Fuliza Kuzaa Matunda Kwa Uvumilivu
1 Akiandikia kundi katika Kolosai, miaka inayopungua 30 baada ya kifo na ufufuo wa Yesu Kristo, mtume Paulo angeweza kusema kwamba ukweli wa habari njema ulikuwa ukizaa matunda na kuongezeka katika ulimwengu wote. (Kol. 1:5, 6) Kwa kadiri yenye utukufu zaidi leo, Mashahidi wa Yehova wamefikia kwa uhalisi “sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia” wakiwa na habari njema ya Ufalme. (Mdo. 1:8, NW; Yn. 14:12) Wakati wa mwaka wa utumishi wa 1989, kulikuwako ongezeko la asilimia 5.6 katika wastani wa hesabu ya wahubiri wa Ufalme ulimwenguni kote, nasi tulifikia kilele kipya cha wahubiri 3,787,188 katika nchi 212!
2 Katika nchi ambazo kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu ni marufuku na ripoti si kamili, ongezeko lililo kubwa hata zaidi la asilimia 7.6 liliripotiwa! Yajapokuwa matatizo mengi yaliyopo katika mabara hayo, wahubiri waendelea “kuzaa matunda kwa uvumilivu.” (Luka 8:15, NW) Katika sehemu fulani fulani misongo imepungua, lakini hali ngumu zaendelea vilevile katika nchi nyinginezo.
3 Katika nchi ambazo kuna uhuru mkubwa zaidi ya kuendelea na utendaji mbalimbali wa kuhubiri Ufalme, twakabili matatizo tofautitofauti. Kutojali na ubaridi mwingi hukutwa, hasa sehemu zenye ufanisi wa kimwili. Watumishi wa Yehova lazima wajihadhari wasiwe na mitazamo hiyo. Hatutaki masilahi ya kimwili, anasa, tafrija, na vikengeushi vingine vifyonze utendaji wetu mbalimbali wa kitheokrasi. La sivyo tungeweza kuwa wasiojali na kushindwa kuthamini uhitaji wa kufuliza kuzaa matunda kwa uvumilivu.—Luka 21:34-36.
UVUMILIVU NA KUJIKAKAMUA VYAHITAJIWA
4 Uvumilivu ni takwa, tuwe tunakabili upinzani wa habari njema au tuwe tuna uhuru wa kadiri wa kutimiza madaraka yetu ya Kikristo. Katika baadhi ya mabara, ndugu zetu wamekuwa wakifanya kazi chini ya hali zenye uhasama kwa miongo mingi. Uvumilivu wao chini ya uhasama huo umetokeza hali yenye kukubalika, na sasa wao wanavuna baraka tele. (Rum. 5:3-5; Gal. 6:9) Hata tuwe tunakabili matatizo gani, twataka kufuliza kuvumilia. Lazima ushahidi wa Ufalme utolewe, na sisi sote lazima tuendelee kudhihirisha ukamilifu wetu. Kwa kuvumilia upande wetu, tutasalimisha nafsi yetu, au uhai.—Mk. 13:10; Luka 21:19.
5 Twaweza kudhihirisha kwamba hatuchukui mambo ya kiroho vivi hivi kwa kujikakamua kwa nguvu katika utumishi wa Yehova, bila kuchoka katika kazi ya kuhubiri. Katika baadhi ya mabara ambako usafirishaji ni wenye tatizo zaidi, ambako vitu vya kimwili vya lazima hukosekana, na ambako kuna matatizo ya kiuchumi, hakuna kulegea katika kuhubiri habari njema. Katika nchi chache za namna hiyo, wahubiri wa kundi hufikia kwa kawaida wastani wa saa 14 hadi 17 katika utumishi wa shambani kila mwezi. Hesabu za mapainia zinaongezeka daima pia. Hayo yanatufanya wale kati yetu walio na faida za kimwili watue na kufikiri. Je! tunaweza kuongeza ushiriki wetu katika kazi ya maana zaidi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi?
JE! TWAWEZA KUFANYA ZAIDI?
