali ambapo ningeweza kumbeba kwa gari katika mwendo uliobakia. Baadaye alikufa akiwa Shahidi mwaminifu.

Mkuu wa polisi alipinga kazi yetu na mara kwa mara alitisha kumrudisha Koos nchini kwao. Mara moja kwa mwezi alimwita Koos ili kumhoji. Uhakika wa kwamba sikuzote Koos alimpa majibu ya moja kwa moja kutoka kwa Biblia ulimfanya awe na uhasama mwingi hata zaidi. Katika kila pindi alimwonya Koos aache kuhubiri, lakini kila pindi alipokea ushahidi. Aliendelea kupinga kazi hiyo hata baada ya Koos kuondoka St. Helena. Kisha Mkuu huyo, mwanamume mkubwa, mwenye nguvu, kwa ghafula akawa mgonjwa na kukonda kama ufito. Madaktari hawangeweza kubainisha tatizo lake. Tokeo lilikuwa kwamba, aliondoka kisiwani.

Ubatizo na Ukuzi Thabiti

Baada ya Koos kukaa kwenye kisiwa hicho kwa miezi mitatu, alihisi kwamba ilifaa kuwa na huduma ya ubatizo. Tatizo lilikuwa kupata dimbwi linalofaa. Tuliamua kuchimba shimo kubwa, kulipiga sementi, na kubeba maji na kulijaza. Usiku uliotangulia ubatizo, kulinyesha, na asubuhi iliyofuata tulifurahi kuona dimbwi likiwa limejaa maji pomoni.

Asubuhi ya Jumapili hiyo, Koos alitoa hotuba ya ubatizo. Alipoomba wataka kubatizwa wasimame, 26 kati yetu tulisimama na kujibu maswali yale ya kawaida. Tulipata pendeleo la kuwa Mashahidi wa kwanza kubatizwa katika kisiwa hicho. Hiyo ilikuwa pindi yenye furaha zaidi maishani mwangu kwa sababu sikuzote nilikuwa na wasiwasi kwamba Har–Magedoni ingekuja kabla sijabatizwa.

Hatimaye makutaniko mawili yalianzishwa, moja katika Levelwood na jingine katika Jamestown. Kila juma watatu au wanne kati yetu tulisafiri kilometa 13 hadi kwenye kutaniko moja kuongoza Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi Jumamosi jioni. Baada ya utumishi wa shambani Jumapili asubuhi, tulirudi na kuwa na mikutano hiyo hiyo, vilevile Funzo la Mnara wa Mlinzi, katika kutaniko letu alasiri na jioni. Kwa hiyo miisho-juma yetu ilijaa utendaji wa kitheokrasi wenye shangwe. Nilitamani kufanya kazi ya kuhubiri ya wakati wote, lakini nilikuwa na familia ya kuruzuku. Kwa hiyo mnamo 1952, nilirudia utumishi wa serikali nikiwa daktari wa meno mwenye kufanya kazi ya wakati wote.

Katika mwaka wa 1955 wawakilishi wasafirio wa Sosaiti, waangalizi wa mzunguko, walianza kuzuru kisiwa hicho kila mwaka, na walikaa katika nyumba yangu kwa muda fulani wa ziara yao. Waliathiri familia yetu kwa njia inayofaa. Karibu wakati huohuo, mimi pia nilikuwa na pendeleo la kushiriki kuonyesha filamu tatu za Sosaiti kisiwani kote.

Kusanyiko Lenye Kusisimua la Mapenzi ya Kimungu

Katika mwaka wa 1958, kusudi niweze kuhudhuria Kusanyiko la Kimataifa la Mapenzi ya Kimungu katika New York, niliacha kazi tena katika utumishi wa serikali. Kusanyiko hilo lilikuwa tukio kuu maishani mwangu—fursa iliyonipa sababu ya kushangilia katika Yehova. Kwa sababu ya tatizo la usafiri wa kawaida kwenye kisiwa, tuliondoka kwa muda wa miezi mitano na nusu. Kusanyiko hilo lilichukua muda wa siku nane, vipindi vikianza saa tatu asubuhi na kumalizika saa tatu usiku. Lakini sikuchoka kamwe, na nilitazamia kwa hamu siku iliyofuata. Nilikuwa na pendeleo la kuwakilisha St. Helena kwa dakika mbili kwenye programu hiyo. Kuhutubia umati mkubwa katika Stediamu ya Yankee na Polo Grounds kulikuwa jambo lenye kujaribu kwelikweli.

