Sababu Waweza Kuutumaini Unabii wa Biblia
MFALME PIRO wa Epirus, kaskazini-magharibi mwa Ugiriki, alipambana kwa muda mrefu na Milki ya Roma. Akitaka sana kupata habari yenye kutegemeka kuhusu matokeo ya pambano hilo, alienda kutafuta habari katika madhabahu ya uaguzi ya Delphi. Lakini jibu alilopata lingeweza kueleweka katika mojawapo ya njia hizi mbili: (1) “Nasema kwamba wewe mwana wa Æacus unaweza kuwashinda Waroma. Wewe utaenda, wewe utarudi, hutaangamia vitani kamwe.” (2) “Nasema kwamba Waroma wanaweza kukushinda wewe, mwana wa Æacus. Wewe utaenda, wewe hutarudi, utaangamia vitani.” Aliamua kuelewa habari zilizotolewa katika sehemu ya kwanza ya jibu hilo, hivyo akafanya vita dhidi ya Roma. Piro alishindwa kabisa.
Visa kama hivyo vilifanya habari za waaguzi wa kale ziwe na sifa mbaya kwa kuwa hazikutolewa waziwazi nazo zilikuwa na maana zaidi ya moja. Lakini namna gani unabii wa Biblia? Wachambuzi fulani husisitiza kwamba unabii mbalimbali unaopatikana katika Biblia ni sawa tu na habari za waaguzi. Wachambuzi hao hukisia kwamba matabiri ya Biblia yalikuwa tu ubashiri wa werevu wa matukio ya wakati ujao, uliotolewa na watu wenye akili nyingi na wenye kufahamu mambo vizuri, kwa kawaida watu wa jamii ya kikuhani. Tuseme kwamba watu hao, kwa kujionea mambo tu au kupitia ukoo wao mbalimbali wa pekee, walijua kimbele jinsi ambavyo hali fulani zingekuja kuwa kiasili. Kwa kulinganisha sifa tofauti-tofauti za unabii mbalimbali wa Biblia na habari za waaguzi hao, tutakuwa katika hali nzuri zaidi kuamua mambo ifaavyo.
Mambo Yanayotofautiana
Habari za waaguzi zilitambuliwa kwa kuwa na maana zaidi ya moja. Kwa mfano, mjini Delphi majibu yalitolewa kwa sauti zisizoeleweka. Hilo lilifanya iwe lazima kwa makuhani kuzifasiri na kubuni mistari ambayo ingeweza kutoa fasiri zilizo tofauti kabisa. Jibu lililopewa Croesus, mfalme wa Lidia, ni mfano halisi. Alipotafuta habari kwenye madhabahu ya uaguzi, aliambiwa hivi: “Croesus akivuka Halys, ataharibu milki yenye nguvu.” Kwa kweli, “milki yenye nguvu” iliyoharibiwa ilikuwa yake mwenyewe! Wakati Croesus alipovuka mto Halys ili kushambulia Kapadokia, alishindwa na Koreshi Mwajemi.
Kinyume kabisa na habari za waaguzi, unabii mbalimbali wa Biblia unatambuliwa kwa kuwa sahihi na wazi. Mfano mmoja ni ule unabii kuhusu kuanguka kwa Babiloni, ambao umerekodiwa katika kitabu cha Biblia cha Isaya. Miaka ipatayo 200 kabla ya tukio hilo, nabii Isaya alitabiri kinaganaga na kwa usahihi jinsi Muungano wa Umedi na Uajemi ungepindua Babiloni. Unabii huo ulifunua kwamba mshindi huyo angeitwa Koreshi, ukafunua mkakati hasa wa kukausha mto uliokuwa kama handaki ya kujikinga na kufunua pia kule kuingia ndani ya jiji lenye kuta kupitia malango yaliyokuwa wazi. Hayo yote yalitimizwa kwa usahihi. (Isaya 44:27–45:2) Pia ilitabiriwa kwa usahihi kwamba baadaye Babiloni lingekuwa ukiwa kabisa.—Isaya 13:17-22.
