Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 11/15 kur. 4-7
  • Biblia Hujibu Maswali Muhimu ya Wakati Wetu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Biblia Hujibu Maswali Muhimu ya Wakati Wetu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Mungu Huruhusu Kuteseka?
  • Ni Nini Kusudi la Uhai?
  • Anachotutarajia Mungu Tufanye
  • Mwanga Wenye Kutegemeka wa Njia Yetu
  • Kusudi Lenyewe la Uhai
    Amkeni!—1992
  • Uhai Una Kusudi Tukufu
    Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai?
  • Mungu Ana Kusudi Gani kwa Wanadamu?
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
  • Je! Mungu Anajali?
    Je! Mungu Anajali?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 11/15 kur. 4-7

Biblia Hujibu Maswali Muhimu ya Wakati Wetu

JE, BIBLIA inafaa leo? Ili kujibu ndiyo, bila shaka ni lazima kitabu hiki cha kale kiwape wasomaji wake mwongozo juu ya habari zenye kupendeza zinazohusiana na wakati huu. Je, Biblia hutoa mashauri yenye manufaa juu ya habari ambazo hasa ni muhimu katika ulimwengu wa leo?

Ebu tuchunguze masuala mawili ya wakati huu. Kwa kufanya hivyo, tutachunguza yale Biblia isemayo kuhusu masuala hayo.

Kwa Nini Mungu Huruhusu Kuteseka?

Kwa kufikiria hali ulimwenguni leo, swali ambalo watu huuliza sana ni: Kwa nini Mungu huruhusu watu wasio na hatia wateseke? Swali hilo linafaa, kwa kuwa watu wanazidi kuathiriwa na uhalifu wenye jeuri, ufisadi, maangamizi ya jamii nzima-nzima, misiba ya kibinafsi, na kadhalika.

Kwa mfano, katika Juni 1998 garimoshi la moja kwa moja liligonga daraja huko kaskazini mwa Ujerumani, na kusababisha vifo vya abiria zaidi ya mia moja. Hata madaktari na zimamoto wenye ujuzi waliowahudumia majeruhi na waliokufa walihuzunishwa na vifo hivyo. Askofu mmoja wa Kanisa la Kievanjeli aliuliza: “Ee Mungu, Kwa nini haya yalitukia?” Hata askofu mwenyewe hakuwa na jibu.

Imeonekana kwamba watu wasio na hatia wanapopatwa na uovu na wasielezwe sababu, wakati mwingine wanakuwa wenye uchungu sana. Wakati huo ndipo Biblia iwezapo kutoa msaada, kwa kuwa hiyo hueleza ni kwa nini watu wasio na hatia hupatwa na uovu na kuteseka.

Yehova Mungu alipoumba dunia na kila kitu kilichomo duniani, yeye hakukusudia wanadamu wataabishwe na uovu na kuteseka. Kwa nini tuna hakika? Kwa sababu baada ya kukamilisha uumbaji wake, “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.” (Mwanzo 1:31) Jiulize, ‘Kama ningeona kitu kiovu, je, ningekitangaza kuwa “chema sana”?’ La, hasha! Kwa njia hiyohiyo, Mungu alipotangaza kila kitu kuwa “chema sana,” hakukuwepo na uovu wowote duniani. Hivyo uovu ulianza lini na jinsi gani?

Punde tu baada ya kuumbwa kwa wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, kiumbe wa roho mwenye nguvu alimwendea mwanamke na kupinga ukweli na haki ya enzi kuu ya Yehova. (Mwanzo 3:1-5) Baadaye kiumbe huyo, Shetani Ibilisi, alidai kwamba wanadamu hawangedumisha uaminifu-mshikamanifu kwa Mungu chini ya shida. (Ayubu 2:1-5) Yehova alichukua hatua gani kuhusiana na hali hiyo? Aliruhusu wakati upite ili ithibitike kwamba wanadamu hawawezi kuelekeza hatua zao kwa mafanikio bila kumtegemea. (Yeremia 10:23) Viumbe wanapotenda kinyume cha sheria na kanuni za Mungu, matokeo yanakuwa dhambi, ambayo hutokeza hali mbaya. (Mhubiri 8:9; 1 Yohana 3:4) Hata hivyo, licha ya hali hizo mbaya, Yehova alijua kwamba wanadamu fulani wangedumisha uaminifu-maadili kwake.