6 Kutumia wakati mwingi zaidi katika utumishi wa shambani huenda kukataka kurekebisha ratiba zetu kidogo. Endapo tumekuwa tukitumia saa moja katika huduma ya shambani siku ya Jumapili, je! tungeweza labda kurefusha wakati huo kwa kutumia saa nyingine moja kufanya ziara za kurudia au kuongoza funzo la Biblia? Au endapo tunaongoza funzo la Biblia moja, je! tungeweza kutia ndani saa moja hivi ya utumishi wa nyumba kwa nyumba au kufanya ziara za kurudia chache kabla ya funzo hilo? Siku ya Jumamosi baada ya kutumia saa mbili katika utendaji wa magazeti, labda tungeweza kupokeza magazeti kwa mtu ambaye tumefanya akawa wa kupelekewa magazeti kwa ukawaida au kujaribu kufanya ziara za kurudia chache. Wanaoishi katika eneo la jijini huenda wakaona ina faida kutumia wakati fulani katika utoaji ushahidi wa barabarani. Katika njia hizo au nyinginezo, huenda tukaweza kuongeza ushiriki wetu katika utumishi wa shambani. Matokeo mazuri hayana budi kuongezeka kwa kadiri iyo hiyo.
7 Kutumia wakati zaidi katika utumishi wa shambani katika kufanya ziara za kurudia bila shaka kutatokeza mafunzo ya Biblia zaidi yenye kuongozwa. Muda si muda hilo litamaanisha watu zaidi kuja kwenye ukweli na kutusaidia kutimiza kazi ya kuhubiri Ufalme.—Mt. 28:19, 20.
SALA NI MUHIMU
8 Endapo tutafuliza kuzaa matunda kwa uvumilivu, ni lazima tutafute baraka ya Yehova na kukubali mwelekezo wa roho yake. Ni lazima tufanye huduma yetu kuwa jambo la sala kwa Yehova. Tunaposali kwa Yehova juu ya utendaji wetu wa shambani, tunakumbushwa kwamba sisi ni wafanya kazi wenzake. (1 Kor. 3:9) Kwa msaada wa Yehova, tunaweza kuvumilia katika huduma yetu hata tusipoona matokeo ya mara moja. Katika baadhi ya maeneo, ongezeko limetokea baada ya miaka mingi tu ya uvumilivu wa uaminifu kwa upande wa wapiga mbiu ya Ufalme. Tunapotazama wakati ujao, ni jambo la lazima sikuzote kutafuta uongozi na msaada wa kimungu ili tusiache bali tutimize huduma yetu kikamili. (2 Tim. 4:5) Kungali matunda mengi yanayozaliwa katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi.
9 Yesu alikazia uhitaji wa sisi kusali sikuzote. (Luka 18:1) Paulo alisihi hivi: “Ombeni bila kukoma.” (1 The. 5:17) Kuna sababu zenye uharaka tudumu katika kusali sasa. Madaraka mengi yanahusika katika kuangalia kundi lenye kukua mwaka baada ya mwaka. Twataka kuwasaidia wengine wazae matunda kwa uvumilivu. Uangalifu lazima utolewe kwa mahitaji mbalimbali ya wahubiri mmoja mmoja na tengenezo kwa ujumla. Tukiwa twaona uhitaji wa upaji wa kutegemeza kazi hiyo na kuwezesha uchapishaji wenye kuendelea wa fasihi zenye msingi wa Biblia, twataka kusali kwamba Yehova atafuliza kumotisha watu wenye kuhofu Mungu wawe wakarimu katika jambo hilo.—2 Kor. 9:8-11.
10 Kwa kadiri ambavyo visehemu vya shamba la ulimwenguni kote zinavyofunguka kwa ajili ya usitawi wa kitheokrasi kwa kadiri kubwa zaidi ya wakati mwingineo uliopita, nasiha ya Kimaandiko katika Wakolosai 4:2, NW, yawa yenye maana zaidi: “Muwe mkidumu katika sala, mkibaki mmeamka katika hiyo pamoja na utoaji shukrani.” Sala zetu zapasa kuwa kwa ajili ya ndugu zetu kila mahali ili waendelee kuzaa matunda, kusaidia wengine wenye mfano wa kondoo wanaopatikana katika maeneo ambayo utoaji wa ushahidi umekuwa mgumu zaidi wakati uliopita.
ONYESHA WAZI SHUKRANI
11 Jinsi tulivyo wenye shukrani kwa ajili ya maandalizi tele ya kiroho tunayoonea shangwe sana! Twataka kumshukuru Yehova kwa ajili ya hayo, na pia twasali kwa ajili ya baraka yake yenye kuendelea juu ya kazi ya mtumwa mwaminifu na Baraza Linaloongoza lake. Jitihada zao za unyenyekevu, zisizochoka kwa ajili yetu na kwa ajili ya wenye mfano wa kondoo kuuzunguka ulimwengu zathaminiwa sana.
12 Katika kupanda mbegu ya Ufalme, kiasi kikubwa sana cha fasihi kimeangushwa. (Mt. 13:3-8, 18-23) Hata hivyo, kuna uhitaji wenye kuendelea kwa ajili ya Biblia na fasihi ya Biblia shambani. Ripoti ya ulimwengu yaonyesha kwamba kadiri kubwa ya upandaji na unyunyizaji maji kwa namna ya ziara za kurudia na mafunzo ya Biblia ya nyumbani imefanywa. Tunapoendelea kufanya sehemu yetu katika sehemu hizi za maana za huduma yetu, twamshukuru Yehova kwa ajili ya baraka yake yenye kuendelea inayofanya vitu vikue. Kweli kweli, twasali kwa ajili ya baraka hiyo.—1 Kor. 3:6, 7.
MAHITAJI MENGINE
13 Kwa sababu ya kuwa katika ulimwengu wajapokuwa si sehemu yao, Wakristo wataendelea kukabili mitihani na majaribu, nayo bado itazidi katika hizi siku za mwisho. Baadhi sasa wanavumilia mnyanyaso au matatizo mengine. Wengine walazimika kuendelea na utendaji wao mbalimbali wa Kikristo katika mabara yenye vita. Ndugu zetu wamepatwa na majanga kama vile matetemeko ya dunia, vimbunga, na tufani. Hilo linapotokea, twapaswa kusali kwa ajili ya ndugu zetu katika sehemu hizo. (Linganisha Matendo 12:5; 2 Wakorintho 1:11.) Nyakati nyingine huwa lazima kufikia au kuandikia wakuu katika vyeo vya juu kuhusu marufuku juu ya kazi yetu, mnyanyaso wa ndugu zetu, au mambo mengine yanayoathiri masilahi ya Ufalme. Chini ya hali hizo, sisi hufanya tuwezayo kibinafsi, na hutoa sala kuhusu watu hao ili kwamba wawe na mbetuko mzuri kuelekea watumishi wenzetu.—1 Tim. 2:1, 2.
14 Kuna misongo mingi inayoletwa juu ya familia zinazoishi katika ulimwengu mbovu wa Shetani. (2 Kor. 4:4) Jamaa waliooana huenda wakakabiliwa na matatizo mazito. Wapaswa kutiwa moyo wasali kwa ajili ya uongozi wa kimungu, nasi pia twaweza kusali kwa ajili yao. (1 Kor. 7:5; 1 Pet. 3:7) Vichwa vya familia wapaswa kuthamini kwamba Yehova atasikiliza sala zao za moyo mweupe za kutaka mwelekezo katika kusimamia vema nyumba zao. (Amu. 13:8; Flp. 4:6, 7) Vijana na wazee pia hukabiliwa na hali zenye kujaribu. Huenda hilo likawa shuleni, kwenye kazi ya kimwili, wakati wa kusafiri, au katika hali nyinginezo. Sala hutusaidia tukinze roho ya huu ulimwengu mbovu na kufuliza kuzaa matunda tunapoendelea kufanya yanayopendeza machoni pa Mungu.—Mt. 6:13; Efe. 6:13-18; 1 Yn. 3:22.
15 Yehova ndiye Msikiaji mkuu wa sala. (Zab. 65:2) Nyakati zote twahitaji kumtupia mahangaiko yetu. (Zab. 55:22) Tuna fursa za kuonyesha hangaiko letu kupitia sala kwa ajili ya masilahi yote ya Ufalme na kwa ajili ya hali njema ya ndugu zetu kila mahali. Tunapotafakari juu ya kazi ya wale wanaoongoza katika kundi na wale wanaoelekeza programu ya upanuzi ya ulimwenguni pote, wakati tunaposhughulika na walio wagonjwa kiroho, au wakati wa kuangalia matatizo mengine yawe ni madogo au makubwa, sisi sote twapaswa kuyaweka mambo mbele ya Yehova katika sala. (1 The. 5:25; Yak. 5:14-16) Ndiyo, mahangaiko yetu yapasa kutupwa juu ya Yehova kwa uhakika kamili kwamba hata tumwombe nini kwa kupatana na mapenzi yake, yeye atatusikia. (1 Pet. 5:7; 1 Yn. 5:14) Na tuwe na bidii katika utumishi wa Ufalme na kuendelea kumtazamia Yehova atusaidie tufulize kuzaa matunda kwa uvumilivu.