Kusanyiko hilo liliimarisha azimio langu la kupainia. Hotuba ya watu wote, “Ufalme wa Mungu Watawala—Je, Mwisho wa Ulimwengu Umekaribia?,” ilikuwa yenye kutia moyo hasa. Baada ya kusanyiko hilo, tulizuru makao makuu ya Sosaiti katika Brooklyn na kuzuru kiwanda. Nilizungumza na Ndugu Knorr, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo, kuhusu maendeleo ya kazi katika St. Helena. Alisema kwamba angependa kuzuru kisiwa hicho siku moja. Tulirudi na mirekodio ya kaseti ya hotuba zote vilevile sinema nyingi za kusanyiko hilo ili kuzishiriki pamoja na washiriki wa familia na marafiki.

Nafikia Mradi wa Utumishi wa Wakati Wote

Niliporudi, niliajiriwa tena kazi yangu ya zamani, kwa kuwa hakukuwa na daktari wa meno kwenye kisiwa hicho. Hata hivyo, nilieleza kwamba nilinuia kuingia huduma ya wakati wote. Baada ya kushauriana kwa muda mrefu ilikubaliwa kwamba ningeweza kufanya kazi siku tatu kwa juma, lakini kwa mshahara wa juu zaidi ya niliopata nilipokuwa nikifanya kazi siku sita kwa juma. Maneno ya Yesu yalithibitika kuwa ya kweli: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi mtaongezewa.” (Mathayo 6:33) Haikuwa rahisi sikuzote kusafiri juu ya mandhari zenye milima kwa miguu yangu dhaifu. Ijapokuwa hivyo, nilipainia kwa muda wa miaka 14 na niliweza kusaidia wengi wa wakazi wenzangu wa kisiwani wajifunze kweli—kwa hakika hiyo ikiwa sababu ya kushangilia sana.

Mnamo 1961 serikali ilitaka kunituma kwenye Visiwa vya Fiji kwa mtaala usiokuwa na malipo wa miaka miwili ili niweze kuwa daktari wa meno aliyehitimu kikamili. Hata walijitolea kunituma pamoja na familia yangu. Hili lilikuwa toleo lenye kushawishi, lakini baada ya kulifikiria kwa uzito, nililikataa. Sikutaka kuwaacha akina ndugu kwa kipindi kirefu namna hiyo na kuacha pendeleo nililokuwa nalo la kuwatumikia. Afisa mkuu wa kitiba aliyepanga safari hiyo ndiye aliyefadhaika zaidi. Alisema: “Ikiwa wafikiri mwisho uko karibu sana, bado unaweza kutumia pesa utakazochuma kwa wakati uliopo.” Lakini nilisimama imara.

Mwaka uliofuata nilialikwa Afrika Kusini kuhudhuria Shule ya Huduma ya Ufalme, mtaala wa mwezi mmoja kwa waangalizi wa makutaniko. Tulipokea maagizo yenye thamani yaliyotusaidia kushughulikia migawo yetu ya kutaniko kwa njia yenye matokeo zaidi. Baada ya shule, nilipokea mazoezi zaidi kwa kufanya kazi pamoja na mwangalizi asafiriye. Kisha nilitumikia makutaniko mawili katika St. Helena kwa zaidi ya miaka kumi nikiwa mwangalizi wa mzunguko wa badala. Baada ya muda, ndugu wenye kustahili walipatikana, na tukatumia utaratibu wa kubadilishana.