Tangu uasi huo wenye kusikitisha katika Edeni, miaka ipatayo 6,000 imepita. Je, huo ni muda mrefu mno? Yehova angeweza kumharibu Shetani na wanaomwunga mkono karne nyingi zilizopita. Lakini je, si imekuwa afadhali kungoja hadi kila jambo liwezalo kuleta shaka juu ya haki ya enzi kuu ya Yehova na uaminifu-maadili wa wanadamu kwake liondolewe? Je, sivyo ilivyo na taratibu za hukumu za sasa kwamba kesi ya mahakama ya kuamua aliye na hatia na asiye na hatia yaweza kuchukua miaka mingi?

Kwa kufikiria umuhimu wa masuala yanayomkabili Yehova na wanadamu—enzi kuu ya ulimwengu na uaminifu-maadili wa wanadamu—lilikuwa jambo la hekima kama nini kwa Mungu kuruhusu wakati upite! Sasa twajua vizuri kinachotukia wanadamu wanapopuuza sheria za Mungu na kujiongoza wenyewe. Matokeo yanakuwa uovu wenye kuenea. Na hiyo ndiyo sababu watu wengi wasio na hatia huteseka leo.

Lakini inafurahisha kwamba Neno la Mungu laonyesha kuwa uovu hautadumu milele. Kwa kweli, karibuni Yehova atakomesha uovu na wale wanaousababisha. “Bali waovu,” lasema andiko la Mithali 2:22, “watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.” Kwa upande mwingine, wale walio waaminifu kwa Mungu wanatazamia kwa hamu wakati, ulio karibu sana sasa, ambapo “kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe.”—Ufunuo 21:4.

Hivyo basi, Biblia hueleza wazi ni kwa nini watu wasio na hatia huteseka. Pia hiyo hutuhakikishia kwamba karibuni uovu na kuteseka zitaisha. Hata hivyo, tunapokabili shida za sasa za maisha, twahitaji kujibiwa swali jingine muhimu.

Ni Nini Kusudi la Uhai?

Labda sasa, kuliko wakati mwingineo wowote katika historia ya mwanadamu, watu wanajaribu kujua kusudi la uhai. Wengi hujiuliza, ‘Kwa nini niko hai? Naweza kupataje kusudi katika maisha yangu?’ Hali mbalimbali huwachochea kuuliza maswali hayo.

Huenda maisha ya mtu yakaathiriwa vibaya sana anapopatwa na msiba. Kwa mfano, mapema mwaka wa 1998 msichana mwenye umri wa miaka 12 aliyekuwa akiishi Bavaria, Ujerumani, alitekwa nyara na kuuawa kimakusudi. Mwaka mmoja baadaye, mamake alikiri kwamba kila siku yeye hutafuta kusudi la maisha—bila mafanikio yoyote. Vijana wengine huchochewa kutaka kujua kusudi la uhai. Wao hutafuta usalama, utimizo, na uhusiano wa karibu, lakini hukata tamaa waonapo unafiki na ufisadi ambao umeenea sana. Watu wengine hushughulika tu na kazi-maisha, lakini wao hugundua kwamba uwezo, umashuhuri, na mali hazitoshelezi ile hamu ya ndani ya kutaka kujua ni kwa nini wako hai.

Swali kuhusu kusudi la uhai lafaa kujibiwa kwa makini na kwa njia yenye kuridhisha hata mtu awe anachochewa na nini kuliuliza. Kwa mara nyingine, Biblia yaweza kuwa yenye manufaa sana. Hiyo huonyesha Yehova kuwa Mungu wa kusudi, Mungu ambaye hufanya kila jambo akiwa na sababu nzuri. Tunauliza, Je, ungejenga nyumba bila sababu yoyote? Yaelekea sivyo, kwa kuwa kujenga nyumba kwahitaji utumie pesa nyingi sana na kwaweza kuchukua miezi au miaka kadhaa. Wewe hujenga nyumba ili wewe au mtu mwingine aweze kuishi humo. Twaweza kusababu vivyo hivyo kumhusu Yehova. Hakufanya jitihada zote za kuumba dunia na viumbe juu yake bila sababu yoyote, bila kusudi lolote. (Linganisha Waebrania 3:4.) Kusudi lake kwa dunia ni nini?