Fikiria pia, udhahiri wa onyo hili lililotolewa na nabii Yona: “Baada ya siku arobaini Ninawi utaangamizwa.” (Yona 3:4) Hakuna maana zaidi ya moja hapa! Ujumbe huo ulikuwa wenye kutokeza sana na wa moja kwa moja hivi kwamba papo hapo watu wa Ninawi “wakamsadiki Mungu; wakatangaza kufunga, wakajivika nguo za magunia.” Kwa sababu ya toba yao, Yehova hakuleta maafa dhidi ya Waninawi wakati huo.—Yona 3:5-10.
Habari za waaguzi zilitumiwa kama njia ya kuwa na uvutano wa kisiasa. Mara nyingi watawala na viongozi wa kijeshi walitaja fasiri waliyopendelea ili waendeleze masilahi na shughuli zao za kibinafsi, hivyo wakitoa “wonyesho wa upendeleo wa kimungu.” Hata hivyo, jumbe za Mungu za unabii zilitolewa bila kufikiria hadhi ya watu binafsi.
Kwa mfano: Nathani, nabii wa Yehova, hakusita kumkaripia Mfalme Daudi mwenye kukosa. (2 Samweli 12:1-12) Wakati Yeroboamu wa Pili alitawala ufalme wa Israeli wa makabila kumi, manabii Hosea na Amosi walimchambua vikali mfalme huyo mwenye kuasi pamoja na wale waliomwunga mkono kwa sababu ya uasi wao na mwenendo wao wenye kumshushia Mungu heshima. (Hosea 5:1-7; Amosi 2:6-8) Onyo hili ambalo Yehova alimtolea mfalme huyo kupitia kinywa cha nabii Amosi ndilo lililokuwa kali zaidi: “Nami nitaondoka nishindane na nyumba ya Yeroboamu kwa upanga.” (Amosi 7:9) Nyumba ya Yeroboamu iliangamizwa kabisa.—1 Wafalme 15:25-30; 2 Mambo ya Nyakati 13:20.
Mara nyingi, habari za waaguzi zilitolewa kwa ada fulani. Yule aliyetoa ada kubwa zaidi ndiye angepokea habari alizotaka. Wale waliotafuta habari kwenye madhabahu ya uaguzi ya Delphi walilipa ada kubwa sana kwa habari zisizofaa kitu na kwa njia hiyo wakajaza hekalu la Apolo, na majumba yaliyoongezwa kwenye hekalu hilo, vitu vyenye thamani kubwa. Kinyume cha hilo, unabii na maonyo mbalimbali ya Biblia yalitolewa bila malipo na bila upendeleo wowote. Hivyo ndivyo ilivyokuwa bila kujali cheo au utajiri wa mtu ambaye kwa ajili yake yalitolewa, kwa kuwa nabii wa kweli hangeweza kupokea rushwa. Nabii Samweli, aliyekuwa pia mwamuzi, angeweza kuuliza hivi kwa moyo mweupe: “Kwa mkono wa nani nimepokea rushwa inipofushe macho?”—1 Samweli 12:3.
Kwa kuwa habari za waaguzi zilipatikana tu katika sehemu hususa, mtu alilazimika kujitahidi sana kusafiri kwenda huko ili kuzipokea. Kwa mtu wa kawaida, ilikuwa vigumu sana kufika kwenye nyingi za sehemu hizo kwa sababu zilikuwa katika maeneo kama Dodona lililokuwa kwenye Mlima Tomarus huko Epirus na Delphi lililokuwa katika sehemu ya milima-milima ya Ugiriki ya kati. Kwa kawaida, ni matajiri tu na watu wenye uwezo ambao wangeweza kutafuta habari kutoka kwa miungu katika madhabahu hizo za uaguzi. Isitoshe, “mapenzi ya miungu” yalifunuliwa siku chache tu kwa mwaka. Kinyume kabisa cha hilo, Yehova Mungu aliwatuma wajumbe wake manabii waende moja kwa moja kwa watu ili kuwatangazia unabii mbalimbali waliohitaji kusikia. Kwa mfano, wakati wa uhamisho wa Wayahudi huko Babiloni, Mungu alikuwa na angalau manabii watatu waliokuwa wakitumikia miongoni mwa watu wake—Yeremia jijini Yerusalemu, Ezekieli miongoni mwa wahamishwa, na Danieli katika jiji kuu la Milki ya Babiloni.—Yeremia 1:1, 2; Ezekieli 1:1; Danieli 2:48.
Kwa kawaida, habari za waaguzi zilitolewa faraghani ili yule aliyezipokea aweze kutumia fasiri ya habari hizo kwa faida yake mwenyewe. Kinyume cha hilo, unabii mbalimbali wa Biblia ulitolewa hadharani ili wote waweze kusikia ujumbe na kuelewa maana yake. Mara nyingi nabii Yeremia alisema hadharani huko Yerusalemu, ingawa alijua kwamba ujumbe wake haukupendwa na viongozi na wakazi wa jiji hilo.—Yeremia 7:1, 2.
Leo, habari za waaguzi huonwa kuwa sehemu ya historia ya kale. Hazina thamani yoyote yenye kutumika kwa watu wanaoishi katika nyakati zetu zenye hatari. Hakuna habari kama hizo zinazohusiana na wakati wetu au wakati ujao. Kinyume cha hilo, unabii mbalimbali wa Biblia ni sehemu ya “neno la Mungu [lililo] hai na hukazia nguvu.” (Waebrania 4:12) Unabii mbalimbali wa Biblia ambao tayari umetimizwa huandaa kiolezo cha namna Yehova alivyoshughulika na watu na pia hufunua sehemu kuu za makusudi yake na utu wake. Kwa kuongezea, unabii mbalimbali wa Biblia, ulio muhimu, utatimizwa hivi karibuni. Akifafanua mambo yajayo, mtume Petro aliandika hivi: “Lakini ziko mbingu mpya [Ufalme wa Kimesiya wa kimbingu] na dunia mpya [jamii ya kibinadamu yenye uadilifu] ambazo tunangojea kulingana na ahadi yake [Mungu], na katika hizo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13.
Huenda ulinganisho huo mfupi wa unabii wa Biblia na habari za waaguzi wa dini zisizo za kweli ukafanya ufikie mkataa sawa na ule ambao umeonyeshwa katika kitabu chenye kichwa The Great Ideas: “Kwa habari ya ujuzi wa kimbele wa wanadamu wawezao kufa, manabii Waebrania waonekana kuwa wa kipekee. Tofauti na waaguzi au watabiri wapagani, . . . hawahitaji kutumia ufundi au mbinu ili kufahamu siri za Mungu. . . . Kwa sehemu kubwa, yaonekana walitoa unabii wenye kueleweka, tofauti na ule wa waaguzi. Angalau nia yaonekana ni kufunua wala si kuficha mpango wa Mungu kuhusu mambo hayo, kwa kuwa Yeye Mwenyewe hutaka wanadamu wajue kimbele jinsi ya kuenenda kwa busara.”
Je, Utautumaini Unabii wa Biblia?
Unaweza kuutumaini unabii wa Biblia. Kwa kweli, unaweza kufanya Yehova na kutimizwa kwa neno lake la unabii kuwa mambo yaliyo muhimu zaidi maishani mwako. Unabii wa Biblia si rekodi ya matabiri yaliyotimizwa tayari ambayo hayatumiki sasa. Unabii mwingi unaopatikana katika Maandiko unaendelea kutimizwa sasa au unangojea kutimizwa karibuni. Tukiamua mambo kulingana na wakati uliopita, tunaweza kuwa na hakika kabisa kwamba huo pia utatimizwa. Kwa kuwa unabii huo mbalimbali wakazia nyakati zetu na wahusisha hasa wakati wetu ujao, twafanya vema kuuchukua kwa uzito.
Kwa kweli unaweza kuutumaini unabii wa Biblia upatikanao kwenye Isaya 2:2, 3: “Itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya BWANA utawekwa imara juu ya milima . . . Na mataifa mengi yatakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa BWANA, . . . naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.” Kwa kweli leo mamilioni ya watu wanakubali ibada ya Yehova iliyokwezwa na wanajifunza kutembea katika mapito yake. Je, utakubali fursa ya kujifunza mengi juu ya njia za Mungu na kutwaa ujuzi sahihi kumhusu yeye na makusudi yake ili utembee katika mapito yake?—Yohana 17:3.
Kutimizwa kwa unabii mwingine wa Biblia kwahitaji tuchukue hatua ya haraka. Kuhusu wakati ujao karibuni, mtunga-zaburi aliimba hivi kiunabii: “Watenda mabaya wataharibiwa . . . Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo.” (Zaburi 37:9, 10) Wewe unafikiri ni nini kinachohitajika ili kuepuka uharibifu unaokaribia wa waovu na vilevile wale ambao hudhihaki unabii mbalimbali wa Biblia? Zaburi hiyohiyo yajibu hivi: “Wamngojao BWANA ndio watakaoirithi nchi.” (Zaburi 37:9) Kumtumaini Yehova humaanisha kuwa na imani thabiti katika ahadi zake na kupatanisha maisha yetu na viwango vyake.—Mithali 2:21, 22.
Maisha yatakuwaje wakati ambapo wale wanaomtumaini Yehova watairithi dunia? Tena, unabii mbalimbali wa Biblia wafunua kwamba wakati huo ujao mtukufu wakaribia kwa ajili ya wanadamu watiifu. Nabii Isaya aliandika hivi: “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba; maana katika nyika maji yatabubujika; na vijito jangwani.” (Isaya 35:5, 6) Mtume Yohana aliandika maneno haya yenye kutumainisha: “Naye [Yehova] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali. Na Yeye aketiye juu ya kiti cha ufalme akasema: . . . ‘Andika, kwa sababu maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.’”—Ufunuo 21:4, 5.
Mashahidi wa Yehova wanajua kwamba Biblia ni kitabu cha unabii wenye kutegemeka. Nao wakubaliana kabisa na himizo hili la mtume Petro: “Kwa sababu hiyo tuna neno la unabii likiwa limefanywa hakika zaidi; na mnafanya vema kulikazia uangalifu kama vile kwa taa yenye kung’aa mahali penye giza, hadi siku ipambazuke na nyota ya mchana izuke, katika mioyo yenu.” (2 Petro 1:19) Tunatumaini kwa moyo mweupe kwamba utatiwa moyo na matazamio bora yatolewayo na unabii wa Biblia kwa ajili ya wakati ujao!
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]
MADHABAHU YA UAGUZI YA DELPHI ndiyo yaliyokuwa maarufu zaidi katika Ugiriki ya Kale.
Mivuke yenye kulevya iliyotoka kwenye tundu hili ilimfanya nabii huyo wa kike afikie upeo wa shangwe
[Picha]
Kuhani wa kike aliagua akiwa ameketi juu ya kigoda hiki
Sauti alizotoa ziliaminika kuwa na ufunuo mbalimbali kutoka kwa mungu Apolo
[Hisani]
Kigoda: From the book Dictionary of Greek and Roman Antiquities; Apolo: The Complete Encyclopedia of Illustration/J. G. Heck
[Picha katika ukurasa wa 7]
Matabiri yaliyotolewa kwenye madhabahu ya uaguzi ya Delphi hayakuwa yenye kutegemeka hata kidogo
[Hisani]
Delphi, Ugiriki
[Picha katika ukurasa wa8]
Unaweza kuutumaini kabisa unabii wa Biblia kuhusu ulimwengu mpya