Kufuata Kielelezo Chetu Tukiwa Wachukuaji-Nuru
1 Yesu alitangaza kujihusu: “Mimi ndimi nuru ya ulimwengu.” Kwa kufuata kielelezo chake, wanafunzi wa Yesu pia walikuwa “nuru ya ulimwengu.” (Mt. 5:14) Akiwa “nuru ya ulimwengu,” Yesu angeweza kusema kwamba wote wanaomfuata watapata “nuru ya uzima.” (Yn. 8:12) Hilo hutufanya tuwe wachukuaji-nuru wa kiroho, ambao hawapaswi kuficha au kusetiri nuru hiyo.
2 Tengenezo la Yehova huandaa mazoezi ya kutuonyesha jinsi ya kuwa wachukuaji-nuru wenye matokeo. Tukifuata kwa uangalifu shauri na mwelekezo tunaopata, tutaweza kunurisha watu wa aina zote kuhusu kweli ya Ufalme. (1 Tim. 4:6) Kutumika tukiwa wachukuaji-nuru hutia ndani si kuongea kweli katika kila fursa peke yake bali pia kudumisha mwenendo mzuri tukiwa Wakristo. Mwenendo wa Kielelezo chetu ulikuwa bila lawama. Tukiwa wafuasi wake, twapaswa kuonyesha kwamba Ukristo ni njia yetu ya maisha ya kila siku. (Efe. 5:9; Tito 2:7, 8, 10) Ni lazima tutokeze kazi nzuri ambazo wengine waweza kuona, zikiwasukuma kumtukuza Mungu.—Mt. 5:16.
3 Shahidi mmoja alikabili ombi lisilo la kawaida alipokuwa akienda nyumba kwa nyumba. Mwanamume wa nyumba hiyo pamoja na mke wake walikuwa wagonjwa sana, lakini walihitaji kuweka fedha fulani katika benki. Walimwomba Shahidi huyo kama angefanya hivyo. Alikubali naye akapewa $2,000 [badili kulingana na thamani yenu] apeleke benki! Aliporudi, yeye aliuliza: “Mngewezaje kuniamini hata bila kunijua?” Jibu: “Twajua, na kila mtu awaye yote ajua, kwamba Mashahidi wa Yehova ndio watu tu wa kutumaini.” Twaweza kushukuru kama nini kwamba kushikilia kwetu kanuni za adili za Biblia hutokeza sifa kama hiyo ya kumheshimu Mungu!
4 Mwalimu mmoja wa darasa la kwanza alielezea darasa lake kwa nini Shahidi mwenye umri wa miaka sita hakuwa akishiriki katika kupaka rangi picha za sikukuu ya Hallowini. Mwalimu huyo alisema alimwonea fahari msichana huyo kwa kuwa na moyo mkuu wa kuwa tofauti kwa sababu ya yale anayoamini. Ikiwa tunaamini jambo fulani kwa uhakika, mwalimu huyo akaeleza, twapaswa kuwa wenye moyo mkuu wa kulitetea. Usiku huo mwalimu huyo alichunguza itikadi zake mwenyewe na kukubali kwamba hakuwa ameonyesha moyo mkuu kama huo wa kutetea masadikisho yake. Siku iliyofuata alitangaza kwamba hangehusisha darasa lake tena katika sherehe za sikukuu zozote za wakati ujao, ambazo baadhi yazo hakuwa akiziamini mwenyewe!
5 Watu wa Yehova wana hamu ya kuacha nuru yao iangaze, bila kujali wako wapi. Mwenendo mzuri wa vijana shuleni umevutia kwa uzuri wanashule wenzi na walimu. Mashahidi walio watu wazima wanaoonyesha mwenendo mzuri katika ujirani wamefanya wengine waongee vizuri juu ya ujumbe wa Ufalme. Ushahidi wa vivi hivi chini ya hali nyingi huvutia watu wanyoofu wanaotaka kujifunza mengi. Hata bidii yetu na ufuatiaji wa haki kazini hutoa ushahidi. Naam, bila kujali mahali tulipo au tufanyalo, twaweza kuamsha kupendezwa katika kweli.
6 Kwa kuweka macho yetu kwenye kiolezo cha maisha kisicho na lawama cha kielelezo chetu kikubwa, twaweza kuendelea kuboresha stadi zetu tukiwa wanafunzi wake. Kuiga kielelezo chake kutahakikisha kwamba nuru yetu “yawaangaza wote.”—Mt. 5:15; 1 Pet. 2:21.