Unabii wa Isaya waonyesha Yehova kuwa ‘Mungu aliyeiumba dunia na kuifanya.’ Kwa kweli, yeye ndiye “aliyeifanya [dunia] imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Naam, tangu dunia iumbwe, limekuwa kusudi la Yehova ikaliwe. Andiko la Zaburi 115:16 lasema: “Mbingu ni mbingu za BWANA, bali nchi amewapa wanadamu.” Hivyo, Biblia yaonyesha kwamba Yehova aliiumba dunia ili ikaliwe na wanadamu watiifu, ambao wangeitunza.—Mwanzo 1:27, 28.

Je, uasi wa Adamu na Hawa ulimfanya Yehova abadili kusudi lake? La. Kwa nini tuna hakika? Fikiria jambo hili: Biblia iliandikwa maelfu ya miaka baada ya uasi katika Edeni. Ikiwa Mungu alikuwa ameacha kusudi lake la hapo awali, kwa nini jambo hilo halikutajwa katika Biblia? Tunaweza pasipo shaka kufikia mkataa kwamba yeye hakubadili kusudi lake kuhusu dunia na wanadamu.

Isitoshe, kusudi la Yehova halishindwi. Kupitia Isaya, Mungu atoa uhakikisho huu: “Kama vile mvua ishukavyo, na theluji, kutoka mbinguni, wala hairudi huko; bali huinywesha ardhi, na kuizalisha na kuichipuza, ikampa mtu apandaye mbegu, na mtu alaye chakula; ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”—Isaya 55:10, 11.

Anachotutarajia Mungu Tufanye

Basi, ni wazi kwamba tunaweza kuwa na hakika katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu la kuruhusu wanadamu waaminifu wakae duniani milele. Ikiwa tutakuwa miongoni mwa hao wenye pendeleo la kuishi milele duniani, yatupasa kufanya yale Mfalme Solomoni mwenye hekima aliyosema: “Mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.”—Mhubiri 12:13; Yohana 17:3.

Kuishi kwa kupatana na kusudi la Yehova kwa wanadamu humaanisha kupata kumjua Mungu wa kweli na kuishi kwa kupatana na matakwa yake yaliyoonyeshwa katika Maandiko Matakatifu. Tukifanya hivyo sasa, tunaweza kuwa na tumaini la uhai udumuo milele kwenye dunia paradiso, ambapo hatutakoma kujifunza mambo mapya kumhusu Mungu na uumbaji wake wa ajabu. (Luka 23:43) Ni tumaini lenye kusisimua kama nini!

Wengi wanaotafuta kusudi la uhai huiendea Biblia nao hupata furaha nyingi hata sasa. Kwa mfano, kijana mmoja aitwaye Alfred alishindwa kupata kusudi la uhai. Alichukizwa na kujiingiza kwa dini katika vita, akasikitishwa na unafiki na ufisadi katika siasa. Alfred aliwazuru Wahindi wa Amerika Kaskazini akitumainia kupata ufafanuzi kuhusu kusudi la uhai, lakini akarudi Ulaya akiwa ametamauka. Kwa kukata tamaa, aligeukia dawa za kulevya na muziki wenye makelele. Hata hivyo, baadaye kuchunguza Biblia kwa ukawaida na kwa makini kulimsaidia Alfred atambue kusudi la kweli la uhai na kupata uradhi.

Mwanga Wenye Kutegemeka wa Njia Yetu

Hivyo basi, tunaweza kufikia mkataa gani kuhusu Biblia? Je, inafaa leo? Bila shaka, ndiyo, kwa sababu inatoa mwongozo juu ya masuala ya wakati huu. Biblia hufafanua kwamba Mungu hasababishi uovu nayo hutusaidia kupata kusudi lenye kuridhisha maishani. Isitoshe, Biblia ina habari nyingi kuhusu mambo yenye kupendeza sana leo. Habari kuhusu ndoa, kulea watoto, mahusiano ya wanadamu, na tumaini la wafu zinazungumziwa katika Neno la Mungu.

Tafadhali chunguza kwa makini habari zilizomo ndani ya Biblia ikiwa bado hujafanya hivyo. Ukitambua thamani ya kweli ya miongozo yake kwa maisha, unaweza kuhisi kama alivyohisi mtunga-zaburi aliyemtegemea Yehova Mungu kupata mwongozo na kuimba: “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.”—Zaburi 119:105.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Je, wajua ni kwa nini Mungu huruhusu watu wasio na hatia wateseke?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Unaweza kufurahia maisha yenye kusudi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki