Sanduku la Swali
◼ Je, inafaa kuchangia usafiri unaoandaliwa na wengine?
Wengine wetu tuna hali zinazotufanya tutegemee msaada wa wengine katika kuhudhuria mikutano kwa ukawaida na kushiriki katika utumishi wa shambani. Kwa fadhili, ndugu na dada wengi hujitahidi kipekee kutumia wakati wao, magari yao, na mali zao ili kutuandalia usafiri. Ingawa huenda wakalazimika kujitayarisha mapema kuliko vile wangefanya kwa kawaida na wanachelewa kurudi nyumbani, wao huandaa usafiri kwa roho ya hiari.
Kama vile sehemu nyingine ya huduma yetu ya Kikristo, kanuni ipatikanayo kwenye Wagalatia 6:5 hutumika: “Kila mtu atalichukua furushi lake mwenyewe.” Kwa hiyo, mtu akituandalia usafiri kwa ukawaida, twapaswa kuonyesha uthamini si kwa maneno tu bali pia, tukiweza, kwa mchango ufaao wa kusaidia kutunza gharama zinazohusika.—Mt. 7:12; 1 Kor. 10:24.
Hata kama mtu anayetumia gari lake haombi usaidizi wa kifedha na haonekani akiuhitaji, sikuzote utoaji wa mchango wenye unyoofu huthaminiwa. Dereva huenda akakataa kuchukua kitu chochote; na bila shaka, huo wapaswa kuwa uamuzi wake. Lakini inafaa utoe kitu. Ikiwa huwezi kuchangia kitu chochote wakati huo, unaweza kukumbuka jambo hilo; unaweza kutoa kitu cha ziada wakati unaofuata unapokubali kupelekwa kwa gari.—Luka 6:38.
Ni jambo lenye upendo kwa wale walio na magari kuandaa usafiri kwa wengine ambao huenda wasiweze kuhudhuria mikutano au kushiriki katika huduma ya shambani. (Mit. 3:27) Wakati uleule, pia ni jambo la upendo kwa wale wanaonufaika na fadhili kama hiyo kuonyesha shukrani zao kwa kuchanga kulingana na hali zao.—Kol. 3:15.