Wazazi Walio na Shangwe!
1 Ikiwa wewe ni kijana anayeishi katika nyumba ya Kikristo, kuna njia ya pekee uwezayo kufanya wazazi wako wawe wenye furaha. Ukifuatia mwendo wa uadilifu, ‘baba yako na mama yako watafurahi.’ (Mit. 23:22-25) Bila shaka wazazi wako wanakutakia yaliyo bora zaidi. Hakuna jambo ambalo lingewapendeza zaidi kuliko kukuona ukiifanya kweli iwe yako mwenyewe na kuweka maisha yako wakfu kwa Yehova.
2 Waweza kuwa mwenye shukrani kuwa na wazazi walio katika kweli. Tokea kuzaliwa kwako, wamekulisha, kukuvisha, na kukuandalia makao pia kukulea hata wakati wa ugonjwa. Hata la maana zaidi, wamejitahidi kukufundisha juu ya Yehova na njia zake za uadilifu; haya ni mazoezi yanayoweza kukuhakikishia uhai wa milele. (Efe. 6:1-4) Waweza kuonyeshaje uthamini wako?
3 Fanya Kweli Iwe Yako Mwenyewe: Wazazi wako wamekufundisha kuichukulia kweli kwa uzito, kufanya maendeleo ya kiroho, na kuwa karibu na tengenezo la Yehova. Waweza kuonyesha uthamini kwa kuwa na upendezi katika funzo la familia bila kushurutishwa. Onyesha tamaa ya kuhudhuria mikutano, kuchukua hatua mwenyewe ya kuwa tayari ili familia ifike kwa wakati. Keti pamoja na wazazi wako wakati wa mikutano, na usikilize kwa makini kwa kufuatia pamoja na vichapo vinavyotumiwa kujifunza. Shiriki mikutano kwa kutoa maelezo. Jionyeshe kuwa mwanafunzi mwenye hiari katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ukikubali migawo na kufanya vema ili kuitimiza. Jitolee usaidie kutunza kazi zilizo kwenye Jumba la Ufalme, msaada wako ufaapo. Kujihusisha katika utendaji kama huo kwaweza kufanya moyo wako ukazie yaliyo mema kwa hali yako ya kiroho.
4 Weka Miradi Yenye Maendeleo: Stahili kwa ajili ya ushiriki wa utumishi wa shambani wenye maana, ukionyesha tamaa ya kustahili kuwa mhubiri. Endelea na usomaji wa Biblia wa kila juma au hata kwa faida zaidi, soma Biblia nzima wewe mwenyewe. Azimia kwamba utafikia matakwa ya wakfu na ubatizo. Wazazi wako wanaweza kukusaidia upange masomo yako shuleni kwa uangalifu, ukiwa na maoni ya kupata mazoezi yatakayokusaidia uwe na ushirika kamili katika utumishi wa Yehova. Kazia kusitawisha aina ya sifa itakayochochea wengine wakupendekeze kwa mapendeleo ya pekee kama vile upainia au utumishi wa Betheli. (Mdo. 16:1, 2) Kufikia miradi kwaweza kukusaidia ‘upate kuyakubali yaliyo mema; ili upate . . . kujazwa matunda ya haki.’—Flp. 1:10, 11.
5 Ujana ni wakati wa kujifunza, kupata maarifa, na kujipatia stadi katika kushughulika na wengine. Ni wakati wa kufurahia maisha bila mikazo yo yote na madaraka yanayokuja kutokana na utu mzima. Sulemani alisema: “Wewe, kijana, uufurahie ujana wako, na moyo wako ukuchangamshe siku za ujana wako.” (Mhu. 11:9) Ukiazimia moyoni mwako kumtumikia Yehova katika ujana wako, utavuna baraka zitakazodumu milele.—1 Nya. 28:9.
6 ‘Ukifuata haki’ badala ya “tamaa za ujanani,” utaondolea wazazi wako mzigo mzito wa mahangaiko na maumivu. (2 Tim. 2:22) Moyo wako mwenyewe utakuwa na sababu ya kuwa na shangwe. (Mit. 12:25) Zaidi ya yote, utaletea shangwe Muumba wako, Yehova Mungu.—Mit. 27:11.