Tumia Vizuri Wakati Wako
1 Yehova ni mwenye kutambua wakati. Yeye ataka sisi tutambue wakati pia. Kupitia tengenezo lake anatusaidia tutambue wakati. Sikuzote twasihiwa tuwe na ‘mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’ (1 Kor. 15:58, NW) Kwa njia hii, twaweza kuwa wenye matokeo zaidi katika utumishi wa Yehova.
2 Kila mmoja wetu ana kiwango kilekile cha wakati kila juma—saa 168. Sisi hutumia wakati wetu vizuri jinsi gani? Je, sisi huonyesha kwamba kwa kweli twajua tumo katika wakati gani kutokana na maoni ya Yehova? Je, twakengeushwa na utendaji usio muhimu?
3 Ni jambo la maana kwamba tuwe wenye mpango mzuri. Wengi hujaribu kudumisha orodha ya vitu vinavyopewa nafasi ya kwanza. Kila jambo linawekwa kwenye orodha kulingana na umaana walo. Hilo laweza kuamuliwaje? Biblia husema kwamba mtu apaswa ‘kuona mema katika kazi yake yote ya bidii.’ (Mhu. 3:13, NW) Kazi nyingine huwa na matokeo bora kuliko nyingine. Fikiria matokeo ambayo kila moja yazo italeta. Je, kumaliza hiyo kazi kutatokeza manufaa za maana? Je, ‘utaona mema’ kwa kazi yako ya bidii? Ikiwa sivyo, huenda isiwe kazi ya kupewa nafasi ya kwanza zaidi.
4 Katika Huduma Yetu: Twathamini wengine wafikapo kwenye mikutano ya utumishi kwa wakati, kusikiliza maagizo kwa uangalifu, na kuondoka kwa wakati kuelekea kwenye eneo. Ni afadhali tuwe wenye shughuli tukihubiri badala ya kungoja. Bila shaka Paulo alihisi kwa mkazo uhitaji wa utaratibu mzuri alipoandika: “Mambo yote na yatendeke kwa uzuri na kwa utaratibu.”—1 Kor. 14:40.
5 Tunapokuwa nje katika utumishi wa shambani, twaweza kupoteza wakati wenye thamani kwa ajili ya kahawa. Ingawa hivyo, wengi hupendelea kuendelea kutolea watu ushahidi na kuacha kushirikiana na akina ndugu wakati wa mapumziko ya kunywa kahawa katika wakati uliowekwa kando kwa ajili ya huduma. Usawaziko wahitajiwa.
6 “Naam, koikoi . . . ajua nyakati zake zilizoamriwa” za kuhama, naye chungu “hukusanya chakula chake wakati wa mavuno” ili awe tayari wakati wa kipupwe, Biblia yasema. (Yer. 8:7; Mit. 6:6-8) Hapo ndipo pana siri ya kutumia wakati vizuri. Sisi pia twapaswa ‘kujua nyakati zetu zilizoamriwa.’ Bila ya kuwa wenye kushikilia mambo mno, twapaswa kutambua wakati. Twahitaji kujua si yale tu tupaswayo kufanya bali pia wakati lipaswapo kufanywa. Twapaswa kuwa wenye zoea la kufikiria mapema, tukiruhusu uchelewaji wowote uwezao kutokea. Na pia twapaswa kuwa tayari kufupiza utendaji fulani ili tuweke wakati wa jambo fulani la maana zaidi, kama vile utayarishaji kwa ajili ya mikutano yetu, utumishi wa shambani, na utendaji mwingineo wa kitheokrasi.
7 Twataka kuwa kama Baba yetu wa kimbingu, Yehova Mungu, ambaye hutufunza kwamba “kwa kila jambo kuna majira yake.” (Mhu. 3:1) Kwa kutumia vizuri wakati wetu, twaweza ‘kutimiza kikamili huduma yetu.’—2 Tim. 4:5, NW.