Katika wakati huohuo, tulikuwa tumehama kutoka Jamestown hadi Levelwood, mahali palipokuwa na uhitaji mwingi zaidi, na tulikaa huko kwa miaka kumi. Wakati huo, nilikuwa nikifanya kazi nyingi sana bila kupumzika—kupainia, kufanya kazi ya serikali siku tatu kwa juma, na kusimamia duka dogo la vyakula. Kwa kuongezea, nilikuwa na mambo ya kutaniko ya kushughulikia, na mimi na mke wangu tulikuwa tukitunza familia ya watoto wanne waliokuwa wakikua. Ili kukabiliana na hali hiyo, niliacha kazi yangu ya siku tatu, nikauza duka hilo, na kuchukua familia nzima hadi Cape Town, Afrika Kusini, kwa likizo ya miezi mitatu. Kisha tulihamia Kisiwa cha Ascension na kukaa huko kwa mwaka mmoja. Wakati huo, tuliweza kusaidia wengi wajipatie ujuzi sahihi wa kweli ya Biblia.

Tuliporudi St. Helena, tulihamia tena Jamestown. Tulirekebisha upya nyumba iliyokuwa imeunganishwa na Jumba la Ufalme. Ili kujipatia mahitaji ya kimwili, mimi na mwana wangu John tulijenga gari la aiskrimu kwa kutumia lori aina ya Ford, na tuliuza aiskrimu kwa miaka mitano iliyofuata. Muda mfupi baada ya kuanzisha biashara hiyo, nilipata aksidenti nikiwa na gari hilo. Liliinama upande mmoja na kunasa miguu yangu. Tokeo lilikuwa kwamba, neva zilizo chini ya magoti zilifishwa, na ilinichukua muda wa miezi mitatu kupona.

Baraka Nyingi Wakati Uliopita na Wakati Ujao

Kwa miaka mingi iliyopita, tumekuwa na baraka nyingi—sababu zaidi za kushangilia. Mojawapo ya hizi ilikuwa safari tuliyofunga kuelekea Afrika Kusini kuhudhuria mkusanyiko wa kitaifa katika mwaka wa 1985 na kuzuru makao mapya ya Betheli, ambayo yalikuwa bado yakijengwa. Nyingine ilikuwa kushiriki fungu dogo, pamoja na mwana wangu John, kujenga Jumba la Kusanyiko zuri karibu na Jamestown. Pia tunafurahi kwamba watatu kati ya wana wetu wanatumika wakiwa wazee, na mjukuu wa kiume mmoja anatumika katika Betheli ya Afrika Kusini. Na kwa kweli tumevuna shangwe na uradhi mwingi kwa kusaidia wengi wajipatie ujuzi sahihi kuhusu Biblia.

Shamba kwa ajili ya huduma ni dogo, likiwa na watu wapatao 5,000 tu. Hata hivyo, kufanyia kazi eneo hilohilo mara kwa mara, kumeleta matokeo mazuri. Ni watu wachache sana wanaotuonyesha ujeuri. Kisiwa cha St. Helena kinajulikana kwa watu wake wenye urafiki, na utasalimiwa mahali popote uendapo—unapotembea barabarani au unapoendesha gari lako. Jambo ambalo nimejionea ni kwamba unapowajua watu vema, ndivyo iwavyo rahisi kuwatolea ushahidi. Sasa tuna wahubiri 150, ijapokuwa wengi wamehamia ng’ambo.

Watoto wetu wote wakiwa wamekua na kuhama, mimi na mke wangu tuko peke yetu tena, baada ya miaka 48 ya ndoa. Upendo wake mwaminifu na utegemezo wake ambao amenionyesha kwa miaka iliyopita vimenisaidia kuendelea kumtumikia Yehova kwa shangwe kujapokuwa majaribu. Nguvu zetu za kimwili zinapungua, lakini nguvu zetu za kiroho zinafanywa upya kila siku. (2 Wakorintho 4:16) Mimi, pamoja na familia na marafiki zangu, twatazamia kwa hamu wakati ujao wa ajabu ambapo nitarudishiwa afya ya kimwili iliyo bora zaidi kuliko ile niliyokuwa nayo nikiwa na umri wa miaka 17. Tamaa yangu kubwa zaidi ni kufurahia ukamilifu katika kila maana na, zaidi ya yote, kutumikia milele Mungu wetu mwenye upendo na anayejali, Yehova, na Mfalme wake anayetawala Yesu Kristo.—Nehemia 8:10.

[Picha katika ukurasa wa 26]

George Scipio pamoja na wana wake watatu, wanaotumika wakiwa wazee

[Picha katika ukurasa wa 29]

George Scipio pamoja na mke wake, Doris

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki