Kuanzisha Mafunzo ya Biblia na Kitabu Kuishi Milele
1 Upendo kwa watu wapaswa utuchochee tuwe wepesi kurudi ili kuwasaidia wale wanaoona njaa na kiu ya ile kweli. (Mt. 5:6) Twapaswa kutambua na kusitawisha kupendezwa kokote ambako huenda tukapata ikiwa hatutaki kuishe. Kujitayarisha ndio ufunguo wa mafanikio.
2 Mradi wetu wapaswa uwe kuanzisha mafunzo ya Biblia. (Mt. 28:20) Nakala za kwanza za kitabu Kuishi Milele zilitia ndani maelezo haya ya utangulizi: “Hiki kwa kweli ni kitabu bora sana cha kutumia kujifunza na kila mtu, kijana au mzee, bila kujali kiwango chao cha elimu.” Kimeandikwa kwa njia ambayo hufanya kujifunza kuwe rahisi, kikiwezesha hata wahubiri wapya washiriki. Kufanikiwa kwetu katika kuanzisha mafunzo mapya kwategemea matokeo yetu katika kufanya ziara za kurudia.
3 Twaweza Kuanzishaje Mafunzo? Tunaporudi, kwa kawaida ni vizuri kuunganisha mazungumzo na jambo fulani au swali lililotajwa katika ziara yetu ya kwanza. Labda mlizungumza juu ya hali ya wafu, ukiacha swali, “Kuna tumaini gani kwa wapendwa wetu waliokufa?” Eleza kwamba ufufuo si tumaini lisilo na msingi; Biblia yarekodi vielelezo kadhaa vya ufufuo ambavyo vimekwisha kutukia. Pitia vielezi kwenye kurasa 167-9. Kisha zungumza juu ya yale yaliyotajwa katika mafungu 1 na 2 kwenye ukurasa 166. Panga kurudi ili uendeleze mazungumzo.
4 Huenda ikawa uliongea na mzazi ambaye alionyesha hangaiko juu ya kuongezeka kwa matatizo yanayoonwa katika kulea watoto. Kwa maneno yako mwenyewe, unaweza kusema jambo kama hili:
◼ “Wazazi wote huwatakia watoto wao yaliyo bora. Biblia ina maagizo yanayoweza kusaidia wazazi wazoeze watoto wao kupata maisha yenye kuridhisha yaliyo na maana na kusudi. Kwa sababu hiyo, twapendekeza sana kwamba familia zijifunze Biblia pamoja. [Rejezea fungu la 23 kwenye ukurasa 246.] Ujuzi unaopatikana waweza kuletea familia nzima baraka za milele.” Soma Yohana 17:3. Onyesha nia yako ya kurudi ili uonyeshe familia jinsi ya kuanzisha funzo lao.
5 Ikiwa wewe ni mhubiri mchanga au mpya zaidi na uliongea kifupi juu ya Paradiso katika ziara ya kwanza, ukiwa na kitabu hicho fungua ukurasa 3, eleza kwa usahili jambo kama hili:
◼ “Biblia yaahidi kwamba wale wanaofanya mapenzi ya Mungu wanaweza kutazamia kuishi katika ulimwengu kama huu, mahali ambapo kutakuwa na furaha na amani. Kitabu hiki chaonyesha yale tunayopaswa kufanya ili tufurahie baraka hiyo.” Eleza kifupi taratibu yetu ya kujifunza, nawe jitolee kumwonyesha.
6 Tukiwa wanafunzi wa Yesu, tuna wajibu wa kusaidia watu. (Rum. 10:14) Ikiwa tuliangusha fasihi au tulikuwa na mazungumzo mazuri, tuna daraka la kusitawisha kupendezwa. (Mt. 9:37, 38) Tukitimiza mgao huu ifaavyo, wote wanaweza kushiriki baraka zinazotokana nao.—1 Tim. 4:16.