Kuharibu Vitu Kimakusudi Kunaweza Kukomeshwa
“SIKUZOTE kuharibu vitu kimakusudi kunakofanywa na matineja kumeonwa kuwa wonyesho wa uhasama na ukosefu wa staha kwa watu wazima na viwango vyao,” waandishi Jane Norman na Myron W. Harris wanaeleza. Ingawa vijana wengi wanaamini kwamba hakuna jambo lolote liwezalo kufanywa ili kubadili hali, “kijana mmoja kati ya kila vijana 3 anafikiri kwamba kuharibu vitu kimakusudi kunaweza kuzuiwa ikiwa wazazi wanakuwa waangalifu zaidi kwa watoto wao, na kama matineja hawangalikuwa wenye kuchoshwa sana,” waandishi hao wakaripoti. Ingawa kuharibu vitu kimakusudi kunaweza kupunguzwa kwa kuwapa vijana jambo la kufanya na kuwadhibiti ukiwa mzazi, je hayo pekee yataondoa visababishi vikuu vya kuharibu vitu kimakusudi?
Wanapokuwa peke yao, vijana wengi si wakorofi, lakini wakiwa katika kikundi au wawili-wawili, wanaweza kujaribu kuvuta uangalifu, wakifanya mambo mabaya na ya kipumbavu. Ndivyo ilivyokuwa na Nelson ambaye, akiwa ametumia dawa za kulevya au kileo, mara nyingi alidhihirisha hasira yake na kutoridhika kwa kuharibu vitu kimakusudi. Kwa kuchochewa na mahubiri katika Kanisa Katoliki kuhusu ugawaji wa mashamba na haki za wafanyakazi, José alionelea kwamba angepaswa kushiriki katika migomo, akapanga kuharibu vitu kimakusudi ili kudhihirisha mateto yake. Hata hivyo, Nelson na José waligundua kitu bora kushinda ghasia au kuharibu vitu kimakusudi.
Baadhi ya Visababishi Vikuu Zaidi vya Kuharibu Vitu Kimakusudi
Acheni tuchunguze kwa makini zaidi sababu zinazofanya vijana waharibu vitu kimakusudi. Vijana wengi wanaobalehe wametatanika nao “huufafanua ulimwengu huu kuwa mahali penye mvurugo na penye kichaa palipojaa watu wenye kichaa.” Hata hivyo, kinyume cha vile wengi huamini, ripoti moja ilisema hivi: “Matineja huhangaika kuhusu mwelekeo wa maisha yao. Wanahangaika kuhusu ulimwengu zaidi ya vile watu wazima wanavyofikiri.” Awe anafahamu au la, kijana anayeharibu vitu kimakusudi anaweza kuwa anadhihirisha kuvunjika moyo kwa ndani kabisa, matatizo ambayo bado hayajatatuliwa, au mahitaji ambayo bado hayajatimizwa. Kulingana na uchunguzi ambao umetajwa hapo mwanzo, “hakuna yeyote kati ya watu hao waliohojiwa aliyetetea kuharibu vitu kimakusudi kuwa halali, hata wale [waliokuwa] wameshiriki kufanya hivyo.”
Huenda kijana asisikie sana neno la kumshukuru au la kumtia moyo. Huenda kijana akakosa uhakika kwa kuwa elimu inazidi kuwa muhimu nazo kazi nyingi zaidi zahitaji kiasi fulani cha ujuzi maalum au ustadi wa kiufundi. Isitoshe, huenda wazazi, walimu, au marika wakawa wenye kukosoa-kosoa na wenye kudai sana, wakitilia mkazo yale kijana anayotimiza wala si vile alivyo kibinafsi. Wengi huasi au kuharibu vitu kimakusudi kwa sababu tu wametamauka. Je, upendo na uangalifu wa wazazi haungepunguza kwa kiasi kikubwa msononeko huo?
Huenda ukawa umefahamu kwamba ingawa wenye mamlaka fulani waonekana kuwa wameacha kujaribu kuzuia kuandika kwenye kuta na aina nyinginezo za uhalifu, kwa ujumla, watu wenye kuhangaika hutegemea walimu na wafanyakazi wa shule wazuie kuharibiwa kwa vitu. Kuhusu utekelezaji wa sheria, kichapo The World Book Encyclopedia chasema hivi: “Adhabu ya kuharibu vitu kimakusudi ni kutozwa faini au kutiwa gerezani. Mamlaka fulani za wilaya zina sheria ambazo hufanya wazazi wawajibike kwa vitendo vya kuharibu vitu kimakusudi vinavyofanywa na watoto wao. Lakini watu hawaadhibiwi kwa vitendo vilivyo vingi vya kuharibu vitu kimakusudi. Ni vigumu kutekeleza sheria katika hali kama hizo, nayo hasara inayotokana na kuharibiwa kwa kitu kimoja-kimoja, sio kubwa kiasi cha kustahilisha kuchukua hatua ya kisheria.” Ripoti moja ilionyesha kwamba ni asilimia 3 tu ya wakosaji waliotiwa mbaroni.
Yaelekea utakubali kwamba malezi ya wazazi yafaayo yaweza kuwa ndiyo njia nzuri zaidi ya kupambana na kisababishi kikuu cha uhalifu. Lakini maisha ya familia yanapoharibika, jumuiya huteseka. Profesa Ana Luisa Vieira de Mattos, wa Chuo Kikuu cha São Paulo, Brazili, asema kwamba baadhi ya sababu zinazofanya tuwe na matatizo ya vijana ni “usimamizi hafifu wa wazazi, ukosefu wa sheria na mawasiliano, kutochungwa, ubaridi au kutojali.”
Bila shaka, katika wakati wetu tumeona utimizo wa maneno ya Yesu: “Kwa sababu ya kuongezeka kwa uasi-sheria upendo wa idadi iliyo kubwa zaidi utapoa.” (Mathayo 24:12) Na ni nani awezaye kukanusha kwamba maneno yaliyoandikwa kwenye 2 Timotheo 3:1-4 hayabainiki kuwa kweli? Mtume Paulo aliandika hivi: “Jua hili, kwamba katika siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, wenye kujitanguliza, wenye kiburi, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio waaminifu-washikamanifu, wasio na shauku ya kiasili, wasiotaka upatano wowote, wachongezi, wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wasio na upendo wa wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kututumuka kwa kiburi, wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu.” Ukweli ni kwamba, kuishi tu kati ya watu wenye sifa kama hizo humfanya mtu awe mhalifu. Hata hivyo hatuhitaji kuvunjika moyo. Jumuiya kwa ujumla zimeshindwa kukomesha kuharibiwa kwa vitu, lakini tunaweza kupata watu ambao wamefaulu kubadili mtindo-maisha wao, ambao si watovu wa adabu tena wala wenye kuharibu vitu kimakusudi. Watu ambao wameacha kuharibu vitu kimakusudi.
Mwongozo Ufaao kwa Vijana
Ni nini ambacho kimewasaidia watu wanaoharibu vitu kimakusudi na wengineo wabadili utu wao? Ingawa huenda likawa jambo lenye kuwashangaza walimu na wazazi fulani, Biblia hutoa mwongozo bora na wenye kufaa wakati huu. Kwa kuifuata, wale walioharibu vitu kimakusudi wamesukumwa kutii sheria hii hususa ya Mungu: “Usiandamane na mkutano kutenda uovu.” (Kutoka 23:2) Wengi wamevutiwa na kweli ya Neno la Mungu kuhusu itikadi na mafundisho ambayo hawakuwa wamepata kuyaelewa hapo awali, na yale ambayo wamejifunza yamewafanya kuwa watu wema zaidi. Fikiria kisa cha José, kijana mmoja wa huko São Paulo. Aliamini juu ya kutumia sanamu katika ibada tangu utotoni. Alipojifunza kwamba Mungu ana jina, Yehova, na kwamba Hakubali ibada ya sanamu, José alifanya mabadiliko ili afanye yale yapendezayo machoni pa Mungu.—Kutoka 20:4, 5; Zaburi 83:18; 1 Yohana 5:21; Ufunuo 4:11.
Badala ya kupatwa na mfululizo wa hali zenye kuvunja moyo katika magenge yenye jeuri na migomo, Nelson alipata tumaini halisi la wakati ujao, na hilo limemtuliza sana. Yeye asema hivi: “Badala ya kukataliwa na familia yetu kwa sababu ya mashirika mabaya na maisha yangu nikiwa mraibu wa dawa za kulevya, sasa mimi ndiye ninayestahiwa zaidi nyumbani. Mara nyingi baba huniomba niwashauri kaka zangu. Tangu nianze kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, nimekuwa na furaha kwa sababu sasa nina kusudi maishani.” Na kuhusu Marco, kijana wa mjini aliyezoea kuishi katika eneo lenye jeuri, kule kujua kwamba Ufalme wa Mungu utafanya dunia iwe paradiso kumemchangamsha kwelikweli.—Ufunuo 21:3, 4.
Fikiria pia kisa cha mtu mmoja aliyekuwa mshiriki wa genge fulani, ambaye alikuwa mpiganaji wa barabarani, na mwenye kuharibu vitu kimakusudi. Akiwa yatima aliyekulia katika hali zenye kusikitisha sana, Valter alivutiwa kujua kwamba katikati ya mfumo mfisadi na mwovu, Mungu ana watu. Wao hujitahidi kwa unyofu kutumia kanuni za Biblia katika maisha yao, wakionyesha huruma, ufikirio, na fadhili. Valter aeleza hivi: “Kwa kupatana na ahadi ya Yesu, sasa nina familia kubwa, ‘akina ndugu na dada na akina mama na baba.’ Kuhusu wakati ujao, ninatazamia kwa hamu wakati ambapo watu wataishi kwa furaha na umoja chini ya serikali ya Mungu yenye uadilifu.”—Marko 10:29, 30; Zaburi 37:10, 11, 29.
Kitu Bora Kushinda Kuteta
Mbali na kuwaonyesha upendo na ufikirio wanadamu wenzao, wale walioharibu vitu kimakusudi wamejifunza pia ‘kuchukia uovu.’ (Zaburi 97:10; Mathayo 7:12) Namna gani wewe? Hata ikiwa wewe unateseka kutokana na matokeo ya kuharibiwa kwa vitu ambako kumeenea sana, kujifunza Neno la Mungu kutafanya Yehova awe halisi kwako akiwa Baba wa kimbingu mwenye upendo anayetaka kukutunza. (1 Petro 5:6, 7) Mungu anaweza kukusaidia kukua kiroho, licha ya udhaifu mbalimbali wa kibinafsi au umaskini. Hilo lenyewe ni jambo la kustaajabisha!
Kwa kweli, Yehova na Mwana wake Yesu Kristo wanataka watu wa aina zote wapate fursa ya kujifunza kweli ya Biblia. Neno la Mungu laweza kuwasaidia sana watu waache kuharibu vitu kimakusudi sasa. Linaweza kuwachochea wafanye maendeleo zaidi katika kutumia kanuni za Mungu. Matokeo yakiwa kwamba wanakuwa washiriki wa udugu wa kimataifa unaojulikana kwa usafi na adabu nzuri, kutaniko la ulimwenguni pote la Mashahidi wa Yehova. Kwa kupatana na Waefeso 4:24, Wakristo hao wanyofu “[wamevaa] utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.” Karibuni ulimwengu utajaa watu wa aina hiyo kwa sababu hao tu ndio watakaookoka na kuishi milele.—Linganisha Luka 23:43.
Inawezekana Kuwa na Ulimwengu Mpya Ambapo Vitu Haviharibiwi Kimakusudi
Je, unaamini kwamba kuharibu vitu kimakusudi kunaweza kwa kweli kukomeshwa? Ikiwa ndivyo, badiliko kubwa kama hilo litawezekanaje? Karibuni Ufalme wa Mungu utakomesha mfumo huu mwovu. Wakazi wa dunia watawajibika kwa uvunjaji wowote wa kimakusudi wa sheria za Mungu za uadilifu. (Linganisha Isaya 24:5, 6.) Ingawa “wakosaji wataangamizwa pamoja,” wapenda-uadilifu wataokolewa. “BWANA huwasaidia na kuwaopoa; huwaopoa na wasio haki na kuwaokoa; kwa kuwa wamemtumaini Yeye.”—Zaburi 37:38-40.
Kwa kweli, visababishi vya kuharibu vitu kimakusudi vitaondolewa kabisa. Na ndivyo ilivyo na uhalifu, uonevu, kuteseka, na uovu. Badala yake, watu wataishi kwa amani, uadilifu wa kweli, utulivu, na usalama katika ulimwengu mpya. Andiko la Isaya 32:18 lafafanua jambo ambalo litatokea kikweli: “Watu wangu watakaa katika kao la amani; na katika maskani zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu.” Naam, paradiso ya ulimwenguni pote itakaliwa na watu wanaowapenda na kuwafikiria wengine.
Wale walioharibu vitu kimakusudi, hali kadhalika mamilioni ya wengineo, tayari wana uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu. Hawashiriki kabisa katika vitendo vya kuharibu vitu kimakusudi. Je, wewe utaruhusu Neno la Mungu likuongoze kufikia uhai katika ulimwengu wake mpya? Kwa nini usimwige mtunga-zaburi wa zamani aliyeandika tangazo hili la Yehova: “Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; nitakushauri, jicho langu likikutazama.”—Zaburi 32:8.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Uangalifu na upendo wa wazazi hulinda vijana